Aug 24, 2011

Kanali Gaddafi alishakosa uhalali wa kuongoza

Kanali Muammar Gaddafi

 Waasi wakikanyanga sanamu ya Gaddafi

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

WAKATI naandika makala hii (siku ya Jumatano), kulikuwepo taarifa za waasi kuyazingira na kuyadhibiti makazi ya kiongozi wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi, mjini Tripoli, huku taarifa zingine zinasema kuwa kiongozi huyo ameapa kupigana na waasi hao hadi kifo au ushindi.

Televisheni inayomuunga mkono Kanali Gaddafi, al-Urubah, imesema kuwa kiongozi huyo ambaye bado hajulikani alipo, ametoa hotuba akisema kuwa kuondoka kutoka kwenye makazi yake kulikuwa ni “mpango”. Makazi hayo ndiyo yaliyokuwa maeneo ya mwisho chini ya udhibiti wa Kanali Gaddafi mjini Tripoli.

Waasi wamekuwa wakisheherekea mafanikio yao katika bustani ya Green Square, mjini Tripoli huku picha za televisheni zikiwaonesha wapiganaji hao wakiivunja sanamu ya kiongozi huyo na kuipiga mateke baada ya kuuteka Bab al-Aziziya siku ya Jumanne.

Akizungumza na redio moja mjini Tripoli, Kanali Gaddafi ameahidi “kifo au ushindi” katika mapigano dhidi ya majeshi ya NATO na waasi wa Libya, redio ya al-Urubah ilisema.

Siku za nyuma Kanali Gaddafi aliwahi kukaririwa kusema ameleta heshima kwa Libya, jambo ambalo siwezi kubisha kwani inaeleweka wazi kuwa Gaddafi amewasaidia sana wananchi wake katika mambo fulanifulani. Amefanikiwa sana kukuza uchumi wa Libya na kuwafanya waishi kama wapo peponi, lakini hiyo haikumpa uhalali wa kukiuka misingi ya haki za binadamu na kutaka kutawala milele pamoja na kuanzisha utawala kama wa kisultani.

Uhalali wa utawala wake uliisha pale alipoamuru jeshi kuwashambulia kwa risasi za moto wananchi waliokuwa wanaandamana na hivyo kupoteza kabisa uhalali wa kuongoza. Wengi waliokuwa wakimshangilia ilikuwa ni katika kujikomba tu, au walifanya hivyo kwa hofu ya kupoteza maisha yao.

Azimio la Umoja wa Mataifa kuhusu Haki msingi za Binadamu linatamka bayana na kusisitizia uhuru wa mawazo, hii ni dhamana ya kila Serikali kuhakikisha kwamba, watu wake wanatekelezewa uhuru huo, badala ya kuendekeza dhuluma, ubaguzi na mateso hata kama umesaidia kukua kwa uchumi wa nchi.

Kilichokuwa kinaendelea Libya kinaakisi hali halisi ya kisiasa katika bara la Afrika, nchi nyingi katika bara hili bado zina changamoto kubwa kama vile: kudumisha misingi ya haki na amani pamoja na kutetea zawadi ya maisha hasa ya wale ambao ni wanyonge zaidi ndani ya jamii.

Wakenya bado wanakumbuka kwa namna ya pekee, machafuko ya kisiasa yaliyojitokeza kunako mwaka 2007 mara baada ya uchaguzi mkuu. Si rahisi kufuta picha ya mateso na mahangaiko ya wananchi wa Kenya katika kipindi hiki, mateso ambayo hayakuwa na msingi wowote ule!

Uvunjwaji wa haki za binadamu ni tatizo kubwa barani Afrika. Sheria mbaya, mahakama zisizokuwa huru, na vyombo vya dola vinavyofanya kazi kwa kufuata matakwa binafsi ya viongozi wa serikali, badala ya katiba na sheria, vimesababisha haki za binadamu katika nchi zetu kuwa katika hali mbaya.

Kimsingi shughuli zote za mwanadamu na mahusiano ya watu hapa duniani yalipaswa kuwa ni kwa ajili ya kuboresha hali yake kimwili, kiakili, kiroho na kuongeza ubora wa mahusiano yake na viumbe wengine. Hivyo, mchakato wa kila shughuli afanyayo ulipaswa kuwa katika namna ambayo haina dhuluma, uonevu, madhalilisho, taabu, ubaguzi, wala vikwazo kwa mwanadamu awaye yeyote na kwa kiumbe hai kingine chochote.

Kilele cha uwepo wa haki ni kuzalishwa na kutunzwa kwa furaha ya jamii na ya dola. Jamii kamwe haiwezi kuwa na furaha ya kweli kama haki haitawali na wala dola haliwezi kusimama imara pasipo kutunzwa kwa kiwango kikubwa haki ndani ya mipaka ya dola husika.

Jamii zote za wanadamu zina mfumo wa kimsingi wa kijamii, kiuchumi, na taasisi za kisiasa zilizo rasmi na zisizo rasmi. Ili kutambua kama mfumo fulani unaathiri mipangilio ya kijamii na una uhalali, mtu hana budi kutazama kukubalika kwa mfumo huo miongoni mwa watu wanaoongozwa na mfumo husika.

Uhuru wa kisiasa (mfano kuwepo kwa taasisi za demokrasia ya uwakilishi, uhuru wa kujieleza, wa vyombo vya habari na wa kukusanyika) uhuru wa kujumuika na kushirikiana na wanajamii uhuru wa mtu kwenda atakako na kuchagua kazi aitakayo bila kukinzana na misingi ya uadilifu, uhuru wa kupata haki binafsi zinazolindwa na utawala wa sheria.

Alamsiki

No comments:

Post a Comment