Jun 22, 2011

FREDERICK CHILUBA: Kutoka urais, kushtakiwa kwa ufisadi hadi mauti yake

 Frederick Chiluba
 
Frederick Chiluba na mkewe enzi za uhai wao
 
LUSAKA
Zambia
RAIS wa zamani wa Zambia, Frederick Chiluba, amefariki, akiwa na umri wa miaka 68. Msemaji wa rais huyo mstaafu alisema kuwa Chiluba kwa muda mrefu amekuwa akisumbuliwa kwa matatizo ya moyo na figo ambayo ndiyo yamesababisha kifo chake.

Chiluba aliingia madarakani kwa kishindo katika uchaguzi wa 1991 wakati Afrika ikiwa inaanza kuingia katika demokrasi ya vyama vingi, katika uchaguzi wa kwanza wa mfumo wa vyama vingi akichukua madaraka hayo toka kwa rais wa zamani wa nchi hiyo, Kenneth Kaunda aliyemkosoa kwa sera zake za kushindwa kukuza uchumi wa taifa hilo wakati wa mfumo wa vyama vingi ulipoanza.

Aliingia kupitia chama cha Movement for Multiparty Democracy (MMD) ambapo aliiongoza nchi hiyo hadi mwaka 2001 alipoachia madaraka. Kabla ya hapo alikuwa kiongozi wa wafanyakazi.

Aliingia madarakani wakati Zambia ilikuwa imeshafilisika, naye alipoondoka aliacha rushwa ikistawi. Mara baada ya kuingia madarakani Chiluba alibinafsisha zaidi ya makampuni 250 ya serikali hatua iliyokosolewa vikali na wapinzani wake ambao baadaye aliwakamata na kuwafungulia mashtaka.

Aling'atuka madarakani mwaka 2001 baada ya kushindwa jaribio lake la kutaka kubadili katiba ya nchi hiyo na kuiongoza nchi hiyo kwa miaka mitatu na hatimaye kumpisha marehemu Levy Mwanawasa ambaye baada ya kushika madaraka alimfungulia mashtaka ya rushwa kiongozi huyo na kupatikana na hatia.

Mwaka 2007 mahakama kuu nchini Uingereza ilitangaza kuzuia mali zote za kiongozi huyo wa zamani wa Zambia zilizokuwa na thamani ya zaidi ya dola za marekani bilioni 4. Pia Chiluba alilaumiwa sana kwa kupenda maisha ya anasa.

Akiwa madarakani Chiluba pia aliweza kushinda jaribio la kutaka kupinduliwa mwaka 1996 na wanajeshi waasi ambapo aliwakamata viongozi kadhaa wa upinzani akiwemo Kenneth Kaunda na baadhi ya waandishi wa habari akiwashutumu kuhusika na upangaji njama wa kufanya mapinduzi.

Historia yake

Frederick Jacob Titus Chiluba alizaliwa Aprili 30, 1942 na alikuwa mwanasiasa wa Zambia ambaye alikuwa Rais wa pili wa Zambia kuanzia 1991 hadi 2001. Chiluba, kiongozi wa chama cha wafanyakazi, alishinda katika uchaguzi wa rais wa vyama vingi mwaka 1991 akiwa mgombea wa Movement for Multiparty Democracy (MMD), akimwangusha rais wa muda mrefu, Kenneth Kaunda.

Alichaguliwa tena kuiongoza Zambia mwaka 1996. Kwa kuwa hakuweza kugombea katika awamu ya tatu mwaka 2001, aliyekuwa Makamu wa Rais, Levy Mwanawasa aligombea badala yake kwa chama cha MMD. Baada ya kuondoka madarakani, Chiluba alikuwa chini ya uchunguzi wa muda mrefu na kesi kuhusu madai ya rushwa, hatimaye aliachiwa huru mwaka 2009

Maisha ya awali

Alizaliwa na wazazi Jacob Titus Chiluba Nkonde na Diana Kaimba na kukulia Kitwe, Zambia. Chiluba alioa mara mbili. Frederick Chiluba alisoma katika Shule ya Sekondari Kawambwa katika eneo la Kawambwa, ambapo alifukuzwa akiwa mwaka wa pili kwa kujishughulisha na mambo ya kisiasa. Alifanya kazi ya ukondakta wa basi na baadaye akawa dereva wa basi.

Ni wakati huo ndipo alipoufahamu uwezo wake wa kuwa mwanasiasa kutokana na haiba yake. Baadaye alifanya kazi kama diwani kabla ya kuwa msaidizi wa mweka hazina wa Atlas Copco, na kupanda hadi, mjini Ndola ambako alijiunga na Umoja wa Kitaifa ya Ujenzi.

Maisha binafsi

Frederick Chiluba na mke wake wa kwanza, Vera Tembo, ambaye amezaa naye watoto tisa, walitalikiana mwaka 2000 baada ya miaka thelathini na mitatu ya ndoa. Tembo aliamua kuendelea na kazi ya kisiasa kivyake, na kuwa Mwenyekiti wa MMD wa Mambo ya Wanawake, alichaguliwa katika Bunge la Zambia, na kuwa naibu Waziri wa Mazingira mwaka 2006. Mei 6, 2002, Chiluba alioa mke wa pili, Regina Mwanza, Mwenyekiti wa zamani wa masuala ya wanawake wa MMD, mjini Lusaka.

Chiluba siku zote alionekana nadhifu sana katika umbo lake fupi (akiwa na mita 1.5). Kuhusiana na madai ya rushwa kwa nchi za Ulaya dhidi yake katika miaka ya 2000 mwishoni, iligundulika kwamba duka la Uswisi lilizalisha jozi 100 za viatu namba 6 kwa ajili yake vikiwa na visigino inchi mbili, vingi vikifanana. Muonekano wake makini na suti nzuri vikawa ndiyo nembo yake, na vilibainishwa wakati wa kesi yake ya rushwa.
Katika mfano mkali, mwandishi wa gazeti la Zambia Post, Roy Clarke ambaye ni mwandishi wa safu ya mara kwa mara ambayo ilimshutumu Rais wakati alipokuwa madarakani alimfananisha kama "kazi bure, msalaba-wenye mavazi, mvaa-visigino virefu, mgoni, kibete".

Wapinzani wake wa kisiasa walimbeza wakati wakikosoa utawala wake. Michael Sata, kwa mfano, alimshutumu Chiluba kwamba "uwezo wake wa kufikiri ni mrefu kama kimo chake... hatuibi fedha, hatuteki nyara, hatununui suti, hatununui viatu. Hatuhongi wasichana nyumba..."
Kaunda aliyejulikana kwa Chiluba kama "kibete mwenye futi nne" wakati wa kupanda kwa Chiluba katika ulingo wa siasa za upinzani. Chiluba aliachiwa huru kutokana na mashitaka ya rushwa mwezi Agosti 2009. Chiluba alielezewa na BBC kama "Mkristo motomoto aliyezaliwa mara ya pili... ambaye "...maisha yake binafsi yalikuwa kiini cha uvumi mwingi."

Vyama vya Wafanyakazi

Chiluba alishinda uenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Zambia (ZCTU). Yeye na viongozi kadhaa katika ZCTU waliwekwa kizuizini mwaka 1981 na Rais Kenneth Kaunda kwa kuanzisha mgomo mkubwa uliopoozesha zaidi uchumi wa Zambia. Viongozi hao wa vyama waliachiwa baada ya Jaji kusema kuwekwa kwao kizuizini ilikuwa kinyume cha katiba. Mwaka 1987, alifanikiwa kuleta changamoto ya uenyekiti wake wa NUBEGW, ambao uliiweka nafasi yake ZCTU katika hatari.

Siasa

Mwaka 1990 alisaidia kuundwa kwa Movement for Multiparty Democracy (MMD), chama ambacho, Chiluba kama mgombea wake wa urais, kilifanikiwa na kuleta changamoto kubwa katika utawala wa Kaunda katika uchaguzi wa 1991. Chiluba alikuwa mzungumzaji mzuri mwenye kipaji cha asili. Chiluba aliingia madarakani Novemba 2 mwaka huo. Alishinda tena katika uchaguzi huo kwa kipindi cha pili cha miaka mitano mwaka 1996, licha ya kesi ya kuhoji uzawa wake.

Chiluba alijaribu kumfukuza nchini humo Kaunda kwa madai kuwa alikuwa na asili ya Malawi. Alifanya marekebisho ya katiba ili kuzuia wananchi wenye asili ya kigeni kugombea urais, kwa lengo la kumfanya Kaunda asigombee. Baadhi ya wagombea katika uchaguzi wa rais wa 1996 walidai Chiluba hakustahiki, kwa madai kwamba yeye au baba yake alizaliwa Zaire. Hata hivyo, hakuna shaka kwamba alilelewa katika eneo la Copperbelt la Zambia.

Mwishoni mwa 2001, Chiluba alimtaliki mke wake, Vera, ambaye wamezaa watoto tisa; Helen, Miko, Hortensia, Castro, Chongo, Kaindu, Hulda, Frederick Jr na Verocia. Kwa mke wake mwingine wana watoto, Tito na Nikombe.

Baadaye alimuoa Mwenyekiti wa Wanawake wa MMD, Regina Mwanza, aliyekuwa katalikiwa. Pamoja na chama chake kushinda kwa wingi katika bunge, alishindwa kuungwa mkono katika jitihada zake za marekebisho ya katiba kuruhusu kugombea awamu ya tatu. Hakuna mbunge aliyeongoza msukumo kufanyia marekebisho katiba ya nchi, serikali haikuwahi kuwasilisha pendekezo lolote juu ya jambo hilo wala hapakuwa na kura ya maoni ya kurekebisha katiba ya nchi.

Mjadala mrefu wa tatu ulikuwa kati ya makundi mbalimbali ndani na nje ya chama cha MMD. Chiluba mwenyewe alikuwa kimya kuhusu hilo. Aliachia ngazi mwishoni mwa muhula wake siku ya Januari 2, 2002, na nafasi yake kuchukuliwa na Levy Mwanawasa, makamu wake wa rais. Chiluba katika uongozi wake alianza kama mjamaa, lakini akikubali mageuzi kadhaa ya kiuchumi.

Ufisadi

Baada ya kuondoka madarakani, Chiluba alikuwa shabaha ya kampeni za Mwanawasa dhidi ya rushwa: Februari mwaka 2003, alishtakiwa pamoja na wakuu wake wa zamani wa usalama, mawaziri wa zamani kadhaa na viongozi waandamizi, kwa makosa 168 ya wizi wa jumla ya zaidi ya dola 40m.

Ilidaiwa kuwa fedha zilihamishwa kutoka Wizara ya Fedha hadi akaunti iliyopo tawi la London la Benki ya Biashara ya Zambia (Zanaco). Chiluba alisema akaunti hiyo ilitumiwa na huduma za usalama wa nchi kufadhili shughuli za nje ya nchi. Mashtaka mengi yaliyofunguliwa dhidi yake baadaye yalifutwa, lakini mengine yalibaki. Aidha, mke wake Regina alikamatwa kwa kupokea bidhaa za wizi.

Kifo

Chiluba amefariki Jumamosi ya Juni 18, 2011, muda mfupi baada ya usiku wa manane. Msemaji wake, Emmanuel Mwamba, alitangaza kifo chake. Mwamba alisema kuwa Chiluba alikuwa na siku ya kawaida Juni 17, na hata alikuwa na muda wa kukutana na baadhi ya wanasheria wake. Baadaye alianza kulalamika kuhisi maumivu ya tumbo.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa mashirika mbalimbali ya habari ya kimataifa

No comments:

Post a Comment