Jun 22, 2011

Hili la posho ya vikao ni aina nyingine ya ufisadi

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda

Wabunge katika Bunge la Jamhuri mjini Dodoma

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

KWA watu wenye uelewa wanafahamu fika kwamba ufisadi nchini mwetu umekua na kustawishwa na mfumo uliohalalishwa na watawala, japo tuna serikali inayojivuna kupambana na ufisadi. Kwa utamaduni huu waliojiwekea watawala wetu wa posho za vikao hata kwa mikutano ya kikazi ya idara katika mfumo mzima wa serikali na mashirika yake hauna tofauti kabisa na ufisadi tunaoupigia kelele.

Inashangaza sana hata pale kiongozi tunayemfahamu kwa uadilifu wake anapoinuka na kutetea/kuhalalisha ufisadi huu kwa kisingizio kwamba upo kisheria! Anasahau kwamba Watanzania wa leo si wa jana na wameishavuka kiwango cha kudanganywa kwa hoja dhaifu kama hizo zinazotolewa na wateule hao kuhalalisha ufisadi.

Serikali inapoamua kuhalalisha mtu alipwe mishahara miwili kwa kazi moja - kwa maana ya mshahara halisi na “mshahara posho”, ni sawa na kushiriki katika kujenga misingi ya ufisadi ambayo inapambana nayo. Bahati mbaya tumefika mahali ambapo wahusika hawawezi kuona soni kuhalalisha ufisadi kwa kuwa wanaamini kuwa wanachofanya ni halali.

Bajeti ya Serikali ya Tanzania kwa mwaka wa fedha 2011/12, imepita huku serikali ikitangaza kodi na tozo ambazo imezipunguza katika bidhaa ya petroli ili kuhakikisha bidhaa hiyo inashuka bei na kutoa ahueni ya maisha kwa wananchi.

Akihitimisha hotuba ya Bajeti ya Serikali bungeni, Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo alisema, Serikali imekubaliana na ushauri wa Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi na ushauri wa wabunge wengine kuondoa kodi na tozo kwa bidhaa hiyo ya petroli.

Kwa upande wa posho, Waziri Mkulo alisema kuwa uamuzi wa kuzifuta na kuzirekebisha baadhi ya posho hizo umefikiwa na Serikali yenyewe. Alisema katika hotuba yake alisisitiza kuwa ili kupunguza matumizi yasiyo ya lazima, Serikali itapunguza posho zisizo na tija na safari za nje ambazo hazina tija, jambo ambalo kwa mtazamo wangu ni habari njema kwa Watanzania endapo itatekelezwa na si maneno matamu ya kisiasa.

Pia waziri Mkulo alisema suala la posho limekuzwa isivyo kawaida na kwa kutumia takwimu ambazo si sahihi, huku akisisitiza kuwa posho zingine haziwezi kuondolewa kwani zipo kisheria hivyo hazifutwi na akatoa mfano wa posho za joho la jaji au posho za madaktari.

Pamoja na maelezo hayo ya Mkulo, Kambi ya Upinzani iliikataa Bajeti hiyo kwa madai kuwa hoja zao hazijazingatiwa hata baada ya baadhi kuelezwa na Mkulo kuwa zilikuwa za uongo. Kutokana na madai hayo, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Freeman Mbowe, alitangaza kurejesha gari 'shangingi' alilopewa na Bunge ili lipigwe mnada.

Mbowe pia alilitaka Bunge kufanya uamuzi mgumu wa kukubali kufutwa kwa posho ya vikao, kufutwa kwa matumizi ya magari ya kifahari kwa baadhi ya viongozi na kupambana na ufisadi katika manunuzi ya umma. Binafsi nakubaliana na Mbowe kwa asilimia mia moja kwa kuwa haiwezekani Serikali ijidai kuwa inapambana na ufisadi wakati huohuo ikipalilia na kustawisha mfumo wa ufisadi huu wa kupeana posho hata katika mazingira ambayo si sawa.
Mbowe pia alisema wamemwandikia Katibu wa Bunge kumweleza kuwa wabunge wa Chadema hawatasaini fomu za posho pamoja na kuwepo madai ya kuwa baadhi ya wabunge wa chama hicho hawakupenda kususia posho. Aliongeza kuwa baadhi ya wabunge wameitafsiri vibaya hoja hiyo ya kutaka kufutwa kwa posho za vikao kwa wabunge kwa kudhani kuwa wabunge wa Chadema wanashinikiza ili posho zote za wabunge zifutwe.

Mbowe aliwataka wabunge bila kujali itikadi za siasa kuungana pamoja na kukubali kushinikiza kuchukuliwa kwa uamuzi huo mgumu wa kufutwa kwa posho za vikao kwa wabunge na watumishi wote wa serikali ili kuliokoa taifa.

Na alibainisha kuwa yapo maeneo ambayo viongozi wa serikali wamekuwa wanalipana hadi kati ya Shilingi milioni 1.5 na Shilingi milioni mbili kama posho za kuhudhuria vikao, hatua ambayo imewalemaza viongozi wengi wa serikali na wakati mwingine kususa kushiriki vikao wanavyoona havina posho. Hii ni hatari sana kwa ukuaji wa uchumi wa nchi hii.

Kwa hali hii, kuna jambo moja nimekuwa nikijiuliza mara kwa mara, kama mfumo huu wa posho uliwekwa kwa nia njema kama ambavyo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ameutolea kauli ya kuuhalalisha, basi afahamu kuwa nia hiyo imegeuka kuwa ufisadi, na tunatakiwa kuubadilisha.

Na kama kweli suala hili la posho lilikuwa na lengo zuri kama ambavyo imesemwa basi limetumiwa vibaya kwa maslahi ya wachache wenye hulka ya ubinafsi. Ni ufisadi ambao wanaonufaika nao hawataki kukiri au kuuona kuwa ni ufisadi bali wanatumia maneno haya na yale kuuhalalisha uendelee kuwepo.

Ndio maana nimekuwa na mashaka na hiki kinachoitwa 'Utawala Bora' kwa kuwa kwa walio wengi kimegeuka kuwa wimbo mtamu unaoimbwa na kufanyiwa semina elekezi ilimradi wateule walipane posho zao, na kushibisha matumbo yao basi!

Naomba kuwasilisha...

No comments:

Post a Comment