Dec 28, 2011

Mwaka 2011 ndiyo mwisho wa mashambulizi ya al-Qaida?

Aliyekuwa kiongozi wa al-Qaida, Osama bin Laden

Wanachama wa al-Qaida

BISHOP HILUKA
Dar es salaam

TUKIWA tunaumaliza mwaka huu hapo kesho na kuuanza mwaka mwingine siku ya Jumapili, bado kuna kumbukumbu zilizotikisika dunia. Kumbukumbu hizo ni pamoja na nguvu za umma zilizowang’oa baadhi ya viongozi waliokita mizizi katika nchi za Kiarabu, na kifo cha kiongozi wa kundi la al-Qaida, Osama bin Laden.

Kifo cha bin Laden ndicho kilichotikisa zaidi dunia kwani baada ya kifo chake dunia ilitawaliwa na hofu. Kuna walioamini kuwa baada ya kifo hicho, kundi la al-Qaida litakuwa limesambaratika, lakini wengine wakihofu ghadhabu zaidi kutoka kwa wafuasi wa kundi hilo. Uingereza na nchi nyingine za Magharibi zinaendelea kuchukua tahadhari kutokana na hofu kwamba mauaji ya Osama yanaweza kuibua mashambulizi mapya ya ugaidi. Tanzania tulionja adha ya al-Qaeda pale Ubalozi wa Marekani jijini Dar es Salaam uliposhambuliwa kwa bomu na kusababisha vifo kadhaa. Lakini sijui kama kufuatia shambulizo hilo tumekuwa tunachukua tahadhari stahili baada ya kifo cha Osama ingawa kwa siku za karibuni tumekuwa macho dhidi ya ‘watoto’ wa al-Qaeda wanaotokea Somalia kwa jina la al-Shabab.

Kwa Uingereza, baada ya kifo cha Osama Wizara ya Mambo ya Nje, ilitoa tahadhari kwa raia wake wanaoishi nje kufuatilia vyombo vya habari ndani ya nchi walimo kuangalia wanavyochukulia, kuuawa kwa Osama na wawe macho. Pamoja na hali hiyo Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza, William Hague, aliziamuru balozi zote za Uingereza kupitia upya mpangilio wao wa ulinzi na usalama. Hakuna uchunguzi wa kiintelijensia ulioonesha shambulio  lolote dhidi ya Uingereza hivyo kiwango cha ugaidi kikabakia kuwa 'kikali'.

Wataalamu wa masuala ya ulinzi waliamini kwamba katika muda mfupi tishio kubwa lingeweza kuwa kwa raia wa nchi za Magharibi na hata mali na maslahi yao nje ya nchi na hususani kwenye maeneo ya Mashariki ya Kati na Asia. Kufuatia hali hiyo Polisi wa Kimataifa (Interpol) walichukua hatua ya kuonya kuhusu kuongezeka kwa kiwango cha mashambulizi ya kigaidi na kuutaka umma kuwa macho.

Mashambulizi ya Osama na al-Qaeda  

Baadhi ya mashambulizi ya kigaidi ambayo yameshafanywa na mtandao wa al-Qaeda chini ya Osama bin Laden yalitokea kati ya 1993 na 2011 ni pamoja na kulipuliwa kwa gari kwenye Kituo cha Kimataifa cha Biashara Oktoba mwaka 1993, jijini New York ambapo watu sita waliuawa.

Juni 1996 kulipuliwa lori lililokuwa na mafuta kwenye eneo la Khobar, Saudi Arabia kwenye ubalozi wa Marekani ambalo lilisababisha vifo vya askari 19 wa Marekani na kujeruhi watu 400. Agost 1998 mabomu kwenye balozi za Marekani kwenye miji ya Dar es Salaam na Nairobi yalilipuka na kuua wa 224 wakiwemo Wamarekani 12. Oktoba 2000 shambulizi la mabomu dhidi ya meli ya kivita ya Marekani kwenye bandari ya Aden lilisababisha vifo vya mabaharia 17.  

Septemba 11, 2001, magaidi 19 waliziteka ndege nne za abiria na kuzielekeza kugonga minara pacha ya Kituo cha Biashara duniani (WTC) ambayo iliteketea na kuangamiza, saa mbili baadaye, ndege ya tatu  ilielekezwa kwenye  jengo la makao makuu ya jeshi la Marekani Pentagon jijini Washington. Ndege ya nne iliianguka kwenye  uwanda wa Pennsylvania. Katika shambulizi hilo kwenye minara pacha ya WTC takribani watu 3,000 na waliokuwa kwenye ndege  waliuawa. 

Oktoba 7, 2001, kwenye kanda ya video iliyooneshwa na Televisheni ya Al Jazeera, Osama alisikika akisema kuwa Marekani haitaishi kwa amani hadi hapo Palestina nao watakapoishi kwa amani. Mwanzoni mwa mwaka 2002, mwandishi wa habari wa gazeti la Wall Street Journal, Daniel Pearl, alitekwa nyara nchini Pakistan na baadaye aliuawa kwa kukatwa kichwa na video yake kurekodiwa na al-Qaeda.

Aprili 11, 2002; lori lililipuka karibu na sinagogi la El Ghriba kwenye kisiwa cha Djerba, Tunisia kusini na kuua Wajerumani 14, raia watano wa Tunisia na Mfaransa mmoja, ambapo al-Qaeda ilidai kuhusika na shambulizi hilo. Oktoba 12, 2002 bomu lililipuka kwenye klabu ya usiku kwenye ufukwe wa Kuta, Bali nchini Indonesia na kuua watu 202 tukio hilo lilifanywa na kundi la Jemaah Islamiyah, linalohusiana na al-Qaeda.

Novemba  28, 2002 shambulizi la kujitoa mhanga lililipua  hoteli inayotumiwa sana na Waisreali nchini Kenya mjini Mombasa na kuua watu 15. Siku hiyo hiyo mizinga miwili nusura ilipue ndege ya Boeing 757 ya Israeli ikiwa na abiria 261 wakati ikiondoka kwenye uwanja wa ndege wa Mombasa na al-Qaeda wakadai kuhusika.

Mei 12, 2003 watu 35 wakiwemo Wamarekani tisa waliuawa kwenye uwanja wa Riyadhi, Saudi Arabia na mlipuko mwingine ukatokea Casablanca, Morroco na kuua watu 45 wakiwemo walipuaji 13 na kujeruhi  watu 60. Agosti na Septemba 2003 ulipuaji wa Hoteli ya Canal ambayo ilikuwa inatumika kama makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini Baghdad na kuua watu 22 akiwemo balozi wa Umoja wa Mataifa, Sérgio Vieira de Mello.

Machi 11, 2004 milipuko mfululizo wa mabomu kwenye treni mjini Madrid ilisababisha vifo vya watu zaidi ya 200 na kujeruhi wengine 1,500. Julai 7, 2005 watu wanne walijitoa mhanga na kuua watu 52 katika shambulio lililofanyika kwenye treni ipitayo chini ya ardhi.

Aprili 11, 2007 mabomu ya kujitoa mhanga yalisababisha vifo vya watu 33 katikati ya Algiers na shambulizi jingine lilifanyika Desemba ambapo milipuko miwili ilisababisha vifo vya watu 41 wakiwemo maofisa 17 wa Umoja wa Mataifa kwenye ofisi ya Umoja wa Mataifa mjni Algiers. Aprili 28, 2011, mlipuko wa bomu ulisababisha vifo vya watu 15 wakiwemo wageni kumi mjini Marrakesh, Morroco.

KIM JONG-UN: Mrithi wa utawala Korea Kaskazini aliyewapiku kaka zake wakubwa

Kim Jong-un

PYONGYANG
Korea

KIM Jong-un, mtoto wa kiongozi wa Korea Kaskazini aliyefariki, Kim Jong-il, ametajwa kuwa ndiye kamanda mkuu kabisa wa jeshi lenye nguvu la taifa hilo la kikomunisti.

Gazeti la chama tawala nchini humo limetoa wito kwa Kim Jong-un kuiongoza Korea Kaskazini kufikia ushindi wa daima. Hii ni mara ya kwanza kwa shirika la habari la taifa kumtaja kiongozi huyo kuwa kamanda mkubwa kabisa.

Kabla ya hapo aliitwa mrithi mkubwa kabisa, baada ya baba yake kufariki. Gazeti hilo limeahidi kuunga mkono sera iitwayo "songun", yaani jeshi ndio muhimu kabisa, sera inayoyapa kipaumbele matumizi juu ya jeshi la Korea Kaskazini.

Historia yake

Kim Jong-un ambaye pia anajulikana kama Kim Jong-Eun, zamani aliitwa Kim Jong-Woon, alizaliwa tarehe 8 Januari 1983 au 1984, ni mtoto wa tatu wa marehemu kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong-il na mke wake Ko Young-hee. Tangu mwishoni mwa 2010, Kim Jong-un alionekana dhahiri kuwa ndiye mrithi wa uongozi wa taifa, na hivyo kufuatia kifo cha baba yake, alitangazwa kama "mrithi mkuu" na kituo cha televisheni cha taifa. Tarehe 24 Desemba 2011, alitangazwa kuwa Kamanda Mkuu wa Jeshi la Watu wa Korea Kaskazini.

Ni Daejang katika Jeshi la Watu wa Korea, kijeshi cheo hicho ni sawa na Jenerali. Inasemwa kuwa Kim alisomea sayansi ya kompyuta kibinafsi nchini Korea ya Kaskazini. Alipata shahada mbili, moja katika fizikia kutoka katika Chuo Kikuu cha Kim Il Sung na nyingine katika Chuo cha Kijeshi cha Kim Il Sung.

Maisha ya awali

Kim anadhaniwa kuwa alizaliwa mwaka 1983 au 1984. Vyanzo vya Usalama vinasema tarehe ya kuzaliwa kwake ni tarehe 8 Januari 1984.

Alihudhuria mafunzo ya lugha ya Kiingereza katika Shule ya Kimataifa ya Bern, Uswisi, hadi 1998 kwa kutumia jina bandia. Wanafunzi wenzake wa zamani wameelezea kuwa alisoma katika Shule ya Kimataifa ya Gümligen au shule ya umma ya Liebefeld. Jina alilotumia akiwa Gümligen lilikuwa "Pak Chol" na alidai kuwa yeye ni mtoto wa dereva, ingawa hapo Liebefeld, mwalimu wa darasa aliwaambia wanafunzi kuwa anatoka Korea ya Kaskazini.

Kim anaelezewa kuwa alikuwa mtoto mwenye aibu aliyeepuka kujichanganya na watu asiowafahamu na alikuwa anajulikana kwa tabia yake ya ushindani, hasa katika michezo, na alivutiwa sana na liga ya mpira wa kikapu ya Marekani (NBA) huku akimhusu sana mchezani wa kimataifa wa nchi hiyo wa mpira wa kikapu, Michael Jordan. Moja wa marafiki zake alidai kuwa alikutana na hata kupiga picha na Kobe Bryant na Toni Kukoč, lakini hana uhakika alipiga picha wapi na wakali hao katikaNBA. Aliripotiwa kukaa Uswisi – akiwa hafungamani na upande wowote katika mgogoro kati ya Korea Kaskazini na Kusini, hadi mwishoni mwa mwaka 1999 au mapema 2000 wakati mwanafunzi mmoja alipodai "kutoweka" kwake shuleni hapo.

Balozi wa Korea Kaskazini nchini Uswisi, Ri Tcheul, alikuwa na uhusiano wa karibu na Kim na alikuwa mshauri wake. Familia ya Kim inasemekana iliandaa mikutano ya kifamilia katika Ziwa Geneva na Interlaken.

Kwa miaka mingi, ni mmoja tu aliyethibitisha picha ya Kim kwamba alikuwa anajulikana pia nje ya Korea Kaskazini, na inaonekana kupigwa katika miaka ya 1990, alipokuwa na miaka kumi na moja. Ni Juni 2010 tu, muda mfupi kabla ya kupewa rasmi nafasi ya kutambulishwa hadharani kwa watu Korea Kaskazini, picha zaidi za Kim zilinyeshwa, na hasa zilichukuliwa wakati alipokuwa akisoma nchini Uswisi. Picha yake rasmi ya kwanza katika utu uzima ilikuwa ni picha ya kikundi iliyotolewa tarehe 30 Septemba, 2010 mwishoni mwa mkutano wa chama ikielezea ufanisi wake, ambayo yeye ameketi katika mstari wa mbele, nafasi mbili kutoka kwa baba yake. Hii ilifuatiwa na picha zake za kuhudhuria mkutano huo.

Kaka yake mkubwa, Kim Jong-nam, ndiye mwanzoni alirakuwa kuwa mrithi, lakini imeripotiwa alipoteza sifa baada ya mwaka 2001, alipokamatwa akijaribu kuingia Japan kwa kutumia hati bandia ya kusafiria ili kutembelea Tokyo Disneyland.

Mpishi binafsi wa zamani wa Kim Jong-il, Kenji Fujimoto, amemebainisha maelezo kuhusu Kim Jong-un, ambaye alikuwa na uhusiano naye mzuri, na kusema kwamba aliandaliwa kuwa mrithi wa baba yake. Fujimoto pia alidai kuwa Jong-un alipendekezwa na baba yake kati ya ndugu yake, Kim Jong-chul, na sababu kubwa Jong-chul ana tabia za kupenda sana wanawake, wakati Jong-un ni "kama baba yake hasa".

Fujimoto alisema zaidi kuwa "Kama madaraka yatakabidhiwa basi ni Jong-un anayefaa. Amejengeka kimwili, ni mnywaji mkubwa na kamwe hakubali kushindwa."  Wakati Jong-un alipokuwa na miaka 18, Fujimoto alielezea tukio ambapo Jong-un alihoji kuhusu maisha yake ya kifahari, akamwuliza, "Tupo hapa, tunacheza mpira wa kikapu, tunaendesha farasi, tunaendesha Skis Jet, tuna furaha. Lakini vipi kuhusu maisha ya watu wasio na uwezo na wasiopata fursa kama hizi zetu?"

Januari 15, 2009 shirika la habari la, Yonhap la Korea Kusini, lilitoa taarifa kwamba Kim Jong-il amemteua Kim Jong-un kuwa mrithi wake.

Machi 8, mwaka 2009, BBC ilitangaza kuwepo uvumi kuwa Kim Jong-un alionekana kwenye kura kwa ajili ya uchaguzi wa Bunge Kuu la Watu, bunge la Korea Kaskazini. Baadaye taarifa zilionesha kuwa jina lake halikuwa katika orodha ya watunga sheria. Hata hivyo, baadaye alipandishwa katika nafasi ya kati katika Tume ya Taifa ya Ulinzi, ambayo ni tawi la kijeshi la Korea Kaskazini.

Kuhusu afya yake licha ya kujengeka kimwili, ripoti pia zimefichua kuwa Jong-un ni mgonjwa wa kisukari na anakabiliwa na shinikizo la damu.

Kuanzia mwaka 2009, ilieleweka kwa diplomasia za nje kwamba Kim alikuwa mrithi wa baba yake Kim Jong-il kama mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Korea na kiongozi wa Korea ya Kaskazini. Baba yake pia aliwataka wafanyakazi wa balozi nje ya nchi kuwa waaminifu kwa mtoto wake. Pia kulikuwepo taarifa kuwa wananchi wa Korea ya Kaskazini walihimizwa kuimba "wimbo wa sifa" kwa Kim Jong-un, kwa mtindo sawa na ule wa nyimbo za sifa zinazohusiana na Kim Jong-il na Kim Il-sung.

Baadaye mwezi Juni, Kim aliripotiwa kutembelea China kwa siri na "kujitambulisha mwenyewe" kwa uongozi wa China, ambao baadaye walionya dhidi ya Korea ya Kaskazini kufanya jaribio lingine la kinyuklia. Wizara ya Nje ya China ilikanusha vikali kuwepo ziara hii.

Baada ya kifo Kim Jong-il

Desemba 17, 2011, Kim Jong-il alifariki.  Pamoja na mipango ya Kim mkubwa, haikufahamika mara moja baada ya kifo hicho kama Jong-un atachukua madaraka kamili, na nini nafasi yake kamili katika serikali mpya. Baadhi ya wachambuzi waliamini kwamba baada ya kifo cha Kim Jong-il, Chang Sung-taek angechukua hatua kama mtawala wa muda, kwa kuwa Jong-un hana uzoefu wa kuongoza nchi na bado ni ‘mtoto’.

Lakini kwa sasa ametangazwa hadharani kuwa Kamanda Mkuu wa Jeshi la Watu wa Korea, Jumamosi ya tarehe 24 Desemba 2011, hatua inayoonesha kuwa atatwa madaraka ya nchi punde.

Makala haya yameandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

Dec 21, 2011

KIM JONG-IL: Kifo chake chazua simanzi kubwa, masoko ya hisa ya Asia yashuka

Kim Jong-il

PYONGYANG
Korea

KIONGOZI wa Korea Kaskazini, Kim Jong-il, aliyefariki dunia kwa mshtuko wa moyo katika umri wa miaka 69 au 70, amesababisha mamia  ya raia wa Korea Kaskazini kugubikwa na huzuni isiyoelezeka, na wameonekana wakimlilia kiongozi wao huyo waliyempachika jina la ‘Kiongozi Mpendwa’ katika mji mkuu Pyongyang.

Mwanaye wa tatu, Kim Jong-un anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 28, ameelezewa na Shirika la habari la Korea Kaskazini (KCNA) kuwa atakuwa "mrithi mkuu" ambaye Wakorea Kaskazini hawana budi kumuunga mkono na kuwa nyuma yake. Raia jirani wa Pyongyang wako katika hali ya tahadhari, ambapo taarifa zisizothibitishwa kutoka Korea Kusini zinasema kuwa Korea Kaskazini imefanya majaribio ya nyuklia Jumatatu wiki hii.

Shirika la habari la Yonhap mjini Seoul, lillisema kuwa kombora la nyuklia la masafa mafupi lilitupwa pwani ya mashariki ya nchi hiyo maskini iliyojitenga na yenye kumiliki nyuklia lakini haikujulikana haraka iwapo jaribio hilo linahusiana na tangazo la kifo cha Kim Jong-il.

Korea Kusini imeweka silaha zake kwa tahadhari baada ya tangazo hilo, ikisema nchi hiyo ilikuwa kwenye mgogoro unaofukuta. Serikali ya Japan imefanya mkutano wa dharura. Uhusiano wa China na Korea Kaskazini na wabia katika biashara walionesha kushtushwa na habari za kifo hicho na kuahidi kuendeleza na kuimarisha "mchango wa amani na utulivu katika rasi ya ukanda huo."

Tangazo la kifo cha Kim Jong-il lilitolewa kwa kusomwa kupitia televisheni ya Taifa huku mtangazaji, akiwa na mavazi meusi, alijitahidi kuzuia machozi wakati akisema kuwa Kim Jong-il alikufa kutokana na kufanya kazi za nguvu na kiakili kupita kiasi.

Baadaye shirika la habari la KCNA likaripoti kuwa alikufa kutokana na "maumivu makali ya kifua yaliyoambatana na mshtuko wa moyo (myocardial infarction)" saa mbili na nusu siku ya Jumamosi kwa saa za Korea. Wakati huo alikuwa kwenye treni katika moja ya ‘safari zake elekezi vijijini’, KCNA lilisema.

Historia yake

Kim Jong-il alizaliwa 16 Februari 1941. Alikuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Korea, chama tawala tangu 1948, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Ulinzi ya Korea ya Kaskazini, na kamanda mkuu wa Jeshi la Watu wa Korea, jeshi la nne kwa ukubwa duniani.

Aprili 2009, katiba ya Korea Kaskazini ilifanyiwa marekebisho ili kumuunga mkono kama "kiongozi mkuu". Pia alijulikana kama "Kiongozi Mpendwa", "Baba yetu", na "Mkuu". Mtoto wake, Kim Jong-un, alipandishwa cheo na kuwa katika nafasi za juu katika Chama cha Wafanyakazi na mrithi wake. Mwaka 2010, alikuwa katika nafasi ya 31 katika Orodha ya Watu wenye nguvu zaidi duniani kwa mujibu wa jarida la Forbes.

Kuzaliwa

Maelezo ya kuzaliwa kwa Kim Jong-il yanatofautiana kulingana na vyanzo tofauti. Kumbukumbu za Urusi zinaonesha kwamba alizaliwa katika kijiji cha Vyatskoye, karibu na Khabarovsk, mwaka 1941, ambako baba yake, Kim Il-sung, aliongoza Battalion ya 1 katika Brigade ya 88 ya Kisoviet. Mama wa Kim Jong-il, Kim Jong-suk, alikuwa mke wa kwanza wa Kim Il-sung.

Wasifu rasmi wa Kim Jong-il unasema kwamba alizaliwa katika kambi ya jeshi la siri katika milima ya Baekdu mpakani mwa Japan na Korea tarehe 16 Februari 1942. Waandika wasifu walidai kwamba kuzaliwa kwake katika milima ya Baekdu kulitabiriwa, na kuonekana kwa upinde wa mvua mara mbili juu ya mlima na nyota mpya katika mbingu.

Mwaka 1945, Kim alikuwa na miaka mitatu au minne wakati Vita Kuu ya Pili ikiishia na Korea ikipata uhuru kutoka Japan. Baba yake alirejea Pyongyang mnamo Septemba, na mwishoni mwa Novemba Kim akarudi Korea kwa meli ya Urusi, akifikia Sonbong. Familia ilihamia katika nyumba ya afisa wa zamani wa Kijapani mjini Pyongyang, yenye bustani na bwawa la kuogelea. Ndugu wa Kim Jong-il, "Shura" Kim (Kim Pyong-il wa kwanza), alikufa maji kwenye bwawa hilo mwaka 1948. Taarifa ambazo hazijathibitishwa zinaonesha kwamba Kim Jong-il  aliyekuwa na miaka mitano huenda alisababisha kifo hicho. Mwaka 1949, mama yake alikufa katika uzazi. Taarifa zisizothibitishwa zinaonesha kwamba mama yake huenda alipigwa risasi na kutokwa na damu nyingi kulikosababisha kifo.

Elimu

Kwa mujibu wa wasifu wake rasmi, Kim alipata elimu yake kati ya Septemba 1950 na Agosti 1960. Alihudhuria Shule ya Msingi na Shule ya Kati mjini Pyongyang. Lakini wasomi wa kigeni wanaamini uwezekano wa kuwa alipata elimu yake ya awali nchini China kama tahadhari ili kuhakikisha usalama wake wakati wa vita vya Korea.

Wakati akisoma, Kim alishirikishwa katika siasa. Alishiriki kikamilifu katika Umoja wa Watoto na Jumuia ya Vijana, akishiriki katika makundi ya masomo ya nadharia za kisiasa na maandiko mengine ya ki-Marxist. Septemba 1957 akawa makamu mwenyekiti wa Jumuia ya vijana wa tawi la shule.

Kim pia alipata elimu ya lugha ya Kiingereza katika Chuo Kikuu cha Malta katika miaka ya 1970, katika siku za sikukuu katika Malta akiwa mgeni wa Waziri Mkuu, Dom Mintoff.

Kim mkubwa wakati huohuo alioa tena na kupata mtoto mwingine, Kim Pyong-il (alimpa jina la ndugu wa Kim Jong-il aliyekufa maji). Tangu 1988, Kim Jong-il alifanya kazi katika balozi za Korea Kaskazini katika Ulaya na ubalozi wa Korea Kaskazini nchini Poland. Wachambuzi wa kigeni wanahisi kuwa Kim Jong-il alipelekwa kutumikia nafasi hizi mbali na nchi yake na baba yake ili kuepuka kugombea madaraka kati ya watoto wake wawili.

Baadhi ya vyanzo vya Korea Kaskazini vinasema Kim Jong-il aliteuliwa kuwa mrithi mnamo Februari 1974. Kim Pyong-il aliingia madarakani kufuatia kifo cha baba yake, Kim Il Sung mnamo Julai 8, 1994.

Mahusiano ya Nje

Mwaka 1998, Rais wa Korea Kusini, Kim Dae-jung, alitekeleza Sera ya "kuboresha mahusiano” ya Kaskazini na Kusini na kuruhusu makampuni ya Korea Kusini kuanza miradi Kaskazini. Kim Jong-il alitangaza mipango ya kuagiza na kuendeleza teknolojia mpya ili kuendeleza programu ya teknolojia nchini Korea Kaskazini. Matokeo ya sera mpya, eneo la viwanda la Kaesong Park lilijengwa mwaka 2003 kaskazini ya eneo la de-jeshi, pamoja na mpango wa ushiriki wa makampuni 250 ya Korea Kusini, na kuajiri Wakorea Kaskazini 100,000, mwaka 2007. Hata hivyo, Machi 2007, eneo hilo lilikuwa na makampuni 21 tu – na kuajiri wafanyakazi Wakorea Kaskazini 12,000. Mei 2010 zilipatikana ajira kwa wafanyakazi zaidi ya 40,000 wa Korea Kaskazini.

Mwaka 1994, Korea ya Kaskazini na Marekani zilisaini makubaliano ya kufunga mpango wa silaha za nyuklia kwa Korea Kaskazini ili kupatiwa misaada katika kuzalisha nishati ya nyuklia. Mwaka 2002, serikali ya Kim Jong-il ilikiri kuzalisha silaha za nyuklia tangu makubaliano ya 1994. Utawala wa Kim ulisema uzalishaji wa siri ulikuwa muhimu kwa ajili ya usalama - akionesha Marekani inavyomiliki silaha za nyuklia nchini Korea ya Kusini na mvutano mpya na Marekani chini ya Rais George W. Bush. 9 Oktoba 2006, Shirika la Habari la Korea Kaskazini lilitangaza kwamba kulikuwa na mafanikio ya majaribio ya nyuklia.

Ziara za kigeni 2010 na 2011

Kim aliripotiwa kutembelea Jamhuri ya Watu wa China Mei 2010. Aliingia katika nchi hiyo akiwa kwenye treni binafsi tarehe 3 Mei, na kukaa katika hoteli mjini Dalian. Mei 2010, Naibu Waziri wa Marekani wa Mambo ya Mashariki ya Asia na Pacific, Kurt Campbell, aliwaambia maafisa wa Korea Kusini kwamba Kim alikuwa na miaka mitatu tu ya kuishi. Kim alisafiri hadi China tena Agosti 2010, wakati huu akiwa na mwanaye, uvumi ulienea kwamba alikuwa tayari kukabidhi madaraka kwa mwanaye, Kim Jong-un. Alirejea China tena Mei 2011, kwenye sherehe ya miaka 50 ya kutiliana saini mkataba wa urafiki, Ushirikiano na Usaidizi baina ya China na Jamhuri ya Korea Kaskazini. Mwishoni mwa Agosti 2011, alisafiri kwa treni kwenda Urusi kukutana na Rais Dmitri Medvedev kwa ajili ya mazungumzo yasiyojulikana.

Maisha binafsi

Hakuna taarifa rasmi zilizopatikana kuhusu maisha ya ndoa ya Kim Jong-il, lakini anaaminika kuoa mara moja na amewahi kuwa na wanawake kadhaa. Ana watoto wanne, wakiume watatu: Kim Jong-nam, Kim Jong-chul na Kim Jong-un, na mtoto wa kike, Kim Sul-song.

Makala haya yameandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

Dec 14, 2011

Inashangaza pale mwakilishi wa watu anapokosa busara kwa sababu ya posho

Peter Selukamba, mbunge wa Kigoma Mjini (CCM)

Nape Nnauye, Katibu Mwenezi wa CCM

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

MIAKA hamsini ya uhuru wa nchi yetu inashuhudia kutamalaki kwa ufisadi nchini mwetu, ufisadi ambao umekua na kustawishwa na mfumo uliohalalishwa na watawala, ingawa ni watawala haohao wanaojivuna kupambana na ufisadi, huku wakija na kaulimbiu ya “Tumethubutu, Tumeweza na Tunasonga mbele”.

Kwa utamaduni huu waliojiwekea watawala wetu wa posho za vikao hata kwa mikutano ya kikazi ya idara katika mfumo mzima wa serikali, taasisi na mashirika yake, hakuna tofauti kabisa na ufisadi tunaoupigia kelele. Na sasa kuna viongozi wanaojitokeza kutetea ongezeko la posho za vikao kwa kiwango hiki cha kutisha kutoka sh 70,000/ kwa siku hadi sh 200,000/ kwa siku. Watafiti wanasema kwamba kwa ongezeko hilo, Bunge likiketi mbunge atakuwa anaingiza jumla ya 330,000/- kwa siku!

Inashangaza sana kuona mbunge aliyechaguliwa na wananchi masikini na anayewakilisha jimbo masikini zaidi kujisifu kwa uadilifu kwamba ametumwa na watu wa jimbo lake kuwatetea, lakini anainuka na kutetea/kuhalalisha ufisadi huu kwa kisingizio cha ugumu wa maisha mjini Dodoma ambako Bunge hufanya mikutano yake! Je, mbunge huyo anategemea pesa zitoke wapi za kuwapa barabara, shule, maji, umeme na kadhalika wananchi wake wakati anataka akiwa Dodoma afanye matanuzi?

Hivi anasahau kwamba Watanzania wa leo si wa jana na wameshavuka kiwango cha kudanganywa kwa hoja dhaifu kama hizo anazozitoa kuwatetea na si kuhalalisha ufisadi?

Kwa kweli leo sikufikiria kabisa kuandika makala kuhusu suala hili la ongezeko la posho kwa kuwa niliamini kabisa yote yaliyoandikwa na waandishi wengine kuhusu ongezeko hili yalitosha kufikisha ujumbe, na sikuona kama kuna jambo jipya hasa baada ya chama tawala (CCM) kuvunja ukimya na kupinga ongezeko hili.

Lakini kitendo kilichofanywa na Mbunge mmoja wa jimbo moja lililopo Magharibi kabisa mwa nchi yetu, ambaye licha ya chama chake kupinga ongezeko hili yeye amejitosa kutetea wabunge kuongezewa posho kwa nguvu zote kupitia akaunti yake ya twitter. Tena akichangia katika hali inayojionesha waziwazi kuwa ni ya jazba!

Mbunge huyo, ambaye hata hivyo anafahamika kwa kuwa kigeugeu katika masuala muhimu, amediriki kwenda mbali kidogo kwa kusema eti kama tunaona tatizo la wafanyakazi wa umma kulipwa kidogo ni sababu ya posho za wabunge basi ubunge ufutwe kabisa ili wafanyakazi wa umma wapate mishahara minono! Haya ni mawazo ya ajabu kabisa na hayakupaswa kutolewa na mtu mwenye hadhi ya ubunge kama yeye.

Hapa chini nanukuu baadhi ya hoja zake kupitia twitter.com (kama kuna makosa yoyote ya kiuandishi ieleweke kuwa sijahariri chochote kwenye maandishi yake):

“Msiwe na monopoly ya akili jamani na kudhani wengine hawafikili, you are wrong dam wrong!... Mshahara wangu ni 2,560,000 kabla ya kodi! Upotoshaji tuache!... Tujifunze na tuvumilie wanaofikilia tofauti tujadili hoja matusi sio uungwana!...”

“Anayesema alipoteza kura yake! Kwanza naamini hakunichagua! Na hatuwezi
watu wote kuna msimamo sawa! Let us think msikwepe hoja yangu! Mnaonaje tukifuta bunge! Ili tupate pesa nyingi tulipe watumishi vizuri… This is the radica thinking tujadili! Tufute bunge ili watumishi walipwe vizuri!...”

Hizi ni baadhi ya kauli za mwakilishi ambaye nimekuwa nina wasiwasi na uelewa wake, huku jimbo lake likiongoza kwa umasikini ingawa lina rasilimali nyingi mno.

Baada ya kubanwa sana na wasomaji wa mtandao, mbunge huyo alionesha kukerwa zaidi na watu wasiotaka posho ziongezwe kwa kuandika yafuatayo:

“Hakuna kuzira! Kama nyie mnaishi bila kuwa wabunge na sisi tunaweza kuishi bila ubunge! Tufute bunge kuondoa maneno!... Hakuna panic we can live without ubunge! Tufute tu! Tumesoma tutafuta kazi kwingine!...

“Nataka tufikilie jambo hili kwa mapana yake! Serikalini na mashirika yake kuna watu wanalipwa 20 mil kwa mwezi! Tujadili mfumo wote...”  
    
Huyu ndiye mwakilishi wa watu! Kwa kweli inashangaza kuona akikosa busara kwa sababu ya kutaka kuhalalisha alipwe mishahara miwili kwa kazi moja - kwa maana ya mshahara halisi na “mshahara posho nono”, jambo ambalo ni sawa na kushiriki katika kujenga misingi ya ufisadi ambayo bunge linapaswa kupambana nayo. Bahati mbaya tumefika mahali ambapo wahusika wanakosa kabisa busara na hawawezi kuona soni kuhalalisha ufisadi kwa kuwa wanaamini kuwa wanachofanya ni halali.

Anachokisema mbunge huyu kuwa kuna wafanyakazi katika mashirika hulipwa milioni 20 kwa mwezi, binafsi siwezi kukizungumzia sana kwa kuwa sina uhakika na hilo, lakini bado hakumfanyi yeye kama mbunge kung’ang’ania alipwe hizo sh 330,000/- kwa siku kama posho tu, achilia mbali mshahara. Kimsingi hakuna anayepinga mtu kulipwa vizuri lakini kwa uchumi na kipato gani cha serikali? Wabunge wakitaka kulipwa hilo, na inawezekana, wajitahidi kuisaidia na kuibana serikali katika matumizi sahihi ya rasilimali ili kipato cha nchi kipanuke. Tunaambiwa wakati tunapata uhuru mwaka 1961, nchi kama Singapore, Thailand, Malaysia na zingine kadhaa tulikuwa sawa kimaendeleo lakini leo wametuzidi maradufu. Kwa vile tumejaaliwa rasilimali kibao basi wabunge watusaidie kuifikisha nchi yetu zilikofika hizo Singapore ili wapate uhalali wa malipo zaidi

Wajue kwamba kama ni suala ni ugumu wa maisha mjini Dodoma ambako Bunge hufanya mikutano yake, ina maana maisha yamepanda mjini Dodoma tu, tena kwa wabunge peke yao? Hawajui wakati wa Bunge kuna maofisa mbalimbali ambao pia huenda huko wakiwemo waandishi wa habari? Hao hawaoni ugumu wa maisha? Au ndo ule msemo wa mwenye kisu kikali ndiye anayekula nyama!

Nakumbuka wakati ule Bunge likijadili bajeti, kiongozi wa kambi ya upinzani aliwahi kubainisha kuwa yapo maeneo ambayo viongozi wa serikali wamekuwa wanalipana hadi kati ya Shilingi milioni 1.5 na Shilingi milioni mbili kama posho za kuhudhuria vikao, hatua ambayo imewalemaza viongozi wengi wa serikali na wakati mwingine kususa kushiriki vikao wanavyoona havina posho, jambo analoona mbunge huyu (mpenda posho) kuwa ni halali kwa kisingizio cha ugumu wa maisha mjini Dodoma.

Tangu awali suala la posho lilikuwa likilalamikiwa, kwa kuwa limetumiwa vibaya kwa maslahi ya wachache wenye hulka ya ubinafsi. Ni ufisadi ambao wanaonufaika nao hawataki kukiri au kuuona kuwa ni ufisadi bali wanatumia maneno haya na yale kuuhalalisha uendelee kuwepo. Ikumbuke posho hizi zinazolalamikiwa ni zile za vikao. Yaani mbunge kwa kukaa tu Bungeni analipwa wakati ni kazi yake na analipwa mshahara.

Ndio maana nimekuwa na mashaka na hiki kinachoitwa 'Utawala Bora' kwa kuwa kwa walio wengi kimegeuka kuwa wimbo mtamu unaoimbwa na kufanyiwa semina elekezi ilimradi wateule kama huyu walipane posho zao, na kushibisha matumbo yao basi!

Naomba kuwasilisha...

YAHYA JAMMEH: Ajigamba kuitawala Gambia hata kwa miaka bilioni

Rais wa Gambia, Yahya Jammeh

BANJUL
Gambia

WASWAHILI wanasema ukistaajabu ya Mussa, utaona ya Firauni. Rais wa Gambia, Yahya Jammeh, ameliambia Shirika la Habari la Uingereza (BBC) kwamba ataongoza kwa miaka "bilioni moja", kama Mungu akipenda. Anasema wale wanaomkosoa na kumshutumu kuwa alishinda uchaguzi wa mwezi uliopita kwa kutumia vitisho na ufisadi "wanapoteza muda wao".

Shirika la Afrika Magharibi Ecowas lilisema kuwa wapiga kura "walitishwa" na serikali ya Jammeh aliyekuwa akipania kurejea madarakani. Jammeh, aliyeingia madarakani kwa mapinduzi mwaka 1994, alichaguliwa tena kwa asilimia 72, kwa mujibu wa takwimu rasmi.

Rais huyo mwenye umri wa miaka 46 anasema haogopi kile kilichomtokea Rais wa Misri aliyeondolewa madarakani kwa nguvu ya umma, Hosni Mubarak au Muammar Gaddafi wa Libya ambaye aliuawa.

"Hatima yangu iko mikononi mwa Mwenyezi Mungu," Jammeh alimwambia mwandishi wa BBC.

"Nitawatimizia raia wa Gambia na kama nitatawala nchi hii kwa miaka bilioni moja, nitafanya hivyo, Mungu akipenda."

Uchaguzi wa mwezi Novemba ulikuwa wa nne tangu Jammeh alipompindua rais wa kwanza aliyeingia madarakani wakati nchi hiyo ilipopata uhuru, Dawda Jawara, akiwa na umri wa miaka 29.

Wagombea wa upinzani, Ousainou Darboe na Hamat Bah walipata asilimia 17 na 11. Darboe aliyataja matokeo hayo kama "yasiyo halali, ya kifisadi na ya kipuuzi".

Historia yake

Alhaji Dk. Yahya Abdul-Aziz Jemus Junkung Jammeh alizaliwa Mei 25, 1965. Amekuwa Rais wa Gambia tangu mwaka 1994. Kama afisa wa jeshi kijana, alichukua madaraka mwezi Julai 1994 katika mapinduzi ya kijeshi na alichaguliwa kuwa Rais mwaka 1996; alichaguliwa tena mwaka 2001, 2006, na mwaka huu wa 2011.

Rais Jammeh alipata elimu ya sekondari nchini Gambia kisha akajiunga na Jeshi la Taifa la Gambia mwaka 1986. Alipata cheo cha Luteni mwaka 1989, na mwaka 1992 akawa Kamanda wa Polisi Jeshi (Military Police) katika jeshi la Gambia. Alipata mafunzo ya kina ya kijeshi katika nchi jirani ya Senegal na katika Shule ya Jeshi la Marekani.

Julai 22, 1994, kundi la maafisa wadogo katika Jeshi la Taifa la Gambia lilichukua madaraka kutoka kwa Rais Dawda Jawara katika mapinduzi ya kijeshi na kuchukua udhibiti wa vifaa muhimu katika mji mkuu, Banjul. Mapinduzi yalifanyika bila ya umwagaji damu na kukutana na upinzani kidogo. Kundi lilijitambulisha kama Baraza la Utawala la Muda la Kijeshi (AFPRC). Jammeh, ambaye alikuwa na umri wa miaka 29 wakati huo, ndiye alikuwa mwenyekiti wa AFPRC. AFPRC iliahirisha katiba na kufunga mipaka, na kutekelezwa kwa amri ya kutotoka nje.

Wakati serikali mpya ya Jammeh ikihalalisha mapinduzi na kupiga vita rushwa na ukosefu wa demokrasia chini ya utawala wa Jawara, wanajeshi pia hawakuridhishwa na mishahara yao, hali ya maisha, na matarajio ya maendeleo yao.

Uchaguzi

Jammeh alianzisha chama cha kisiasa cha Alliance for Patriotic Reorientation and Construction.  Alichaguliwa kama rais mwezi Septemba 1996. Waangalizi wa nje walichukuliwa kuwa uchaguzi ulikuwa huru na wa haki. Alichaguliwa tena Oktoba 18, 2001 kwa asilimia 53 ya kura; uchaguzi huu kwa ujumla ulichukuliwa kuwa huru na wa haki na waangalizi, licha ya baadhi ya mapungufu makubwa ya waziwazi na vitisho vya serikali dhidi ya wapiga kura kwa kupotosha mchakato ili kumpendelea mtawala aliyepo madarakani.

Jaribio la mapinduzi dhidi ya Jammeh liliripotiwa kufanywa tarehe 21 Machi, 2006; Jammeh, ambaye alikuwa nchini Mauritania, alilazimika kurudi nyumbani haraka. Mkuu wa Jeshi, Kanali Ndure Cham, anayedaiwa kuongoza njama hizo, aliripotiwa kukimbilia nchi jirani ya Senegal, wakati wengine walikamatwa na walifunguliwa kesi ya uhaini. Aprili 2007, maofisa kumi wa zamani waliotuhumiwa kuhusika walipatikana na hatia na kuhukumiwa; wanne kati yao walihukumiwa kifungo cha maisha jela.

Jammeh aligombea kwa awamu ya tatu katika uchaguzi wa rais uliofanyika tarehe 22 Septemba, 2006; uchaguzi awali ulipangwa kufanyika Oktoba lakini ulisogezwa mbele kwa sababu ya mwezi mtukufu wa Ramadhani. Alichaguliwa tena kwa asilimia 67.3 ya kura na kutangazwa kuwa mshindi wa uchaguzi; mgombea urais wa upinzani Ousainou Darboe alishika nafasi ya pili, kama ilivyokuwa mwaka 2001.

Novemba, 2011, Jammeh alichaguliwa tena kama rais kwa awamu ya nne, alipata asilimia 72 ya kura.

Mahusiano ya nje

Jammeh alisafiri kwenda Marekani kukutana na Prince George, Mtendaji Mkuu wa Kata ya Maryland, Jack Johnson mnamo Mei 2004.  Wakati katika Washington, eneo la DC metro, alitoa hotuba kwa Chuo cha mtakatifu Mary - Maryland wakati wa mahafali ya 2004. Katika hotuba hiyo alisisitiza dhamira ya kuinua elimu tangu alipochukua madaraka nchini Gambia.

Mwanzoni mwa Desemba 2006, Jammeh alifanya ziara ya siku tatu Iran, ambako alikutana na Rais wa Iran, Mahmoud Ahmadinejad na Kiongozi Mkuu Ali Khamenei; Ahmadinejad alisema kuwa Iran itatoa misaada ya kusaidia katika maendeleo ya Gambia, na walizungumza jinsi ya kuimarisha uhusiano kati ya nchi hizo mbili. Desemba 2007, alisafiri hadi Taiwan kwa lengo la kuendeleza mahusiano ya biashara kati ya nchi mbili.

Ushoga

Mei 15, 2008, Jammeh alitangaza kuwa serikali yake ingeanzisha sheria dhidi ya mashoga ambazo zitakuwa "kali zaidi kuliko zile za Iran", na kwamba "atakata kichwa" cha shoga au msagaji yeyote atakayegundulika katika nchi yake. Habari za magazeti zilionesha nia ya serikali yake kwa mashoga wote nchini humo kuuawa. Katika hotuba iliyotolewa Tallinding, Jammeh alitoa "mwisho wa mwisho" kwa mashoga au wasagaji nchini Gambia kuondoka nchini humo.

Madai ya kutibu

Januari 2007, Jammeh alidai anaweza kutibu VVU/UKIMWI na pumu kwa mimea ya asili. Alidai mpango wake ni pamoja na kuwasaidia wagonjwa kusitisha kuchukua dawa za kurefusha maisha (ARV). Madai yake yalikosolewa kwa kutangaza matibabu yasiyo ya kisayansi ambayo yanaweza kuwa na matokeo ya hatari, kutokana na imani kwamba walioruhusiwa kutoka mpango wake hawezi kuambukiza wengine. Desemba 2011, wakati wa mahojiano alirudia madai kwamba tiba ya VVU/UKIMWI "ilikwenda vizuri sana".

Gwaradzimba Fadzai, mwakilishi wa Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini Gambia, aliamriwa kuondoka nchini humo baada ya yeye kuonesha wasiwasi kuhusu madai hayo na akasema tiba hiyo itahamasisha tabia hatarishi. Agosti 2007,

Jammeh alidai kutengeneza dripu ya mitishamba dozi moja ambayo inaweza kutibu shinikizo la damu. Jammeh pia alidai kuanzisha matibabu ya utasa kwa wanawake kama sehemu ya kile kinachoitwa Programu ya Tiba Mbadala wa Rais (PATP).

Dini

Rais Jammeh, kama walivyo Wagambia wengi, ni Muislamu. Mwezi Julai 2010, Jammeh alisisitiza kwamba watu wanapaswa kumwamini Mungu, akisema kuwa "Kama humwamini Mungu, huwezi kuwa na shukrani kwa ubinadamu na pia una hadhi ya chini kuliko ya nguruwe."

Vikwazo kwa uhuru wa habari

Jammeh amekuwa akituhumiwa kuzuia uhuru wa vyombo vya habari. Sheria mpya kali kwa waandishi wa habari zilifuatiwa na mauaji ya kutatanisha ya Deyda Hydara, mhariri wa gazeti la Point. Hydara, ambaye alikuwa mkosoaji wa utawala wa Jammeh, aliuawa kikatili Desemba 2004.  Alhagie Martin, mmoja wa wasaidizi wa karibu wa kijeshi wa Jammeh, amekuwa akitajwa kuhusiana na mauaji ya Hydara. Hata hivyo, bado haijathibitishwa kuhusu madai ya Martin na mauaji ya Hydara. Inaaminika kwamba Jammeh anawajibika na mauaji ya Hydara. Jammeh amekanusha vyombo vya usalama wala yeye mwenyewe kushiriki katika mauaji hayo.

Aprili 2004, alitoa wito kwa waandishi wa habari kutii serikali yake "au kwenda kuzimu". Juni 2005 alisema katika redio na televisheni kwamba ameruhusu "kujieleza sana" katika nchi.

Maisha ya binafsi

Ndoa ya kwanza ya Jammeh iliishia katika talaka. Jammeh alioa mke wa pili, Zeinab Suma Jammeh, mwaka 1999, na wana watoto wawili: Mariam Jammeh, na Muhammed Yahya Jammeh. Watoto wake wote wawili walizaliwa mjini Washington, DC, na uraia wa Marekani uliombwa kwa mtoto wa kwanza - lakini ombi lake lilikataliwa.

Makala haya yameandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.