Aug 10, 2011

MANUEL PINTO DA COSTA: Arudi madarakani baada ya kutawala miaka ya 70 kwa ‘mkono wa chuma’

Manuel Pinto da Costa

SAO TOME

MWISHONI mwa wiki iliyopita imeshuhudia wapiga kura nchini Sao Tome na Principe wakimchagua kiongozi wa wakati wa uhuru wa Taifa hilo dogo la Afrika Magharibi kuwa Rais wao.

Manuel Pinto da Costa, mchumi wa ‘Ki-Marxist’ mwenye umri wa miaka 75, ambaye alitawala visiwa hivyo kwa 'mkono wa chuma' kwa miaka 15 baada ya uhuru kutoka kwa utawala wa mkoloni wa Kireno mwaka 1975.

Ulikuwa ni uchaguzi wa amani siku ya Jumapili iliyopita katika visiwa vya Sao Tome na Principe wakati wa duru ya pili ya uchaguzi wa rais uliomuingiza madarakani kiongozi huyo wa zamani wa wakati wa uhuru wa taifa hilo dogo lililopo Afrika Magharibi.

Tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1991, Rais amegawana madaraka na Waziri Mkuu.

Pinto da Costa, mwenye umri wa miaka 75, amepata ushindi mwembamba dhidi ya mgombea kutoka chama cha Waziri wake mkuu katika duru ya pili ya uchaguzi siku ya Jumapili iliyopita. Mgombea aliyeshindwa, Evaristo Carvalho, ambaye ni Spika wa Bunge la nchi hiyo alipata asilimia 47 ya kura.

Hakuna tukio baya lililoripotiwa wakati vituo vya kupigia kura vya taifa hilo la visiwa vidogo kufungwa ilipotimu saa 12:00 jioni kwa saa za huko. "Mchakato wa kupiga kura upo kila mahali, katika Sao Tome na nje ya nchi. Kazi ya kuhesabu kura imeanza," alisema msemaji wa tume ya uchaguzi, Joao Ramos alipokuwa akizungumza na vyombo vya habari.
Watu karibu watu 92,000 walipiga kura, kutoka kwenye idadi ya watu wa nchi hiyo ambayo ni 200,000. Baadhi ya watu 30,000 walijitoa katika raundi ya kwanza mnamo Julai 17 na vijiji vitano vilianzisha mgomo wa kupiga kura katika maandamano kupinga hali duni ya maisha katika visiwa.

Hata hivyo, Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) kupitia kipindi chake cha Network Africa limeelezwa kuwa wakazi wengi wa visiwa hivyo wapatao 165,000 ni vijana na hawana kumbukumbu za enzi za utawala wa chama kimoja wa da Costa.

Lakini wanatarajia Rais Mteule kuweka shinikizo kadhaa kwa serikali inayoongozwa na Waziri Mkuu Patrice Trovoada – kutatua baadhi ya matatizo ya nchi. Kampeni za Pinto da Costa zililenga katika utengamano wa kisiasa na aliahidi kupambana na ufisadi uliosambaa.

Visiwa vya Sao Tome na Principe, vilivyokuwa mwanzoni wazalishaji wa kwanza kwa kakao vina utajiri wa mafuta na uzalishaji wa kibiashara utaanza miaka michache ijayo.

Hata hivyo umezuka mjadala juu ya namna gani matumizi yake yatafanyika na kusababisha hali tete ya kisiasa.

Historia ya da Costa:
Manuel Pinto da Costa amezaliwa mnamo 5 Agosti 1937, ni mchumi na mwanasiasa ambaye aliwahi kuwa Rais wa kwanza wa nchi hiyo baada ya uhuru. Amechaguliwa tena katika uchaguzi wa Agosti 2011 kutumikia muhula wa pili. Anatarajiwa kuanza rasmi madaraka hayo mnamo 3 Septemba 2011.

Akiwa mkuu wa nchi hiyo baada ya uhuru mwaka 1975 hadi 1991, aliongoza kwa kusimika mfumo wa ujamaa wa chama kimoja cha siasa cha Movement for Liberation of Sao Tome and Principe (Kireno: Movimento de Libertação de São Tomé e Príncipe, MLSTP). Pia aliwahi kuwa waziri mkuu mara mbili, mara ya kwanza chini ya rais wa kwanza wa kidemokrasia wa nchi, Miguel Trovoada.

Alipata elimu katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani (Ujerumani Mashariki), na anaongea kwa ufasaha lugha za Kireno na Kijerumani.

Hadi miaka ya mwanzo ya 1990, chama chake (MLSTP) kiliimarisha mahusiano ya kina na Angola na chama tawala cha MPLA, kwa Pinto da Costa mwenyewe alifurahia zaidi uhusiano wa kirafiki kati yake na Jose Eduardo dos Santos, Rais wa Angola, wakipanua zaidi urafiki wao wa wakati wao walipokuwa vijana.

Mwaka 1991, ulipohalalishwa mfumo wa vyama vingi na kufuatiwa na uchaguzi wa kwanza chini ya mfumo wa kidemokrasia, Pinto da Costa hakugombea uchaguzi na badala yake alitangaza kustaafu siasa.

Chama chake cha MLSTP hakikuwa na mgombea mbadala wa Pinto da Costa na kumfanya Travoada Miguel achaguliwe kuwa rais bila kupingwa. Pamoja na kauli yake ya awali ya kustaafu siasa, Pinto da Costa alirejea kugombea katika uchaguzi wa 1996, lakini alishindwa kwa ushindi mwembamba na Trovoada kwa kupata asilimia 47.26 ya kura zote. Mwaka 2001, aligombea tena dhidi ya Rais anayemaliza muda wake, Fradique de Menezes, ambaye alishinda kwa wingi wa kura katika raundi ya kwanza.

Pinto da Costa alichaguliwa kuwa kiongozi wa chama cha MLSTP mnamo Mei 1998. Alijiuzulu katika chama mnamo Februari 2005 na Guilherme Posser da Costa alichaguliwa kushika nafasi yake.

Katika uchaguzi wa mwezi Julai 2011, Pinto da Costa aliingia kwenye kinyang'anyiro kama mgombea binafsi. Alishinda uchaguzi katika duru ya kwanza lakini akishindwa kupata asilimia zinazotosha kuchukua madaraka.

Katika duru hiyo alipata asilimia 35.58 ya kura baada ya kampeni zake za uchaguzi kulenga kuwepo haja ya utulivu katika taifa ambayo alidai kuwa limeshuhudia mawaziri wakuu 18 wakiwa madarakani katika miaka 21 tu baada ya nchi kuingia katika mfumo wa vyama vingi mwaka 1990. Pia aliahidi kupambana na ufisadi mkubwa ambao umedumaza maendeleo ya kiuchumi ya Sao Tome.

Mpinzani wake, Carvalho, mwenye umri wa miaka 70, alipata asilimia 21.74 ya kura katika duru ya kwanza ya uchaguzi, ni mwanachama wa chama cha Independent Democratic Action (Kireno: Acção Democratica Independente, ADI). Pia aliahidi kupambana na rushwa kama ahadi ya ilani yake muhimu.

Chini ya sheria ya Sao Tome, rais anayemaliza muda wake, Fradique de Menezes, ambaye alichaguliwa kwa mara ya kwanza mwaka 2001 na kuchaguliwa tena mwaka 2006, hawezi kugombea kwa mara ya tatu.

Katika tukio linalosemekana kutohusiana na siku ya kupiga kura ya Jumapili, mtu mmoja mwenye umri wa miaka 37 alipigwa risasi na kuumizwa katika mguu na walinzi wa Waziri wa Vijana na Michezo wa Sao Tome, Abnildo d'Olivera.

Katika raundi ya pili ya marudio ya uchaguzi mnamo tarehe 7 Agosti, da Costa alimshinda mpinzani wake, Evaristo Carvalho kutoka chama tawala cha Independent Democratic Action, kwa kupata asilimia 58 ya kura.

Wakati wa kampeni zake zilizolenga haja ya siasa za utulivu na ahadi za kukabiliana na ufisadi mkubwa. Jitihada zake zilipata sapoti kubwa kutoka kwa wagombea wengine wakubwa, akiwemo Waziri Mkuu wa zamani, Maria das Neves, ambaye alidai kuwa "mpango wa Pinto da Costa utaleta matumaini zaidi kwa nchi yetu".

Baadhi ya wachambuzi wa mambo, hata hivyo, walionesha wasiwasi wao kwamba ushindi wa rais huyo wa zamani unaweza kurejesha enzi za utawala wa kimabavu ulioonekana katika kipindi chake cha zamani cha madaraka.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment