Jun 15, 2011

FAZUL MOHAMMED: Kifo chake chaleta ahueni katika Afrika Mashariki

 Fazul Abdullah Mohammed

MOGADISHU
Somalia

KUUAWA kwa kiongozi wa Al Qaeda katika Afrika Mashariki, Fazul Abdullah Mohammed, mjini Mogadishu Somalia, kumewafanya wakazi wa kanda hii kupumua kidogo. Serikali ya mpito ya Somalia ilisema kuwa Fazul Mohammed aliuawa kwa kupigwa risasi siku ya Jumatano Juni 8, 2011, na ukaguzi wa DNA umethibitisha kuwa ni yeye.

Kifo chake kinafuatia shutuma alizokuwa akipewa na Marekani kuwa alipanga mashambulio ya kigaidi ya mwaka wa 1998 dhidi ya balozi za Marekani nchini Kenya na Tanzania, na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 224.

Mchambuzi wa masuala ya kisiasa na mwandishi wa habari, Ahmed Rajab, amekaririwa akisema: “Si ajabu kuwa Fazul ameuawa mjini Mogadishu, kwa sababu kwa muda mrefu akijulikana kuwa alikuwa kamanda wa kikundi cha wapiganaji wa Somalia, al Shabab. Lakini tukumbuke kulikuwa na taarifa zamani kwamba aliuliwa na Marekani, na taarifa hizo zikawa si za kweli”.

Kikundi cha al-Shabab kimekanusha taarifa na kusema kuwa Fazul Mohammed hakuuawa.

Rais wa Somalia, Sheikh Sharif Sheikh Ahmed, ametoa maelezo zaidi kuhusu kuuawa kwa kiongozi huyo wa Al Qaeda Afrika Mashariki. Rais huyo alisema kuwa Marekani ilisaidia kuthibitisha utambulisho wa Mohammed, na ukaguzi ulifanywa nje ya nchi.

Aliwaonesha waandishi wa habari, ile ambayo alisema, ni hati ya kuzaliwa ya Fazul Mohammed, picha za familia yake, na ramani ya pengine malengo ya kushambulia mjini Mogadishu.

Waziri wa Mashauri ya Nchi za Nje wa Marekani, Hillary Clinton, amevipongeza vikosi vya serikali ya Somalia kwa kufanikiwa kumuua mtu huyo ambaye ni mmoja wa watuhumiwa wakuu wa ugaidi waliohusika na mlipuko wa mabomu katika balozi za Tanzania na Kenya mwaka 1998. Clinton alikuwa Tanzania na kuweka shada la maua kwenye jengo la ubalozi wa Marekani, lililoshambuliwa kwa bomu na Al Qaeda mwaka 1998.

Clinton amesema kuuawa kwa Mohammed ni ushindi kwa nchi ya Somalia na dunia kwa ujumla wakati huu ambapo dunia inapambana kutokomeza vitendo vya ugaidi duniani.

Clinton aliyasema hayo muda mfupi baada ya kuwasili katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es slaam Tanzania kwa ziara ya siku tatu. Mohammed amekuwa akisakwa kwa udi na uvumba na serikali ya Marekani kuhusiana na kushiriki kupanga njama za kulipua ubalozi wa Marekani nchini Tanzania na Kenya.

Mara baada ya kutekeleza shambulio hilo Mohammed alikimbilia Somalia ambako mwaka 2007 alinusurika katika shambulio la vikosi vya Marekani na hakuonekana tena mpaka alipouawa na vikosi vya Somalia mjini Mogadishu.

Msemaji wa polisi mjini Mogadishu amesema kuwa Mohammed aliuawa alipokuwa akijaribu kuwatoroka polisi ambapo kulitokea majibizano ya risasi kati yao na baadaye kufanikiwa kumuua.

Afisa huyo ameongeza kuwa awali hawakubaini kama ni Mohammed hadi walipofanikiwa kupekua begi alilokuwa amebeba na kukuta ana pasi ya kusafiria ya Afrika Kusini yenye jina la Daniel Robinson. Mbali na mtuhumiwa huyo kukutwa na pasi hiyo ya kusafiria ya Afrika Kusini pia walimkuta na kiasi cha dola za Marekani elfu arobaini.

Historia yake:

Fazul Abdullah Mohammed alizaliwa Agosti 1972, au Februari 25, 1974, au 25 Desemba 1974. Alikuwa mwanachama wa al-Qaeda, na kiongozi katika Afrika Mashariki kuanzia Novemba 2009. Mohammed alizaliwa visiwa vya Moroni, na alikuwa na uwezo wa kuongea lugha za Kingereza, Kifaransa, Kiswahili, Kiarabu na Kingazija.

Nafasi katika al-Qaeda

Mohammed na watu wengine kadhaa walikuwa wanakabiliwa na mashitaka nchini Marekani kwa madai ya kushiriki katika mashambulizi ya balozi za Marekani mwaka 1998 Afrika ya Mashariki. Mohammed alikuwa kwenye orodha ya FBI ya magaidi wanaosakwa zaidi tangu kuanzishwa kwake Oktoba 10, 2001. Yalitangazwa malipo kwa ajili ya kumtafuta Mohammed ya dola za Marekani milioni 5.

Nchini Kenya, Mohammed aliwahi kuwa katibu, na kuishi katika nyumba moja na, Wadih el-Hage. El-Hage alishtakiwa na amekutwa na hatia. Kuna barua ilioneshwa iliyoandikwa kwenda kwa el-Hage, ilidhaniwa kutoka kwa Mohammed.

Mohammed alitumia muda wake mwingi akiwa Mogadishu akipanga mipango ya kuandaa lori lenye mabomu dhidi ya Umoja wa Mataifa ulioanzishwa nchini humo, na alikuwepo mjini hapo Oktoba 3, 1993, wakati wanamgambo wa Somalia walipoziangusha helikopta mbili za Marekani na kuua wanajeshi 18 wa kikosi maalum.

Vita dhidi ya ugaidi:

Mohammed anatuhumiwa kuhusika katika mashambulizi mawili mjini Mombasa, Kenya mnamo Novemba 26, 2002. Shambulio moja likihusisha lori lililotegwa bomu katika hoteli ya Paradise, ambapo 15 waliuawa. Jingine ni lile la uzinduzi wa makombora mawili kwenye shirika la ndege la Israel; hakukuwa majeruhi.

Mei 26, 2004, Mwanasheria Mkuu wa Marekani, John Ashcroft na Mkurugenzi wa FBI, Robert Mueller walitangaza kuwa ripoti ilionesha kuwa Mohammed alikuwa mmoja kati ya watu saba wanachama wa al Qaeda waliokuwa na mipango ya kigaidi wakati wa majira ya kiangazi mwaka 2004.

Kulingana na ripoti ya mahojiano ya FBI, mmoja wa washirika wake alikiri kwamba wapiganaji hao walipewa mafunzo na al-Qaeda na Osama Bin Laden nchini Afghanistan. Ahmed Ghailani, pia katika orodha hiyo, alikamatwa nchini Pakistan mwezi mmoja baadaye. Mara baada ya hapo, vyombo kadhaa vya habari vikatoa taarifa, vikidai vyanzo rasmi vya Umoja wa Mataifa na Marekani, vilielezea ushiriki wa wanachama kadhaa wa al-Qaeda, wakiwemo Mohammed na Ghailani, kujihusisha na harakati na kununua almasi nchini Liberia.

Wakati meli ya MV Bukoba ilipozama katika Ziwa Victoria mwaka 1996, na kusababisha kifo cha mwanzilishi mwenza wa al-Qaeda, Abu Ubaidah al-Banshiri, Mohammed ndiye aliyepelekwa eneo hilo la ajali na al-Qaeda, ili kuthibitisha kwamba Abu Ubaidah alikuwa amekufa.

Mwaka 2007, wakati wa Vita ya Somalia, inaaaminiwa kuwa Mohammed alikuwa katika mpaka karibu na eneo la Ras Kamboni akishirikiana na Muungano wa Mahakama za Kiislamu. Januari 8, 2007, ndege ya kivita ya Marekani, AC-30 iliwashambulia al-Qaeda katika eneo hilo.

Kuna uwezekano kuwa yeye ndiye aliyekuwa mlengwa, kama Pentagone walivyosema: "Mlengwa alikuwa ni kiongozi muhimu wa al-Qaeda katika kanda." Viongozi wa serikali ya Somalia walisema kuwa kifo chake kilithibitishwa katika ripoti ya kiusalama iliyokabidhiwa Somalia na mamlaka ya Marekani. Hata hivyo, katika mahojiano na Shirika la Habari la Uingereza, BBC, balozi wa Marekani nchini Kenya, Michael Ranneberger, alikana kwamba Mohammed hakuwa ameuawa katika mashambulio ya anga, na alisema kuwa msako wa watuhumiwa watatu wa al-Qaeda bado unaendelea.

Mashambulizi hayo yalisababisha vifo vya raia wasiopungua 70 na wengine wengi kujeruhiwa zaidi wakati walipokuwa wakitafuta chanzo cha maji usiku. Akasema kuwa mabaki ya Mohammed, kama yakipatikana yanaweza kutambuliwa kwa msaada wa sampuli ya DNA nchini Comoro.

Mmoja wa wake wa Mohammed na watoto wake walikamatwa wakijaribu kutorokea Kenya wakitokea Somalia. Walikamatwa katika eneo la Kiunga na kupelekwa Nairobi kwa ajili ya mahojiano. Kabla ya mke wa Mohammed kurudishwa Somalia na serikali ya Kenya, kompyuta aliyokuwa nayo ilidhaniwa kuwa ya Mohammed na kwamba kulikuwa na uwezekano "ilikusanya taarifa muhimu za kigaidi juu ya mafunzo na ukusanyaji wa taarifa za kiusalama ikiwa ni pamoja na upelelezi." Mohammed aliaminika "kuwa mtaalamu mzuri katika kompyuta".

Wakati ikiwa haijathibitishwa kama Mohammed alitoroka mapigano nchini Somalia au alikuwepo huko wakati machafuko yakitokea, gazeti kubwa la nchini Madagascar, Midi Madagasikara, liliripoti mnamo Februari, 2007, kwamba Mohammed alikuwa akiishi katika kisiwa cha taifa hilo. Hii ilikuwa tofauti na taarifa za Abdirizak Hassain, akisema kwamba Mohammed aliuawa katika vita ya Ras Kamboni na mashambulizi ya anga ya Marekani. Likinukuu taarifa za kijeshi na "vyanzo vingine," gazeti lilidai kuwa alikuwa katika mji wa Mahajanga.

Agosti 2, 2008, Mohammed aliwatoroka polisi huko Malindi, Kenya, lakini wasaidizi wake wawili walikamatwa. ilisemekana kuwa alipelekwa Kenya kutoka Somalia siku chache kabla, kwa matibabu ya matatizo ya figo. Polisi walitaifisha pasipoti zake mbili na laptop, miongoni mwa mali nyingine. Operesheni ya polisi ilifanyika siku kadhaa kabla ya kumbukumbu ya maadhimisho ya miaka 10 tangu mabomu ya Ubalozi 1998.

Novemba 11, 2009 Mohammed alisimikwa kuwa kamanda katika sherehe ya wazi Kusini mwa Somalia katika mji wa Kismayo, kulingana na tafsiri iliyopokewa na kuchapwa na jarida la The Long War, na tovuti inayowaunga mkono waasi, inayoendeshwa na ukoo wa Kisomalia, wa Hawiye. Kwa mujibu wa tovuti hiyo, alitoa "hotuba yake ndefu".

Akizungumzia kuteuliwa kwake na Osama Bin Laden na kumsifu mtangulizi wake, Saleh Ali Saleh Nabhan, aliyeuawa na kikosi maalum cha majeshi ya Marekani katikati ya mwezi Septemba, Mohammed alikubali jukumu lake wakati wa mabomu ya ubalozi wa Marekani mwaka 1998 ya Kenya na Tanzania. Aliahidi kuwa al-Qaeda na Shabaab watapambana na nchi jirani. Na kuapa kuwa "Baada ya Somalia tutaendelea Djibouti, Kenya na Ethiopia."

Baada ya mashambulizi ya Kampala, Julai 2010 nchini Uganda, yaliyowalengwa watu waliokuwa wakiangalia fainali ya Kombe la Dunia, kiongozi wa kiroho wa al-Shabaab, Sheikh Mukhtar Abu Zubayr alitishia kufanya mashambulizi zaidi katika ardhi ya kigeni, hasa Burundi na Uganda, kutokana na kuwepo kwa askari wa kulinda amani kutoka nchi hizo huko Somalia.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment