Aug 24, 2011

JORGE CARLOS FONSECA: Mpinzani aliyeshinda urais wa Cape Verde

Jorge Carlos Fonseca

Cape Verde

JORGE Carlos Fonseca, mgombea wa upinzani ameshinda katika uchaguzi wa urais wa Cape Verde, dhidi ya Manuel Inocencio Sousa, kutoka chama tawala. Fonseca alipata takriban asilimia 55 ya kura zote katika duru ya pili ya uchaguzi siku ya Jumapili, ukilinganisha na Sousa aliyepata asilimia 45.

Fonseca kutoka chama cha upinzani cha Movement For Democracy (MFD), alishinda kwa zaidi ya asilimia 37 ya kura zilizopigwa katika duru la kwanza la uchaguzi, kabla ya uchaguzi wa marudio uliomwingiza madarakani.

Viongozi hao wawili wamewania nafasi hiyo baada ya Rais Pedro Pires kung'atuka kufuatia kumaliza vipindi vyake viwili.
Wachambuzi wanasema, Cape Verde ni moja ya nchi zenye demokrasia thabiti barani Afrika.

Fonseca, mwenye umri wa miaka 60, aliyekuwa waziri wa mambo ya nje alisema atalenga zaidi kuujenga uchumi wa Cape Verde. Amenukuliwa na shirika la habari la AFP akisema, "ushindi wangu ni wa kidemokrasia, kwa heshima ya watu wa Cape Verde walioamini mipango yangu."

Historia yake

Jorge Fonseca Carlos de Almeida amezaliwa 20 Oktoba 1950, ni mwanasiasa, mwanasheria na profesa wa chuo kikuu, ambaye kwa sasa ndiye mshindi wa urais wa Jamhuri ya Cape Verde, kutoka chama cha Movement for Democracy (MfD).

Jorge Fonseca alimaliza elimu yake ya msingi na ya sekondari kati ya Praia na Mindelo, na baadaye, elimu yake ya juu mjini Lisbon. Alihitimu shahada ya kwanza katika Sheria na shahada ya uzamili wa Sheria katika Kitivo cha Sayansi ya Sheria, Chuo Kikuu cha Lisbon.
Alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa uhamiaji wa Cape Verde kati ya 1975 na 1977, na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Cape Verde kati ya 1977 na 1979.

Alikuwa mkufunzi msaidizi wa Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha Lisbon kati ya 1982 na 1990, Profesa mwalikwa wa sheria ya jinai katika Taasisi ya Tiba kuchunguza mauaji ya Lisbon mwaka 1987 na mkurugenzi mkazi na profesa mwalikwa katika kozi ya Sheria na Utawala katika Chuo Kikuu cha Asia ya Mashariki, Macau mwaka 1989 na 1990. Pia alikuwa profesa msaidizi na mwenyekiti wa bodi ya Taasisi ya Sheria na Sayansi ya Jamii katika Cape Verde.

Kati ya 1991 na 1993 alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje katika serikali ya kwanza ya Jamhuri ya Pili, na mgombea wa Rais wa Jamhuri mwaka 2001, nafasi ambayo ameitumia tena katika uchaguzi wa Agosti 7, 2011, wakati huu kwa kutumia chama cha upinzani cha MfD, na kushinda katika raundi ya 1 (kwa asilimia 38 ya kura) na duru ya pili, na hivyo kuwa Rais wa nne katika historia ya uhuru wa Cape Verde.

Pia ni mwanzilishi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa taasisi ya “Direito e Justica”, mwanzilishi na mkurugenzi wa gazeti la “Direito e Cidadania”, mshiriki wa gazeti la “Revista Portuguesa de Ciência Criminal”, na mwanachama wa bodi ya wahariri ya “Revista de Economia e Direito”.

Pia ni mwandishi wa vitabu kadhaa na makala zaidi ya hamsini za kisayansi na kiufundi katika uwanja wa sheria, na amechapisha vitabu viwili vya mashairi. Amepewa tuzo kadhaa na Serikali ya Cape Verde.

Makala hii imeandaliwa na Bishop Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment