Feb 24, 2012

ABD MANSOUR HADI: Kaimu Rais aliyekuwa mgombea pekee wa urais Yemen

Abd Rabbu Mansour Hadi

SANAA

Yemen



SIKU ya Jumanne wiki hii, raia wa Yemen waliamkia katika vituo vya kupigia kura kumchagua rais wao mpya baada ya nchi kukumbwa na ghasia kwa mwaka mzima. Kila mtu alikuwa anajua kuwa atakayeshinda ni makamu wa Rais wa nchi hiyo, Abd Rabbu Mansour Hadi.



Uchaguzi huo umefanyika baada ya mwaka mmoja wa ghasia na maandamano ya kupinga utawala wa Rais Ali Abdullah Saleh. Kabla ya uchaguzi huu kampeni zilikuwa zikiendelea kumuunga mkono makamu huyo wa rais, Abd Rabbu Mansour Hadi, ingawa ndiye aliyejitokeza na kuwa mgombea pekee asiye na mshindani.



Mshindi wa tuzo ya Nobel, raia wa Yemen, Bi Tawwakol Karman, aliwataka raia wote wa Yemen kujitokeza kumuunga mkono makamu huyo wa rais.



“Tunawaomba watu wote wa Yemeni wakiwemo vijana wajitokeze hii leo tarehe 21 Februari, sio kuunga mkono uchaguzi peke yake, bali kumuunga mkono Mansour Hadi kuwa Rais wa mpito katika kipindi hiki cha mpito,” alisema Bi Karman siku ya Jumanne wiki hii.



Huku Mshindi huyo wa Tuzo ya Nobel akimpigia debe Mansour Hadi kuwa rais, tayari imeripotiwa kuwa ghasia zimeanza upya nchini Yemen. Pia kumeripotiwa kuwepo kwa mfululizo wa milipuko na mashambulio katika vituo vya kupigia kura na sehemu nyingine.



Historia yake



Field Marshal Abd Rabbuh Mansur Al-Hadi alizaliwa mwaka 1945. Ni askari na mwanasiasa ambaye amekuwa Makamu wa Rais wa Yemen tangu tarehe 3 Oktoba 1994. Kati ya Juni 4  na Septemba 23, 2011 alikuwa akikaimu urais wa Yemen, wakati Ali Abdullah Saleh alipoondoka kwenda nchini Saudi Arabia kwa ajili ya matibabu, baada ya kujeruhiwa katika mashambulizi yaliyolenga ukumbi wa rais wakati wa maandamano ya kuipinga serikali ya  Yemeni mwaka 2011.



Ndipo, tarehe 23 Novemba, Abd Mansour al-Hadi akawa kaimu rais tena, baada ya Saleh kuachia madaraka "katika kile kinachosemwa ni kwa ajili ya kupata kinga dhidi ya mashtaka." Al-Hadi "anatarajiwa kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na pia kutoa mwito wa kuitisha uchaguzi wa rais mapema ndani ya siku 90" wakati Saleh akiendelea kutumika kama rais kwa jina tu.



Maisha ya awali



Al-Hadi alizaliwa mwaka 1945 katika eneo la Abyan. Jina lake pia linaweza kuandikwa Abd Rabu Mansur Hadi, Abd Rabbah Mansour Hadi au Abdurabu Mansour Hadi, miongoni mwa vifupi vingine tofauti.



Alijiunga na Jeshi la Yemen Kusini mwaka 1970 na kuwa Meja Jenerali mwanzoni mwa mwaka 1990.



Kazi ya siasa



Alikuwa Makamu wa Rais wa Yemen baada ya Ali Salim al-Beidh kujiuzulu na kushindwa katika vita vya wenyewe kwa wenyewe. Al-Hadi aliteuliwa na Rais Ali Abdullah Saleh kama Makamu wa Rais tarehe 3 Oktoba 1994. Kabla ya uteuzi wake kama Makamu wa Rais, alikuwa Waziri wa Ulinzi.



Al- Hadi ndiye aliyejitokeza kuwa mgombea pekee katika uchaguzi wa rais uliofanyika siku ya Jumanne ya tarehe 21 Februari 2012. Ugombea wa Al-Hadi umeungwa mkono na chama tawala pamoja na bunge la upinzani. Ingawa kupiga kura kimsingi ni mfano wa demokrasia lakini ni sababu moja tu inayomfanya mgombea Al-Hadi ambaye tayari ni kaimu Rais kuungwa mkono, nayo ni nia ya kukamilisha uhamisho wa madaraka kutoka kwa Saleh kwenda kwa Al-Hadi.



Licha ya Al-Hadi kutumikia nafasi ya umakamu wa rais kwa kipindi kirefu cha miongo miwili, Hadi ni mtu ambaye raia wa Yemeni wanamfahamu kidogo mno. Kamanda wa zamani wa kijeshi kutoka Kusini, Al-Hadi, mwenye umri wa miaka 66, alikwama kwa Saleh wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Yemen kati ya Kaskazini na Kusini vya mwaka 1994. 



Katika miezi ya hivi karibuni, ikiambatana na kuanguka kwa Saleh, majukumu yanamwangukia yeye kusimamia mageuzi ya kikatiba, urekebishaji wa nchi hiyo na kusafisha njia kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa vyama vingi mwaka utakaofanyika mwaka 2014.



Hata hivyo, kwa sababu alijikuta akilazimika kufanya kazi kwa muda mrefu katika serikali ya Saleh, wengi bado wana shaka iwapo atakuwa na msimamo unaoweza kuleta mshikamano wa kisiasa na kuvunja ushawishi uliowekwa na bosi wake wa zamani. Mahudhurio ya chini ya watu siku ya Jumanne ni kama utabiri, inaweza kupunguza uhalali wake zaidi.



Vyanzo vya kidiplomasia vya Marekani viliyotolewa na WikiLeaks vimemuelezea Al-Hadi kama mzushi aliyepandikizwa, angalau ni mtu ambaye alikuwa akifurahia mshikamano mdogo miongoni mwa madalali wa madaraka nchini Yemeni.



"Bingwa anayedhaniwa wa mageuzi, msimamo wa Al-Hadi kama makamu wa rais kwa kiasi kikubwa ni sherehe na haiwezi kumfanya kuwa na ushawishi mkubwa kwa [serikali] watoa maamuzi," kulingana na taarifa za WikiLeaks za 2004.



"Pamoja na kutoka kanda ya kusini ya Abyan, Abd Mansour Al-Hadi aliongoza kampeni dhidi ya YSP (Yemeni social party), chama cha kijamaa cha Yemeni, na aliwahi kuwa waziri wa ulinzi wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo.



"Kuteuliwa kwake katika serikali ya muungano mwaka 1994 kunachukuliwa kama malipo (hongo) kwa ajili ya huduma yake kwa eneo la kaskazini," kilisema chanzo cha WikiLeaks.



Chanzo hicho pia kilihusisha mkutano wake na balozi wa Marekani, Thomas Krajeski, ambapo Al-Hadi alimuambia mgeni wake huyo wa Marekani kwamba "Yemen itahitaji msaada wa Marekani katika kupunguza umaskini, kufanikisha mageuzi ya kiuchumi na kidemokrasia, na kuvutia uwekezaji wa kigeni".



Vyanzo vingine vya habari vya kimtandao vilihusisha uungaji wake mkono kwa uongozi wa Syria katika msuguano wake na Israeli, na tuhuma zake kwa Eritrea, ambapo Yemen ilipinga na kuzua mgogoro kuhusu visiwa vya Hanish katika Bahari ya Shamu mwaka 1995.



Eritrea, Al-Hadi aliisema kuwa, ilikuwa ni "thawra" (mapinduzi) zaidi kuliko kuwa "dawla" (nchi).  "Wao wanapambana na kila mmoja," alisema, kulingana na chanzo cha habari za kimtandao.



Makala haya yameandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment