May 25, 2011

Richmond/Dowans Series: Filamu ndefu isiyoisha hamu

 Mitambo ya Dowans

 Rostam Aziz

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

NAKUMBUKA enzi zile tukiwa bado wadogo kabla ya kuenea hizi televisheni zilizozagaa kila mahali tulipenda sana kwenda kuangalia sinema za Kihindi kwenye majumba ya sinema kwa sababu zilikuwa ni ndefu tofauti na sinema zingine, yaani unaangalia na unapata uhondo mwingi: vionjo vingi, unaburudika zaidi na unaona thamani ya pesa uliyotoa ikilingana na kiburudisho unachopata.

Bado nazikumbuka enzi hizo za kina Amitabh Bachchan, Rishi Kapoor, Vinod Khanna, Danny Denzongpa, Mithun Chakraboti, Govinda, Sunjey Dati, Rajesh Khanna, Ramesh Deo, Sumitra na wengine wengi. Sinema zilizotamba enzi hizo ni kama Namak Halal, Disco Dancer, Andhaa Kanoon, Sholay, Kasam Paida Karne Wale Ki, Nastik na nyinginezo. Kwa kweli kipindi hicho ilikuwa unaangalia sinema mpaka unachoka lakini haiishi hamu.

Uhondo ule wa sinema za Kihindi sasa hivi umehamia kwenye tamthilia zilizojizolea umaarufu mkubwa za 'Prison Break', 'Twenty Four Hours' na 'The Unit' ambazo zimeonekana kutishia uhondo wa picha ndefu za Kihindi.

Hapa Tanzania wasanii mbalimbali wamejitokeza kutengeneza sinema nyingi na kuzilazimisha ziwe ndefu mfano wa zile za Kihindi kwa mfumo wa 'Part 1 na 2', na kuishia kutuondolea uhondo tuliokuwa tukiupata kwenye sinema za Kihindi ambao nikiri kuwa haukuwa na mfano wake. Hizi za kwetu za part 1 na 2 zimeshindwa kabisa kukidhi matarajio ya watazamaji kwa kuwa hadithi na visa vinaboa kabla hata sinema haijafika nusu.

Lakini kuna kundi fulani limeamua kuja na sinema kabambe ambayo ilianzia kwenye igizo dogo lenye maudhui ya vita dhidi ya rushwa na ufisadi la Richmond, igizo linaloonesha jinsi watawala walivyo tayari kuumiza wananchi wao ili kutibu majeraha yao wenyewe au rafiki zao. Muendelezo ya igizo hili hatimaye ulizaa filamu ndefu, lakini tamu.

Sinema hii ndefu ilianza kama mzaha vile: wahusika wakuu wakiwa ni wale wanaojua kufisadi Taifa hili. Jinsi sinema ilivyoanza wengi tulidhani itaishia sehemu moja tu ya Richmond, kumbe jamaa ni wajanja sana kwani walipoona kuwa Watanzania tumepiga kelele nyingi kuhusu Richmond, wakatubadilishia 'Angle' na kutuwekea sehemu ya pili ya filamu; Dowans. Na hapo ndipo picha lilipoanza kunoga zaidi.

Naomba nikiri kuwa mwandishi wa kisa hiki cha kusisimua cha Richmond/Dowans ni mwandishi mahiri sana mwenye kuijua vyema kazi yake. Hubadilisha kisa (plot) cha sinema kila anapoona ipo haja ya kufanya hivyo bila kuharibu maudhui yake, mwanzoni tulipohoji tuliambiwa kuwa mmiliki wa Dowans hajulikani! Wakati huohuo Waziri wa Nishati na Madini akikomalia kuilipa Dowans!

Upepo ulipobadilika ghafla baada ya kelele nyingi zilizopigwa na wananchi, mmiliki wa Dowans akajitokeza na kukataa kupigwa Picha. Ila alitaja kuwa alitoa mamlaka kwa Mbunge wetu (ingawa Mbunge huyo aliwahi kuikana) kuisimamia Kampuni ya Dowans hapa Tanzania!

Watazamaji wa sinema hii walitaka kuamini lakini wakaishtukia sehemu hii, mwandishi akaona tena tunaipigia sana kelele Dowans kuwa inaibia Watanzania kwa kutaka ilipwe tozo kufuatia hukumu ya ICC. Akajaribu tena kubadilisha 'angle' na kutangaza kuwa serikali ikinunua mitambo ya Dowans watafuta kesi. Watanzania wakagoma tena safari hii kwa kelele kubwa sana. Sasa ameleta kitu kipya zaidi kinachoitwa Symbion Power!

Hapa ndipo sinema hii inaponoga zaidi, kwani alichokifanya mwandishi wa kisa hiki ni kuuhadaa umma wa Watanzania na mgawo wa umeme ili tuingie mkenge wa nguvu, na tuikukubali Symbion Power ambayo ni Mrithi wa Dowans.

Hii yote ni kuwafanya Watanzania majuha wasiojua kitu au kusoma alama za nyakati. Mimi binafsi hainiingii akilini kuwa Symbion Power na watuhumiwa wa Richmond/Dowans ni vitu viwili tofauti, nahisi kuwa ni walewale ila wamebuni mkakati huu wa kuibua kampuni hii ili kufuta madoa ya Richmond/Dowans usoni kwao. Na tusije kushangaa kuona Tanesco inaingia mkataba na kampuni hiyo ili ituuzie umeme.

'Angle' ya mwandishi katika kisa hiki imebadilika sana baada ya kuona kwamba jina la Dowans halitakiwi kabisa na Watanzania ametuletea jina jipya, na kama tuliukataa umeme wa Dowans basi tutasahau itakapoanza Symbion Power. Na wote tutapongeza maana tutaiona kama mkombozi kwa kuwa tayari tumeghiribiwa kwanza kwa kuletewa mgawo wa umeme mkali ili ionekane kuna shida.

Kampuni ya Symbion Power ni ya Kimarekani yenye makao yake makuu Washington DC, ambayo imethibitisha kwamba imekwishaweka sahihi mkataba wa ununuzi wa mitambo hiyo iliyopo Ubungo Dar es Salaam. Kuthibitishwa huko kulisemwa na Meneja Mtendaji wa Symbion, Paul Hinks, kwa wanahabari katika hoteli ya Kilimanjaro Kempinsky.

Hata hivyo kuna taarifa kuwa mwandishi wa habari, Timoth Kahoho amewasilisha ombi chini ya hati ya dharura kuomba Wakurugenzi wa Kampuni za kufua umeme za Dowans Holdings SA na Dowans Tanzania Limited, wakamatwe kwa kudharau amri ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, baada ya kuchapishwa kwa habari kuwa mitambo ya Dowans imeuzwa kwa Kampuni ya Symbion Power ya Marekani kwa thamani ya Dola za Marekani milioni 120.

Kwangu mimi sinema hii ndefu ya Richmond/Dowans ina mafundisho mazuri sana kwa jamii; mojawapo ni kuwa nchi yetu haipaswi kabisa kuwa na umeme ulio imara kwa kuwa watu watakosa ulaji. Mgawo wa umeme ni lazima uwepo hata kama tulikwishaambiwa kuwa utabaki kuwa historia.

Bila mgawo wa umeme zile kampuni zao za kuuza majenereta zitakufa. Hivyo kwao mgao wa umeme ni dili zuri, zuri mno. Dili litakalowahakikishia ulaji milele na kuendelea kujenga heshima ya kuwa na vitambi vya kuvimbiwa ufisadi.

Wasiwasi wangu tu ni kuhusu mwisho wa sinema hii ndefu isiyochosha, kwani watawala wakizidisha ulafi, wa kunywa mchuzi wote, wananchi wanaweza kuingilia kati na kuamua kumwaga ugali, kama watawala wakimwaga mboga. Yatakayotokea baada ya hapo ni dhambi kuyaeleza.

Naomba tusifikie huko.

SAMUEL WANJIRU: Nyota ya riadha Afrika Mashariki iliyozimika ghafla

 Samuel Wanjiru

NAIROBI
Kenya

ILIKUWA alfajiri ya kuamkia Jumapili, Mei 15, 2011 ambapo Taifa la Kenya na Afrika Mashariki kwa ujumla, hasa wapenzi wa mchezo wa riadha, walipopata pigo kubwa baada ya kumpoteza mwanariadha mahiri aliyekuwa mshindi wa mashindano ya mbio ndefu za Olimpiki ya mwaka 2008 yaliyofanyika nchini China, Samuel Wanjiru “Sammy”.

Kifo cha kijana huyo kimeacha pigo kubwa katika medani ya michezo, kutokana na Wanjiru kufariki dunia akiwa na umri mdogo, ambao bado alikuwa anategemewa kwa maendeleo na ustawi wa taifa lake. Wanjiru amefariki akiwa na umri wa miaka 24, ambapo kifo chake hadi sasa duru za kipolisi nchini Kenya zipo katika uchunguzi wa kina.

Mashabiki wa riadha duniani kote wanaendelea kutuma salamu za rambirambi kwa familia ya mwanariadha huyo. Wanjiru amewahi kuweka rekodi ya dunia katika mbio ndefu (Marathon) kule nchini China katika mashindano ya mwaka 2008, amefariki dunia baada ya kuanguka kutoka katika ghorofa ya kwanza ya nyumba yake iliyoko katika mji wa Nyahururu.

Polisi katika eneo hilo wamesema kuwa kifo cha mwanariadha huyo kimetokea baada ya kuanguka kutoka ghorofa ya kwanza ya nyumba yake na bado uchunguzi unaendelea kubaini Tukio hilo ni la kukusudia ama ajali.

Samuel wakati wa uhai wake alijikuta matatani mara kwa mara baada ya kutiwa nguvuni na polisi kwa tuhuma za kutishia kumuua mke wake, Triza Njeri, baada ya kutokea mtafaruku baina yao, lakini pia alipatikana na makosa ya kumiliki silaha kinyume cha sheria.

Waziri mkuu wa Kenya, Raila Odinga amezunguzia kifo cha mwanariadha huyo kuwa ni pigo kubwa kwa matazamio ya Kenya ya kushinda medali ya dhahabu kwenye michezo ya Olimpiki ya mwaka ujao mjini London, pia sio tu kimeacha pengo kwa familia na marafiki zake bali pia kwa taifa na wapenda michezo duniani kote.

Wanariadha mashuhuri duniani pamoja na wapenzi wa riadha wamekuwa wakielezea masikitiko yao kufuatia kifo hicho cha ghafla cha bingwa wa Olimpiki wa mbio za Marathon.

Habari zaidi za siku ya tukio zilibainisha kuwa mwanariadha huyo alirudi nyumbani usiku akiandamana na mwanamke mwingine, na baadaye mke wake, Triza Njeri alikuja akawakuta chumbani, na kwa hasira akafunga mlango wa chumba hicho huku akimwambia mumewe anakwenda kuwaarifu polisi.

Haijabainika ikiwa Wanjiru aliruka nje kujiua, au kumfuata mkewe, au kwenda kufungua mlango wa chumbani. Polisi waliwahoji wanawake hao wawili kubaini kilichotokea.

Mwezi Desemba Wanjiru alishtakiwa kwa kutishia kumuua mkewe, kumiliki bunduki kinyume cha sheria na pia kumjeruhi mlinzi wa nyumbani. Baada ya mkewe kutupilia mbali kesi inayomhusu walirudiana, na Wanjiru alitazamiwa kufika mahakamani kuhusiana na shitaka la kumiliki silaha kinyume cha sheria.

Ilitazamiwa na wengi kwamba mwanariadha huyo angeweza kuvunja rekodi ya dunia ya mbio za Marathon ambayo kwa sasa inashikiliwa na Haile Gebreselassie wa Ethiopia. Haile ameelezea masikitiko yake kufuatia kifo hicho.
Najiuliza ikiwa sisi kama jamii ya wanariadha tungeweza kusaidia kuepusha tukio hilo,” alisema Haile kwenye mtandao wa Twitter.

Katibu mkuu wa chama cha riadha nchini Kenya, David Okeyo, amesema kifo cha Wanjiru ni pigo kubwa kwa Kenya.
Alikuwa mwenye furaha na tulitazamia angevunja rekodi ya dunia ya mbio za marathon hivi karibuni,” alisema Okeyo.

Bingwa wa zamani wa dunia, Paul Tergat pia kutoka Kenya amesema nchi hiyo imepoteza mwanariadha chipukizi mwenye kipaji.
Ni habari za kusikitisha sana, na ni pigo. Alikuwa mwenye umri mdogo na alikuwa na nafasi ya kukimbia kwa miaka mingi,” alisema Tergat.

Pia kuna habari kuwa Mahakama nchini Kenya imezuia mazishi ya mwanariadha huyo ili kupisha uchunguzi wa kina wa kujua sababu ya kifo chake, huku kamera za CCTV zikishindwa kutoa ushahidi wa moja kwa moja.

Hakimu Anyara Emukule alikubali kutoa siku 14 za uchunguzi, baada ya mama mzazi wa Sammy, Hanna Wanjiru kuiomba mahakama hiyo kumzuia mkwe wake, Teresia Njeri, asiendelee na mazishi ya mumewe. Mama Hanna Wanjiru amekuwa akisisitiza kuwa mwanawe aliuawa na kudai kuwa kulikuwa na damu kwenye chumba alichokuwa anakaa.

Mwili wa marehemu huyo utaendelea kubaki kwenye nyumba ya Lee ya kuifadhia maiti hadi hapo mahakama ya Nakuru itakaposikiliza ushahidi wa pande zote mbili. Mama huyo amemshutumu mkwewe Njeri kwa kuandaa shughuli za mazishi bila kumshirikisha. Pia, hataki kumtambua Njeri kama mke wa mwanae, japokuwa watu wote pamoja na polisi wanamtambua mke huyo.

Historia yake
Samuel Kamau Wanjiru alizaliwa Novemba 10, 1986 katika mji wa Nyahururu. Alikuwa mwanariadha wa Kenya ambaye mbio zake maalum ni mbio za masafa marefu. Amekuwa mwanariadha maarufu katika umri mdogo na kuvunja rekodi ya dunia ya nusu marathon alipokuwa na umri wa miaka 18. Mwaka 2007, alivunja rekodi ya kukimbia ya kilomita 20 na kuboresha rekodi ya nusu marathon kwa zaidi ya sekunde ishirini.

Alihamia hadi marathon kamili na alishinda katika Michezo ya Olimpiki ya Beijing ya mwaka 2008 kwa muda ambao ulikuwa ni rekodi ya Olimpiki wa saa 2:06:32 na kuwa Mkenya wa kwanza kushinda medali ya dhahabu ya Olimpiki katika marathon. Mwaka uliofuata, alishinda marathon zote mbili za London Marathon na Chicago Marathon, kwa kukimbia marathon ya kasi zaidi milele kurekodiwa katika nchi za Uingereza na Marekani.

Wanjiru alianza mbio akiwa na umri wa miaka 15. Mwaka wa 2002, alihamia Japan na akajiunga na shule ya sekondari ya Sendai Ikuei Gakuen katika sehemu ya Sendai, ambapo alihitimu mwaka 2005. Kisha alijiunga na timu ya raidha ya Toyota Kyushu iliyokuwa inafunzwa na mshindi wa medali ya fedha katika mbio za marathon katika Olimpiki ya mwaka 1992, Koichi Morishita.

Muda bora wa Wanjiru katika mbio za mita 5,000 ni dakika 13:12.40, muda aliyouweka akiwa na umri wa miaka 17 mnamo Aprili 2004 mjini Hiroshima, Japan. Akiwa na umri wa miaka 18 tu, Wanjiru alivunja rekodi ya dunia ya nusu marathon, hii ikiwa Septemba 11, 2005 katika Nusu marathon ya Rotterdam kwa muda wa dakika 59:16 na akaivunja rasmi rekodi ya Paul Tergat nusu-marathon ya dakika 59:17.

Hii ilitangulia mapema wiki mbili kwa kuboresha rekodi ya vijana ya dunia ya mita 10,000 kwa karibu sekunde 23 katika michezo ya IAAF Golden League Van Damme Memorial Race mnamo Agosti 26. Rekodi yake ya dunia ya vijana ya dakika 26:41.75 ilikuwa nzuri sana kumpa nafasi ya tatu katika mbio hizo nyuma ya rekodi ya dunia ya Kenenisa Bekele ya dakika 26:17.53 na ya Boniface Kiprop ya dakika 26:39.77.

Ilikuwa ni Kiprop ambaye alikuwa anashikilia rekodi ya dunia ya vijana (dakika 27:04.00) ambayo iliwekwa katika michuano hiyo mwaka uliokuwa umepita kabla yake.

2007-2008
Kwa mara nyingine Wanjiru alichukua tena rekodi ya dunia ya nusu marathon, ambayo Haile Gebreselassie alikuwa amevunja mapema mwaka 2006, kwa dakika 58:53 mnamo 9 Februari 2007 katika nusu marathon ya Ras Al Khaimah na kuiboresha kwa muda wa dakika 58:33 mnamo 17 Machi, 2007 katika City-Pier-City Loop katika mji mkuu wa Hague nchini Uholanzi.

Huku akiiboresha rekodi yake binafsi pia alivunja rekodi ya dunia ya Haile Gebrselassie katika mbio za kilomita 20 kwa muda wa dakika 55:31, uboresho wa sekunde 17.

Wanjiru alikimbia marathon yake kamili ya kwanza katika marathon ya Fukuoka mnamo Desemba 2, 2007 na kuishinda mbio hiyo kwa njia ya kusisimua kwa rekodi ya kozi ya saa 2:06:39. Katika marathon ya London ya mwaka 2008, alimaliza katika nafasi ya pili na kuivunja 2:06 kwa mara ya kwanza. Katika Olimpiki ya mwaka 2008, Wanjiru alishinda medali ya dhahabu katika marathon katika muda wa rekodi ya Olimpiki ya saa 2:06:32 na kuvunja rekodi ya awali ya saa 2:09:2 iliyowekwa na Carlos Lopes wa Ureno katika Olimpiki mwaka 1984.

2009
Wanjiru alikuliwa akisema, “katika muda wa miaka mitano inayokuja najihisi nina uwezo wa kukimbia mbio za marathon kwa muda chini ya saa 2”. Aprili 2009, Wanjiru alishinda marathon ya London kwa muda wa saa 2:05:10.

Alifurahishwa sana na fanikio lake na kusema kuwa alitumai kuvunja rekodi ya dunia ya Haile Gebrselassie baadaye. Katika Nusu Marathon ya Rotterdam, Wanjiru alikimbia kwa muda wa saa 1:01:08 mnamo 13 Septemba, mbio ambayo ilishawahi kushindwa na Sammy Kitwara kwa muda wa dakika 58:58.

Oktoba 2009, Wanjiru alishinda Marathon ya Chicago kwa muda wa saa 2:05:41 na kuweka rekodi mpya ya kozi katika mji huo mkuu na muda wa kasi zaidi katika marathon kukimbiwa nchini Marekani. Ushindi wake katika miji mikuu ya London na Chicago ulimsaidia kufikia nafasi ya juu ya orodha kuu ya dunia katika Marathon mwaka 2009 na kumtuza jackpot ya dola 500,000 za Marekani.

Mdogo wake Wanjiru, Simoni Njoroge ni mkimbiaji wa masafa marefu, na binamu wake, Joseph Riri ni mwanariadha wa daraja ya dunia katika mbio za marathon.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari


May 18, 2011

Mauaji ya Nyamongo na serikali inayodai kufuata utawala bora





 Picha mbalimbali zinazoonesha eneo la mgodi wa Nyamongo kulikofanyika mauaji


BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

WIKI hii vyombo vya habari vilitawaliwa na habari ya mauaji ya watu sita na wengine kadhaa kujeruhiwa katika mgodi wa dhahabu wa kampuni ya African Barrick Gold (ABG), wanaodaiwa kuvamia mgodi huo, yaliyofanywa na Jeshi la Polisi wilayani Tarime.

Mauaji haya yanazidi kujitokeza wakati Serikali ya Awamu ya Nne ikiwa imejivika joho la utawala bora na kudai kuwa imebobea na kuitekeleza dhana ya utawala bora kwa vitendo.

Wakati makala haya yakiandikwa kulikuwa na taarifa za kutatanisha kuhusu idadi kamili ya watu waliofariki wakati polisi waliokuwa doria katika eneo hilo walipowarushia risasi za moto watu waliokuwa karibu na eneo la hifadhi ya mgodi huo kwa lengo la kuokota mchanga wa dhahabu.

Taarifa za vyombo vya habari zilimkariri Mwenyekiti wa kijiji cha Kewanja kilichopo kwenye mji mdogo wa Nyamongo, kuwa watu watano waliuawa katika vurumai hiyo iliyotokea Jumatatu saa 11 alfajiri.

Hata hivyo taarifa hizo zilitofautiana na zile za Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Tarime/Rorya ambapo lilithibitisha vifo vya watu watatu kutokana na risasi za moto, wanaodaiwa kuwa miongoni mwa kundi la wananchi waliotaka kuvamia mgodi huo. Kulikuwa pia na taarifa kuwa waliokufa ni sita.

Nilidokezwa kuwa eneo la kijiografia la mgodi huo ndilo linaloshawishi wananchi kuingia mgodini kwani halijulishi yepi ni makazi ya watu na lipi eneo la mgodi. Ndiyo maana nikawa najiuliza kwamba, hata kama wananchi walivunja sheria na kuingia eneo la mgodi polisi hawakuwa na ruhusa ya kuwaua, kwanza wananchi wenyewe hawakuwa na silaha walitakiwa kutumia mbinu nyingine kuwatawanya, kuua si suluhisho.

Ikumbukwe kuwa nchi yetu imetia saini mkataba wa kimataifa wa haki za binadamu na haikubaliki kumwadhibu mtu anayedaiwa kuvamia mgodi kwa kumuua, badala yake anapaswa kufikishwa katika vyombo vya sheria.

Hali hii ya mauaji ya raia kwenye maeneo ya migodi inatuashiria hatari ya upanuzi wa matabaka na iko wazi kwa kila mtu. Hatujui, kwa mfano, hata suala la wachimbaji wadogo wa madini waliowahi kupigwa risasi katika mgodi wa Mererani, kama wale wachimbaji wakubwa waliowapiga risasi walifikishwa mbele ya vyombo vya sheria.

Wachimbaji hawa wakubwa walistahili kufikishwa mahakamani kujibu suala hili kama ilivyo kwa polisi hawa walioua raia juzi kule Nyamongo wanavyopaswa kuchukuliwa hatua, kwa sababu jambo hili lina dalili zote za uenezi, unyanyasaji kwa watu wasio na uwezo, uhalifu na mauaji.

Hoja ya kwamba polisi walizidiwa kutokana na wananchi waliovamia mgodi kuwa zaidi ya mia nane bado ni hoja dhaifu katika kuhalalisha mauaji kwani wananchi hawakuwa na silaha. Ikiwa raia hawatalindwa na kutetewa na Taifa lao au hawataandaliwa mazingira mazuri ya kutafuta riziki yao kwa njia za halali katika nchi yao, sasa waende wapi?

Kwa kweli katika mauaji haya waliosababisha wana wajibu wa kuwajibika. Uwajibikaji ndiyo kiini na msingi wa utawala bora kwa serikali yoyote. Uwajibikaji hauwezi kusimamiwa kikamilifu na kudaiwa pasipokuwa na uwazi na utawala wa sheria.

Pamoja na kwamba viongozi wetu wamekuwa wakizungumzia sana suala la utawala bora, na hata kuona kuwa ni silaha ya pekee ya kuzuia migogoro ndani ya Taifa, lakini bado pengine uwajibikaji hujapewa uzito unaostahili. Ndiyo maana tunashuhudia mauaji yanayofanywa na Jeshi la Polisi na wahusika hawachukuliwi hatua kwa kisingizio cha habari za kiintelijensia.

Si kwa sababu viongozi hawajali sehemu hii ya utawala bora, bali pengine, hawatambui kwamba kutokuwajibika ndiyo chimbuko hasa la matatizo ya kiuchumi yanayotoa nafasi kubwa sana ya kuendeleza umaskini uliokithiri katika Taifa letu.

Utawala bora una maana ya utendaji wa wazi na unaowajibika juu ya rasilimali yote kwa usawa na juu ya jamii ya watu wake. Rasilimali ya nchi ni pamoja na rasilimali watu (elimu, ujuzi na ufundi), maliasili na uwezo wa ndani na nje wa kiuchumi na kifedha na hii ni pamoja na misaada ya maendeleo kutoka nje.

Kumekuwepo malalamiko ya muda mrefu kuwa wawekezaji huwanyanyasa raia katika eneo la mgodi huo kwa kuwatumia polisi, kuwalaumu tu wananchi bila kutoa elimu ya uraia ili wawe na wigo mpana wa kujua mipaka yao sanjari na wanachopaswa kukifanya pasi na kuvunja sheria za nchi bado hatuwasaidii.

Pale ambapo sheria inapiga marufuku jambo fulani lisitendeke, ni wajibu wa serikali kuwahamasisha raia wake wasitende jambo hilo sanjari na kuweka mfumo wa watendaji wenye taaluma na weredi wa kutosha ili kuwawajibisha wakiukaji wa sheria hizo.

Serikali haina budi kuwa makini kuyaangalia matatizo na changamoto zinazoendelea kujitokeza nchini hasa baina ya wananchi na wawekezaji kwa kukazia zaidi upatanisho, haki na amani sanjari na mikakati ya maendeleo endelevu ili kuepusha damu zaidi kumwagika.

Kwa mtazamo wangu nadhani kuna mambo makuu matatu ambayo serikali inapaswa kuyafanyia kazi kwa ajili ya ustawi wa watu wake ili kusiwepo machafuko zaidi: Utawala bora, wanawake na ujenzi wa amani. Hakuna maendeleo, ikiwa kama misingi ya haki, amani na upatanisho imebomolewa.

Utawala Bora unahitaji ushirikiano wa dhati katika ngazi mbalimbali za maisha. Bajeti za Serikali zilenge zaidi katika mafao ya wengi pamoja na kuwa na matumizi bora ya misaada inayopatikana kutoka nje ya nchi.

Wanawake: wanapaswa kushirikishwa katika mchakato wa utoaji wa maamuzi katika hatua mbalimbali za maisha ya kijamii, kwani hawa ndio wadau wakuu katika jitihada za ujenzi wa upatanisho, haki na amani.

Wajenzi wa amani: Viongozi wa madhehebu ya dini wanapaswa kuwa ni wadau wakuu katika harakati za ujenzi wa misingi ya haki na amani katika maeneo yake, kwa kukazia majadiliano ya kina, mawasiliano ndani na nje ya miundo ya madhehebu. Haki na amani ni masuala yanayopaswa kupewa msukumo wa pekee katika ajenda za maisha.

Mungu ibariki Tanzania

…Watuhumiwa kuandaa mwenyekiti wao UVCCM

 Kaimu Mwenyekiti wa UVCCM Taifa, 
Benno Malisa

Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa UVCCM mkoa wa Dar es Salaam, Augustino Oscar Matefu
Sadifa Juma Khamis

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

KUTOKANA na kile kinachotafsiriwa kuwa ni juhudi za kuutaka urais wa nchi hii mwaka 2015 kwa gharama yoyote, watuhumiwa wa ufisadi, licha ya kutakiwa ‘kujivua gamba’ wanadaiwa kuanza mikakati ya kuhakikisha kuwa mtu wao waliyempandikiza anakuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa CCM Taifa (UVCCM).

Tuhuma hizi zimetolewa na Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa UVCCM mkoa wa Dar es Salaam, Augustino Oscar Matefu, wakati alipoongea kwenye ofisi za gazeti la KuliKoni wiki hii.

Matefu alidai anao ushahidi kuwa mtu aliyepandikizwa na mafisadi ili kujaza nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Mwenyekiti UVCCM, Hamad Yusuf Masauni baada ya kujiuzulu wadhifa huo ni Mbunge wa Jimbo la Donge, Kaskazini Unguja, Sadifa Juma Khamis.

Hata hivyo, mbunge huyo alipoongea na KuliKoni kwa njia ya simu, kwanza alicheka sana kusikia tuhuma hizo kisha akasema hazina ukweli wowote na ndio kwanza anazisikia.

Kama utasoma gazeti la Uhuru, kadri nilivyojieleza, utagundua kwamba mimi nimeamua kugombea ili kuitoa jumuiya yetu katika makundi kama hayo. Ninataka tuwe na umoja wa vijana wa kujitegemea na si wa kutegemea wafadhili fulani,” alisema Sadifa.

Mbunge huyo alizidi kusema: “Kwanza mimi ni mbunge wa juzijuzi tu na umri wangu ni miaka 29, hiyo tu haikufanyi uone kwamba sijawa kwenye siasa kwa kipindi cha muda mrefu kiasi cha kuwa rafiki wa hao mnaowaita mafisadi kwa sababu wao nina hakika ni watu wazima sana.”

Sadifa alisema anaamini Matefu anataka kutumia jina lake kujitafutia umaarufu kwa sababu anachoongea si kweli. “Tafadhali mwambie huyo kijana asitumie jina langu kujitafutia umaarufu kwa kuninasibisha na kundi lolote. Mimi ni mtu huru, mwenye mawazo ya kujitegemea na kamwe sigombei nafasi kwa maslahi ya watu fulani bali kusaidia jamii yangu.”

Mbali na Sadifa, wengine waliochukua fomu ya kuwania uenyekiti wa UVCCM ni Hamidu Bilal Gharib ambaye ni mtoto wa kaka yake Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal, Thabiti Jecha Kombo, Bakar Bakar, Omar Mwadi Mwarabu, Asha Suleiman Shibu, Shinuna Kombo Juma, Mwanawewe Usi Yahya, Laila Burhan Ngozi na Innocent Melleck Shirima.

Kwa mujibu wa Matefu, vijana wa CCM mkoa wa Dar es Salaam wanasikitishwa sana na kitendo cha mafisadi kutumia pesa za wananchi ili kudhoofisha harakati za chama kujivua gamba na wanaipa serikali siku ishirini na moja kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wote wa ufisadi ambao amedai wanafahamika, na kuuvunja uongozi wa UVCCM Taifa.

Jumuiya ya Vijana wa CCM hivi sasa haifanyi kile inachotakiwa kufanya kwa maslahi ya wananchi badala yake watuhumiwa wa ufisadi wanaitumia Jumuia yetu ili kukidhi mahitaji yao binafsi na siyo kwa maslahi ya chama, Jumuia yenyewe ama Watanzania kwa ujumla,” anasema Matefu.

Bado nasisitiza kuwa idadi kubwa ya viongozi wa jumuiya yetu ni mapandikizi ya mafisadi wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti, Beno Malisa na Mjumbe wa Baraza kuu la jumuiya hiyo, Hussein Bashe. Na huyu Bashe siku za karibuni aliongea na waandishi wa habari kuzijibu tuhuma nilizotoa kwa niaba ya watuhumiwa wa ufisadi.”

Hata hivyo Malisa na Bashe walishakanusha tuhuma hizo zinazotolewa na Matefu.

Matefu pia amewatupia lawama Waziri Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond, Edward Lowassa ambaye ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Udhamini la Jumuiya hiyo na mkongwe mmoja wa siasa (jina tunalo) kuwa wameumega umoja wao kwa lengo la kuweka mikakati ya kuhakikisha kampeni ya Rais Kikwete ya kujivua gamba inashindikana.

Matefu amewataka wakongwe hao wa siasa waondolewe kwenye nyadhifa hizo ili wasivuruge maamuzi sahihi ya chama.

Pia huyu Rostam Aziz ndiye kinara na amekuwa akitoa pesa nyingi kwa ajili ya kuwanunua watu mbalimbali wakiwemo wanasiasa wa upinzani kwa lengo la kuhakikisha watuhumiwa akiwemo yeye mwenyewe wanasafishwa. Inasikitisha kuona akitumia rasilimali za nchi ku-invest kwenye makampuni yake na kuwanyonya wananchi kwa maslahi ya kundi dogo,” alidai Matefu.

Alipoulizwa na gazeti hili kuhusu wanasiasa wa upinzani wanaotumiwa na mafisadi, Matefu alisema kwa kujiamini kuwa wana ushahidi kwamba Rostam Aziz amekuwa na mawasiliano na Mwenyekiti wa chama kimoja cha upinzani na kwamba amekuwa akitoa pesa nyingi sana kuhakikisha chama hicho wanawasafisha mafisadi na kushusha lawama kwa Chama Cha Mapinduzi na viongozi wapambanaji wa ufisadi nchini ili kupotosha ukweli.

Kuna kijana mmoja anaitwa Deo alikuwa msaidizi wa mwenyekiti huyo, huyu aliona nyaraka za kifedha zilizotumwa kutoka kwa Rostam Aziz kwenda kwa mwenyekiti huyo, baada ya kujulikana ilibidi akimbie kabla hajashughulikiwa ili asitoe siri. Ushahidi wa kuwa Rostam anawapa wapinzani hawa fedha tunao, wakitaka kwenda mahakamani waende tutauonesha,” alibainisha Matefu.

Inashangaza sana baada ya kuandikwa kwenye vyombo vya habari kuwa, watuhumiwa wa ufisadi watawatumia viongozi wa vyama vya upinzani kumtukana Kikwete na familia yake, haupiti muda wapinzani wanaanzisha madai ya Ridhiwani! Kwa nini haya yafanywe sasa wakati inatangazwa kuwa maadui wa Kikwete watakitumia chama cha upinzani?” Alihoji Matefu.

Hili la kukubali kutumiwa na mafisadi ili kuipaka matope familia ya Rais Kikwete na baadhi ya viongozi waadilifu wa CCM waliojipambanua kupiga vita ufisadi lazima Watanzania wahoji, kulikoni!,” alidai Matefu.

Mwanasiasa huyo kijana aliongeza: “Mwandishi hushangai wanapoacha ajenda zao na kuamua kujibizana na watu wa CCM, hasa suala la kujivua gamba? Kwani wakizungumzia namna ya kupunguza gharama za maisha zinazopanda, na namna ya kuwafaidisha Watanzania na zoezi la mjadala wa katiba mpya hawataeleweka? Kwa nini wasizungumze ni vipi katiba mpya itawasaidia Watanzania kupambana na rushwa, ufisadi na matatizo mengine badala ya kukimbilia kujibizana na watu kama Nape Nnauye, na sasa wameingia kwenye ugomvi na Samuel Sitta, Dk. (Harrison) Mwakyembe na wengine?” Alihoji.

Matefu alidai kuwa mzozo unaoendelea baina ya Chadema na baadhi ya viongozi wa CCM kuhusu nani alitaka kuanzisha chama gani hauwanufaishi Watanzania bali watuhumiwa wa ufisadi, maana sasa hawazungumzwi wao na ajenda ya ufisadi imehama kutoka kwao.

“Hata kama kina Sitta walitaka kujiunga CCJ au Chadema, kuwaumbua huko kunaleta faida au hasara kwa Chadema? Je, kama watu wengine walio ndani ya CCM nao wangependa kuondoka, wataonaje? Hivi Chadema hawawezi kuzungumza kuhusu mustakabali wa Tanzania bila kuizungumzia CCM kwa jazba?” alihoji.

Matefu pia alidai kuwa kama serikali itasita kuwachukulia hatua mafisadi ndani ya siku ishirini na moja, vijana wamepanga kuandamana ili kushinikiza, na tayari baadhi ya mikoa imeshathibitisha kushiriki maandamano hayo ikiwemo mikoa ya Arusha, Mwanza na Tabora.

MAHMOUD JIBRIL: Kiongozi wa Baraza la mpito nchini Libya anayeandaa enzi mpya baada ya Gaddafi

 Mahmoud Jibril

Mahmoud Jibril akiwa na Rais wa Ufaransa, 
Nicolas Sarkozy


TRIPOLI
Libya

VITA vya Libya vimechukuwa sura ya vita vya kidiplomasia kwenye jamii ya kimataifa, huku Urusi na Umoja wa Afrika zikisimama upande mmoja na Umoja wa Mataifa na nchi za Magharibi zikisimama upande mwingine.
Ushindi wa waasi wa Libya mjini Misrata dhidi ya vikosi vya kiongozi wa nchi hiyo, Muammar Gaddafi, unaelezwa kuwa ni wa hatua moja mbele, moja nyuma, kutokana na vikosi vya Gaddafi kuendelea kuushambulia mji huo na kuongezeka kwa idadi ya waathirika.

Taarifa za Jumatano asubuhi ya wiki iliyopita zilithibitisha kuwa makombora kadhaa yamekuwa yakirushwa kutoka upande wa vikosi vya Gaddafi kuelekea bandari ya Misrata na kuilazimisha meli ya Shirika la Kimataifa la Wahamiaji ishindwe kutia nanga kuwaokoa wakimbizi.

Meli hiyo ilikusudiwa kuchukua wakimbizi 550 wa Kiafrika, kati ya 2,000 waliokwama katikati ya vita. Kwa mujibu wa madaktari, wakimbizi watatu wa Kiafrika wameuawa na 20 kujeruhiwa kutokana na mashambulizi hayo.

Katika mji wa Kabao, ripoti zilisema kuwa mapigano makali yalimalizika kwa ushindi wa waasi, ambapo wanajeshi 45 wa serikali waliuawa na wengine 17 kukamatwa mateka. Waasi pia walipoteza wapiganaji wawili na watatu kujeruhiwa.

Kimataifa, vita hivi vimeendelea kuigawa dunia mapande mawili. Umoja wa Afrika, kwa upande wake, umeyalaumu mataifa ya Magharibi kwa kuzihujumu kwa makusudi jitihada zake za kutafuta amani nchini Libya.

Kamishna wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja huo, Ramtane Lamamra, alisema mataifa hayo yanauchukulia mpango wa amani wa Umoja wake kama usio na maana, huku yakiendelea na mashambulizi yake dhidi ya Libya, akikusudia zaidi mashambulizi ya Nato dhidi ya makazi ya Gaddafi.

Kulikuwa na mazungumzo mjini Addis Ababa, kati ya pande mbili zinazozozana zilizoeleza maoni tafauti, ingawa pia zilielezea nia ya kuendelea na mazungumzo. Waziri wa Mambo ya Nje wa Libya, Abdelati Obeidi, alitaka jitihada za Umoja wa Afrika zipewe fursa, huku wawakilishi wa waasi wakiahidi kuendelea na mazungumzo, alimradi tu 'matakwa ya watu ya Libya' yanatimizwa. Kwa waasi, matakwa hayo ya watu wa Libya ni Gaddafi kuondoka madarakani.

Hata hivyo, Waziri Mkuu wa Urusi, Vladimir Putin, akiwa ziarani nchini Denmark, aliyaita mashambulizi ya ya Nato dhidi ya makazi ya Gaddafi kama kitendo kisichokubalika, kwani ni njama ya kumuua kiongozi wa nchi hiyo.

"Dunia ina mataifa mengi yenye hali kama ya Libya. Je, tutakwenda kote huko kupiga mabomu. Kimazungumzo, wanatekeleza azimio la kuzuia ndege kuruka, ambalo ni sawa. Lakini azimio hilo liko wapi ikiwa kila usiku nyumba anayoishi Gaddafi inapigwa kwa mabomu? Nani ameyaruhusu haya?" Aliuliza Putin.

Lugha kama hii pia imetumiwa na rais wa Venezuela, Hugo Chavez, ambaye ameyaita mashambulizi hayo kuwa ni "kuchanganyikiwa kwa mataifa ya Magharibi", aliyoyashutumu kumchukia Gaddafi ili yapate mafuta. Hata hivyo, iliripotiwa kuwa ujumbe wa serikali ya Libya ulikuwa Venezuela katika jitihada za kutafuta uungwaji mkono wa kimataifa.

Pamoja na lawama zote, mataifa wanachama wa Nato yanasema yataendelea na operesheni yao ya kuwalinda raia wa Libya, na kwamba yatafanya hivyo kwa kuviharibu vyanzo vyote vya mashambulizi ya Gaddafi.

Waziri wa Ulinzi wa Uingereza, Liam Fox, ameiita operesheni hiyo ya Nato kuwa ya mafanikio. Akizungumza kwenye Wizara ya Ulinzi ya Marekani, Pentagon, baada ya mazungumzo na waziri mwenzake wa ulinzi, Robert Gates, Fox alisema:
"Tumeshuhudia maendeleo yakipatikana katika siku chache zilizopita. Na ni wazi kwamba utawala wa Gaddafi umeshikwa pabaya. Na madhali serikali inawashambulia raia, nasi tutaendelea kuvichukulia vituo vyao vya kuendeshea mashambulizi hayo kuwa shabaha halali za makombora yetu."

Ndani ya Libya, milio ya mizinga na risasi inaendelea kuwa sehemu ya maisha ya kawaida. Nje ya Libya vita vya maneno vimekuwa mtindo wa sasa. Na tofauti na ilivyokuwa kwa Tunisia na Misri, ngoma ya Libya inaonekana kuwa na mpigaji zaidi ya mmoja na wachezaji wasio na idadi.

Kwa upande wao waasi wa Libya wametoa mwelekeo wa kisiasa kwa nchi hiyo iwapo Kanali Gaddafi ataondoka madarakani. Mwelekeo huo unaonesha kuanzishwa kwa serikali ya mpito wakati katiba mpya inaandikwa na uchaguzi kufanyika.

Kiongozi wa upinzani wa Baraza la Mpito la Taifa la Libya (NTC), Mahmoud Jibril alitoa pendekezo la Libya baada ya Kanali Gaddafi kuondoka katika mkutano wa wajumbe wa nchi zinazounga mkono waasi uliofanyika Rome Italia. Alifafanua kuwa serikali ya mpito itaanza kazi mara moja ili kutoa maelekezo ya utendaji wa siku kwa siku na kuweka ulinzi.

Mahmoud Jibril amekubaliana na mpango wa misaada uliopitishwa na nchi 22 zinazounga mkono waasi hao. Katika habari nyingine, Ufaransa iliwaamuru wanadiplomasia 14 wa Libya wanaomuunga mkono Kanali Gaddafi kuondoka nchini humo ndani ya siku mbili. Waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa alisema maafisa hao wametajwa kuwa 'watu wasiotakiwa nchini humo.'

Pendekezo la Mahmoud Jibril limeungwa mkono na Mwenyekiti wa kamati ya Seneti ya Marekani ya masula ya kigeni, Seneta John Kerry aliposema kuwa wakati raia wa Libya wanalindwa na ushirika wa kijeshi unaoongozwa na Nato, mpango unafanyika wa kutayarisha enzi baada ya Moammar Gadhafi.

Seneta Kerry alizungumza na waandishi wa habari baada ya kukutana na kiongozi huyo wa upinzani wa Baraza la Mpito la Taifa la Libya, Mahmoud Jabril, aliyekuwa ziarani Marekani.

Historia ya Jibril

Mahmoud Jibril amezaliwa mwaka 1952, ni mwanasiasa wa Libya ambaye, tangu Machi 23, 2011, amekuwa Waziri Mkuu wa serikali ya mpito ya Jamhuri ya Libya, moja ya taasisi mbili zenye udhibiti wa Libya. Yeye pia ni Mtendaji mkuu wa Timu ya Baraza la Mpito la Taifa la Libya (NTC). Serikali yake inatambuliwa kama "mwakilishi pekee halali" wa Libya na Ufaransa, Ureno, Uingereza na Qatar, lakini, hadi sasa haijatambuliwa rasmi na idadi kubwa wanachama wa nchi za Umoja wa Mataifa.

Maisha yake ya awali

Jibril amefuzu shahada ya kwanza katika Uchumi na Sayansi ya Siasa kutoka Chuo Kikuu cha Cairo mwaka 1975, kisha akapata shahada ya uzamili katika sayansi ya siasa mwaka 1980 na udaktari katika strategic planning mwaka 1985, zote kutoka Chuo Kikuu cha Pittsburgh. Baada ya hapo alifundisha somo la strategic planning katika Chuo cha Pittsburgh kwa miaka kadhaa, na amechapisha vitabu 10 kuhusu strategic planning na maamuzi, ikiwa ni pamoja na Picha na Itikadi katika sera za Marekani kuelekea Libya, 1969-1982.

Jibril aliongoza timu ambayo iliandaa na kuunda Mwongozo wa Mafunzo ya Umoja wa Kiarabu. Pia ndiye alikuwa na jukumu la kuandaa na kuendesha mikutano miwili ya kwanza ya Mafunzo katika dunia ya Kiarabu katika miaka ya 1987 na 1988. Baadaye alichukua jukumu la usimamizi na utawala wa viongozi wengi wa programu za mafunzo kwa ajili ya usimamizi katika nchi za Kiarabu ikiwemo Misri, Saudi Arabia, Libya, UAE, Kuwait, Jordan, Bahrain, Morocco, Tunisia, Uturuki na Uingereza.

Tangu mwaka 2007 alikuwa katika serikali ya Gaddafi kama mkuu wa Bodi ya Maendeleo ya Uchumi wa Taifa, ambapo alihimiza sera za ubinafsishaji na soko huria.

Tarehe 23 Machi 2011, Baraza la Mpito la Taifa liliundwa rasmi kwa serikali ya mpito na yeye aliteuliwa rasmi kuwa Waziri Mkuu wa serikali ya mpito. Jibril anajulikana kwa kuongoza mkutano na mazungumzo na Rais wa Ufaransa, Nicolas Sarkozy, mkutano ambao ulisababisha Ufaransa kulitambua rasmi Baraza la Mpito la Taifa kama mwakilishi pekee wa watu wa Libya.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari na mashirika ya habari ya kimataifa.


May 11, 2011

Kama semina elekezi isipozaa matunda mawaziri hawa kwanini wasirudi shule?

 Rais Jakaya Kikwete

Chati inayoonesha Baraza la Mawaziri la Tanzania

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

MWEZI uliopita nchi yetu ilishuhudia mkutano mkubwa uliopewa jina la Jukwaa la Uwekezaji. Nikiwa mmoja wa wafuatiliaji nilisoma gazeti la Mwananchi la 19/04/2011 na kukumbana na kichwa cha habari kilichonishtua sana: “Wakili ataka mawaziri warudi darasani”. Habari iliyoambatana na maelezo haya, nanukuu:
Wakili wa Kampuni ya FB Attorneys, Fayaz Bhojani jana alitoa mpya katika Jukwaa la Uwekezaji Afrika, lililoanza jijini Dar es Salaam, baada ya kueleza kuwa Mawaziri wa Serikali za Afrika Mashariki ikiwamo Tanzania, hawana uelewa wa kutosha hivyo wanatakiwa kusoma.

Akichangia hoja katika mkutano huo uliohudhuriwa pia na marais wa nchi hizo, Bhojani alisema mawaziri hao wameshindwa kutekeleza ahadi zao kwa wananchi.

Mawaziri wetu wanatakiwa kurudi shuleni wakasome kwa sababu wanayoyaahidi hawayatekelezi na wakirudi siku nyingine, wanarudia tena kuahidi. Nadhani wanahitaji kwenda shule. Serikali ziwapeleke shule,” alisisitiza Bhojani.

Rais Nkurunzinza ambaye ndiye aliyekuwa Mwenyekiti wa Jukwaa hilo alikuwa wa kwanza kuwajibia mawaziri wake tuhuma hizo kwa kusema: “Mawaziri hawawezi kupelekwa tena shuleni kwa sababu walishamaliza masomo yao.” Kauli hiyo ya Rais Nkurunzinza iliungwa mkono na Rais Kikwete aliyesisitiza kuwa mawaziri hawawezi kurudishwa shuleni.

Habari hiyo ikanikumbusha jinsi wawekezaji katika nchi hii wanavyopewa miaka kumi bure ya kuchimba vito vya thamani kwa mikataba wanayoingia wakati nchi ina matatizo lukuki.

Lakini wiki hii kwa hiki kilichofanyika huko Dodoma katika Semina Elekezi kwa Viongozi na Watendaji Wakuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, semina iliyolizika jana Alhamisi imenifanya niyatafakari tena maneno na wakili Bhojan japo yalionekana kupingwa na Rais Kikwete ambaye hata hivyo wiki hii ameyaunga mkono kwa kuwarudisha darasani mawaziri wake.

Pamoja na mengi lakini Rais Kikwete alionekana kukazia zaidi mambo haya:

-Marufuku Mawaziri kutoelewana;
-Mawaziri wakishakubaliana katika Baraza la Mawaziri ni uamuzi wa wote;
-Ukiona ni vigumu kuafiki ni bora kutoka;
-Lazima kutekeleza uwajibikaji wa pamoja;
-Hata miswada ya sheria bungeni ni ya mawaziri wote;
-Ni kinyume cha maadili Waziri kupinga muswada wa Waziri mwenzake;
-Lazima wawe '
team players';
-Kuhudhuria vikao vya Bunge kwa Mawaziri ni lazima;
-Marufuku kutembelea jimbo wakati wa vikao;
-Katika kikao cha Bunge hatutegemei Waziri kuwa na safari zitakazomuondoa bungeni;
-Kuna udhaifu mkubwa katika kusema mafanikio yaliyopatikana;
-Wakifanya kitu bila kukieleza ni sawa na kwamba hawakukifanya;
-Wananchi wanalaumu serikali kutokana na kuelezwa uongo dhidi yake;
-Wawe wepesi kusahihisha uongo dhidi ya serikali, raslimali zipo, vyombo vya habari vipo, hawavipi habari;
-Kila Wizara kuna wasemaji, hawasemi, wasemaji wengine wanazuiwa kusema;
-Maafisa Habari wapewe fursa waitumie taaluma yao, wao wanajua; wasilaumu kwamba vyombo haviwataki;
-Lazima serikali iwasiliane na watu wake kupitia vyombo vya habari;
-Kama ulikubali kuwa Waziri ni lazima uitumikie, tafuta muda muafaka wa kuhudumia jimbo;
-Mawaziri wengine wanaongozana na kundi la waandishi wa habari majimboni;
-Uadilifu ni muhimu sana: Waziri, Naibu, Katibu Mkuu wanatakiwa kuwa mfano mwema. Mawaziri, Naibu wasinyooshewe vidole. Wasifike saa 5 na kuondoka saa 7 mchana, waache uzembe, wizi, 'michongo', kutumia ofisi kujinufaisha, ulevi, uzinzi wala ubabe;
-Haiwezekani kunywa kwenye baa mpaka wanataka msaada wa kubebwa;
-Ukiwa waziri ni kuwa kuna baadhi utavikosa. Unakatisha wananchi tamaa, waache ubabe, wanadhulumu watu;
-Utelezaji wa ilani kwa miaka mitano nyuma. Mipango ya baadaye na kadhalika katika kuwatumikia wananchi. Kilimo, afya, miundombinu kuboreshwa katika kutekeleza
vision ya 2025;
-Itafika wakati umeme utakuwa haukatiki;
-Bado kuna makosa mengi, kuna upotevu wa fedha za umma
-Kuna maendeleo fulani lakini hayatoshi;
-Watapate kusikiliza kutoka kwa watendaji wa vyombo vya dola kuhusu jitihada zinazofanywa na idara zao;
-Hali ya kupunguza msongamano wa wafungwa, usalama, udhibiti wa madawa ya kulevya na Takukuru;
-Kila Wizara iandike kueleza mafanikio katika wizara yake, ifanye tathmini ili kuhifadhi kumbukumbu kwa vizazi vya baadaye.

Alichokisema Rais Kikwete ni sawa lakini kuna jambo moja la kushangaza: ni kwa nini Kikwete aitishe semina elekezi mjini Dodoma wakati alishatembelea wizara zote? Kwa nini hakuelekeza mambo hayo huko huko kwenye wizara zao wakati alipozitembelea?

Inashangaza pia kwa rais ambaye ndiye mwenyekiti wa CCM, chama kilicho kwenye harakati za kujivua gamba la ufisadi kwa kuwatosa viongozi wenye tuhuma za ufisadi na matumizi mabaya ya pesa za Watanzania, kwamba yeye haoni kama huu nao ni aina nyingine ya ufisadi kwa kutumia pesa za Watanzania vibaya!

Inasikitisha sana kuona nchi yetu inavyoendeshwa na kuhujumiwa na watu wachache tuliowapa dhamana ya kulinda rasilimali zetu. Watu ambao wanatumia kodi za wananchi wanyonge kwa kile wanachokiita “Semina Elekezi”.

Sielewi hii maana yake ni nini hasa? Au maana yake ni kwamba wananchi masikini waendelee kuteseka kwenye umasikini wakati wakubwa wao kila siku wanafikiria jinsi ya kutumia fedha za umma?

Semina hii pia imeniacha na maswali mengi: je, ni kweli wateule hawa wa rais ni watu wasioelewa majukumu na kazi zao? Je, wale waliopata semina elekezi kule Ngurudoto mara tu alipochaguliwa kwa mara ya kwanza amewaweka kwenye fungu lipi?

Pia najiuliza kama rais alishafanya tathmini ya semina elekezi ya Ngurudoto ili kujua mapungufu na faida zake kabla hajatoa semina nyingine?

Nafikiri mapendekezo haya ya rais yangeenda sambamba na kuliangalia upya Baraza la mawaziri ambalo kwa mtazamo wangu ni kubwa na halina kazi za kufanya. Mfano Waziri wa Maji, Waziri wa Kilimo na Ushirika, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Waziri wa Mazingira, Waziri wa Ardhi Nyumba na Makazi, bado sijaelewa mipaka yao ya kazi ili wasiingiliane kwenye majukumu yao. Labda kwenye hili rais alipaswa kuliweka sawa ili kuepuka migongano.

Mfano kama kuna eneo lina mgogoro wa wakulima, wafugaji na mbuga za wanyama ina maana wote watatu wawepo?

MAMADOU TANDJA: Rais wa zamani Niger aliyeonja joto ya jiwe sasa kupata ahueni

 Mamadou Tandja

NIAMEY
Niger

MAHAKAMA ya Rufaa nchini Niger Jumanne wiki hii imeamuru kuachiliwa huru kwa rais wa zamani wa nchi hiyo, Mamadou Tandja, aliyepinduliwa mwezi Februari 2010. Tandja aliyekuwa madarakani kwa miaka 10, anatuhumiwa kwa matumizi mabaya ya fedha za umma.

Viongozi wa mapinduzi hayo walikasirishwa baada ya Tandja kuwania uongozi tena kwa kipindi kingine cha tatu. Mwezi uliopita, uongozi huo wa kijeshi ulikabidhi rasmi utawala kwa kiongozi wa upinzani wa siku nyingi, Mahamadou Issoufou, aliyeshinda uchaguzi wa marudio mwezi Machi.

Katika mzunguko wa kwanza mwezi Januari, Tandja aliondolewa kutoka kwenye nyumba aliyowekwa kizuizini na kupelekwa gerezani. "Mashtaka yote na kesi dhidi ya Mamadou Tandja yamefutwa," mmoja wa wanasheria wake, Souley Oumarou, aliliambia shirika la Habari la AFP siku ya Jumanne wiki hii.

Hata hivyo, mwandishi wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) nchini Niger, Idy Baraou alisema kuwa Tandja alikuwa anatuhumiwa kwa ubadhirifu wa fedha za serikali kiasi cha dola milioni moja. Alikuwa pia anahusishwa na ufisadi wa zabuni ya mbolea yenye gharama kati ya dola milioni 9 na milioni 10.

Katiba mpya ya Niger imepunguza madaraka ya Marais na kuweka kikomo cha urais kuwa miaka kumi.

Historia yake:
Luteni Kanali mstaafu Mamadou Tandja (tamka Mamaduu Tanja), alizaliwa mwaka 1938. Ni mwanasiasa ambaye alikuwa rais wa Niger kuanzia 1999 hadi 2010. Alikuwa Rais wa chama cha National Movement of the Development Society (MNSD) kuanzia 1991 hadi 1999 na bila mafanikio alijaribu kuwania urais akiwa mgombea kupitia MNSD mwaka 1993 na 1996 kabla ya kuchaguliwa kwa mara ya kwanza mwaka 1999. Wakati akiwa Rais wa Niger, alikuwa pia Mwenyekiti wa Jumuia ya Kiuchumi ya Afrika Magharibi (Ecowas) kuanzia 2005 hadi 2007.

Tandja ni mchanganyiko wa makabila ya Fula na Kanuri. Ameweka historia ya kuwa Rais wa kwanza wa Niger ambaye si wa kutoka kabila la Hausa au Djerma.

Kufuatia mgogoro wa kikatiba wa mwaka 2009, ambao ulisababishwa na jitihada za Tandja kutaka kubaki madarakani kwa zaidi ya muda wake, alipinduliwa na jeshi katika mapinduzi yaliyofanyika mwezi Februari 2010.

Mapinduzi ya 1974:
Tandja aliyezaliwa katika eneo la Maine-Soroa, nchini Niger, alishiriki katika mapinduzi ya 1974 yaliyomuingiza madarakani Seyni Kountche, alikuwa mwanachama wa Halmashauri Kuu ya Jeshi.

Mwaka 1976 akawa msimamizi wa Maradi kabla ya kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani Septemba 10, 1979; alikaa katika nafasi hiyo mpaka ilipokabidhiwa kwa Kountche mwenyewe, Agosti 31, 1981. Kisha akawa Msimamizi wa Tahoua kuanzia 1981 hadi Machi 1988, Balozi katika nchi ya Nigeria kuanzia Juni 1988 hadi Machi 1990 na Waziri wa Mambo ya Ndani kwa mara nyingine kuanzia Machi 1990 hadi Machi 1991.

Mwaka 1991, Tandja aliibuka kuwa kiongozi wa kundi moja kati ya makundi mawili yenye nguvu katika chama tawala, MNSD na katika mkutano wa chama uliofanyika Novemba 1991, alichaguliwa kuwa Rais wa MNSD. Tandja alipokea uongozi wa chama kutoka kwa mpinzani wake, Moumouni Adamou Djermakoye na kuonekana kama ishara ya kumalizika kwa utawala wa kabila la Zarma (Djerma) la Djermakoye.

Uchaguzi wa 1993:
Tandja aliwania urais katika uchaguzi mkuu wa 1993, na kuwa wa kwanza katika duru ya kwanza mwezi Februari kwa asilimia 34.22 ya kura, lakini alipoteza nafasi hiyo kwa Mahamane Ousmane katika duru ya pili mwezi Machi, kwa kupata asilimia 45.58 ya kura. Tandja alikubali matokeo na kumpongeza Ousmane.

Tandja alishiriki katika maandamano ya upinzani dhidi ya serikali ya Muungano wa Majeshi ya Mabadiliko Aprili 16, mwaka 1994 na alikamatwa pamoja na watu wengine 90. Ousmane alipinduliwa katika mapinduzi ya kijeshi yakiongozwa na Ibrahim Bare Mainasara Januari 27, 1996.

Uchaguzi wa 1996:
Chini ya uongozi wa Mainassara, uchaguzi mpya wa rais ulifanyika tarehe 7 na 8 Julai, 1996, ambapo Tandja aligombea tena na kuwa wa tatu kwa kuambulia asilimia 15.65 ya kura, nyuma ya Mainassara aliyepata asilimia 52 na Ousmane mwenye asilimia 20, kwa mujibu na matokeo rasmi.

Katika siku ya pili ya kupiga kura alikamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi pamoja na wagombea wengine watatu wa upinzani kwa wiki mbili. Kufuatia maandamano ya kidemokrasia tarehe 11 Januari 1997, Tandja alikamatwa pamoja na Ousmane na aliyekuwa Waziri Mkuu, Mahamadou Issoufou na kushikiliwa mpaka 23 Januari.

Uchaguzi wa 1999:
Aprili 1999, Mainassara aliuawa na serikali ya kijeshi na Meja Daouda Malam Wanke kuchukua madaraka. Baraza la majeshi liliahidi kurejea kwa demokrasia ndani ya mwaka, na uchaguzi ulifanyika Oktoba na Novemba. Tandja alishinda uchaguzi wa rais, kwa asilimia 32 ya kura, katika duru ya kwanza, na asilimia 59.89 katika duru ya pili, na kumshinda Issoufou.

Tandja aliungwa mkono na Ousmane katika duru ya pili ya uchaguzi. MNSD pia kilishinda viti vingi katika uchaguzi wa bunge mwezi Novemba, 1999 na Tandja mwenyewe alichaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Diffa kupiti MNSD, ingawa kutokana na nafasi yake ya Urais, nafasi yake ya ubunge ilijazwa na mbadala wake, Nassourou Samaila. Alichukua rasmi madaraka ya Rais mwezi Disemba 22, 1999. Alimteua Hama Amadou kuwa Waziri Mkuu Januari 2000.

Niger ilikuwa na madeni makubwa na haikupata misaada yoyote toka nje kutokana na mapinduzi ya 1996. Tandja alilenga katika maendeleo ya kiuchumi, mazungumzo na vyama vya wafanyakazi katika utumishi wa umma na wahisani wa kigeni. Wengi hawakukubaliana na hatua ya Tandja kutaka kupunguza matumizi ya serikali.

Mwaka 2001, wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Niamey walifanya maandamano ya nguvu dhidi ya serikali kupunguza fedha zao. Julai 31, 2002, baadhi ya askari katika eneo la Diffa walianza uasi wakidai malipo na kuboresha hali ya maisha; uasi ulienea hadi Niamey siku chache baadaye. Wafuasi wake waliwashinda waasi na kurejeshwa kwa amani 9 Agosti.

Uchaguzi wa 2004:
Tandja aligombea tena mwaka 2004. Katika duru ya kwanza alishika nafasi ya kwanza kwa asilimia 40.7 ya kura, huku wapinzani wake watano wakigawana zilizobakia. Kama 1999, Mahamadou Issoufou alishika nafasi ya pili, na kushiriki katika duru ya pili na Tandja hapo Disemba 4.

Tandja alichaguliwa kwa asilimia 65.53 ya kura, na Issoufou kuambulia asilimia 34.47. Wagombea wote wanne walioshindwa raundi ya kwanza walimuunga mkono Tandja katika raundi ya pili. Aliapishwa kwa muhula wa pili 21 Desemba katika hafla iliyofanyika Uwanja wa Jenerali Seyni Kountche mjini Niamey, iliyohudhuriwa na marais sita wa nchi za Afrika.

Ingawa kulikuwa na uvumi juu ya uwezekano wa mabadiliko ya katiba ili kumwezesha kuwania tena urais mwaka 2009, alisema katika mahojiano na gazeti la Le Monde, yaliyochapishwa 6 Oktoba 2007, alikusudia kuachia ngazi baada ya muhula wake wa pili. Hata hivyo, Disemba 21, 2008, mkutano mkubwa ulifanyika mbele ya jengo la Bunge la Taifa mjini Niamey uliotoa wito wa kuongeza muda wa miaka mitatu kwa Tandja, ili amalize utawala wake Disemba 22, 2012.

Kulingana na pendekezo la wafuasi wake - ambalo pia lilipendekeza kuendeleza mamlaka ya Bunge na taasisi nyingine kwa miaka mitatu kwa kile kilichosemwa kuwa kwa manufaa na maendeleo ya Niger. Waziri Mkuu, Seyni Oumarou alikuwa miongoni mwa washiriki wa mkutano huo. Upinzani ulipinga pendekezo hilo, na maandamano makubwa yalifanyika mjini Niamey siku chache baadaye. Disemba 30, mashirika 20 yasiyo ya kiserikali na vyama, ikiwa ni pamoja na Shirikisho la Kidemokrasia la Wafanyakazi wa Niger (CDTN), walianzisha upinzani, na walitoa wito kwa Tandja kuacha mpango huo.

Mgogoro wa kikatiba 2009:
Katika uchaguzi wa 2009, harakati ya rasimu ya Rais Tandja kugombea awamu ya tatu ilitolewa. Wakiongozwa na mtu muhimu wa MNSD nje ya serikali, kikundi hicho kilichukua kaulimbiu ya Tandja ya 2004, “Tazartche”: neno la Kihausa lenye maana ya “mwendelezo”.

Kupitia mikutano kadhaa ya kampeni za umma iliyofadhiliwa na kuhudhuriwa sana mwishoni mwa 2008, Rais alibaki kimya katika wito wa kumtaka abaki madarakani. Katiba ya 1999 ilieleza ugumu wa kuongoza kwa zaidi ya vipindi viwili (Ibara ya 36), na marekebisho yake kutokuwa halali kwa njia yoyote (Ibara ya 136). Waziri Mkuu Seyni Oumarou alielezea 22 Januari kwamba ratiba ya uchaguzi iliyopangwa itafuatwa na uchaguzi kufanyika kabla ya mwisho wa 2009. Mwezi Machi, wakati wa mikutano yake na Rais wa Ufaransa, Sarkozy, Tandja alisema kuwa hatafuti kuongeza muda wa tatu wa kuongoza.

Mei 2009, alipoulizwa na waandishi wa habari wakati wa ziara yake ya Agadez kuanza mazungumzo ya amani na waasi wa Tuareg, Tandja alitangaza kuwa “watu wanadai nibaki.” Kisha msemaji wake akaainisha mpango wa jinsi kura ya maoni inavyoweza kufanyika katikati ya 2009, na kuifanyia kazi Katiba ya Sita ya Jamhuri ya Niger, ambayo haitakuwa na ukomo wa muda kwa Rais.

Mapinduzi ya 2010:
18 Februari 2010, wakati wa mkutano wa serikali katika ikulu ya rais, askari waasi walishambulia na kumpindua Tandja katika mapinduzi ya kijeshi, na kuanzisha Serikali ya Baraza la Kijeshi linaloitwa Baraza Kuu kwa ajili ya Matengenezo ya Demokrasia (CSRD). Tandja akakamatwa na kushikiliwa katika kambi ya kijeshi nje ya jiji la Niamey.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari.