Sep 28, 2011

MIAKA 50 YA UHURU: Rasilimali za nchi bado hazijawanufaisha wananchi

 Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi

 Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa

 Rais Jakaya mrisho Kikwete

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

HIVI sasa inaonekana dhahiri kuwa kipaumbele kikubwa cha viongozi walio wengi katika serikali yetu kipo katika mikakati ya kuandaa sherehe za miaka 50 ya uhuru zitakazofanyika wiki chache zijazo, mnamo Disemba 9 mwaka huu, zikisindikizwa na kaulimbiu ya “Tumethubutu, Tumeweza na Tunasonga mbele”. Licha ya kaulimbiu hiyo tamu, ukweli unabaki palepale kwamba wananchi walio wengi wanaendelea kuogelea kwenye lindi la umasikini hata baada ya uhuru wao. Kila kukicha maisha yanakuwa magumu afadhali ya jana!

Wakati wa kupigania uhuru kwa nchi zilizokuwa chini ya utumwa wa kikoloni moja kati ya malengo yaliyowasukuma wapigania uhuru wa wakati huo yalikuwa ni wananchi kujiamulia mambo yao katika matumizi ya rasilimali zao. Tanganyika (kwa maana ya Tanzania Bara) ni moja kati ya nchi za Afrika zilizopata uhuru mwanzoni mwa miaka ya 1960 ikiwa na matumaini mapya ya kutumia rasilimali zake katika kujiletea maendeleo.

Wakati huu tunapojiandaa kwa sherehe za miaka 50 baada ya uhuru huo, matumaini ya wananchi wa nchi hii kutumia rasilimali zao yamepotea kabisa huku kiwango cha umasikini kwa wananchi hao kikizidi kuongezeka, na pengo kati ya walionacho na wasionacho likizidi kuongezeka kwa kuwa ni wananchi wachache sana ndiyo wanaofaidi rasilimali za nchi hii.

Tanzania imejaaliwa rasilimali nyingi; watu, ardhi yenye rutuba, maji (bahari, mito na maziwa), kuwa katika eneo la kimkakati la kijiografia kwa biashara, na maliasili ikiwemo za utalii na madini. Hata hivyo, tukiwa tunajigamba kwa kuthubutu, kuweza na kusonga mbele kama kaulimbiu yetu inavyojieleza, tunaonekana kuwa na laana ya rasilimali hizi hali ambayo inafanya wananchi walio wengi kuendelea kuwa katika lindi la umasikini na wakiendelea kusukumwa pembezoni nje ya urithi ambao taifa hili linao.

Katika Tanzania ya leo na miaka mingi ijayo, hakuna jambo lolote muhimu kwa wanajamii wa nchi hii kuliko ardhi na rasilimali zao. Kama alivyowahi kusema mwanazuoni, Profesa Issa Shivji, rasilimali ndiyo chanzo cha uhai, kielelezo cha utamaduni, utambulisho wa ubinadamu, tegemeo la kuishi maisha ya kujitegemea, ya heshima na ya kifahari.

Rasilimali ardhi ndiyo rasilimali kubwa kabisa kwa wananchi, kwa sasa rasilimali hii inamilikiwa na watu wachache wenye uwezo kifedha hasa baada ya serikali hii kupitisha sera ya uwekezaji, na kumekuwepo matukio mengi ya uporaji wa ardhi za vijiji yanayofanywa na wawekezaji wa ndani na nje – kifisadi – kwa kisingizio cha uwekezaji.

Kwa hali hii, hivi sasa tunakabiliwa na tishio kubwa la usalama na amani katika taifa letu linalotokana na migogoro hii ya kirasilimali, hasa ardhi na madini, katika maeneo mbalimbali ya nchi ambayo haina tofauti na bomu litakalotulipukia wakati wowote endapo tu kasi ya ukuaji wa uchumi wenye kutoa fursa kwa wengi itaendelea kupuuzwa na haitaongezwa.

Mbali na ardhi, kumekuwepo pia taarifa za kuporwa kwa rasilimali nyingine kama vile wanyamapori, madini, maji na misitu, ambazo kwa sasa zinamilikiwa na matajiri huku masikini walio wengi wakizipata kwa taabu. Hali hii imekuwa ikisababisha Watanzania walalahoi wa mijini na vijijini kupoteza kabisa matumaini ya maisha kutokana na kushindwa kufaidika na rasilimali zao, japo kama Taifa tunajigamba kuthubutu, kuweza na kusonga mbele.

Tukiwa tunapanga mikakati na kujiandaa katika sherehe za kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru, Taifa bado lipo gizani kutokana na mgawo wa umeme unaoendelea, pia bado kuna idadi ndogo sana ya Watanzania waliounganishwa kwenye gridi ya taifa, ingawa tunajivunia kaulimbiu yetu ya kuthubutu, kuweza na kusonga mbele.

Tatizo hili sugu la mgawo wa umeme ambalo sasa limekomaa na kuwa janga la taifa pamoja na ahadi mbalimbali zinazotolewa mara kwa mara za kulimaliza ambazo zimegeuka ndoto za alinacha, limetokana na ufisadi na udhaifu wa kiuongozi na kiutendaji ambao umeikabili sekta ya nishati nchini kuanzia Awamu ya Pili, likaongezeka katika Awamu ya Tatu na kukomaa zaidi katika Awamu hii ya Nne ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, licha ya kuthubutu, kuweza na kusonga mbele.

Kwa Serikali yoyote makini yenye kujali watu wake isingekimbilia kuandaa sherehe kama hii na kutumia pesa za wananchi bali ingetumia fursa ya miaka hamsini kukaa chini na kuyaangalia kwa makini mapungufu yaliyopo, hasa katika katiba, ili wananchi wapewe kipaumbele katika madai na matakwa yao kuhusu ardhi na rasilimali zao.

Alamsiki


MAHMOUD ABBAS: Je atauweza mfupa uliomshinda Yasser Arafat?

 Mahmoud Abbas

Yasser Arafat

RAMALLAH
Palestina

RAIS wa Mamlaka ya Taifa ya Palestina, Mahmoud Abbas, alipokelewa kama shujaa aliporudi nyumbani kutoka Umoja wa Mataifa, ambako alikwenda kuomba Mamlaka ya Wapalestina iwe mwanachama kamili wa Umoja wa Mataifa.

Abbas aliuambia umati uliomshangilia mjini Ramallah, kwamba hawatoshiriki kwenye mazungumzo na Israel, ikiwa hawatotambuliwa kimataifa, na kama Israel haitaacha kujenga makazi katika Ukanda wa Magharibi.

Mkuu huyo wa mamlaka ya Palestina akiwa jijini New York, Marekani alisema kwamba hawezi kuwa kigeugeu, anataka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lizungumze lolote kuhusu ombi lake la kutaka kuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa. Kiongozi huyo aliwasilisha ombi hilo siku ya Ijumaa Septemba 23, licha ya juhudi kutoka pande mbalimbali kumtaka asifanye hivyo.

Mahmoud Abbas amesema tangu achukuwe uamuzi wa kwenda kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutaka Palestina kuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa, amekuwa katika hali ngumu, kwani alikuwa anapokea maombi kutoka pande tofauti kumtaka aachane na mpango huo.

Historia yake

Mahmoud Abbas, ambaye pia anajulikana kama Abu Mazen, alizaliwa Machi 26, 1935, amekuwa Mwenyekiti wa Shirika la Ukombozi wa Palestina ( PLO ) tangu 11 Novemba 2004 na akawa Rais wa Mamlaka ya Palestina ya Taifa tangu alipochaguliwa kuwa rais wake mnamo Januari 2005 kwa tiketi ya Fatah.

Alichaguliwa kuongoza hadi tarehe 9 Januari 2009, aliongoza hata baada ya muda wake kwisha kwa mwaka mmoja zaidi na kuendelea hata baada ya mhula wa pili kwisha. Matokeo yake, wapinzani wakuu wa Fatah, chama cha siasa cha Hamas kilitangaza kuwa kutomtambua Abbas kama rais halali. Abbas alichaguliwa kama Rais wa Serikali ya Palestina na Halmashauri Kuu ya PLO mnamo 23 Novemba 2008, nafasi aliyoishikilia kiholela tangu Mei 8, 2005. Abbas aliwahi kuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Mamlaka ya Palestina Machi hadi Oktoba 2003, alipojiuzulu akitoa sababu za kukosa msaada kutoka Israeli na Marekani na "uchochezi wa ndani" dhidi ya serikali yake. Kabla ya kuwa waziri mkuu, Abbas aliiongozwa Idara ya Mambo ya Mazungumzo ya PLO.

Wasifu kabla ya kifo cha Yasser Arafat

Abbas alizaliwa katika mji wa Safed katika Galilaya. Yeye na familia yake walikimbilia Syria wakati wa vita vya Waarabu na Israel vya 1948. Alihitimu katika Chuo Kikuu cha Damascus kabla ya kwenda Misri ambako alisoma sheria.
Abbas baadaye alijiunga na masomo katika Chuo Kikuu cha Patrice Lumumba jijini Moscow, ambako alipata shahada ya Sayansi (kwa Urusi ni sawa na PhD). Maudhui ya tasnifu yake ya udaktari ilikuwa "upande wa pili: mahusiano ya siri kati ya Nazism na uongozi wa harakati wa Kizayuni" ambapo alijaribu kuthibitisha kuwa mauaji ya Kinazi kwa Wayahudi hayajawahi kutokea. Profesa wake aliyemsimamia alikuwa Yevgeny Primakov.

Amemuoa Amina Abbas na wana watoto watatu wa kiume. Mtoto mkubwa, Mazen Abbas, alikuwa anaendesha kampuni ya ujenzi jijini Doha na alifia nchini Qatar kutokana na mshtuko wa moyo mwaka 2002 akiwa na umri wa miaka 42. Abu Mazen ina maana ya "baba wa Mazen". Mtoto wao wa pili, Yasser Abbas, ni mfanyabiashara wa Canada aliyepewa jina hilo la kiongozi wa zamani wa Palestina, Yasser Arafat. Mtoto wa mwisho ni Tareq, mfanyabiashara.

Katika miaka ya 1950 katikati, Abbas alishiriki kikamilifu katika siasa za chini za Palestina, na kujiunga na idadi ya Wapalestina waliokuwa uhamishoni nchini Qatar, alikokuwa Mkurugenzi wa Utumishi wa Huduma za Kijamii wa Emirate. Akiwa bado huko, mwaka 1961, aliajiriwa na kuwa mwanachama wa Fatah, iliyoanzishwa na Yasser Arafat na Wapalestina wengine nchini Kuwait katika miaka ya 1950. Wakati huo, Arafat alianzisha msingi wa Fatah kwa kuhusisha Wapalestina matajiri walioko Qatar, Kuwait, na mataifa mengine ya Ghuba.

Waziri Mkuu

Mnamo mwaka 2003, Israeli na Marekani kwa pamoja zilionesha kukataa majadiliano na Yasser Arafat, Abbas alianza kuibuka katika ugombea wa nafasi ya uongozi. Kama mmoja wa wanachama wachache waliobakia ambao ni waanzilishi wa Fatah, alikuwa akiaminiwa ndani ya Wapalestina, na ugombea wake uliimarishwa na ukweli kwamba Wapalestina wengine waliokuwa katika ngazi za juu walikuwepo kwa sababu mbalimbali ambazo si nzuri.

Sifa ya Abbas ya kuongozwa kwa sera za kisayansi ilimsaidia kwa nchi za Magharibi na baadhi ya wabunge wa Palestina, na shinikizo lililetwa kwa Arafat kumteua waziri mkuu. Arafat akafanya hivyo tarehe 19 Machi 2003. Awali, Arafat alijaribu kuidhoofisha nafasi ya waziri mkuu, lakini hatimaye alilazimishwa kumpa Abbas baadhi ya madaraka.

Hata hivyo, muda wa Abbas kama waziri mkuu uliendelea kuwa na sifa ya migogoro kadhaa baina yake na Arafat kuhusu mgawanyo wa madaraka kati yao. Abbas mara nyingi aligusia kujiuzulu kama hakupewa mamlaka zaidi katika utawala wake. Mwanzoni mwa Septemba 2003, alikabili bunge la Palestina kuhusu suala hili. Marekani na Israeli zilimshutumu Arafat mara kwa mara kumdhoofisha Abbas na serikali yake.

Aidha, Abbas aliingia katika mgogoro na wapiganaji wa makundi ya Palestina, hasa Palestinian Islamic Jihad Movement na Hamas kwa sababu sera zake za kisayansi zilikuwa kinyume na mbinu zao. Hata hivyo, aliweka wazi kabisa kwamba alikuwa analazimishwa kuachana na matumizi ya silaha dhidi ya raia wa Israel kwa muda huo.

Kwanza, aliahidi kutotumia nguvu dhidi ya wanamgambo, ili kuepuka vita vya wenyewe kwa wenyewe, na badala yake alijaribu njia ya mazungumzo. Hii ilifanikiwa kidogo, ilisababisha kutolewa kwa ahadi kutoka makundi mawili kusitisha-mapigano kwa heshima ya nchi moja ya Palestina. Hata hivyo, kuendelea kwa vurugu na Israel "kulenga kuua" viongozi wanaojulikana kulimlazimisha Abbas kuchukua hatua ili kutekeleza upande wa Mamlaka ya Palestina katika kutafuta amani. Hii ilisababisha kugombea madaraka na Arafat juu ya udhibiti wa huduma za usalama wa Wapalestina; Arafat alikataa kutoa udhibiti kwa Abbas, hivyo kumzuia kutumia wanamgambo.

Abbas alijiuzulu uwaziri mkuu mnamo Oktoba 2003, akitoa sababu za kukosa msaada kutoka Israeli na Marekani na "uchochezi wa ndani" dhidi ya serikali yake.
Uchaguzi wa rais 2005

Baada ya kifo cha Yasser Arafat, Mahmoud Abbas alionekana, angalau kwa Fatah, kuwa mrithi wake. Tarehe 25 Novemba 2004, Abbas alipitishwa na Baraza la Mapinduzi la Fatah kama mgombea wake kwa uchaguzi wa rais, uliopangwa kufanyika Januari 9, 2005.

14 Disemba, Abbas alitoa wito wa kumalizika kwa ghasia katika Intifada ya pili na amani. Abbas aliliambia gazeti la Asharq Al-Awsat kwamba "matumizi ya silaha yamekuwa yakiharibu na lazima yakomeshwe". Hata hivyo, alikataa kupokonya silaha wanamgambo wa Palestina na matumizi ya nguvu dhidi ya makundi ambayo Israel, Marekani na Umoja wa Ulaya wanayatambua kama mashirika ya kigaidi.

Vikosi vya Israel vilikamata na kuzuia harakati za wagombea wengine, Hamas wakasusia uchaguzi, na kampeni za Abbas zikapewa asilimia 94 ya matangazo kwenye vituo vya TV katika Palestina, ushindi wa Abbas ulikuwa dhahiri, na tarehe 9 Januari, Abbas alichaguliwa kwa asilimia 62 ya kura kama Rais wa Mamlaka ya Taifa ya Palestina.

Makala hii imeandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.


Sep 21, 2011

MICHAEL SATA: Tishio la Rais Rupiah Banda wa Zambia katika nafasi ya urais

 Michael Sata

LUSAKA
Zambia

UCHAGUZI mkuu wa Zambia umefanyika Jumanne (Septemba 20) huku ukiacha homa na joto la uchaguzi katika kila pembe ya nchi hiyo. Michael Sata, kiongozi wa chama cha upinzani cha Patriotic Front (PF) na Rais Rupiah Banda wa chama tawala cha Movement for Multiparty Democracy (MMD) wamechuana vikali katika kinyang'anyiro cha kuwania urais wa nchi hiyo. Kumekuwa na milolongo mirefu nje ya vituo vya kupigia kura wakati Wazambia walipokuwa wanapiga kura katika kinyanganyiro kikali zaidi katika historia ya uchaguzi nchini Zambia.

Pia ziliripotiwa taarifa za kuchelewa kwa shughuli hiyo na kuwepo kwa ghasia lakini wachunguzi wa uchaguzi wamesema utaratibu mzima wa upigaji kura umekuwa mzuri. Tangu uchaguzi wa mwaka 2008, watu wengine, ikiwa ni zaidi ya milioni moja wamejiandikisha kuwa wapigaji kura, wengi wao ni vijana ambao hawana ajira. Bei ya juu ya madini ya shaba imeimarisha ukuaji wa uchumi wa Zambia lakini wananchi wa kawaida wanasema hawajapata faida yoyote kutokana na ukuaji huo.

Maelfu ya Polisi walipelekwa sehemu mbalimbali ili kuepusha ghasia na uuzaji wa shoka na vifaa vingine ambavyo vina uwezo wa kutumika kama silaha umepigwa marufuku katika kipindi hiki cha uchaguzi.

Watu milioni 5.2 walitarajiwa kupiga kura, hii ikiwa ni idadi kubwa zaidi ya watu waliojiandikisha kuwa wapiga kura katika uchaguzi wa Rais, wabunge na wawakilishi wa serikali za mitaa. Upigaji kura ulianza saa kumi na mbili asubuhi saa za Zambia na kumalizika saa kumi na mbili jioni ambapo wakati makala hii ikiandaliwa matokeo yalikuwa hayajaanza kutoka.

Chunguzi za maoni zilizofanywa kuhusiana na nafasi ya kushinda urais aliyonayo kila mgombea zilitoa matokeo yenye kutofautiana. Tawi la vijana la chama tawala liliamini kuwa Rais Rupiah Banda angeibuka mshindi katika uchaguzi huo wakati ambapo uchunguzi mwingine uliofanywa unaonesha kuwa Michael Sata angeshinda kwa asilimia 55 ya kura.

Sata aliyekuwa mwanachama wa chama tawala cha zamani cha UNIP cha kiongozi wa harakati za uhuru wa Zambia, Dk. Kenneth Kaunda, lakini aliamua kukihama chama hicho na kujiunga na chama kipya cha MMD ambacho kilichuana na UNIP katika uchaguzi wa rais wa mwaka 1990. Katika uchaguzi huo, Fredrick Chiluba, aliyewania kiti hicho kwa tiketi ya MMD aliibuka mshindi na kubaki madarakani kwa muda wa muongo mzima.

Hata hivyo, katika uchaguzi wa mwaka 2001 kinyume na matarajio ya Michael Sata, viongozi wa MMD walimteua Levy Mwanawasa badala yake kuwa mgombea urais katika uchaguzi wa rais kitendo ambacho kilimfanya Sata aamue kukihama chama hicho pia na kuunda chama chake cha Patriotic Front. Katika uchaguzi wa rais wa mwaka 2006 Sata alijitosa kwenye kinyang'anyiro hicho lakini alishindwa na Mwanawasa.

Mwaka 2008 Rais wa wakati huo wa Zambia, Levy Mwanawasa, alifariki dunia na kupelekea kuitishwa uchaguzi wa kabla ya wakati ambapo mara hiyo Michael Sata alichuana na Rupiah Banda. Ingawa Banda alitangazwa mshindi kwa kujipatia asilimia 40 ya kura akimshinda Sata kwa kura 35,000 tu, lakini Sata aliyepata asilimia 38 alidai kuwa matokea ya uchaguzi huo yalichakachuliwa. Hali hii ilisababisha ghasia kubwa ambazo zilizochochewa na baadhi ya wafuasi wa upinzani katika ngome zao za mijini.

Historia yake

Michael Chilufya Sata amezaliwa mwaka 1937 ba kabla ya kuanzisha chama chake cha Patriotic Front, Sata alikuwa waziri katika serikali ya Chiluba iliyoongozwa na Movement for Multiparty Democracy (MMD). Kama kiongozi wa chama cha upinzani cha Patriotic Front (PF), Sata, maarufu kama "King Cobra", amejitokeza kama mgombea urais na mpinzani katika kipindi cha marehemu Rais Levy Mwanawasa katika uchaguzi wa rais 2006, lakini alishindwa.

Miaka ya mwanzo

Michael Sata alizaliwa na kukulia katika eneo la Mpika, Mkoa wa Kaskazini. Alifanya kazi kama afisa wa polisi, afisa katika shirika la reli na mfanyakazi wa vyama vya wafanyakazi na biashara wakati wa utawala wa kikoloni. Sata alianza kushiriki kikamilifu katika siasa za Rhodesia ya Kaskazini ya wakati huo, mwaka 1963. Alifanya kazi kwa njia yake kupitia ngazi mbalimbali wakati wa chama tawala cha United National Independence Party (UNIP), na akawa kiongozi wa Lusaka mwaka 1985.

Kama kiongozi alijijengea jina kama mtu wa utekelezaji kwa mbinu mbalimbali. Alisafisha mitaa, alitia viraka barabara na kujenga madaraja katika mji. Baadaye alikuja kuwa Mbunge wa jimbo la Kabwata katika Lusaka. Ingawa alikuwa karibu na aliyekuwa Rais wa wakati huo, Kenneth Kaunda, aliamua kuwa mbali kutokana na mtindo wa kidikteta wa Kaunda na kisha alijiondoa kabisa katika chama cha UNIP na kujiunga na chama cha Movement for Multiparty Democracy (MMD) wakati wa kampeni za vyama vingi vya siasa mwaka 1991.
Baada ya Frederick Chiluba kumshinda Kaunda mwaka 1991, Sata alikuwa mmoja wa watu waliotambulika sana nchini Zambia. Chini ya chama cha MMD, alikuwa waziri wa serikali za mitaa, kazi na, afya ambapo, anajigamba, "mageuzi yake yameleta mfumo bora wa afya".

Mwaka 1995, aliteuliwa kuwa waziri asiye na wizara maalum, katibu wa maandalizi wa taifa katika chama wakati ambao mtindo wake wa kisiasa ulielezewa kama "unazidi kuchukiza".
Kuanziasha Patriotic Front

Mwaka 2001, rais wa wakati huo wa Zambia, Fredrick Chiluba alimteua Levy Mwanawasa kama mgombea wa MMD katika uchaguzi wa 2001. Katika kuchanganyikiwa, Sata alijiondoa MMD na kuanzisha chama kipya, Patriotic Front (PF). Aligombea katika uchaguzi wa 2001 lakini hakufanya vyema - chama chake kiliambulia kiti kimoja tu katika Bunge. Sata alikubali kushindwa na akaendelea na kampeni.

Sata aligombea tena uchaguzi wa rais wa Septemba 2006 kama mshindani aliyetumia umasikini katika sera ya mageuzi ya kiuchumi ya Mwanawasa. Sata wakati wote alitoa hotuba za kudhihaki. Katika tukio moja la kampeni, Sata alirarua kabichi mbele ya wafuasi wake. Kabichi hiyo ilimaanisha kigugumizi cha hotuba ya Mwanawasa, ambayo ni matokeo ya kujeruhiwa katika ajali ya 1992 ya gari.

Pia alimshutumu Mwanawasa kwa "kuiuza" Zambia kwa maslahi ya kimataifa, na katika tukio moja, aliifananisha Hong Kong kama nchi na Taiwan kama taifa huru. Kama majibu, China, ambayo ni mwekezaji katika shaba ya Zambia, ilitishia kukata mahusiano na Zambia kama akichaguliwa.

Matokeo ya uchaguzi wa awali yalimpa Sata ushindi, lakini matokeo zaidi yalimweka Mwanawasa katika nafasi ya kwanza na kumsukuma Sata nafasi ya tatu. Matokeo ya Muda ya kura kutoka majimbo 120 kati ya 150 yalihesabiwa na kumweka Mwanawasa juu zaidi ya asilimia 42 ya kura; Hakainde Hichilema asilimia 28; na Michael Sata asilimia 27. Wafuasi wa upinzani walipopata habari kwamba Sata yupo nafasi ya tatu, maandamano yalizuka mjini Lusaka. Oktoba 2, Tume ya Uchaguzi ya Zambia ilitangaza kuwa Mwanawasa alikuwa mshindi rasmi wa uchaguzi, na Sata katika nafasi ya pili kwa kuwa na asilimia 29.

Sata alikamatwa mnamo Desemba 2006, akituhumiwa kutoa tangazo la uongo la mali zake alipoomba kuwania urais mwezi Agosti, pamoja na mashtaka mengine. Alihojiwa na polisi na kutolewa kwa dhamana. Angepatikana na hatia, angefungwa kifungo jela miaka miwili. Kwa hatia hiyo, hangeruhusiwa pia kushikilia madaraka katika ofisi ya umma. Sata alisema madai dhidi yake yalikuwa ya kisiasa, na aliyakana mahakamani. Desemba 14, mashtaka yalifutwa na madai kuwa tamko la mali halikufanywa chini ya kiapo.

Mnamo Machi 15, 2007, Sata alifukuzwa Malawi muda mfupi baada ya kuwasili. Sata alisema kwamba alikwenda kukutana na wafanyabiashara, na alidai serikali ya Zambia inaeneza uongo kuwa alikuwa Malawi kumsaidia rais wa zamani wa nchi hiyo, Bakili Muluzi. Serikali ya Zambia ilikana, wakati serikali ya Malawi haikutoa maelezo yoyote. Aprili 6, mwanasheria wa Sata alisema kwamba alifungua kesi dhidi ya serikali ya Malawi kwa kukiuka haki ya mteja wake.

Baada ya kupoteza pasipoti yake jijini London mwishoni mwa 2007, Sata alipata nyingine, hata hivyo, Novemba 10, 2007, Waziri wa Mambo ya Ndani, Ronnie Shikapwashya, alisitisha pasipoti ya Sata kwa muda kwa sababu hakufuata taratibu muhimu na kuthibitisha kwamba alihitaji pasipoti mpya.

Sata alipata mshtuko wa moyo Aprili 25, 2008 na alihamishiwa Hospitali ya Milpark ya mjini Johannesburg, Afrika Kusini, ambapo alisemwa kuwa katika hali njema mwezi Aprili 26. Alipatanishwa na Rais Mwanawasa Mei 2008.

Kifo cha Mwanawasa na uchaguzi 2008

Baada ya Mwanawasa kupata kiharusi na kulazwa hospitali nchini Ufaransa, Sata alihoji rasmi afya ya Mwanawasa Julai 15, 2008 na kutoa mwito wa timu ya madaktari kupelekwa na Baraza la Mawaziri kumchunguza Mwanawasa, timu hii ingefichua hali halisi ya Mwanawasa. Mwanawasa alifariki dunia Agosti 2008. Agosti 25, Sata alipojaribu kuhudhuria mazishi ya Mwanawasa huko Chipata katika Jimbo la Mashariki, Maureen Mwanawasa, mjane wa Mwanawasa, aliamuru Sata aondoke, akisema kwamba alitumia tukio hilo kisiasa na kwamba hakuwahi kupatana na familia ya Mwanawasa. Sata, aliyeondolewa kutoka eneo hilo na usalama, alisema kwamba alikwenda pale kumuomboleza Mwanawasa na kwamba alikuwa na nia ya kuusindikiza mwili, alisisitiza kwamba upatanisho wake na Mwanawasa mwenyewe ulitosha kuhalalisha uwepo wake. Pia alisema kuwa Maureen Mwanawasa hakumtendea sawa.

Makala hii imeandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari.


Sep 14, 2011

SAADI GADDAFI: Mfanyabiashara, mwanasoka na kamanda wa vikosi Maalum vya Libya anayeshikiliwa Niger



Al-Saadi al-Gaddafi

NIAMEY
Niger

WAZIRI wa Masuala ya Haki wa Niger, Marou Amadou, amethibitisha kuwa Saadi Gaddafi aliyesemekana kuwemo katika msafara ulioelekea mji mkuu wa Niger, Niamey, kuwa yupo nchini humo. Lakini hadi sasa haijulikani Gaddafi mwenyewe yuko wapi.

Hadi sasa wapiganaji wanaokabiliana na vikosi vya Gaddafi sasa wanadhibiti maeneo mengi nchini Libya, ukiwemo mji mkuu Tripoli, na wamekuwa wakijaribu kuchukua udhibiti wa miji mingine, iliyo chini ya wanaomuunga mkono Gaddafi, ikiwemo miji ya Bani Walid na Sirte.

Jumapili ya wiki iliyopita vikosi vya waasi vilianza mashambulio katika mji wa Bani Walid, vikisaidiwa na mashambulio ya angani ya Nato. Maafisa wamesema vikosi vyao sasa viko karibu kufika katikati mwa mji wa Bani Walid.

Baadhi ya watu wa jamii ya Gaddafi wamekimbilia Algeria. Misafara kadhaa ya watu waliokuwa wakimuunga mkono Gaddafi imeonekana ikivuka mpaka wa Kusini mwa Libya na kuingia Niger hivi karibuni.

Msemaji wa serikali ya Niger na waziri wa masuala ya haki amesema kuwa Saadi Gaddafi alikuwa kwenye msafara huo na watu wengine wanane. Msemaji huyo anasema kuwa msafara huo ulikuwa njiani kuelekea Agadez Kaskazini mwa Niger na kwamba Saadi pamoja na alioandamana nao waliruhusiwa kuingia kwa kuzingatia misingi ya kibinaadamu.

Serikali ya Niger inautambua utawala wa Baraza la Kitaifa la Mpito la Libya, lakini ikasema bado hawajaamua kama watamruhusu Gaddafi kuingia nchini humo. Hata hivyo msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani amesema, serikali ya Niger imethibitisha kuwa itamweka mbaroni mtoto huyo wa Muammar Gaddafi, Saadi al Gaddafi.

Amesema ingawa Saadi hayupo kwenye orodha ya watu waliowekewa vizuizi vya azimio Na. 1970 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, lakini serikali ya Niger imeliarifu Baraza la Mpito la Taifa la Libya kuwa itashirikiana na baraza hilo katika kushughulikia suala la maofisa wa utawala wa Gaddafi wanaoingia nchini humo.

Waziri mkuu wa Niger aliwaambia waandishi wa habari kuwa, maofisa 32 wa utawala wa Muammar Gaddafi, akiwemo mtoto wake Saadi wamekwishaingia nchini Niger kwa nyakati tofauti kuanzia tarehe 2 mwezi huu.

Historia yake

Al-Saadi al-Gaddafi alizaliwa Mei 25, 1973, ni mtoto wa tatu wa Muammar al-Gaddafi. Saadi alikuwa mfanyabiashara wa Libya na mchezaji wa zamani wa mpira wa miguu. Pia alikuwa kamanda wa vikosi Maalum vya Libya na ameshiriki katika vita vya wenyewe kwa wenyewe vya 2011 nchini Libya.

Taarifa ya Interpol (orange notice) imetolewa dhidi yake. Yeye ni sehemu ya baraza muhimu la baba yake. Mnamo 11 Septemba 2011, al-Saadi alikimbilia nchi hiyo jirani ya Niger, ambapo serikali imeamua kumpeleka kwenye mji mkuu wa Niamey na kumshikilia. Saadi amefunga ndoa na binti wa kamanda wa kijeshi wa Libya.

Fani ya soka

Saadi alicheza soka nchini Libya akiichezea timu ya Al Ahly ya Tripoli. Mnamo Juni 6, 2000, taarifa za BBC zilisema kwamba Saadi alikuwa na mkataba na mabingwa Maltese Birkirkara FC na alipaswa kuichezea timu hiyo katika Ligi ya Mabingwa. Lakini walishindwa kuafikiana.

Soka la Libya lilikuwa la upendeleo kwa Saadi. Moja ya sheria zilikataza kutangaza jina la mchezaji yeyote wa mpira wa miguu isipokuwa Saadi. Ni namba tu za wachezaji wengine zilizotangazwa badala ya majina yao. Waamuzi pia waliipendelea timu ya Saadi na vikosi vya usalama vilitumika kuzima maandamano yoyote dhidi ya timu hiyo.

Saadi aliingia mkataba na timu ya Perugia ya Italia inayoshiriki ligi kuu nchini humo (Serie A) mwaka 2003, ambapo aliichezea timu hiyo mechi moja tu kabla ya kushindwa kupima vipimo kwa ajili ya dawa za kulevya. Aliwahi kuwa kwenye bodi ya timu ya Juventus ya Italia, ambapo asilimia 7.5 ya hisa za timu inamilikiwa na muungano wa Libya, lakini aliamua kutojiunga tena na Perugia.

Pia alikuwa nahodha wa timu ya taifa ya kandanda ya Libya, nahodha wa klabu yake ya jijini Tripoli, na Rais wa Shirikisho la Soka la Libya.

Saadi alijiunga na timu iliyofuzu kucheza ligi ya mabingwa Ulaya mwaka 2005-06, Udinese Calcio, alicheza dakika kumi tu katika mechi ya mwisho wa msimu wa ligi dhidi ya Cagliari Calcio. Kisha alijiunga UC Sampdoria wakati wa msimu wa 2006-07, bila ya kucheza mechi hata moja.

Shughuli za biashara

Mwaka 2006, Saadi na Serikali ya Libya walizindua mradi wa kujenga mji eneo litakalokuwa na uhuru nusu mfano wa Hong Kong nchini Libya, likisambaa kilomita 40 kati ya mpaka wa Tripoli na Tunisia. Mji huo mpya ungejengwa kwa kutumia teknolojia ya hali ya juu, huku huduma za kibenki, vituo vya afya na elimu vikiwa havihitaji visa kuingia katika mji huo mpya.

Mji huo ungekuwa na uwanja wake wa ndege wa kimataifa na bandari kuu. Saadi aliahidi kuwepo uvumilivu wa kidini kwa wote; “masinagogi na makanisa” na hakutakuwa na ubaguzi katika mji huo mpya. Mji huo mpya ungekuwa na sheria za biashara za “Kimagharibi” alizodhani kuwa makampuni ya Ulaya na Marekani yangevutiwa kuwekeza biashara.

Saadi pia alichukua riba kubwa katika biashara nyingine nchini Libya ikiwemo kampuni ya Tamoil, ambayo ni kampuni ya kusafisha mafuta na masoko inayomilikiwa na serikali ya Libya. Saadi pia amewahi kuwa mdau na mkurugenzi mtendaji katika kampuni ya asili ya Los Angeles.

Mambo ya kimahakama

Mnamo Julai 2010, Saadi alitakiwa na mahakama ya Italia kuilipa Euro 392,000 hoteli ya kisasa yenye anasa nyingi ya Ligurian kama fidia ya kutolipa bili kwa kukodi mwezi mzima kabla ya muda mrefu aliokaa wakati wa majira ya joto ya 2007.

Vita vya wenyewe kwa wenyewe Libya

Mnamo 15 Machi, kulikuwa na taarifa ambazo hazikuthibitishwa kwamba rubani aliyejulikana kwa jina la Muhammad Mokhtar Osman, aliishambuliwa ngome ya Gaddafi ya Bab al-Azizia mjini Tripoli na kuharibu na pia kumjeruhi Saadi na ndugu yake, Khamis al-Gaddafi.

Akiongea na Shirika la Habari la Uingereza, BBC, askari wa Libya alidai kuwa Saadi mwenyewe aliamrisha kupigwa risasi kwa waandamanaji wasiokuwa na silaha katika mji wa Benghazi wakati alipotembelea kambi ya jeshi ya mji huo mwanzoni wa uasi. Saadi alithibitisha kuwepo katika kambi hiyo lakini alikanusha kutoa amri ya kuwashambulia waandamanaji.

Saadi alikuwa na nguvu kubwa katika mabadiliko ya majeshi ya serikali ya Libya na mbinu walizotumia. Badala ya kupambana na waasi kwa silaha nzito, mizinga na magari ya kivita - ambayo ingeweza kwa urahisi kujulikana na waasi na kisha kuharibiwa na ndege za kivita - vita dhidi ya waasi ilipiganwa katika vipande vidogovidogo, kwa haraka na uhodari.

Waasi hao walidai kumteka Saadi wakati wa vita ya Tripoli, mnamo 21 Agosti, lakini baadaye ikasemekana kuwa ulikuwa ni uongo.

Baada ya jumba la Saadi kutekwa na vikosi vya waasi wakati wa vita, ilitangazwa kupatikana DVD yenye picha za uchi za mashoga iliyoandikwa “Boyz Tracks” ikiwa miongoni mwa nyaraka katika ofisi ya jumba lake.

Agosti 24, Saadi aliwasiliana na CNN, na kusema kuwa alikuwa na mamlaka ya kujadili kwa niaba ya vikosi vya Gaddafi, na alitaka kujadili namna ya kusitisha mapigano na serikali ya Marekani na Nato. 31 Agosti, Saadi aliwasiliana na Al Arabiya, na kusema kwamba baba yake alikuwa tayari kujiuzulu, na kuomba mazungumzo na Baraza la Taifa la Mpito.

5 Septemba, alisema katika mahojiano na CNN kwamba hotuba ya jazba ya ndugu yake, Saif al-Islam, ilisababisha kuvunjika kwa mazungumzo kati ya vikosi vya Baraza la Taifa la Mpito na wafuasi wa Gaddafi katika eneo la Bani Walid, na alisema hajaonana na baba yake katika kipindi cha miezi miwili. Pia alidai kuwa msimamo wake ni kutoegemea upande wowote katika mgogoro na kutolewa kwa upatanisho.

11 Septemba, Saadi alikimbilia nchini Niger na aliruhusiwa kuingia kwa mujibu wa misingi ya kibinadamu. Kulingana na serikali ya Niger, wanapanga kumshikilia Saadi wakati wakifikiria nini cha kumfanya.

Makala hii imeandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.


Sep 7, 2011

Kesi ya Bi Victoire Ingabire na demokrasia finyu barani Afrika

 Ramani ya Bara la Afrika

 Rais mstaafu wa Afrika kusini, Mzee Nelson Mandela

 Rais mstaafu wa Botswana, Sir ketumile Masire

Bi Victoire Ingabire

BISHOP J. HILUKA
Dar es salaam

NI nini Watanzania tunajifunza kutoka mataifa mengine ya Afrika hasa kuhusiana na hali ya demokrasia? Je, sisi pia tunatoa fundisho gani katika demokrasia kwa mataifa mengine ya Afrika, mbali ya kukataa kuwatambua waasi wa Libya na kumshinikiza balozi wa Libya nchini kushusha bendera ya waasi hao?

Vipi kuhusu demokrasia ya nchi za Zimbabwe, Uganda, Rwanda, Libya, Misri, Ethiopia na kadhalika? Kwa nini wanasiasa wa Afrika siku zote wamekuwa wa kwanza kuharibu mambo? Ni Zimbabwe ambayo miaka ya karibuni ilikuwa tegemeo kubwa la Chakula la Afrika! Sasa vipi tena haohao waliotegemewa kwa chakula ndiyo wanaosumbuliwa na njaa na mfumuko wa bei?

Ni Uganda iliyokuwa ya kwanza kuanzisha utawala wa mihula miwili ya urais! Imekuwaje tena rais wa nchi hiyohiyo aliyesimamia uanzishwaji sheria ya mihula miwili kuendelea kuwepo madarakani kwa mihula minne na wala haoneshi dalili ya kuondoka madarakani? Vipi kuhusu kesi ya Rwanda ya wale maelfu waliouwawa mwaka 1994, ilikuwaje yale mauaji yakashindwa kuepukika? Je, Tanzania na mataifa mengine jirani yalifanya nini kukomesha mauaji ya watu wasio na hatia?

Vipi kuhusu nchi ya Libya iliyojiita Jamhuri wakati ilikuwa chini ya utawala wa mfalme Gaddafi kwa miaka 42? Nani alimsikia Gaddafi alipomshauri Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda kukataa kung'atuka madarakani? Je, nchi zingine za Afrika zilisemaje kuhusu hilo? Vipi kuhusu Misri na Ethiopia, nchi ambazo ni vinara wetu wa ustaarabu na uungwana tangu miaka mingi kabla ya Kristo, sasa ubabe wa nini?

Vipi kuhusu nchi nyingine za Afrika na hata Tanzania ambayo ingawa hatuvumi lakini tumo? Kwa nini kila inapofika wakati wa uchaguzi huwa nongwa? Je, upinzani ni uhaini? Hali hii itaendelea hadi lini?

Nchini Rwanda, kesi inayomkabili kiongozi wa chama cha upinzani cha UDF imeanza tena mapema wiki hii huku upande wa mashtaka ukiomba muda zaidi wa kukusanya ushahidi. Victoire Ingabire amefikishwa mahakamani chini ya ulinzi mkali huku wanahabari wakizuiwa kuzungumza naye.

Bibi Ingabire anakabiliwa na mashtaka ya ugaidi ambapo imedaiwa kwamba amekuwa akifadhili shughuli za kundi la FDLR ambalo serikali ya Rwanda imelitaja kuwa ni la kigaidi. Ingabire amekanusha madai hayo na kuituhumu serikali ya Rais Paul Kagame kuwa inatawala kwa mkono wa chuma na kwamba imeshindwa kuvumilia mashinikizo ya wapinzani.

Victoire Ingabire alikamatwa mwanzoni mwa mwaka jana baada ya kurudi nyumbani akitokea Uholanzi alikokuwa akiishi kama mkimbizi wa kisiasa. Alikamatwa na kuzuiwa kugombea katika uchaguzi uliofanyika nchini humo Agosti mwaka jana, licha ya kupendekezwa na muungano wa vyama vya upinzani kwamba yeye ndiye asimame dhidi ya Kagame

Inashangaza kwamba Victoire aliyeamua kurudi nyumbani Rwanda, baada ya miaka 16 uhamishoni alitumia muda mwingi kujifunza, na kufanya kazi huku akiihudumia familia yake nchini Uholanzi, kisha kuchukua uzito sana katika muktadha mpana ambao watu wake wanateseka. Alikaririwa akisema kuwa alirudi nyumbani kwa sababu hakuweza tena kuvumilia kuona watu wake wa Rwanda wanateseka chini ya udikteta wa kikatili. Kwa wakati huo, Januari 2010, alijitokeza kuwa kiongozi msomi mwenye msukumo zaidi ndani na nje ya Rwanda.

Kukamatwa kwa Ingabire ni cheche kinzani za kijamii zinazoendelea kujionesha kwa kasi na kwamba, demokarasia ya kweli barani Afrika inazidi kutoweka. Afrika limekuwa bara ambalo ukijiunga katika chama cha upinzani unahesabika kama mhaini. Ni bara ambalo si ajabu kusikia chama cha siasa cha upinzani kinapigwa marufuku, licha ya Katiba kuunga mkono tamko la haki msingi za binadamu lililotolewa na Umoja wa Mataifa.

Ni bara ambalo kuna matamko ya Serikali yanayowapokonya wananchi haki zao za msingi katika masuala ya kujieleza, kukutana na kuunda vyama mbalimbali vya kisiasa na kijamii. Kutokana na msimamo huu, nchi nyingi za bara hili zinakuwa ni nchi zinazotawaliwa kwa misingi ya kijeshi. Serikali zimeendelea kuwashughulikia wapinzani na wanaharakati wanaopania kuleta mageuzi kwa kutumia sheria dhidi ya vitendo vya kigaidi.

Bara la Afrika licha ya kukabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi na kijamii, lakini pia lina idadi kubwa ya wagonjwa wa Ukimwi. Watu wengi wanaangamia kutokana na ugumu wa maisha baada ya kuondolewa na serikali zao kwenye maeneo yao yenye utajiri wa rasilimali, madini, mbao, ardhi nzuri ya kilimo, maji safi, mafuta na gesi asilia, ili kuendeleza mfumo wa kibepari wa kimataifa.

Je, nchi hizi za Kiafrika ikiwemo Tanzania zinaichukuliaje kesi ya Ingabire ama kwa sababu anashitakiwa na Rais mwenzao, Kagame? Je, kama Ingabire anadaiwa kuwa mhaini, kwa nini serikali ya Kagame isingelimwacha agombee huku yenyewe ikipeleka ushahidi kwa wananchi kuwa hafai hivyo wasimchague?

Pamoja na mapenzi makubwa niliyonayo kwa Kagame kama rais mchapakazi na anayesimamia vyema ufisadi nchini mwake kiasi kwamba Wanyarwanda wanapiga hatua haraka sana kulinganisha na sisi, lakini kila nikifumba macho na kufumbua naona Ingabire hatendewi haki katika hili. Kuna mkono wa kisiasa hapa. 
 
Tanzania na dunia nzima kwa ujumla tunapaswa kumwambia Kagame amwachie mwanamke huyu. Ana haki ya kugombea urais. Marais mliostaafu kwa heshima mko wapi? Joachim Chisano, Nelson Mandela, Ketumile Masire, Sam Nujoma, Ali Hassan Mwinyi na wengine wengi mko wapi? Tumieni busara zenu kumwambia Kagame amwachie huru Ingabire kwa sababu mahakama nzuri kuliko zote lilikuwa sanduku la kura. Kwa nini wananchi hawakuruhusiwa kutoa hukumu kupitia sanduku hilo?


VICTOIRE INGABIRE: Mwanamke jasiri aliyejitokeza kuwa mpinzani wa Kagame

 Victoire Ingabire

 Rais wa Rwanda, Paul kagame

KIGALI
Rwanda

JAJI wa Rwanda ameamuru kesi inayomkabili kiongozi wa upinzani, Victoire Ingabire iendelee. Victoire anatuhumiwa kwa kueneza propaganda za chuki na za kikabila na "kukana kutokea kwa mauaji ya kimbari" - mashtaka anayosema yamechochewa kisiasa.

Upande wa mashtaka ulitaka kesi hiyo iahirishwe mpaka ushahidi zaidi uwasilishwe kutoka Uholanzi, ambapo Victoire aliishi mpaka Januari 2010 alipoamua kurejea Rwanda. Alikamatwa mwezi Aprili na kuzuiwa kugombea katika uchaguzi wa Agosti mwaka jana.

Alifikishwa mahakamani akiwa na pingu, na kuvaa sare ya wafungwa wa Rwanda ya rangi ya waridi huku akiwa amenyolewa kipara. Mwandishi wa Shirika la Habari la Uingereza (BBC), Geoffrey Mutagoma, aliyeko mjini Kigali alisema ni kawaida kwa wafungwa wa Rwanda kunyolewa vipara kutokana na sababu za kiafya.

Wakili wa Victoire Ingabire anayetokea nchini Uingereza, Iain Edwards, alitaka kesi hiyo ianze kusikilizwa kama ilivyokuwa imepangwa na Jaji Alice Rulisa akakubali. "Mwendesha mashtaka alisema tangu mwanzo kwamba wako tayari kwa kesi hiyo kuanza kusikilizwa, na wana ushahidi wote wa kuweza kuanza kesi hiyo," alisema.

"Sasa wanasema wanahitaji muda zaidi." Kesi hiyo imeshacheleweshwa katika vipindi viwili tofauti.

Kiongozi huyo wa chama cha Unified Democratic Forces anatuhumiwa kula njama na aliyekuwa afisa wa jeshi la Kihutu kununua na kusambaza silaha za kutishia usalama wa taifa. Victoire amesema kuwa mashtaka hayo si ya kweli na yamechochewa kisiasa. Ikiwa atakutwa na hatia, huenda akapewa kifungo cha maisha.

Victoire ni Mhutu na wengi miongoni mwa 800,000 waliouawa kwenye ghasia za mwaka 1994 walikuwa ni Watutsi. Rais Paul Kagame, aliyekuwa kiongozi wa waasi wa chama cha Rwandan Patriotic Front (RPF) chenye Watutsi wengi alisitisha mauaji hayo ya kimbari, alishinda kwa kipindi cha pili cha urais Agosti mwaka jana kwa jumla ya asilimia 93 ya kura zote.

Ni nani huyu Victoire Ingabire?

Victoire Ingabire Umuhoza alizaliwa Oktoba 3, 1968, ni Mwenyekiti wa Unified Democratic Forces (UDF); muungano wa vyama vya upinzani nchini Rwanda. Alikuwa mgombea wa chama kwenye uchaguzi wa rais wa mwaka 2010, lakini alizuiliwa kuwania nafasi hiyo. Kwa sasa yupo chini ya ulinzi kwa madai ya ugaidi na kutishia usalama wa taifa.

Familia yake na kazi

Ameolewa na ni mama wa watoto watatu, amepata mafunzo katika sheria ya biashara na uhasibu na kufuzu katika uchumi na usimamizi wa biashara wa makampuni nchini Uholanzi. Victoire alifanya kazi kama afisa wa kampuni ya kimataifa ya uhasibu nchini Uholanzi ambapo alikuwa kiongozi wa idara ya uhasibu katika matawi 25 barani Ulaya, Asia na Afrika.

Mwezi Aprili 2009, alijiuzulu kazi na kujiingiza katika siasa na kujiandaa kurudi katika nchi yake, kama mkuu wa chama cha kisiasa, ili kuchangia katika ujenzi wa nchi yake. Januari 2010, Victoire alirejea nchini mwake, baada ya miaka 16 ya uhamishoni, kama kiongozi mkuu wa chama cha upinzani cha kisiasa nchini Rwanda.

Kazi ya siasa

Tangu mwaka 1997, Victoire amekuwa akishiriki katika mapambano ya kisiasa za upinzani nchini Rwanda akiwa uhamishoni. Amekuwa akinukuliwa kusema "Lengo langu ni kuiingiza Rwanda katika utawala wa sheria na hali ya kikatiba ambapo viwango vya kimataifa vya kidemokrasia vinaheshimiwa, ambapo uzalendo utakuwa msingi wa mwisho kwa taasisi zote za umma."

Shughuli zake za kisiasa zinazingatia wazo la haki ambapo watu binafsi watachagua vyama vyao kwa kuzingatia matarajio yao ya pamoja ya kisiasa badala ya ukabila au ukanda. Pia ameanzisha mijadala katika kutoa wito wa kuwapatia uwezo zaidi wanawake nchini Rwanda.

Mwaka 1997, alijiunga na Republican Rally for Democracy nchini Rwanda. Mwaka mmoja baadaye, akawa Rais katika tawi lake lililopo Uholanzi na mwaka 2000, aliteuliwa kuwa Rais wa RDR katika ngazi ya kimataifa. Kuanzia 2003 hadi 2006, alichukua nafasi ya Rais wa Unified Rwandan Democratic Forces (UFDR), ambao ni umoja wa vyama vya siasa vya upinzani na kuviongoza kutokea uhamishoni, ambapo RDR ni mwanachama hai.

Kupigania umoja wa kisiasa wa upinzani akiwa uhamishoni kuliongoza kazi yake ya kisiasa. Novemba 2004, jijini Amsterdam, Uholanzi aliandaa mkutano uliojulikana kama "Jukwaa la Amani, Usalama, Demokrasia na Maendeleo katika Ukanda wa Maziwa Makuu" ambalo lilifuatiwa na Mpango wa Amsterdam wenye lengo la kujenga jukwaa jipya kwa ajili ya ushirikiano.

Mnamo Oktoba 2005, Victoire alianzisha mawasiliano na vyama vingine vya upinzani na waliandaa mikutano yote ya umoja kwa ajili ya vyama vyote vya kiraia vya Rwanda na vyama vya siasa. Makubaliano ya kawaida dhidi ya utawala wa Paul Kagame hatimaye yalifikiwa.

Kuanzia Aprili 2006, alishiriki kwenye uanzishwaji wa Umoja wa vyama na alichaguliwa kuwa Rais wa ajenda ya kisiasa. Umoja huo ulikuwa na lengo la kuanzisha utawala wa sheria nchini Rwanda, kama heshima ya maadili ya kidemokrasia ilivyoainishwa katika Azimio la Haki za binadamu na haki nyingine za kimataifa zinazohusiana na demokrasia na utawala bora.

Victoire alishiriki kikamilifu katika mijadala inayoihusu Rwandaj Barcelona, ​​Hispania mwaka 2004, 2006 na mwezi Aprili - May 2009 kwa msaada wa Juan Carrero Saralegui, aliyeteuliwa kuwania tuzo ya Amani ya Nobel na Adolfo Pérez Esquivel, mshindi wa tuzo ya Amani ya Nobel, na Federico Mayor Zaragoza, Makamu wa Rais wa Muungano wa Asasi za Kiraia.

Alitoa mapendekezo yafuatayo na kutoa wito kwa mageuzi kwa ajili ya mabadiliko katika maisha ya kila siku ya Wanyarwanda wote na njia ya wao kuhusiana na siasa: Uanzishwaji wa Kamati ya Haki, Ukweli na Maridhiano kusaidia Wanyarwanda katika upatanisho wa kweli; Uanzishwaji wa tume ya mambo yasiyo ya kisiasa katika uandikwaji na kutafsiri historia halisi ya Rwanda; Kupitisha muswada wa haki ya umiliki binafsi na kwa ajili ya ulinzi wa wanachama dhaifu wa umma, kwa ajili ya dhamana ya kisheria ya fursa sawa na upatikanaji wa mikopo na ajira kwa wananchi wote.
Mwezi mmoja baada ya kuwasili Rwanda mnamo Januari 2010, pamoja na viongozi wengine wawili wa kisiasa wa upinzani nchini humo, alianzisha Baraza la Ushauri la Kudumu kwa Vyama vya Upinzani, kuweka pamoja juhudi zao za kuongeza nafasi za kisiasa kwa vyama vya upinzani na kwa kuimarisha mchakato wa kidemokrasia nchini Rwanda.

Victoire Ingabire Umuhoza ni mwanachama mwanzilishi wa vyama vingi na mashirika katika sekta ya muungano: Chama cha Mawasiliano, Dialogue et Hatua Caritatives (CODAC) ambacho kinataka kutoa maadili, ushauri wa kisheria na msaada wa vifaa kwa waathirika wa Kanda ya Maziwa Makuu nchini Uholanzi au katika maeneo yao; Chama cha URAHO cha wanawake wakimbizi kutoka Rwanda nchini Uholanzi, kinacholenga kupata wanawake wa Rwanda waliotengwa nje ya nchi na kuwaunganisha katika jamii ya Kiholanzi, kusaidia watoto na kuwatafutia hifadhi.

Chama cha PROJUSTITIA-Rwanda, kinachopigania haki sawa kwa waathirika wote wa janga la Rwanda; HARAMBE, jukwaa la vyama vya wanawake wa Afrika nchini Uholanzi kwa nia ya kukuza maendeleo ya wanawake katika bara la Afrika. Victoire pia alikuwa mwanachama wa kamati ya utendaji ya ZWALU, jukwaa linalowaleta pamoja wanawake wa kigeni nchini Uholanzi na kuendeleza ukombozi wao

Machapisho

Victoire ni mwandishi wa makala mbalimbali na machapisho ambapo yeye alionesha maoni yake juu ya masuala muhimu yanayohusiana na matukio ya sasa katika nchi yake na ile ya kanda ya Maziwa Makuu. Miongoni mwa hayo ni:
  • "What is the Outlook for Peace in Central Africa?" (2001),
  • "International Justice After the Crisis in Rwanda" (2002),
  • "Conflicts in the Great Lake region of Africa: Origins and Solution Proposals" (2003),
  • "National Reconciliation As a Requirement for Security and Sustainable Peace in Rwanda and in the Countries of the African Great Lakes" (2004),
  • "Pleading for a True National Reconciliation in Rwanda, Requirements for Sustainable Peace" (2005).

Makala hii imeandaliwa na Bishop J. hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

 

Sep 2, 2011

DOMINIQUE STRAUSS-KAHN: Kuutaka urais wa Ufaransa kulimponza

*Hata hivyo mahakama yamfutia mashitaka

 Dominique Strauss-Kahn

PARIS

JAJI ambaye alikuwa anasikiliza kesi ya tuhuma za ubakaji iliyokuwa inamkabili Mkurugenzi wa zamani wa Shirika la Fedha Duniani IMF, Dominique Strauss-Kahn, ametupilia mbali mashtaka hayo na hivyo kumuacha huru kigogo huyo.

Jaji Michael Obus alilazimika kuitupilia mbali kesi hiyo baada ya waendesha mashtaka kuwasilisha pendekezo la kufutwa kwa mashtaka hayo wakiamini hayana ukweli wowote na yalikuwa na lengo la kumchafua tu.

Baada ya Jaji Obus kutoa uamuzi huo ndipo Mwanasheria wa Strauss-Kahn, Benjamin Brafman, akachukua nafasi hii kuzungumza na waandishi wa habari ambapo alisema umma ulikosea kutokana na kuchukua hatua ya kuhukumu.

Naye Mwanasheria wa Nafissatou Diallo, Kenneth Thompson ametoa malalamiko kwa mahakama kwa hatua yake ya kutupilia mbali ombi lake la kuletwa kwa mwendesha mashtaka mwingine ambaye angesimamia kesi hiyo.

Strauss-Kahn mwenyewe baada ya kufutiwa mashtaka yaliyokuwa yanamkabili alimshuru mkewe pamoja na familia yake kwa kuwa naye pamoja kwenye kipindi kigumu cha kukabiliwa na tuhuma.

Hata hivyo, inasemekana kuwa Wafaransa wengi wanamuheshimu sana mwanasiasa huyu mwenye mwendo wa madaha, ambaye ni mashuhuri kwa jina la mkato la DSK. Mwenyewe amewahi kusema kwamba ana udhaifu katika mambo matatu: pesa, wanawake na uyahudi wake.

Upande mmoja wa familia ya Dominiques Strauss-Kahn ni Mayahudi wenye asili ya Morocco, nchi ya Kaskazini mwa Afrika na iliyokuja kuwa miongoni mwa makoloni ya Hispania.

Dominique Gaston Andre Strauss-Kahn alizaliwa Aprili 25, 1949 katika eneo la Neuilly Sur-Sein, karibu na mji mkuu wa Paris, Ufaransa. Amekulia Morocco kabla ya kuhamia Monaco na kusomea baadaye mjini Paris.

Mara nyingi akijulikana katika vyombo vya habari kama DSK, ni Profesa wa kiuchumi wa Ufaransa, mwanasheria, na mwanasiasa, na mwanachama wa Chama cha Kisoshalisti cha mrengo wa kushoto. Amekuwa pia akiwika katika jukwaa la kisiasa nchini Ufaransa kwa miongo miwili sasa.

Strauss-Kahn alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha Duniani (IMF) tangu tarehe 28 Septemba 2007, kwa msaada wa Rais Nicolas Sarkozy, na ametumikia katika nafasi hiyo hadi alipojiuzulu tarehe 18 Mei 2011.

Mei 2011, Strauss-Kahn alikamatwa katika mji wa New York na kushtakiwa kwa unyanyasaji wa kijinsia wa mfanyakazi wa hoteli aliyeingia chumbani kwake, lakini mashitaka yote yalifutwa baadaye kwa ombi la upande wa mashtaka. Strauss-Kahn alikana mashtaka yote. Mwanasheria wa Wilaya ya New York aliondoa mashtaka tarehe 22 Agosti 2011, kutokana na upande wa mlalamikaji kushindwa kuthibitisha, na mahakama ilikubali.

Strauss-Kahn au DSK, kama ulivyo umaarufu wake kwenye siasa za Ufaransa, alifuata nyayo za wazee wake na kuelemea mrengo wa kushoto. Alijiunga mapema na Chama cha Kisoshialisti ambacho mnamo mwaka 1971 kilikuwa nguvu muhimu ya mrengo wa kushoto uliokuwa ukiongozwa na Francois Mitterand.

Katika miaka ya ’80 na ’90 alikabidhiwa nyadhifa tofauti za kisiasa, hadi mnamo mwaka 1997 alipochaguliwa kuwa Waziri wa Uchumi, Fedha na Viwanda.

Yeye ndiye aliyetandika misingi ya Ufaransa kuweza kujiunga na sarafu ya euro. Wengi wanakiri kwamba Strauss-Kahn alifanikiwa kuunganisha mawazo yakinifu ya kiuchumi na yale ya ujamaa wa kidemokrasia. Kwa mfano, yeye ndiye aliyepunguza muda wa kufanya kazi kwa wiki na wakati huo huo kuanzisha utaratibu wa kubinafsishwa mashirika ya serikali.

Mnamo mwaka 1999, Strauss-Kahn alijiuzulu kwa tuhuma za kuhusika na rushwa, ingawa baadaye alitakaswa na tuhuma hizo. Baada ya kujizulu, DSK alikuwa akijishughulisha zaidi na kazi yake ya kusomesha kwenye vyuo vikuu.

Miongoni mwa mengineyo, alikabidhiwa jukumu la kusimamia chuo kikuu mashuhuri cha Institut d’Etudes Politiques (IEP), ambako binafsi ndiko alikosomea. Wakati huo huo akateuliwa kuwa mshauri wa Shirika la Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo barani Ulaya (OECD).

Staruss-Kahn alirejea katika jukwaa la kisiasa mwaka 2001 na kuongoza kampeni ya uchaguzi ya Lionel Jospin mnamo mwaka 2002 alipopigania kuwa rais wa Ufaransa.

Akiwa mbunge, Strauss-Kahn alipigania sana masuala yanayohusu Ulaya na kuunga mkono ushirikiano kati ya Ujerumani na Ufaransa kama injini ya Umoja wa Ulaya. Yeye alikuwa miongoni mwa wale waliokuwa wakiunga mkono katiba ya Umoja wa Ulaya iliyokataliwa na Ufaransa mnamo mwaka 2005.

Magazeti ya Ufaransa yakiandika taarifa za kashfa ya Strauss-Kahn; baada ya kukaa kwenye upande wa upinzani kwa miaka kadhaa, Strauss-Kahn akajitokeza kutaka kupigania kiti cha rais mwaka 2006 kwa tiketi ya chama chake cha Kisoshalisti cha mrengo wa kushoto, lakini alishindwa na Ségolène Royal. Wakati huo, Strauss-Kahn alikuwa akifikiria umuhimu wa kuunda chama kipya cha mrengo wa kushoto.

Lakini kabla ya kufanya hivyo, akajikuta anateuliwa kuwa mkuu wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), akiwa amependekezwa na mpinzani wake wa kisiasa, Rais Nicolas Sarkozy.

Lakini mara tu baada ya kuchaguliwa kuongoza shirika hilo, IMF ikakafanya uchunguzi dhidi ya kiongozi wake mpya. Lengo lilikuwa kutaka kujua ikiwa bosi huyo alitumia vibaya madaraka yake na kumpendelea mtaalamu wa kike wa kiuchumi, Piroska Nagy.

Naggy, ambaye alisemekana kuwa na uhusiano na Strauss-Kahn, alikubali kupokea fidia mnamo Agusti mwaka 2008 na kuacha kazi yake kutoka IMF.

Baada ya Straúss-Kahn kuomba radhi wakati ule, baraza la shughuli za utawala likapiga kura kwa sauti moja kumruhusu kuendelea na kazi yake. Uchunguzi haukutoa ushahidi wowote wa madai ya kutumia vibaya madaraka yake.

Februari mwaka 2010, Strauss Kahn alisema katika mahojiano ya radio kwamba anaweza kuamua kutetea kiti cha rais kwa tiketi ya Chama cha Kisoshalisti dhidi ya Rais Sarkozy wa kutoka chama tawala cha UMP na, kwa hivyo, kuachana na IMF kabla ya wakati wake kumalizika.

Maisha binafsi

Strauss-Kahn amemuoa mwandishi habari na mtangazaji wa televisheni, Anne Sinclair, tangu mwaka 1991. Ana watoto wanne wa kike kutoka ndoa zake mbili za mwanzo, mmoja kati yao ni kwa mke wake wa pili, Brigitte Guillemette, aliyemuoa mwaka 1984.

Ukiacha lugha yake ya Kifaransa, anazungumza pia kwa ufasaha Kiingereza na Kijerumani na pia ana ujuzi mzuri wa Kihispania na Kiarabu.

Nafasi muhimu alizoshika

  • Waziri wa Viwanda na Biashara ya Nje, 1991-1993.
  • Waziri wa Fedha, Uchumi na Viwanda, 1997-1999 (kujiuzulu).
  • Mbunge wa Bunge la Ufaransa kupitia Val d'Oise, 1986-1991 (na waziri 1991), akachaguliwa tena 1997, kisha akawa waziri 2001-2007 (alijiuzulu baada ya kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa IMF 2007).
  • Alichaguliwa tena miaka ya 1986, 1988, 1997, 2001, 2002, 2007.
  • Diwani wa Mkoa wa Ile-de-France, 1998-2001 (kujiuzulu).
  • Meya wa Sarcelles, 1995-1997 (kujiuzulu).
  • Naibu meya wa Sarcelles, 1997-2007 (alijiuzulu baada ya kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa IMF 2007), akachaguliwa tena mwaka 2001.
  • Diwani wa manispaa ya Sarcelles, 1989-2007 (alijiuzulu baada ya kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa IMF 2007), alichaguliwa tena 1995, 2001.
  • Rais wa jamii wa Agglomeration katika Val de France, 2002-2007 (alijiuzulu baada ya kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa IMF 2007).
  • Mwanachama wa jumuiya ya Agglomeration wa Val de France, 2002-2007 (alijiuzulu baada ya kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa IMF 2007).
  • Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Fedha Duniani, 2007-2011 (alijiuzulu kwa tuhuma za shambulio la ngono).

Makala hii imeandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa