Jun 8, 2011

DIMEJI BANKOLE: Spika wa Nigeria anayeonja chungu ya ufisadi

 Dimeji Bankole

 Dimeji Bankole baada ya kutiwa nguvuni

ABUJA
Nigeria

MMOJA wa wanasiasa mashuhuri wa Nigeria amekamatwa na polisi wa kupambana na ufisadi. Spika wa bunge la wawakilishi linalomaliza muda wake, Dimeji Bankole alizuiliwa kuhusiana na madai ya ubadhilifu wa mamilioni ya dola,fedha za serikali ya nchi hiyo.

Alikamatwa baada ya makao yake katika mji mkuu wa nchi hiyo, Abuja kuzingirwa.

Alipoapishwa kuchukua madaraka wiki iliyopita, Rais wa Nigeria, Goodluck Jonathan aliahidi kukabiliana na ufisadi uliokita mizizi nchini Nigeria kwa nguvu zake zote.

Taarifa zilizomkariri mwandishi wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Jonah Fisher, zilisema kukamatwa kwa Bankole si suala ambalo halikutarajiwa, baada ya wiki kadhaa za tetesi zilizochapishwa katika magazeti ya nchi hiyo kwamba atakamatwa.

Msemaji wa tume ya kukabiliana na uhalifu wa kiuchumi na kifedha nchini humo (EFCC), alisema kuwa tume hiyo ilipokea taarifa kwamba Dimeji Bankole alikuwa akipanga kutoroka nchini humo.

Sawa na wabunge wengine, muhula wa spika huyo, Dimeji Bankole, ulimalizika Ijumaa iliyopita, na bunge jipya linatarajiwa kuapishwa Jumatatu.

Bankole alipoteza kiti chake katika uchaguzi wa mwezi Aprili, taarifa ya EFCC inasema kuwa Spika huyo anatafutwa kujibu shutuma zinazomkabili za ufisadi.

Miongoni mwa shutuma hizo ni pamoja na matumizi mabaya ya dola milioni 60, na kuchukua dola milioni 65 kama mkopo binafsi akitumia akaunti ya bunge kama dhamana.

Awali msemaji wa Bankole, Idowu Bakare, alitoa taarifa kuwa spika huyo "hakuwahi kunufaika" kwa kutumia nafasi yake. Liliripoti shirika la habari la AP.

Historia ya Dimeji Bankole

Oladimeji Sabur Bankole amezaliwa Novemba 14, 1969. Ni mwanasiasa wa Nigeria na Spika wa Baraza la Wawakilishi anayemaliza muda wake Ijumaa hii. Ni mtoto wa Chifu wa Abeokuta, Alan Bankole, alikuwa mfanyabiashara kabla ya kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge. Alichaguliwa katika umri wa miaka 37, na hivyo kuweka historia ya kuwa Spika mdogo katika historia ya Bunge la Nigeria.

Maisha ya awali, elimu, na michezo

Bankole alizaliwa katika eneo la Abeokuta, ambalo sasa ni sehemu ya Jimbo la Ogun, Novemba 14, 1969. Wazazi wake ni Alan Bankole, mfanyabiashara, na Makamu Mwenyekiti wa zamani wa Taifa wa chama cha All Nigerian Peoples (ANPP) na Seriki Jagunmolu wa Egbaland, na mke wake, Atinuke Bankole, Ekerin Iyalode wa Egbaland.

Gazeti la moja la Thisday liliwahi kubainisha elimu ya Bankole kuwa alisomea shule ya Baptist Boys High School, iliyopo Abeokuta alipoanza mwaka 1979, Chuo cha Albany, kilichopo London, Uingereza kuanzia 1985, Chuo Kikuu cha Reading, kilichopo Reading, Uingereza kuanzia 1989, Chuo Kikuu cha Oxford, kilichopo Oxford, Uingereza mwaka 1991; na Chuo Kikuu cha Havard, Cambridge, Massachusetts, Marekani mwaka 2005.

Mtandao wa All African.com ulitoa taarifa kuwa Bankole ana cheti cha kitaaluma katika usimamizi wa Fedha za Umma kutoka Chuo Kikuu cha Harvard, Marekani.

Bankole alibainisha kuwa hajawahi kwenda chuo cha kijeshi cha Sandhurst lakini alichukua mafunzo ya maafisa wa kijeshi katika Chuo Kikuu cha Oxford ambapo alikuwa katika Kikosi cha Mizinga.

Bankole ni mchezaji wa mchezo wa wapanda farasi wa kupiga tufe kwa fimbo (polo), na ni mwanachama wa chama cha mchezo huo maaruf kama Lagos Polo Club, ambapo nafasi yake katika mchezo ni ya ulinzi. Pia huwa anafurahia sana mchezo wa soka.

Kazi ya Biashara

Bankole alikuwa Mkurugenzi wa Kampuni ya Wakala wa Ndege Nigeria, kuanzia mwaka 1995 hadi 1998, Mkurugenzi Mtendaji wa Uendeshaji wa kampuni ya Chuma ya Afrika Magharibi (West African Aluminium Products Ltd) kuanzia mwaka 1998 hadi 2003 na Mkurugenzi wa kampuni ya ASAP Limited kuanzia mwaka 2000 hadi 2003. Pia yeye ni mchumi.

Kazi ya kisiasa

Mwaka 2002, Bankole alichaguliwa kwenye Baraza la Wawakilishi kwa tiketi ya People's Democratic party (PDP) kuwakilisha eneo la Abeokuta Kusini katika Jimbo la Shirikisho la Ogun. Alikuwa Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Fedha wakati Amim Bello Masaari alipokuwa Spika, (Farouk Lawan alikuwa Mwenyekiti wa kamati) na aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ardhi ya Usafiri. Kamati zingine alizopitia ni ya Ulinzi, Mambo ya Ndani na Benki, na Fedha.

Bankole alichaguliwa tena mwezi Aprili 2007. Alichukulia utashi wake katika ubunge kuuhusha na ulinzi na fedha.

Baraza la Wawakilishi

Uspika: Mwezi Septemba 2007, kamati ilimhoji Spika, Patricia Etteh kuhusu matumizi yake ya milioni 628 (dola milioni 4.8) kwa ajili ya ukarabati wa nyumba na magari.

Spika huyo alikana makosa hayo, lakini wawakilishi wengi hawakuwa na furaha kutokana na jitihada zake za kujitetea mwenyewe, juhudi zikazidishwa na wawakilishi hao katika kuhakikisha suala hilo linashughulikiwa. Rais wa zamani, Olusegun Obasanjo na wanachama ngazi za juu wa PDP waliendelea kumuunga mkono Etteh, lakini sehemu kubwa ya chama, wakiongozwa na Lawan na pamoja na Bankole, walimtaka ajiuzulu. Kulikuwa na taarifa kwamba Bankole, alikuwa ni miongoni mwa wagombea wengine, waliokuwa na matumaini makubwa ya kumrithi Etteh mwezi Oktoba 5, 2007.

Baada ya Etteh kujiuzulu nafasi ya uspika mnamo Oktoba 30 (pamoja na naibu wake, ambaye pia aliingizwa kwenye kashfa hiyo), mwanachama wa Kundi la waadilifu (waliompinga Etteh), Terngu Tsegba akawa Spika wa mpito. Samson Osagie wa Jimbo la Edo alimpendekeza Bankole kuwania nafasi ya Spika, na Lynda Ikpeazu wa Jimbo la Anambra akaunga mkono pendekezo hilo.

Tarehe 1 Novemba, Bankole alichaguliwa kushika nafasi iliyoachwa wazi na Etteh. Mpinzani wake mkubwa alikuwa ni Mwakilishi wa Jimbo la Osun, George Jolaoye, ambaye alimshinda kwa kupata kura 304 dhidi ya kura 20 (na kura 4 hazikupigwa).

Etteh alikuwa ni miongoni mwa wale ambao hawakumpigia kura Bankole. Naibu Spika mpya alikuwa Usman Nafada Bayero.


Wakati wa kuchaguliwa kwake, Bankole alisema "Nachukua vazi la uongozi katika wakati mgumu sana, lakini hizi ni nyakati ngumu, tunahitaji kujenga imani tena na kuwahakikishia watu kwamba sisi bado ni wawakilishi wao. Nahitaji kuwa na Bunge huru ambalo Wanigeria watajivunia, hii ni kazi yangu ya kwanza."

Wiki moja tu baada ya kuchaguliwa, wapinzani wake wa kisiasa walidai kuwa Bankole hakukamilisha mafunzo yake ya Jeshi la Vijana la Kujenga Taifa (National Youth Service Corp, NYSC), ambayo ni ya lazima kwa Wanigeria wote wanaohitimu Chuo Kikuu wakiwa chini ya umri wa miaka thelathini, na wakataka ajiuzulu kwa sababu ya suala hilo. Uongozi wa Jimbo la Bankole wakatoa uthibitisho wake wa kumaliza NYSC, na kukomesha uvumi.

Mnamo Juni 22, 2010, Bankole aliwasimamisha wawakilishi 11 wa Bunge kwa muda usiojulikana kwa kuonesha utovu wa nidhamu na kupigana ndani ya Bunge.


Kashfa ya 2009

Mwaka 2009, Bankole alishitakiwa kwa matumizi makubwa ya zaidi ya Naira bilioni 52 zilizotumika kama gharama za usafiri, kitendo kilichoelezwa na wajumbe wengi wa Baraza la Wawakilishi kama 'ubinafsi na ulaghai', kwa kuzingatia kiwango cha sasa cha umaskini miongoni mwa asilimia kubwa ya wakazi wa Nigeria.

Kukamatwa 2011

Dimeji Bankole anatiwa mbaroni na kikosi cha polisi cha kupambana na rushwa kwa tuhuma za wizi wa mamilioni ya pesa za serikali. Bankole alitiwa mbaroni muda mfupi baada ya kuwepo taarifa za kutaka kutoroka nchini.

Msemaji wa taasisi ya kuzuia rushwa nchini Nigeria alisema kuwa alipata taarifa kwamba Bankole alikuwa na mipango ya kutoroka nchini humo ndiyo maana wameharakisha kumkamata. Spika huyo anadaiwa kukopa zaidi ya dola za Marekani milioni 60 benki kwa kutumia jina la Bunge wakati mkopo huo ulikuwa ni binafsi.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyombo mbalimbali vya habari vya kimataifa.


No comments:

Post a Comment