Jun 15, 2011

Tuhuma za kuwadhalilisha wasanii wa kike zinaichafua tasnia ya filamu



 Picha hizi za juu zinawaonesha baadhi ya 
wasanii wa kike wanaounda Bongo Movie Club
 

 Hatmann Mbilinyi, mwenyekiti wa Bongo Movie Club

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

KATIKA karne hii ya 21 vyombo mbalimbali vya mawasiliano, kama vile, magazeti, simu, redio, kinasa sauti, runinga, video, mtandao na kadhalika, vinachangia sana katika kuifanya dunia yetu kuwa ndogo sana. Vinachangia pia katika kuuendeleza utandawazi, na katika usambazaji wa utamaduni wa Kimagharibi kwa nchi zetu.

Vyombo hivi vimekuwa vikitumika kwa ajili ya kujielimisha na kujiburudisha, na maendeleo ya vyombo hivi yanakua kila siku kutokana na kuvumbuliwa kwa teknolojia mpya na rahisi kutumia.

Hali hii imetufanya sisi vijana kuvutiwa sana na mambo mapya (hasa ya kigeni), hata maendeleo ya vyombo vya mawasiliano yamekuwa yanatushangaza sana. Sisi vijana tunapenda pia kuunganika daima na vijana wengine kwa njia ya kuvitumia vyombo hivi.

Dunia ya mawasiliano imeweza kuchochea ubunifu wa vijana. Imeweza kutusaidia kujielimisha na kujiburudisha. Kwani wakati mwingine huhitaji kusafiri ili kujua kile kinachoendelea Barani Ulaya au Marekani, bali kwa kutumia mawasiliano ya kiteknolojia. Aidha, imeweza kwa kiasi kikubwa kuleta mabadiliko ya kiutamaduni hasa kati yetu vijana.

Mabadiliko haya, ingawa sehemu nyingine ni chanya, lakini kwa upande mwingine yameanza kutuletea athari mbaya na tunaonekana kuelekea uelekeo ambao Wazungu wanajitahidi kuondoka kwa kuwa umeshawaletea matatizo makubwa sana.

Juzi Jumatano nilibahatika kuusoma ujumbe mmoja uliotumwa na msanii muigizaji wa filamu mmoja wa kike (jina nalihifadhi) ambao ulikusudiwa kwenda kwa viongozi wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF) akiwalalamikia kwa kutochukua hatua kutokana na kile alichodai unyanyasaji wanaofanyiwa na baadhi ya viongozi wao wa klabu inayokutana kwenye viwanja vya Leaders Club, jijini Dar es Salaam, maarufu kama Bongo Movie Club.

Ujumbe huo ulikuwa ukiwataarifu viongozi wa shirikisho la filamu kuwa kumekuwepo unyanyasaji mkubwa kwenye Club, huku ngono, majungu na ufisadi vikitawala, na ikaelezwa kuwa msanii mmoja wa kike (jina tunalo) alifanyiwa unyanyasaji na mmoja wa vigogo wa club (jina tunalo) walipokuwa ziarani Mwanza ambako walicheza na timu ya waandishi wa habari.

Hata hivyo, ujumbe huo uliendelea kueleza kwamba kiongozi mmoja wa club amekuwa na tabia ya kuwafanyia unyanyasaji mabinti na tayari ameshawafanyia vitendo kama hivyo wasanii wawili (majina tunayo), na bado kuna wengine anawahitaji, tena kwa kutishia kuwa wasipoonesha ushirikiano watapotezwa kabisa kwenye soko la filamu.

Ujumbe huo haukuishia hapo bali ulielezea pia tabia mbaya inayooneshwa na viongozi wengine wawili ambao wameamua kuigeuza Club hiyo kuwa sehemu ya kujipatia pesa kwa vigogo maarufu kama 'mapedeshee'.

Pia yapo madai kuwa club hiyo imeundwa mahsusi ikichukua sura ya danguro kwani wasanii wa kike wanaonekana kama wapo sokoni wakinadiwa kwa 'mapedeshee' na wakubwa.

Wakati leo, Ijumaa, Bongo Movie wanatarajiwa kucheza mechi yao na Wabunge mjini Dodoma, huku Dar es Salaam wameacha skendo hii ambayo hata hivyo wamejitahidi sana kuizima isijulikane kwenye vyombo vya habari kabla hawajacheza na wabunge.

Taarifa za kuaminika zinabainisha kuwa kwa siku mbili mfululizo walikuwa na vikao kwa ajili ya kuweka mambo sawa ili kuhakikisha kuwa habari hii haisambai. Hata waandishi wa habari waliowafuata kutaka ukweli walinyimwa kabisa ushirikiano!

Baada ya kupata taarifa hii nilijaribu kuwapigia simu baadhi ya waathirika wa vitendo hivi waliotajwa kwenye ujumbe huo ambao hata hivyo walisita kuniambia chochote kwa kuwa hawakuruhusiwa kabisa kuongea na vyombo vya habari, na nilipomtafuta mmoja wa viongozi anayetuhumiwa kwa unyanyasaji simu yake ilikuwa haipatikani.

Sikuishia hapo, nilimtafuta rais wa shirikisho la filamu Tanzania, Simon Mwakifwamba, ambaye alikiri kupokea ujumbe huo na kuniambia kuwa hata yeye alishangazwa na kile kinachoendelea pale na kuahidi kufuatilia ili kujua ukweli. Hadi tunakwenda mitamboni sikuwa nimepata taarifa zaidi.

Niseme tu kuwa sina uhakika na habari hizi lakini kama ni kweli basi itanisikitisha sana kuona tabia kama hizi zikijitokeza kwa watu ambao jamii inawaamini, waliopaswa kuwa mfano mzuri kwenye jamii yetu. Pia ikumbukwe kuwa mimi ni mdau muhimu kwenye tasnia hii, kwa kuwa nimekuwa naandika miongozo ya filamu, naongoza filamu na wakati mwingine nashirikishwa hata kuigiza sehemu ndogo ndogo za kupita.

Nawaheshimu sana wasanii kwani ni watu muhimu sana kwenye jamii yoyote kwa kuwa huwa wanawakilisha ujumbe mahsusi kuhusu mila, desturi na tabia za jamii hiyo kwenye jamii zingine, hivyo huchangia kwa kiasi kikubwa katika suala zima la kuwaonesha wananchi njia nzuri ya kupita, hasa katika dunia ya sasa ya utandawazi.

Sitegemei kama watu ambao jamii inawaamini kuwa kile wanachokiigiza kina mafundisho mazuri kwao leo hii ndiyo wawe wa kwanza kukengeuka, tena kwa kiwango cha kustaajabisha kinachotia kichefuchefu hata kukielezea!

Nachukua nafasi hii kuishangaa serikali kwa kuonekana kukikumbatia kikundi cha watu kadhaa ambacho hakina hata usajili wowote kwa maana ya kutambulika kisheria, lakini ndiyo kimekuwa kikipapatikiwa, kikikaribishwa na kuchukuliwa kama nembo ya tasnia ya filamu, nadhani kwa sababu tu ya umaarufu wa wahusika.

No comments:

Post a Comment