Aug 24, 2011

ANNA HAZARE: Mwanaharakati India anayeitoa jasho serikali kuhusu ufisadi

Anna Hazare

India

MWANAHARAKATI nguli nchini India, Anna Hazare, ameweka nadhiri ya kufanikisha mapinduzi nchini mwake wakati huu ambapo ameanza kutekeleza ahadi yake ya kufunga kula na kunywa kwa kipindi cha siku kumi na tano.

Mwanaharakati huyo anahurumiwa na wengi nchini India na tayari maandamano ya kumuunga mkono yanazidi kuvutia idadi kubwa ya watu kote nchini humo. Hazare anashinikiza kufanyika kwa mageuzi katika sheria za kupambana na rushwa na alikuwa amepanga kuanza kukesha bila chakula ili kushinikiza hilo lifanyike.

Watu wengi wanaomuunga mkono wamejitokeza na mabango huku wakikemea serikali wakitaka aachiwe huru. Raia hao wa India wanasema lazima serikali ichukue hatua za kukabili ufisadi uliokithiri nchini humo.

Uamuzi wa Mwanaharakati Hazare una lengo la kuishinikiza serikali nchini India kutunga sheria kali zaidi dhidi ya viongozi ambao wanajihusisha na vitendo vya ulaji rushwa vilivyotawala kwenye taifa hilo.

Hazare aliitaka serikali kushughulikia mapendekezo yake ya namna ya kushughulikia suala la rushwa siku moja baada ya kufanyika kwa sherehe za kumbukumbu ya uhuru wa nchi hiyo ambapo Waziri Mkuu, Manmohan Singh alitangaza mikakati ya kukabiliana na hali hiyo.

Hata hivyo, Singh, amemkosoa mwanaharakati huyo akisema, ingawa nia yake ni nzuri anatumia dhana potofu kulazimisha bunge lifuate matakwa yake. Mshirika wa karibu wa Hazare amesema kuwa sasa amekubali kuondoka jela baada ya polisi kuridhia kuwa anaweza kufanya mgomo huo wa kususia chakula kwa siku kumi na tano kwenye bustani moja mjini Delhi.

Hazare na wafuasi wake wapatao 1,200 walitiwa nguvuni na polisi wakiwa kwenye bustani ya JP Park saa chache kabla hawajaanza kususia chakula.

Mwezi April Hazare alivunja mgomo wake wa kususia chakula baada ya siku nne pale serikali ilipokubali kuwa anaweza kuhusika kuandaa muswada wa kupambana na ufisadi nchini humo ambapo kutakuwa ofisi maalum ya kuchunguza wanasiasa na watumishi wa serikali wanaoshukiwa kuhusika na ufisadi.

Serikali ya Waziri Mkuu Singh imekuwa ikikosolewa vikali kutokana na kushindwa kudhibiti vitendo vya ulaji rushwa ambavyo vimekuwa vikifanywa na baadhi ya mawaziri.

Historia yake

Kisan Baburao Hazare, maarufu kama ya Anna Hazare amezaliwa Juni 15, mwaka 1937 ingawa machapisho mengine yanaonesha kuwa alizaliwa Januari 15 mwaka 1940 katika eneo la Bhingar, Ahmednagar, wilaya ya Maharashtra.

Baba yake alikuwa mfanyakazi asiyekuwa na ujuzi wowote na alimiliki ekari 5 ya ardhi kwa ajili ya kilimo. Hali mbaya ya kilimo iliisukuma familia yao katika mtego wa umaskini na mwaka 1952, Hazare alihamia katika nyumba yake ya mababu huko Ralegan Siddhi. Alilelewa na mama mmoja asiye na mtoto aliyemlipia pesa kwa ajili ya elimu yake mjini Mumbai, lakini kukosekana kwa fedha kulimsukuma kuuza maua kwa ajili ya kuishi na aliacha masomo baada ya darasa la saba.

Mara baada ya kuajiriwa katika Jeshi la India na kupatiwa mafunzo ya udereva wa magari aliajiriwa mjini Punjab. Siku zake katika utumishi wa Jeshi alizitumika kusoma vitabu mbalimbali vya falsafa za wanafalsafa wakubwa kama Swami Vivekananda, Mahatma Gandhi na Acharya Vinoba Bhave. Mawazo yao ndiyo yaliyomuongoza kujitoa maisha yake kwa kazi ya jamii.

Makala hii imeandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa mashirika mbalimbali ya habari
 

No comments:

Post a Comment