Feb 15, 2012

BASHAR AL-ASSAD: Sasa akalia kuti kavu nchini Syria

Rais wa Syria, Bashar al-Assad

DAMASCUS

Syria



MUUNGANO wa nchi za Kiarabu unaendelea kutoa wito kwa Assad kukabidhi madaraka kwa naibu wake ambaye ataunda serikali ya muungano wa kitaifa na sasa unaungwa mkono na Marekani, Uingereza na Ufaransa. Lakini Moscow imesema kuwa mpango huo "hauna usawa" na "utatoa mwanya'' wa uingiliaji wa masuala ya ndani ya Syria.



Marekani imetoa wito kwa mataifa yote kutoa msimamo wao kuhusiana na kile ilichokitaja kuwa udhalimu serikali ya Syria. Imesema kuwa mataifa ya kirafiki yanayoitakia Syria utawala wa Kidemokrasia yanapaswa kuungana katika kumshutumu kiongozi wa taifa hilo Rais Assad. Waziri wa mashauri ya Kigeni wa Marekani, Hillary Clinton, alisema ni jambo la kusikitisha kuwa Urusi na China zilipiga kura za turufu kupinga azimio la kuikosoa Syria katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.



Alitoa wito kwa jamii ya kimataifa iunge mkono makundi ya upinzani nchini Syria. Ni wazi kwamba Marekani pamoja na wanadiplomasia wa mataifa mengine ya Magharibi wameghadhabishwa mno na hatua ya Urusi na China kupinga azimio la kuikosoa Syria.



Clinton alizungumza akiwa Bulgaria ambako amesema Marekani pamoja na mataifa mengine zitashinikiza Rais Assad aondoke madarakani. Alizungumzia kuhusu kuwekwa vikwazo zaidi pamoja na kuwataja watu ambao wanafadhili na kuipa silaha serikali ya Syria.



Mataifa ya magharibi yanajiandaa kupigia debe azimio kali kwenye mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusiana na mgogoro uliopo nchini Syria. Katibu mkuu wa muungano wa Mataifa ya Kiarabu Nabil al-Arabi anatarajiwa kutoa ombi kwa Baraza la Usalama kuunga mkono mpango mpya wa muungano huo unaotaka rais wa Syria Bashar al-Assad ajiuzulu.



Historia ya Assad



Bashar al-Assad alizaliwa Septemba 11, 1965, mbai na urais pia ni Katibu wa Mkoa wa Chama cha Ba'ath.  Baba yake Hafez al-Assad alitawala Syria kwa miaka 29 hadi kifo chake mwaka 2000. Al-Assad alichaguliwa mwaka 2000, na kuchaguliwa tena mwaka 2007, bila kupingwa.



Maisha ya awali



Bashar al-Assad alizaliwa katika Dameski, ni mtoto wa Aniseh (nee Makhluf) na Hafez al-Assad. Nyumba aliyokulia ilikuwa na vuguvugu la siasa chini ya kivuli cha baba yake, Hafez Assad, ambaye alichukua madaraka ya urais wa Syria katika Mapinduzi ya 1970. Tofauti na ndugu zake, Basil na Maher, dada zake Bushra, Bashar, alikuwa kimya na hakupenda siasa au kazi ya kijeshi.



Alipata elimu yake ya msingi na sekondari katika shule ya mchepuo wa Kiarabu-Kifaransa ya al-Hurriya, Damascus na alikuwa mwanafunzi mfano bora aliyefanya vizuri sana kimasomo. Mwaka 1982, alihitimu shule ya sekondari na kwenda kusomea tiba katika Chuo Kikuu cha Damascus. Mwaka 1988, Bashar Assad alihitimu masomo ya tiba na kufanya kazi kama daktari katika hospitali kubwa ya kijeshi, "Tishrin", nje kidogo ya Damascus.



Miaka minne baadaye, alikwenda Uingereza kuanza mafunzo ya Udaktari bingwa wa macho (Ophthalmology) katika Western Eye Hospital, sehemu ya makampuni ya mafunzo ya St Mary jijini London. Wakati huo Bashar hakuwa na matarajio ya kisiasa. Baba yake alimwandaa kaka wa Bashar, Basil al-Assad, kuwa rais wa baadaye. Hata hivyo, Bashar aliitwa mwaka 1994 kujiunga na jeshi, baada ya kifo cha Basil kisichotarajiwa katika ajali ya gari.



Kifo cha Basil



Muda mfupi baada ya kifo cha Basil, Hafez Assad alifanya uamuzi wa kumfanya Bashar kuwa mrithi wake mpya. Katika kipindi cha miaka sita na nusu iliyofuata, hadi kifo chake mwaka 2000, Hafez aliandaa utaratibu kwa ajili ya Bashar kuchukua madaraka. Maandalizi kwa ajili ya kipindi cha mpito yalifanywa katika ngazi tatu. Kwanza, alijengwa ndani ya jeshi na vyombo vya usalama. Pili, picha ya Bashar ilijengwa ili afahamike zaidi kwa umma. Na mwisho, Bashar alifanywa kuzoea taratibu za kuendesha nchi kabla.



Kupata sifa ya kijeshi, mwaka 1994 Bashar alijiunga katika chuo cha kijeshi cha Homs, Kaskazini mwa Dameski, na alipitia safu haraka hadi nafasi ya Kanali Januari 1999. Ili kuandaa msingi imara kwa Bashar katika jeshi, makamanda wakongwe walitakiwa kustaafu, na damu changa, maafisa vijana watiifu kwake walichukua nafasi zao. Sambamba na kazi yake ya kijeshi, Bashar alishiriki katika masuala ya umma. Alipewa mamlaka makubwa na akawa mshauri wa kisiasa kwa Rais Hafez al-Assad, mkuu wa ofisi ya kupokea malalamiko ya rufaa ya wananchi, na aliongoza kampeni dhidi ya rushwa. Kama mkuu wa kampeni dhidi ya rushwa, Bashar alipata uwezo wa kuondoa wapinzani wake wenye uwezekano wa kuwania urais.



Mwaka 1998, Bashar alichukua mamlaka ya faili la masuala ya Syria-Lebanon, ambalo lilikuwa linashikiliwa na aliyekuwa Makamu wa Rais, Abdul Khaddam tangu miaka ya 1970, mmoja wa viongozi wachache wa Sunni katika serikali ya Assad, ambaye hadi wakati huo alikuwa na uwezekano wa kuwa rais. Kwa kuchukua mamlaka ya masuala ya Syria nchini Lebanon, Bashar alikuwa na uwezo wa kushinikiza Khaddam akae kando na kusimika nguvu zake katika Lebanon.



Katika mwaka huo huo baada ya mashauriano madogo na wanasiasa wa Lebanon, Bashar alimweka Emile Lahoud, mshirika wake mwaminifu, kama Rais wa Lebanon na kumuweka kando Waziri Mkuu wa zamani wa Lebanon, Rafic Hariri, kwa kutolipa uzito jina lake katika nafasi ya waziri mkuu. Ili kudhoofisha zaidi mkakati wa zamani wa Syria nchini Lebanon, Bashar alimbadilisha balozi wa mrefu wa Syria nchini Lebanon, Ghazi Kanaan, na mshirika mwaminifu, Rustum Ghazali. Chini ya Bashar, rushwa ya Syria nchini Lebanon, ambayo tayari ilikuwa inakadiriwa kufikia dola bilioni 2.0 kwa mwaka katika miaka ya 1990, na kushindwa kudhibitiwa kulikosababisha kuanguka kwa benki ya Lebanon Al-Madina mwaka 2003.



Al-Madina ilitumiwa kuchukua fedha katika michezo ya kubahatisha (kamari) kinyume cha sheria ya mpango wa Umoja wa Mataifa wa mafuta-kwa-chakula nchini Iraq. Vyanzo vilisema kuwa kiasi kilichohamishwa kwa njia ya benki ya al-Madina ni zaidi ya dola 1 bilioni, na asilimia 25 kwenda kwa viongozi wa Syria na washirika wao wa Lebanon, miongoni mwa wapokeaji wa fedha hizi alikuwa ndugu wa Bashar Assad, Maher, mkwe wa Emile Lahoud, Elias Murr, na Ghazali.



Urais



Wakati Assad mkubwa alipokufa mwaka 2000, Bashar aliteuliwa kuwa kiongozi wa chama cha Ba'ath na Jeshi, na alichaguliwa kuwa rais bila kupingwa katika kile serikali ilichodai kuwa kuungwa mkono kwa wingi (asilimia 97.2 ya kura), baada ya Al Majlis Sha'ab (Bunge) kupunguza umri wa chini kwa mtu anayetaka kugombea kutoka 40 hadi 34 (umri Assad alipochaguliwa). Mei 27, 2007, Bashar alipitishwa tena kuwa rais kwa kipindi kingine cha miaka saba, pamoja na matokeo rasmi ya asilimia 97.6 ya kura katika kura ya maoni bila ya mgombea mwingine.



Katika sera yake ya ndani, amekuwa akikosolewa kwa kupuuza haki za binadamu, kushuka kwa uchumi, na rushwa. Katika sera zake za kigeni, Al-Assad ni mkosoaji mkubwa wa Marekani na Israeli. Chama cha Ba'ath kinabakia katika udhibiti wa bunge, na kikatiba ni "chama kinachoongoza" serikali.



Hadi anakuwa rais, Bashar al-Assad hakuwa akishiriki sana katika siasa; jukumu lake kwa umma lilikuwa ukuu wa Chama cha Kompyuta cha Syria, ambacho kilianzisha huduma ya Internet nchini Syria mwaka 2001. Al-Assad alithibitishwa kuwa rais kwa kura ya maoni bila kupingwa mwaka 2000.



Alitarajiwa kufuata njia huru zaidi kuliko baba yake. Katika mahojiano alisema kuwa aliona demokrasia nchini Syria kama 'chombo cha maisha bora' lakini baadaye alisema kuwa itachukua muda kwa demokrasia kukomaa na kwamba isiharakishwe.



Kisiasa na kiuchumi, maisha ya raia wa Syria yamebadilika kidogo tangu mwaka 2000. Mara baada ya kuchukua madaraka harakati za mageuzi zimefanywa kwa tahadhari katika Dameski, ambayo yalisababisha al-Assad kufunga gereza la Mezzeh na mamia ya wafungwa wa kisiasa kutolewa.



Makala haya yameandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment