Feb 23, 2011

Saif al-Islam: Mtoto wa nyoka aliyeandaliwa kuwa mrithi wa urais

 Mtoto wa Gaddafi, Saif al-Islamu

Tripoli
LIBYA

UTAWALA wa Kanali Muammar Gaddafi uko katika hali tete, kufuatia maandamano makubwa katika mji mkuu wa Libya yenye lengo la kumshinikiza kuachia madaraka. Kadhalika kujiengua kwa baadhi ya mabalozi kunazidisha shinikizo kwa Gaddafi ambaye amekuwa akiongoza nchi hiyo kwa mkono wa chuma. 
 
Maofisa wa usalama walifyatua risasi na mabomu ya machozi kwa waandamanaji katika mitaa ya Tripoli Jumapili iliyopita, na hata mji wa pili kwa ukubwa, Benghazi, sasa unaonekana uko chini ya udhibiti wa waandamanaji hao.

Hofu ya wimbi hilo imemlazimisha mwana wa Gaddafi, Saif al-Islamu kujitokeza kwa mara ya kwanza tangu harakati hiyo ianze na kutoa ahadi ya kutayarisha katiba mpya itakayojali misingi ya demokrasia. Hatua hiyo pia haikufua dafu kwani imekuja ikiwa imechelewa. 
 
Ili kujaribu kutuliza harakati ya wananchi, Kiongozi wa Libya ametumia hata mbinu ya kuwaajiri mamluki wa Kiafrika ambao wamekuwa wakishiriki katika kukandamiza harakati hiyo. Jinai hiyo imezidisha hasira za wananchi na kuchochea zaidi maandamano. 
 
Kwa kuzingatia hayo yote, wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanasema kuwa jinai na mauaji ya mamia ya watu yaliyofanywa na jeshi la Kanali Gaddafi katika siku chache zilizopita, zimegonga kengele ya kuanza kuporomoka kwa utawala ulioongoza Libya kibabe kwa kipindi cha miaka 42. 
 
Mtoto huyo wa Gaddafi, ameonya kuwa vita vya wenyewe kwa wenyewe huenda vikazuka kama maandamano hayo hayatasitishwa. Katika hotuba ndefu kupitia televisheni, motto huyo wa Gaddafi ametoa mapendekezo ya mabadiliko ya kisiasa, lakini pia kuahidi kuwa utawala huo “utapigana mpaka mwisho” dhidi ya “wachochezi”.

Amesema makundi ya upinzania na wageni wanajaribu kuigawa Libya kuwa katika majimbo madogo madogo, na kwamba iwapo watafanikiwa amesema uwekezaji wa nje utasitishwa na viwango vya maisha vitashuka kwa kasi.

Saif Gaddafi pia amevikosoa vyombo vya habari vya nje kwa kile alichokiita kukisia kiwango cha vurugu zinazoendelea nchini Libya.

Hata hivyo, amekiri kuwa miji ya Mashariki ya Benghazi na al-Badya imechukuliwa na wapinzani na pia amekiri kwamba baadhi ya kambi za jeshi la nchi hiyo na vifaru vinadhibitiwa na wananchi. 
 
Waziri wa sheria, Mustapha Abdul Jalil, amekuwa afisa wa hivi karibuni kujiuzulu. Amesema alikuwa akiachia madaraka yake kwa sababu ya “matumizi makubwa ya nguvu”, amekaririwa na gazeti binafsi la Quryna, siku ya Jumatatu akisema.

Maandamano na machafuko makubwa yanayoendelea nchini Libya na kuongezeka idadi ya watu waliouawa kwa kupigwa risasi vimezidisha wasiwasi mkubwa na kuteteresha nguzo za utawala wa kiongozi wa nchi hiyo, Kanali Muammar Gaddafi. Vyombo vya habari vimeripoti kuwa askari wa usalama waaminifu kwa utawala wa Gaddafi wanatekeleza mauaji dhidi ya wananchi kama wendawazimu katika mitaa ya miji mbalimbali ya nchi hiyo. 
 
Hospitali za Libya zimewekwa katika hali ya tahadhari na inaripotiwa kuwa idadi ya watu waliouawa hadi sasa inakaribia mia tano. Pamoja na hayo maandamano na harakati za wananchi za kutaka kung'oa madarakani utawala wa miaka 42 wa Kanali Gaddafi yanazidi kupamba moto. 
 
Baadhi ya ripoti zinasema kuwa familia ya kiongozi huyo wa Libya imekimbilia nje ya nchi. Kumekuwepo habari za kutatanisha pia kuhusu kukimbia nchi kwa kiiongozi huyo wa Libya, ingawa tetesi hizo zimekanushwa na Gaddafi mwenyewe pale alipojitokeza hadharani kwenye televisheni ya Taifa. Ni wazi kwamba harakati ya sasa ya wananchi wa Libya imesababisha mtetemeko mkubwa katika nguzo za utawala wa kipolisi na kidikteta wa karibu nusu karne wa Kanali Muammar Gaddafi. 
 
Hali ya machafuko imeenea nchini kote na wananchi hawaridhiki na chochote isipokuwa kuondolewa madarakani kwa utawala uliowadunisha na kuwaendesha kipolisi kwa kipindi cha zaidi ya miaka 40.

Jeshi la Libya ambalo ni moja ya nguzo kuu za utawala wa miongo kadhaa wa Gaddafi limegawanyika na inasemekana kuwa baadhi ya kambi za jeshi la nchi hiyo zimejiunga na harakati za mageuzi za wananchi zikilalamikia mauaji na ukandamizaji wa wiki moja sasa unaotekelezwa na vikosi vya usalama. Baadhi ya wanadiplomasia wa Libya katika nchi za kigeni, akiwemo mwakilishi wa nchi hiyo katika Jumuiya ya Nchi za Kiarabu pia wamejiuzulu kulalamikia mauaji yanayotekelezwa na serikali ya Tripoli dhidi ya wananchi wanaoandamana mitaani. 
 
Jambo lisilokuwa na shaka ni kuwa hali ya Libya imeingia katika kipindi nyeti mno na viongozi wa nchi hiyo wanaelewa vyema ukweli huo. Ni kwa sababu hiyo ndiyo maana Kanali Muammar Gaddafi akakusanya majeshi yake katika mji mkuu, Tripoli kutokana na hofu ya dikteta huyo ya kukumbwa na wimbi la hasira za wananchi. Hata hivyo, wimbi la mageuzi sasa limeingia Tripoli na kuenea kwa kasi kama moto unavyochoma nyasi katika majira ya kiangazi.

Historia ya mtoto wa Gaddafi
Saif al-Islam Muammar al-Gaddafi amezaliwa tarehe 25 Juni 1972. Ni mtoto wa pili wa Muammar Gaddafi, kutokana na mke wake wa pili, Safia Farkash.

Elimu na kazi
Mwaka 1994, Saif al-Islam alifuzu shahada ya BSc katika Sayansi ya Uhandisi kutoka Chuo Kikuu cha Al Fateh cha Tripoli, alipata shahada ya Uzamili (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha IMADEC cha Vienna mwaka 2000 na shahada ya Uzamivu (PhD) kutoka Shule ya Uchumi ya London mwaka 2008. Pia ni mtaalam wa majengo (architect) mwenye kumiliki kampuni yake ya uhandisi iliyopo jijini Tripoli inayoitwa “National Engineering Service and Supplies Company”. 
 
Saif pia ndiye Rais wa Chama cha Taifa la Libya cha Udhibiti wa Madawa ya Kulevya (DNAG). Mwaka 1997, alianzisha rasmi taasisi ya hisani, Gaddafi International Foundation for Charity Association, ambayo inahusisha uingiliaji kati mambo ya utekaji yanayohusiana na wanamgambo wa Kiislamu na maambukizi ya VVU nchini Libya.

Saif pia hufanya kazi za kimahusiano ya umma na majukumu ya kidiplomasia kwa niaba ya baba yake. Na amekuwa akitajwa kama mrithi wa urais, ingawa yeye amekanusha hili. Agosti 20, 2008, Saif alisema kwamba hakutaka tena kuhusishwa katika masuala ya serikali ya baba yake. Alibainisha kwamba hapo awali alikuwa “akiingilia kutokana na kukosekana kwa taasisi za kufanya hivyo”, lakini alisema ya kwamba hakuwa tena na sababu ya kufanya hivyo. 
 
Alipuuza maoni kwamba uamuzi huo ulitokana na kutokubaliana na baba yake, akifafanua kwamba yeye na baba yake walikuwa na maelewano mema. Alitoa wito kwa mageuzi ya kisiasa ndani ya mazingira ya mfumo wa Jamahiriya na kukataa wazo la kwamba angeweza kumrithi baba yake, akisema kuwa “Libya si shamba ya kurithi”. 
 
Kulingana na mwandishi Landon Thomas wa New York Times, Saif imeibuka kama rafiki wa nchi za Magharibi katika uso wa Libya na nembo ya matumaini yake kwa ajili ya mageuzi ya kweli na uwazi.

Diplomasia ya kimataifa
Tarehe 10 Desemba, 2004, muda mfupi kabla ya safari na Waziri Mkuu wa Canada, Paul Martin kuelekea Tripoli, Saif aliomba kufanya mahojiano na jalida la The Globe and Mail, kuiomba serikali ya Canada kuomba msamaha rasmi, kwa kujiunga katika kuongeza vikwazo dhidi ya Libya vinavyoongozwa na serikali ya Marekani baada ya mabomu ya Lockerbie, na kwa kummnyima visa ya kwenda kusoma nchini Canada mwaka 1997. 
 
Ombi lake lilionekana la kushangaza sana nchini Canada na serikali ya Canada ilitangaza kwamba hakuna msamaha wowote utakaoombwa. 
 
Saif ilianzisha pendekezo la kudumu la kutatua mgogoro wa Israel-Palestina kwa njia ya kidunia, kishirikisho, ufumbuzi wa Jamhuri ya nchi moja. Maoni ya kwanza kabisa kuhusu tafiti zilizozofanyika kutatua mzozo kati ya nchi mbili za Pakistan na India juu ya udhibiti wa Kashmir, uliofanywa na Chuo cha Mfalme, London, na Shirika la Ipsos-Mori, ilikuwa pia ni wazo la Saif, akiibuka kutoka nje ya majadiliano akiwa na mwanataaluma wa Uingereza, Robert Bradnock, mwandishi wa ripoti ya utafiti ya 2010, Chatham House.

Akihojiwa na gazeti la Kifaransa la 'Le Figaro', Desemba 7, 2007, Saif alisema kuwa Walibya saba waliotiwa hatiani kwa ulipuaji ndege za Pan Am 103 na UTA 772 “hawana hatia”.

Maandamano ya 2011
Tarehe 20 Februari 2011, saa 12:00 jioni kwa saa za Libya, Saif alitoa hotuba ya papo kwa papo kupitia Televisheni ya serikali ya Libya. Katika hotuba hiyo, alielekeza lawama ya kukosekana kwa utulivu nchini Libya kwa makundi ya kikabila na Waislam kutekeleza ajenda zao wenyewe, walevi na wabwia unga. 
 
Aliahidi mageuzi, na kusema mbadala wa haya itakuwa ni vita vya wenyewe kwa wenyewe na kusababisha kutokufanyika biashara, na kwamba hakutakuwa na pesa ya mafuta, na nchi kuchukuliwa na wageni. Alifunga kwa kusema, “Hatutakubali Al Jazeera, Al Arabiya na BBC kutuhadaa.” Wachambuzi wengi wameonesha kuhitalifiana na tathmini yake, ikiwa ni pamoja na Oliver Miles, aliyekuwa Balozi wa Uingereza nchini Libya.

Maisha ya binafsi
Mwaka 2006, Saif al-Islam aliingia katika mahusiano ya kimapenzi na mwigizaji wa Israel, Orly Weinerman. Mwaka 2009, aliandaa sherehe ya miaka 37 ya kuzaliwa kwake mjini Montenegro. Mabilionea Oleg Deripaska, Peter Munk na Prince Albert wa Monaco walihudhuria tukio hilo. 
 
Baadhi ya waalikwa walikwenda huko kwa ndege binafsi na kukaa katika klabu kubwa mbili za ufukweni wakipaki ndege zao jirani ya ufukwe “wa kifahari”, ambapo tukio lilikuwa likifanyika. Kabla ya hapo aliwahi kufanya sherehe ya aina hiyo katika miji ya St. Tropez na Monaco.

Makala hii imeandaliwa na Bishop J. Hiluka, kwa msaada wa Mashirika mbalimbali ya Habari ya Kimataifa.

Kiongozi anapokiuka misingi ya haki za binadamu hukosa uhalali wa kuongoza

 Rais wa Libya, Kanali Muammar al-Gaddafi

 Waandamanaji wanaoupinga utawala wa Libya

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

JUZI Jumatano niliona taarifa kwenye televisheni iliyonishtua sana, kuwa kiongozi wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi, licha ya kugoma kuondoka madarakani kutokana na kuwepo kwa maandamano makubwa ya kupinga serikali, aliliagiza jeshi lake kuwashughulikia wale wote wanaompinga na kutamka kuwa maadui wa Libya watauawa.

Katika hotuba yake kubwa tangu kuanza kwa vuguvugu, Gaddafi alisema dunia nzima inaitazama Libya na kuwa maandamano hayo yana “mhudumia shetani”. Aidha aliwaita waandamanaji kuwa ni mende au panya. Makundi ya haki za binaadamu yanasema zaidi ya watu 300 wameuawa tangu maandamano hayo yaanze.

Ghaddafi akizungumza kwa ghadhabu alisema ameleta heshima kwa Libya jambo ambalo hakuna anayeweza kubisha. Gaddafi amewasaidia sana wananchi wake katika mambo fulanifulani. Amefanikiwa sana kukuza uchumi wa Libya na kuwafanya waishi kama wapo peponi, lakini hiyo haimpi uhalali wa kukiuka misingi ya haki za binadamu na kutaka kutawala milele pamoja na kuanzisha utawala kama wa kisultani.

Kitendo cha kuamuru jeshi kuwashambulia kwa risasi za moto wananchi wanaoandamana kimeyafanya yale yote mazuri aliyoyafanya kufunikwa na mauaji yanayoendelea, hivyo kupoteza kabisa uhalali wa kuongoza.

Azimio la Umoja wa Mataifa kuhusu Haki msingi za Binadamu linatamka bayana na kusisitizia uhuru wa mawazo, hii ni dhamana ya kila Serikali kuhakikisha kwamba, watu wake wanatekelezewa uhuru huo, badala ya kuendekeza dhuluma, ubaguzi na mateso hata kama umesaidia kukua kwa uchumi wa nchi.

Kwa kweli kitendo alichokifanya Gaddafi kinaakisi hali halisi ya kisiasa katika bara la Afrika, karibu nchi zote (ikiwemo Tanzania) bado zina changamoto kubwa kama vile: kudumisha misingi ya haki na amani pamoja na kutetea zawadi ya maisha hasa ya wale ambao ni wanyonge zaidi ndani ya jamii.

Wakenya bado wanakumbuka kwa namna ya pekee, machafuko ya kisiasa yaliyojitokeza kunako mwaka 2007 mara baada ya uchaguzi mkuu. Si rahisi kufuta picha ya mateso na mahangaiko ya wananchi wa Kenya katika kipindi hiki, mateso ambayo hayakuwa na msingi wowote ule!

Uvunjwaji wa haki za binadamu ni tatizo kubwa barani Afrika. Sheria mbaya, mahakama zisizokuwa huru, na vyombo vya dola vinavyofanya kazi kwa kufuata matakwa binafsi ya viongozi wa serikali, badala ya katiba na sheria, vimesababisha haki za binadamu katika nchi zetu kuwa katika hali mbaya.

Jambo lingine ambalo ni kiashiria cha ukiukwaji wa misingi ya haki za binadamu barani Afrika (Tanzania ikiwemo) ni rushwa. Enzi za Awamu ya Kwanza, wakati wa Mwalimu Nyerere tulikuwa tukifundishwa kuwa rushwa ni adui wa haki, kwa kuwa inaua uchumi na kuwanyima wananchi haki ya maisha.

Lakini siku hizi rushwa imekuwa ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku kiasi kwamba unaonekana mtu wa ajabu kama hupokei rushwa. Wapo watu waliomshangaa sana Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipotangaza kuwa siku akichukua rushwa anaomba afe.

Siku hizi, hapa nchini hakuna huduma ya serikali isiyo na rushwa, kuanzia ngazi ya Serikali ya Mtaa hadi Serikali Kuu. Chanzo kikubwa cha rushwa ni ukiritimba wa madaraka, mishahara midogo ya watendaji Serikalini, maamuzi yasiyofuata taratibu zinazoeleweka na kulindana kwa kutowawajibisha wanaoshiriki vitendo vya rushwa.

Kimsingi shughuli zote za mwanadamu na mahusiano ya watu hapa duniani yalipaswa kuwa ni kwa ajili ya kuboresha hali yake kimwili, kiakili, kiroho na kuongeza ubora wa mahusiano yake na viumbe wengine. Hivyo, mchakato wa kila shughuli afanyayo ulipaswa kuwa katika namna ambayo haina dhuluma, uonevu, madhalilisho, taabu, ubaguzi, wala vikwazo kwa mwanadamu awaye yeyote na kwa kiumbe hai kingine chochote.

Kilele cha uwepo wa haki ni kuzalishwa na kutunzwa kwa furaha ya jamii na ya dola. Jamii kamwe haiwezi kuwa na furaha ya kweli kama haki haitawali na wala dola haliwezi kusimama imara pasipo kutunzwa kwa kiwango kikubwa haki ndani ya mipaka ya dola husika.

Jamii zote za wanadamu zina mfumo wa kimsingi wa kijamii, kiuchumi, na taasisi za kisiasa zilizo rasmi na zisizo rasmi. Ili kutambua kama mfumo fulani unaathiri mipangilio ya kijamii na una uhalali, mtu hana budi kutazama kukubalika kwa mfumo huo miongoni mwa watu wanaoongozwa na mfumo husika.

Uhuru wa kisiasa (mfano kuwepo kwa taasisi za demokrasia ya uwakilishi, uhuru wa kujieleza, wa vyombo vya habari na wa kukusanyika) uhuru wa kujumuika na kushirikiana na wanajamii uhuru wa mtu kwenda atakako na kuchagua kazi aitakayo bila kukinzana na misingi ya uadilifu, uhuru wa kupata haki binafsi zinazolindwa na utawala wa sheria.

Alamsiki

Feb 17, 2011

Ben Ali: Nguvu ya umma yamkimbiza nchini Tunisia

 Zine El Abidine Ben Ali
 
 Waandamanaji waliokuwa wakipinga utawala wa Ben Ali
 
Tunis
TUNISIA

SAUDI Arabia imetangaza rasmi kuwa imempokea Rais wa Tunisia aliyepinduliwa, Zine El Abidine Ben Ali na familia yake, baada ya kushinikizwa kuondoka madarakani.

Taarifa ya jumba la kifalme iliyotangazwa na shirika la habari la nchi hiyo SPA imethibitisha kuwa Ben Ali aliwasili nchini humo mapema tarehe 15 Januari, baada ya kuondoka Tunisia tarehe 14 Januari na hivyo kumalizika kwa utawala wake wa miaka 23, kufuatia maandamano makubwa yaliyosababisha umwagaji damu.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa kutokana na wasiwasi wa mazingira ya kipekee yanayowakabili ndugu zao wa Tunisia na katika kuunga mkono usalama na utulivu nchini mwao, serikali ya Saudi Arabia imempokea Rais Ben Ali na familia yake.

Kabla ya kuondoka nchini humo alimkabidhi madaraka ya muda Waziri Mkuu wa Tunisia, Mohammed Ghannouchi.

Akizungumza na wananchi wa Tunisia Ghannouchi alisema ataiongoza kwa muda nchi hiyo hadi hapo uchaguzi wa mapema utakapofanyika na kwamba anachukua madaraka kutokana na rais kutoweza kutekeleza majukumu yake. 
 
Mitaa ya mji mkuu wa Tunis ilikuwa shwari, huku kukiwa na usalama wa hali ya juu, ingawa wachambuzi walihoji iwapo mabadiliko hayo ya uongozi wa juu, yangewaridhisha waandamanaji.

Hata hivyo, Baraza la Katiba la Tunisia limemtangaza spika wa ubunge, Fuad Mbazaa kuwa rais wa mpito wa nchi hiyo hadi uchaguzi utakapofanyika na tayari ameshaapishwa kushika nafasi hiyo ya juu.

Serikali ya Ben Ali ambaye amekuwa madarakani tangu mwaka 1987, ilitangaza hali ya hatari tarehe 14 Januari na ilitoa amri ya kutotoka nje kuanzia usiku hadi alfajiri. Hatua hiyo ilichukuliwa baada ya siku kadhaa za vurugu zilizoanzia miji mingine na kusambaa hadi Tunis na kusababisha watu kuuawa wakati vikosi vya usalama vilipojaribu kuwadhibiti waandamanaji hao wenye hasira.

Kiongozi wa chama cha upinzani nchini Tunisia cha Democratic Progressive, Mohammed Nejib Chebbi, amekielezea kitendo hicho kama mabadiliko ya serikali. Akizungumza na kituo kimoja cha televisheni cha Ufaransa, Bwana Chebbi alisema hiki ni kipindi muhimu kwani kuna mabadiliko ya utawala.

Rais Barack Obama wa Marekani ametoa wito wa kufanyika uchaguzi ulio huru na wa haki nchini Tunisia. Rais Obama pia amepongeza ujasiri na utu wa Watunisia. Alisema analaani matumizi ya nguvu dhidi ya raia ambao wanaelezea maoni yao kwa njia ya amani nchini humo. Aidha, amevisihi vyama vyote kubakia shwari na kuepuka ghasia na ameitaka serikali ya Tunisia kuheshimu haki za binaadamu na kuandaa uchaguzi huru na wa haki hivi karibuni.

Kwa upande wake, Umoja wa Ulaya umetaka kupatikana kwa ufumbuzi wa amani nchini Tunisia wakati ambapo kiongozi wake ameondoka nchini humo. Mkuu wa sera za kigeni wa umoja huo, Catherine Ashton amevitaka vyama vyote kuonesha uvumilivu na kubakia shwari ili kuepusha ghasia na vifo zaidi. Ashton amesema mazungumzo ni muhimu na Umoja wa Ulaya upo tayari kuisaidia Tunisia na umma wake kupata suluhisho la kudumu la demokrasia katika mzozo unaoendelea.

Ghasia hizo zimefuatia machafuko yaliyoanza Desemba 16 eneo la Sidi Bouzid nchini Tunisia na kuutikisa mji mkuu Tunis.

Vikosi vya usalama vilifyatua risasi hewani na kuvurumisha maguruneti ili kuwatawanya waandamanaji waliokuwa wakivunja vunja katika kitongoji cha Ettadamen karibu na mji mkuu, Tunis.

Mamia ya vijana waliwavurumishia mawe polisi kabla ya kuanza kuvunja maduka na kuitia moto benki moja katika eneo hilo. 
 
Ghasia hizo zimetokana na kijana mmoja mwenye umri wa miaka 26, mwenye shahada ya chuo kikuu na ambaye hana kazi, Mohammed Buazizi, ambaye alijichoma moto katika mji wa kati wa Sidi Buzeid akipinga kukamatwa kwa mkokoteni wake wa matunda na mboga.

Jaribio la Buazizi la kujiua lilifuatiliwa na jaribio jingine kama hilo lililofanywa na karibu vijana wawili ambao wamemaliza elimu ya chuo kikuu wakipinga dhidi ya hali mbaya ya kiuchumi katika taifa hilo.

Ndipo raia wa Tunisia hasa vijana wakaanzisha maandamano kulalamika kuhusu ukosefu mkubwa wa ajira, rushwa na jinsi utajiri wa nchi hiyo unavyonufaisha wachache nchini humo. Pia walipinga hali ngumu ya maisha na kuzidi kuwa vuguvugu la umma dhidi ya serikali kupinga ukandamizaji wa kisiasa nchini humo.

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani, Hillary Clinton aliitolea mwito serikali ya Tunisia “isake ufumbuzi wa amani” kwa mgogoro wa kijamii ulioitikisa nchi hiyo. Katika mahojiano na kituo cha televisheni cha Al Arabiya mjini Dubai, Clinton aliitaka serikali ya Tunisia ijitahidi kubuni nafasi za kazi kwa ajili ya vijana.

Waandamanaji walikuwa wanawasiliana kwa simu za mkono na mtandao, lakini hawakuwa na mwongozo maalum wala shirika lolote la kuwaongoza. 
 
Vyombo vya habari vya nchi za magharibi vimeonekana kutoyapa kipaumbele maandamano ya Tunisia. Matukio hayo ya Tunisia ambayo hayakutarajiwa yalipuuziwa kwa kiasi kikubwa na vyombo vya habari vya mataifa ya Magharibi. Waandishi wa blog katika mtandao wa intaneti pamoja na tovuti ya twita ndio waliokuwa vyanzo muhimu kwa ajili ya kupata taarifa za maendeleo ya kila siku za machafuko hayo.

Kama ilivyo kwa machafuko yanayotokea katika nchi kadhaa za Kiarabu zinazoungwa mkono na mataifa ya Magharibi, polisi walijibu ghasia hizo kwa matumizi makubwa ya nguvu. Kuna ripoti za matumizi ya risasi za moto, msako wa nyumba kwa nyumba kuwakamata wanaharakati, watu kadha kutiwa mbaroni pamoja na mateso dhidi ya watu waliokamatwa.

Polisi kimsingi walivunja maandamano katika mji wa Sidi Buzeid baada ya kukata mawasiliano yote pamoja na barabara katika mji huo, lakini walikabiliana na maandamano zaidi katika miji kadhaa ya jirani.

Utawala wa Ben Ali ulishutumu watu wenye msimamo mkali, na wanaochochea ghasia, pamoja na kundi dogo la mamluki, kwamba ndio wanaochochea ghasia hizo, ikiwa ni shutuma maalum ambazo hutolewa na watalawa wa Kiarabu kila kunapokuwa na ishara za hali isiyo ya utulivu miongoni mwa wananchi wao wanaokandamizwa.

Kabla hajakimbia nchi, muungano wa wafanyakazi wa Tunisia ulikuwa umemtaka Bin Ali kufanya uchunguzi juu ya watu waliouawa katika ghasia nchini humo. Muungano huo uliitaka serikali kuwaachia huru watu waliotiwa mbaroni wakati wa maandamano na kueleza kuwa utafanya mgomo mkubwa katika baadhi ya miji ya kusini mwa nchi hiyo katika kujibu kile ulichokitaja kuwa ni ukandamizaji wa polisi. 
 
Ili kujitakasa, Rais Zine el Abidine Ben Ali alimfuta kazi Waziri wa Mambo ya Ndani Rafik Belhaj Kacem na kusema serikali itachunguza hatua ya polisi kutumia nguvu za ziada kukabiliana na waandamanaji. Kacem alifanya idadi ya mawaziri watatu kufutwa kazi kufuatia machafuko ya ndani ya Tunisia kufuatia kulalamikia hali mbaya ya maisha, umaskini na ufisadi ndani ya taasisi za serikali. Wengine ni mawaziri wa biashara na masuala ya dini walitimuliwa kazi. Lakini hiyo haikusaidia kuwafanya wananchi kuacha maandamano na hatimaye kumng'oa Ben Ali madarakani.

Ben Ali ni nani hasa?
Zine El Abidine Ben Ali alizaliwa katika eneo la Hammam-Sousse tarehe 3 Septemba 1936. Alishika madaraka ya urais tangu Novemba 7, 1987. Aliteuliwa kuwa Waziri Mkuu Oktoba 1987, na mwezi Novemba 1987 akawa rais wa nchi kufuatia mapinduzi ya kijeshi yasiyo ya umwagaji damu yaliyomtoa madarakani Rais Habib Bourguiba. Ben Ali amekuwa akichaguliwa kwa kura nyingi katika kila uchaguzi, mara ya mwisho ilikuwa Oktoba 25, 2009.

Elimu na kazi ya kijeshi
Wakati akiwa mwanafunzi katika Shule ya Sekondari ya Sousse, Ben Ali alijiunga na upinzani wa Taifa wakati wa utawala wa kikoloni wa Ufaransa. Kwa sababu hiyo, alifukuzwa shule na kufungwa. Baadaye alimaliza sekondari, na kisha akapata digrii kutoka Special Inter-service School, Saint-Cyr, Ufaransa, Artillery School iliyopo Chalons-sur-Marne, Ufaransa, Senior Intelligence School (Maryland, USA) na Shule ya Anti-Aircraft Field Artiller (Texas, USA). 
 
Alianza kazi ya kijeshi mwaka 1964 kama afisa wa jeshi. Katika kazi yake ya kijeshi, alianzisha Idara ya Usalama ya Kijeshi na kuongoza shughuli zake kwa miaka 10. Pia alitumikia nafasi za kijeshi nchini Morocco na Hispania kabla ya kuteuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa mwaka 1977.
Mwaka 1980 aliteuliwa kuwa Balozi huko Warsaw, Poland, na kutumikia nafasi hiyo kwa miaka minne.

Familia
Ben Ali na familia yake wanajulikana kwa sababu ya uharibifu wao unaosababishwa na rushwa. Hii ndiyo imepelekea kuwepo maandamano. Wengi ya wanafamilia ya Ben Ali wameondoka nchini Tunisia kwa sababu ya usalama binafsi.

Makala hii imeandaliwa na BISHOP J. HILUKA kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari.

SOURCE: KULIKONI

Alassane Ouattara: Mwathirika mwingine wa mfumo mbovu wa tawala za Kiafrika

 Alassane Ouattara

Abidjan
IVORY COAST

WIKI hii hali ya kisiasa nchini Ivory Coast imezidi kuwa tete baada ya wagombea wote wa urais kujitangaza kushinda na kuapishwa kwa nyakati tofauti, hali inayoondoa matumaini ya kurejea kwa amani kwenye taifa hilo.

Rais aliyekuwa anayetetea kiti chake, Laurent Gbagbo alikula kiapo cha kuongoza muhula mpya katika sherehe iliyofanyika Ikulu na kutangazwa moja kwa moja na televisheni, lakini saa kadhaa baadaye mpinzani wake mkuu, Alassane Ouattara akaapishwa na kuhakikishia umma kuwa yeye ndiye rais wa nchi hiyo.

Hali hiyo ikamlazimu Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki kwenda Ivory Coast kujaribu kupatanisha pande hizo mbili ingawa Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Ulaya (EU) pamoja na Marekani wanashikilia msimamo kuwa watamtambua Ouatarra kuwa mshindi halali na si Gbagbo kama alivyojitangaza.

Ouattara ndiye aliyetangazwa mshindi na Tume ya Uchaguzi, lakini matokeo hayo yalibadilishwa na Baraza la Uchaguzi ambalo linaongozwa na mshirika wa rais Gbagbo.

Tume huru ya uchaguzi ya Ivory Coast ilitangaza kuwa Ouattara ameshinda kwa kupata asilimia 54.1 ya kura. Lakini siku iliyofuata kamati ya katiba ya nchi hiyo ilitangaza upya matokeo ya uchaguzi wa rais ikisema Laurent Gbagbo ameshinda kwa asilimia 51.45 ya kura.

Katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika baadaye, mwakilishi wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia mambo ya Ivory Coast, Choi Young-jin alisema kamati ya katiba kutangaza ushindi wa Gbagbo ni hatua isiyolingana na hali halisi, kwa sababu kura za majimbo 7 yaliyoko kaskazini mwa nchi hiyo hazikujumuishwa kwenye matokeo hayo.

Hali inaonesha kuwa huenda machafuko makubwa zaidi yanaweza kutokea endapo juhudi za makusudi hazitachukuliwa kuepusha machafuko hayo hasa kufuatia kitendo cha wagombea hao kila mmoja kuungwa mkono na upande fulani, Gbagbo anaungwa mkono na jeshi la serikali na taasisi nyingi, ikiwemo ya Baraza la Katiba, huku Ouatarra akiungwa mkono na Jeshi Jipya la Uasi na Jumuiya ya Kimataifa.

Kumekuwepo taarifa za watu kadhaa kufa jijini Abidjan katika ghasia zinazotokana na uchaguzi huo. Mitaani, wafuasi wa upinzani wanaendelea kuandamana pamoja na kuchoma matairi ovyo, wakionesha kupinga kitendo cha Gbagbo kujitangaza mshindi, huku wakisema kuwa hayo ni mapinduzi.

Alassane Ouattara Dramane (tamka Alasan Watara), alizaliwa 1 Januari 1942. Alikuwa Waziri Mkuu wa Ivory Coast kuanzia Novemba 1990 hadi Desemba 1993. Ni Rais wa chama cha Rally of the Republican (RDR), chama ambacho kina wafuasi eneo la kaskazini ya nchi.

Mbali ya kuwa mwanasiasa pia ni mtaalamu wa teknokrasia, mchumi na amewahi kufanya kazi Shirika la Fedha Duniani (IMF) na Benki Kuu ya Afrika Magharibi (BCEAO).

Alassane D. Ouattara alikuwa Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Kimataifa la Fedha tarehe 1 Julai, 1994.
Ouattara alihitimu shahada yake ya kwanza ya B.Sc. (Business Administration) huko Drexel Institute of Technology, Philadelphia (1965), na shahada ya pili katika uchumi, MA (Economics) mwaka 1967, pia alipata shahada ya uzamivu katika uchumi, Ph. D. in economics mwaka 1972 aliyoipata kwenye Chuo Kikuu cha Pennsylvania.

Aliteuliwa kuwa Mchumi katika Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kuanzia mwaka 1968 hadi mwishoni mwa 1973, baada ya hapo alitumikia Benki Kuu ya Afrika Magharibi (BCEAO) mjini Paris mwishoni mwa 1973 hadi mwanzoni mwa 1975, alipoteuliwa kuwa Mshauri Maalum wa Gavana na Mkurugenzi wa Utafiti. Alishikilia nafasi hii hadi alipoteuliwa kuwa Makamu wa Gavana wa BCEAO mwaka 1983. Mwishoni mwa mwaka 1984, alirudi tena IMF na kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Afrika, na wakati huohuo kuanzia 1987, alikuwa Mshauri wa Mkurugenzi Mtendaji.

Oktoba 1988, Ouattara aliteuliwa kuwa Gavana wa BCEAO. Alitumikia nafasi hiyo mwaka 1990 pia kama Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Uratibu wa Mpango wa Udhibiti na Ufufuaji Uchumi Ivory Coast, Abidjan.

Ouattara amewahi kutunukiwa nishani kadhaa, ikiwa ni pamoja na: “Commander of the Ordre du Lion, Senegal”, “Commander of the Ordre du Mono, Togo”, “Commander of the National Order of Niger”, “Grand Officier of the National Order of Côte d'Ivoire”, na Gavana wa heshima, BCEAO.

WAZIRI MKUU
Mwezi Aprili mwaka 1990, Rais wa Ivory Coast Felix Houphouet-Boigny alimteua Ouattara kuwa Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Uratibu wa Mpango wa Udhibiti na Ufufuaji Uchumi Ivory Coast, wakati huohuo akiendelea na nafasi yake kama Gavana BCEAO. Baadaye alikuwa Waziri Mkuu wa Ivory Coast Novemba 7, 1990, huku Charles Konan Banny akichukua nafasi ya Gavana wa BCEAO badala yake.

Wakati akiwa Waziri Mkuu, Ouattara pia alibeba majukumu ya urais kwa miezi 18, ikiwa ni pamoja na kipindi cha kuanzia Machi 1993 hadi Desemba 1993, wakati Houphouet-Boigny alipokuwa mgonjwa. Houphouet-Boigny alikufa Desemba 7, 1993, na Ouattara alilitangazia taifa kuhusu kifo chake, akisema kuwa “Ivory Coast imeachwa yatima”. Ndipo ukafuata msuguano mkubwa baina ya Ouattara na Rais wa Bunge, Henri Konan Bedie, kuhusu mrithi wa urais; Bédié alifanikiwa kushika madaraka ya Urais na Ouattara akaamua kujiuzulu nafasi yake ya Waziri Mkuu Desemba 9. Akarudi IMF kama Naibu Mkurugenzi Mtendaji, akishika nafasi hiyo tangu Julai 1, 1994 hadi Julai 31, 1999.

UCHAGUZI WA MWAKA 1995
Kabla ya uchaguzi wa urais wa Oktoba 1995, katika hali iliyoonekana kuwa inachukuliwa kwa nia ya kumzuia Ouattara asigombee urais, Bunge la Taifa la Ivory Coast lilipitisha kanuni ya uchaguzi ambayo ilimzuia mgombea ambaye aidha wazazi wake wana asili ya nje ya Ivory Coast au kama ameishi nje ya Ivory Coast kwa miaka mitano.

Chama cha upinzani cha Rally of the Republican (RDR) kiliundwa kufuatia mgawanyiko ndani ya chama tawala cha Democratic Party of Ivory Coast (PDCI) mwaka 1994, wakitaka Ouattara awe mgombea urais pamoja na kuwepo kanuni hizo za uchaguzi. Mwishoni mwa Juni 1995, Katibu Mkuu wa RDR, Djeni Kobina alikutana na Ouattara, katika wakati ambao, kulingana na Kobina, Ouattara alisema “Niko tayari kujiunga nanyi”. Chama kilimpitisha Ouattara kuwa mgombea wake wa urais Julai 3, 1995 katika mkutano wake wa kwanza wa kawaida. Serikali hata hivyo haikuweza kubadili kanuni za uchaguzi, na Ouattara aliupinga uteuzi. RDR kiliamua kugomea uchaguzi, pamoja na chama cha Ivorian Pupolar Front (FPI) cha Laurent Gbagbo, na kumuacha mgombea wa PDCI, Rais aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo Henri Konan Bedie kushinda ukirahisi.

RAIS WA RDR
Wakati akiwa Naibu Mkurugenzi IMF, Machi 1998 Ouattara alionesha nia yake ya kurudi Ivory Coast kushiriki tena siasa. Baada ya kuondoka IMF Julai 1999, alichaguliwa kuwa Rais wa RDR tarehe 1 Agosti 1999 katika mkutano wa chama hicho, ikiwa ni pamoja na kuchaguliwa kuwa mgombea kwa ajili ya uchaguzi ujao wa rais. Alisema kwamba alikuwa na haki ya kugombea katika uchaguzi, akionesha nyaraka zilizomtambulisha yeye na wazazi wake kuwa walikuwa wazaliwa wa Ivory Coast.

Alituhumiwa kugushi nyaraka hizo, hata hivyo, uchunguzi ulianza. Rais Bedie alimwelezea Ouattara kuwa mtu wa kutoka Burkina Faso na kusema kuwa Houphouet-Boigny "alimhitaji Alassane Ouattara ili kufufua uchumi tu”. Vyeti vya utaifa wa Ouattara vilitolewa mwishoni mwa Septemba 1999, lakini vikabatilishwa na mahakama Oktoba 27. Kibali cha kukamatwa kwa Ouattara kilitolewa Novemba 29, ingawa kwa wakati huo alikuwa nje ya nchi; hata hivyo alisema kuwa angerudi mwisho wa Desemba.

Desemba 24, jeshi likachukua madaraka, na kumfanya Bedie kukimbilia nje. Ouattara alirejea Ivory Coast Desemba 29 baada ya miezi mitatu ya kuishi Ufaransa, akimtumia salamu Bedie kuwa “hayakuwa mapinduzi ya kijeshi”, bali ni “mapinduzi ya wananchi wote wa Ivory Coast”.

Katiba mpya iliidhinishwa kwa kura ya maoni mwezi Julai 2000, ikiweka kipengele chenye utata wa kuzuiliwa kwa mgombea urais labda tu wazazi wake wote wawili wawe na asili ya Ivory Coast, na kumfanya Ouattara kukosa uhalali wa kugombea kwenye uchaguzi wa rais 2000. Hali hii ilipelekea mvita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Ivory Coast, mwaka 2002.

Alipoulizwa kuhusu uraia wa Ouattara, Rais wa Burkina Faso, Kapteni Blaise Compaore alijibu, “Kwetu jambo hili ni rahisi: yeye hatoki Burkina Faso, si kwa kuzaliwa, kwa ndoa, au uraia. Mtu huyu amekuwa Waziri Mkuu wa Ivory Coast.”

Rais Gbagbo alithibitisha tarehe 6 Agosti 2007 kuwa Ouattara anaweza kugombea katika uchaguzi wa rais wa Ivory Coast ujao. Ouattara aliteuliwa na RDR kuwa mgombea urais Februari 1-3, 2008, apia alichaguliwa tena kuwa Rais wa RDR kwa miaka mingine mitano.

UCHAGUZI WA RAIS 2010
Desemba 2, 2010, baada ya mfululizo wa ucheleweshaji wa matokeo, Tume Huru ya Uchaguzi ya Ivory Coast (CEI) ilimtangaza Alassane Ouattara kuwa mshindi wa raundi ya pili ya uchaguzi wa urais nchini humo huku matokeo hayo yakibadilishwa na Baraza la Uchaguzi.

Makala hii imeandaliwa na BISHOP J. HILUKA kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari.

SOURCE: KULIKONI

MORGAN TSVANGIRAI: Mfano wa viongozi waathirika wa mfumo mbovu wa tawala za Kiafrika

 Waziri Mkuu wa Zimbabwe, Morgan Tsvangirai

Harare
ZIMBAMBWE

WIKI iliyopita Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma alikwenda Zimbabwe alikokutana na viongozi wakuu watatu; Rais Robert Mugabe, Waziri Mkuu Morgan Tsvangirai na Naibu Waziri Mkuu Arthur Mutambara, kushinikiza pande hizo kuingia kwenye makubaliano baada ya kutoafikiana kwenye masuala ya msingi.

Mugabe amekuwa anakataa kutekeleza makubaliano ya kisiasa kwa ukamilifu akidai kuwa anataka vikwazo dhidi ya nchi hiyo viondolewe kwanza na hivi karibuni aliibua chuki dhidi ya Tsvangirai baada ya kuwateua kwa siri magavana wa Zanu-PF kinyume na makubaliano ya kisiasa yanayoainisha kuwa pande zote tatu lazima zishirikiane kwenye uteuzi.

Tsvangirai, aliyekuwa mpinzani mkuu wa Mugabe kabla ya kuapishwa kuwa Waziri Mkuu wa Zimbabwe Februari 11, 2009. Hii ni baada ya maisha yaliyojaa vitisho na baadaye majeraha aliyoyapata katika ajali ya gari tarehe 6 Machi 2009 alipokuwa akielekea kijijini kwake Buhera. Mke wake, Susan Tsvangirai, aliuawa katika ajali hiyo baada ya kupata majeraha kichwani.

Tsvangirai aliyekuwa mgombea wa MDC katika uchaguzi wa rais uliozua utata mwaka 2002, na kushindwa na Mugabe. Baadaye aligombea tena mwaka 2008 kama mgombea wa MDC-T na kupata asilimia 47.8 ya kura kulingana na matokeo rasmi, akiwa mbele ya Mugabe, aliyeambulia asilimia 43.2. Tsvangirai alidai kuwa alishinda kwa kura nyingi na kusema kuwa matokeo yalichakachuliwa katika taarifa ya matokeo rasmi.

Baada ya mvutano hatimaye Tsvangirai alikubali kuingia kwenye raundi ya pili ya uchaguzi dhidi ya Mugabe, lakini alijitoa muda mfupi kabla ya uchaguzi kufanyika, akisema kuwa uchaguzi haukuwa huru na wa haki kutokana na vurugu na vitisho toka kwa wafuasi wa serikali dhidi ya wafuasi wake.

MAISHA YA AWALI
Morgan Tsvangirai Richard alizaliwa Machi 10, 1952, eneo la Gutu, Southern Rhodesia (sasa Zimbabwe), akiwa mtoto mkubwa kati ya watoto tisa wa fundi seremala. Baada ya kuondoka shule mwaka 1974, alianza kufanya kazi kwenye migodi ya Trojan Nickel, Mashonaland ya Kati.

Alifanya kazi kwenye migodi kwa miaka kumi, akipanda ngazi kutoka mfanyakazi wa kawaida na kuwa msimamizi. Kijijini kwake kwa sasa ni Buhera, kilomita 220 kusini mashariki ya Harare. Tsvangirai alimuoa Susan mwaka 1978 na walibahatika kupata watoto sita.

Aprili 4, 2009 Tsvangirai alimpoteza mjukuu wake, Sean Tsvangirai, aliyekuwa mtoto wa mwanaye wa pili Garikai, aliyezama katika bwawa. Familia ilichukulia kifo chake kama ajali ya kawaida na kusema hakukuwa na mchezo wowote mchafu.

HARAKATI ZA KISIASA
Wakati wa uhuru mwaka 1980 Morgan Tsvangirai, ambaye alikuwa na miaka 28, alijiunga na chama cha Zanu-PF kilichoongozwa na mtu aliyekuja kuwa mpinzani wake mkubwa kisiasa, Robert Mugabe.

Pia alijulikana kwa majukumu yake katika harakati za vyama vya wafanyakazi Zimbabwe, ambapo alikuwa na nafasi ya mwenyekiti wa tawi la wafanyakazi wa mgodini, na baadaye kuchaguliwa mtendaji mkuu wa wafanyakazi wa migodini ngazi ya Taifa. Mwaka 1989 akawa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini Zimbabwe.

Tsvangirai aliliongoza shirikisho hilo, huku uwezo wake kiutendaji na harakati zake zikikua, na kupelekea uhusiano wake na Serikali kudhoofika. Amewahi kunusurika kuuawa katika majaribio matatu, ikiwa ni pamoja na mwaka 1997 ambapo washambuliaji wasiojulikana walivamia ofisi yake na kujaribu kumtupa nje kupitia dirishani.

UKOSOAJI WA OPERESHENI GUKURAHUNDI
Miaka mitatu baada ya kuingia madarakani, Robert Mugabe aliiamuru Brigedi ya tano, kitengo maalum kilichopata mafunzo ya kijeshi nchini Korea ya Kaskazini, katika mauaji ya Matebeleland kwa kushirikiana na Waziri wa Ulinzi Enos Nkala, wakiongozwa na Perence Shiri kwa sababu ya tuhuma za madai ya kutaka kufanya mapinduzi yaliyopangwa na Joshua Nkomo. Operesheni hiyo iliitwa Gukurahundi.

Tsvangirai amekuwa akizuru mara kwa mara makaburi ya waathirika katika mauaji hayo maeneo ya Tsholotsho, Kezi, Lupane, Nkayi na maeneo mengine ya vijiji vya Matebeleland.

Akiwahutubia wanakijiji wa Maphisa mwaka 2001 alisema:
Hii ilikuwa ni operesheni ya Zanu-PF. Haikupaswa kutokea. Ni jambo la kusikitisha katika historia yetu na MDC itataka kuona haki ikitendeka siku ikiingia madarakani. Ukiukwaji huu wa haki za binadamu lazima uangaliwe kwa mapana na waliohusika wanapaswa kushughulikiwa kwa mauaji hayo.”

TUZO YA SOLIDAR SILVER ROSE
Mwaka 2001 Morgan Tsvangirai alitunukiwa Tuzo ya Solidar Silver Rose. Tuzo hiyo hutolewa kutambua mafanikio bora ya mtu binafsi au shirika katika shughuli za vyama vya kiraia katika kuifanya jamii iwe yenye haki zaidi.

MDC (KABLA YA 2005)
Mwaka 1999 Tsvangirai alianzisha chama cha MDC (Movement for Democratic Change), chama cha upinzani dhidi ya Rais Robert Mugabe na chama tawala cha Zanu-PF. Alisaidia kushindwa kwa kura ya maoni ya katiba Februari 2000, mafanikio ya kampeni yake dhidi ya Katiba ya Taifa.

Tsvangirai alishindwa katika uchaguzi wa rais wa Machi 2002 na Mugabe. Uchaguzi huo ulioambatana na madai kwamba Mugabe aliiba kura kwa njia ya matumizi ya nguvu, upendeleo wa vyombo vya habari, na ghiliba ya wapigakura katika baadhi ya maeneo ambayo Mugabe alikuwa anaungwa mkono.

KUKAMATWA NA VITISHO VYA KISIASA
Tsvangirai alikamatwa baada ya uchaguzi wa 2002 na kushtakiwa kwa uhaini, madai haya baadaye yalifutwa. Mwaka 2004, Tsvangirai aliachiliwa huru kufuatia mashitaka ya uhaini wa njama za kutaka kumuua Mugabe wakati wa mbio za uchaguzi wa rais 2002. George Bizos, mwanasheria wa haki za binadamu wa Afrika Kusini aliyewahi kuwa sehemu ya timu ya kuwatetea Nelson Mandela na Walter Sisulu katika kesi maarufu ya Afrika Kusini mwaka 1964, aliongoza timu ya utetezi wa Morgan Tsvangirai.

Tsvangirai alikamatwa baada ya serikali kudai kuwa alimtishia Rais Robert Mugabe. Wakati kiongozi huyo wa MDC alipowaeleza wafuasi 40,000 katika maandamano mjini Harare kwamba kama Mugabe hataachia ngazi kabla ya uchaguzi uliopangwa kufanyika mwaka 2002 basi wangemuondoa kwa nguvu.

Hata hivyo, Tsvangirai alisema kuwa alikuwa akimuonya Rais Mugabe kwa kuzingatia historia. "Kuna msururu wa madikteta ambao wamekataa kuachia ngazi kwa amani - na watu wameamua kuwaondoa kwa nguvu," alisema. Mahakama iliyafuta mashtaka.

KUKAMATWA, JUNI 2003
Mwezi Juni, 2003 Tsvangirai alikamatwa muda mfupi baada ya kuongea na waandishi wa habari, kwa madai ya kuchochea vurugu. Katika mkutano na waandishi wa habari alisema:
Kutoka Jumatatu Juni 2, hadi leo, Juni 6, Mugabe hakuwa mkuu wa nchi hii. Alikuwa akiandaa majeshi yake ya ukandamizaji dhidi ya uhuru wa watu wa Zimbabwe. Hata hivyo, katika mazingira hayo ya kihayawani, mioyo ya watu haikukata tamaa. Sauti ya milio ya risasi haitonyamazisha madai yao kwa ajili ya mabadiliko na uhuru.”

KUKAMATWA NA KUPIGWA, MACHI 2007
Machi 11, 2007 siku moja baada ya kutimiza miaka 55 ya kuzaliwa kwake, Tsvangirai alikamatwa akiwa njiani kuelekea kwenye maombi Highfield mjini Harare. Mke wake aliruhusiwa kumwona alipokuwa gerezani, na alitoa taarifa kuwa mumewe aliteswa sana na polisi, na kusababishiwa jeraha kubwa kichwani kwake na macho yake kuvimba vibaya.

Aliteswa na kitengo cha Vikosi Maalum vya Zimbabwe vya jeshi, kambi ya Cranborne tarehe 12 Machi 2007 baada ya kukamatwa na kushikiliwa kituo cha polisi Machipisa katika kitongoji cha Highfield Harare.

UVAMIZI MAKAO MAKUU YA MDC
Tsvangirai aliachiwa, lakini tarehe 28 Machi 2007, polisi wa Zimbabwe waliivamia ofisi ya makao makuu ya kitaifa MDC iliyopo Mavuno House 44, na mara nyingine tena walimkamata, saa chache kabla ya kuzungumza na vyombo vya habari kuhusu vurugu za kisiasa zilizokuwa zimetokea nchini humo.

MLINZI WA TSVANGIRAI AUAWA
Tarehe 25 Oktoba 2007 iliripotiwa kwamba Nhamo Musekiwa, aliyekuwa mlinzi wa Morgan Tsvangirai tangu kuundwa kwa MDC mwaka 1999, alikufa kutokana na majeraha ya Machi, 2007, wakati wa ukandamizaji na serikali. Msemaji wa MDC Nelson Chamisa alisema kuwa Musekiwa alikuwa akitapika damu tangu Machi 11, 2007, ilipodaiwa kuwa alipigwa sana, pamoja na viongozi wengine wa upinzani na wanachama (ikiwa ni pamoja na Tsvangirai mwenyewe).

MAJADILIANO YA KIMATAIFA
Agosti 2007, Tsvangirai alikutana na Waziri Mkuu wa Australia, John Howard mjini Melbourne, baada ya mazungumzo yao aliviambia vyombo vya habari kwamba Australia ina nafasi muhimu sana kusaidia mapambano dhidi ya serikali ya Rais Robert Mugabe.

Septemba 2007, Tsvangirai alikutana na Thabo Mbeki, Rais wa zamani wa Afrika kusini kwa ajili ya mazungumzo muhimu, na Mei 2008, Tsvangirai alikutana na Raila Odinga, Waziri Mkuu wa Kenya, aliyetoa wito uchaguzi dhidi ya Mugabe urudiwe.

UCHAGUZI WA 2008
uchaguzi wa rais na wabunge uliofanyika tarehe 29 Machi 2008. wagombea wakuu walikuwa watatu; Mugabe, Tsvangirai na Simba Makoni. Uchaguzi huo uligubikwa na utata, vitisho na wizi wa kura na kupelekea machafuko nchini Zimbabwe.

MAZUNGUMZO YA KISIASA 2008-2009
Tarehe 22 Julai 2008, Tsvangirai na Mutambara walikutana na Mugabe uso kwa uso na kupeana naye mikono kwa mara ya kwanza kwa zaidi ya miaka kumi wakati wa mazungumzo mjini Harare, mazungumzo yaliyoongozwa na Thabo Mbeki, kwa lengo la kutatua migogoro iliyotokana na uchaguzi ili kupelekea ugawanaji wa madaraka kati ya MDC na Zanu-PF katika ngazi ya utendaji.

Makala hii imeandaliwa na BISHOP J. HILUKA kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari.

SOURCE: KULIKONI

TEODORO OBIANG: mungu-mtu wa Guinea ya Ikweta aliyekabidhiwa dhamana kuiongoza Afrika

 Teodoro Obiang Nguema Mbasogo

Addis Ababa
ETHIOPIA

KAMA itaanzishwa tuzo ya bara ambalo marais wake wameshika madaraka kwa muda mrefu kuliko mabara mengine duniani, nadhani bara la Afrika litaweka rekodi ambayo haiwezi kuvunjwa na bara lingine lolote.

Katika Afrika, viongozi wengi wamekuwa na tabia ya kuingia madarakani kwa kuchaguliwa katika uchaguzi wa kidemokrasia kwa mujibu wa katiba, lakini muda wao wa uongozi unapomalizika wanakuwa vinara wa kubadilisha katiba ili waendelee kutawala.

Na kama itatokea kuwa hawakuchanguliwa kwa kura za wananchi katika uchaguzi mkuu, basi watatumia kila aina ya hila, ujeuri na madaraka waliyonayo kulazimisha ushindi kimabavu.

Hayo yametokea katika nchi nyingi za bara hili, mfano mdogo tu ni nchi za Kenya, Uganda na Zimbabwe. Hata yanayotokea katika nchi za Afrika ya Kaskazini; Tunisia, Algeria na Misri ni mfano hai.

Nchi ndogo iliyopo Magharibi ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Guinea ya Ikweta imemtoa kiongozi wa Umoja wa Afrika kutokana na kikao cha viongozi wakuu wa nchi za Afrika kumchagua rais wa nchi hiyo ndogo kuwa mwenyekiti mpya wa Umoja wa Afrika (AU).

Rais Teodoro Obiang Nguema Mbasogo ndiye rais wa Jamhuri ya Guinea ya Ikweta, na Mwenyekiti mpya wa Umoja wa Afrika, huku suala la Ivory Coast likiwa linatazamiwa kupewa kipaumbele cha kwanza na viongozi wa Umoja wa Afrika (AU) waliokuwa wakikutana mwishoni mwa wiki iliyopita na mwanzoni wiki hii mjini Addis Ababa, Ethiopia.

Nchi hii imepakana na Cameroon kwa upande wa Kaskazini, Gabon kwa upande wa Kusini na Mashariki, na Ghuba ya Guinea kwa upande wa Magharibi, ambapo kisiwa cha Sao Tome na Principe vipo Kusini-Magharibi mwa Jamhuri ya Guinea ya Ikweta.

Nchi hii ilikuwa koloni la Hispania ambapo iliitwa Guinea ya Uhispania, na maeneo yake ambayo yanajulikana (kwa bara kama Rio Muni), na pia kisiwa cha Bioko ambapo mji mkuu umo na Malabo (ambayo iliitwa, Santa Isabela).

Jina la nchi hii linatokana na kuwa nchi hii ipo karibu na Ikweta na pia ipo karibu na Guba la Guinea.

Ni nchi pekee katika bara la Afrika ambayo inatumia lugha ya Kispaniola kama lugha rasmi ya Taifa, hasa ukiacha maeneo ya Hispania iliozungukwa na bara, Ceuta na Melilla na nchi-Isiyotambuliwa-kimataifa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kiarabu ya Sahara.

Rais Teodoro Obiang, alianza harakati za kuingia madarakani katika Jamhuri ya Guinea ya Ikweta mwaka 1979 na kufanikiwa. Baada ya katiba kufanyiwa marekebisho mapya aliendelea kuitawala nchi hiyo hadi Desemba 2002, alipochaguliwa tena kuendelea na wadhifa wake kwa kipindi kingine cha miaka saba kwa mujibu wa katiba ya taifa hilo.

Katika uchaguzi wa mwaka 2002, Teodoro Obiang alipata ushindi wa asilimia 97.1 ya kura zote zilizopigwa. Lakini matokeo hayo yalizua machafuko makubwa yakipingwa kuwa hayakuwa halali na mpinzani wake mkubwa, Simon Mann.

Uchaguzi mwingine wa urais katika Guinea ya Ikweta ulifanyika Novemba 29, 2009 ambapo wagombea watano wa urais akiwemo Teodoro Obiang Nguema ambaye pia ni mwenyekiti wa chama tawala cha Demokrasia cha nchi hiyo waligombea nafasi ya urais kwenye uchaguzi huo.

Kwenye kampeni za uchaguzi wa rais zilizoanza tarehe 5 mwezi huo, Rais Nguema alijigamba kuwa angeungwa mkono na idadi kubwa ya watu kuliko ile ya kwenye uchaguzi wa mwaka 2002 ambao alipata asilimia 97.1 ya kura.

Teodoro Obiang ni nani hasa?
Teodoro Obiang Nguema Mbasogo amezaliwa Juni 5, 1942, ndiye rais wa Jamhuri ya Guinea ya Ikweta, ambaye ameshika wadhifa huo tangu mwaka 1979 na sasa amekuwa Mwenyekiti mpya wa Umoja wa Afrika (AU).

Maisha ya awali
Obiang alizaliwa katika ukoo wa Esangui eneo la Ocoacan, alijiunga na jeshi wakati wa kipindi cha ukoloni, na kuhudhuria Mafunzo ya Jeshi Zaragoza, Hispania.

Alipanda hadi kufikia nafasi ya Luteni wakati wa uchaguzi wa Francisco Nguema Macias. Katika kipindi cha Macías, Obiang alishika nafasi mbalimbali za kiuongozi, ikiwa ni pamoja na kuwa mkuu wa mkoa wa Bioko, mkuu wa Gereza la Black Beach, na kiongozi wa Ulinzi wa Taifa.

Urais
Aliingia madarakani baada ya kumpindua Francisco Macias tarehe 3 Agosti 1979 kufuatia mapinduzi ya umwagaji damu. Macías alifunguliwa kesi kuhusiana na harakati zake katika uongozi wake uliopita na kuhukumiwa adhabu ya kifo.

Harakati hizo zilikuwa ni pamoja na mauaji ya kimbari ya Bubi. Aliuawa tarehe 29 Septemba 1979 kwa kupigwa risasi.

Obiang alitangaza kuwa serikali yake mpya itaanza kufanya kazi mpya ya kuijenga nchi kutoka kwa serikali ya kikatili na ya kikandamizaji ya Macias. Obiang alirithi nchi hiyo ikiwa haina hazina na yenye idadi ya watu iliyoshuka hadi kufikia theruthi ya mwaka 1968, na asilimia 50 ya idadi ya wananchi wake wa zamani wapatao milioni 1.2 waliohamishwa kupelekwa aidha Hispania, au nchi jirani ya nchi za Afrika, au kuuawa wakati wa utawala wa kidikteta wa rais aliyemtangulia.

Obiang alishika rasmi madaraka ya urais mwezi Oktoba, 1979.
Katiba mpya ya nchi hiyo ilipitishwa mwaka 1982, wakati huohuo, Obiang akichaguliwa kwa kipindi cha miaka saba ya urais. Alichaguliwa tena kuwa rais mwaka 1989 akiwa mgombea pekee katika nafasi hiyo.

Baada ya vyama vingine vya siasa kuruhusiwa, alichaguliwa tena kuiongoza Jamhuri ya Guinea ya Ikweta mwaka 1996 na 2002 kwa asilimia 98 ya kura katika chaguzi zilizolalamikiwa kukumbumbwa na ulaghai na waangalizi wa kimataifa. Mwaka 2009, alichaguliwa tena kwa asilimia 97 ya kura huku kukiwa na madai ya kuwepo udanganyifu na vitisho.

Serikali ya Obiang ilibaki na sifa ya wazi ya kimabavu hata baada ya vyama vingine vya siasa kuruhusiwa rasmi mwaka 1991. Ingawa utawala wake ulionekana kuzingatia utu kuliko ule wa mjomba wake, lakini wengi wanadhani umekuwa wa kikatili zaidi kadiri miaka inavyozidi.

Waangalizi wengi ndani na nje ya nchi hiyo wanaona kuwa serikali yake ni moja kati ya serikali zinazoongoza kwa rushwa, ukandamizaji na zisizokuwa za kidemokrasia katika dunia ya leo.

Jamhuri ya Guinea ya Ikweta kwa sasa haina tofauti na serikali ya chama kimoja, kinachoongozwa na chama cha Obiang cha Democratic Party of Equatorial Guinea (PDGE).

Mwaka 2008, mwandishi wa habari wa Kimarekani, Peter Maass alimwita Obiang kuwa mtawala dikteta mbaya zaidi, mbaya zaidi kuliko Robert Mugabe wa Zimbwabwe. Katiba ya nchi hiyo inampa madaraka makubwa Obiang, ikiwa ni pamoja na nguvu ya kutawala kwa amri.

Wabunge wote wa bunge la taifa kasoro mmoja tu katika bunge lenye wabunge mia moja ni wa chama cha PDGE cha Obiang au ni wale wanaoambatana nacho. Upinzani umeathiriwa sana na ukosefu wa vyombo huru vya habari kama njia muhimu kwa ajili ya kutoa maoni yao. Vyombo vyote vya habari ama vinamilikiwa na serikali au kudhibitiwa na washirika wa Obiang (Kituo kimoja cha redio binafsi, kwa mfano, kinamilikiwa na mtoto wa Obiang).

Ukiukwaji chini ya utawala wa Obiang ni pamoja na “mauaji haramu yanayofanywa na vikosi vya usalama, utekaji nyara uliosababishwa na serikali, askari wa usalama kuwatesa wafungwa na mahabusu, hali inayohatarisha maisha katika magereza na vizuizini, kutokujali, ukamataji holela, na kuweka watu kizuizini.”

Julai 2003, redio inayoendeshwa na serikali ilimtangaza Obiang kuwa mungu ambaye “ana mawasiliano ya kudumu na Muumba” na “ana uamuzi wa kuua bila mtu yeyote kumzuia na bila kwenda kuzimu.” Yeye binafsi aliwahi kutoa ufafanuzi unaolingana na huo mwaka 1993.

Pamoja na yote hayo, bado anadai kuwa yeye ni mcha Mungu na Mkatoliki aliyewahi kualikwa Vatican na Papa Yohane Paulo II na baadaye tena na Papa Benedict XVI. Mtangulizi wake, Macias pia aliwahi kujitangaza kuwa mungu.

Kama alivyokuwa mtangulizi wake na madikteta wengine wa Afrika kama vile Idi Amin na Mobutu Sese Seko, Obiang amejipa mwenyewe vyeo kadhaa. Pia anajichukulia kama El Jefe (Bwana Mkubwa).

Jarida la Fobes linaloandika habari za matajiri wa dunia hii linadai kuwa Obiang ni mmoja wa Marais tajiri sana, akiwa na mali zenye thamani ya zaidi ya dola milioni 600 za Kimarekani.

Makala hii imeandaliwa na Bishop J. Hiluka kutokana na vyanzo mbalimbali vya habari.

SOURCE: KULIKONI