Aug 17, 2011

JULIUS MALEMA: Kinda wa Afrika Kusini aliyezua utata masuala ya mashauri ya nchi za nje

Julius Malema

AFRIKA KUSINI

NI kama ilivyokuwa wakati viongozi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) walipotoa tamko katika mkutano wa wajumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la Umoja huo na Jukwaa la Wahariri Tanzania, kwenye hoteli ya Peacock, mjini Dar es Salaam, kukemea bila woga, ndivyo ilivyotokea nchini Afrika Kusini kwa kiongozi mkakamavu wa tawi la vijana la chama tawala cha ANC, Julius Malema, ingawa ni kwa aina tofauti kidogo.

Julius Malema aliingilia kati masuala ya mashauri ya nchi za nje, alipotoa wito kuwa serikali ya nchi jirani ya Botswana, iliyochaguliwa kwa njia ya kidemokrasia inafaa kupinduliwa. Hata hivyo, tawi hilo la vijana la ANC, limeomba msamaha kwa chama.

Mapema mwezi huu, ANC ilililaumu vikali tawi lake la vijana, na kiongozi wake, Julius Malema, kwa matamshi hayo.

Historia yake

Julius Malema Sello amezaliwa 3 Machi 1981, katika eneo la Seshego, ni kijana mwanasiasa wa Afrika Kusini, na Rais wa Tawi la Vijana wa African National Congress (ANC). Malema yupo kwenye nafasi tata ya kisiasa nchini Afrika Kusini; akiibukia kwenye umaarufu kwa msaada wa rais wa ANC, na baadaye Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma.

Malema amekuwa akielezewa na wote, Zuma na Waziri Mkuu wa Limpopo kama "kiongozi wa baadaye" wa Afrika Kusini. Lakini pia amekuwa akitafsiriwa na wengine kama “maarufu asiyejali” mwenye uwezekano wa kuidhoofisha Afrika Kusini na cheche za ubaguzi wa rangi. Alipatikana na hatia ya kutumia lugha ya chuki mnamo Machi 2010.

Maisha ya awali na kazi

Malema alizaliwa katika eneo la Seshego, Mama yake alikuwa mfanyakazi wa ndani na mzazi pekee aliyemlea mwanaye. Alijiunga na Masupatsela ya ANC katika umri wa miaka tisa au kumi ambapo kazi yake kubwa ilikuwa ni kuyaondoa (kuyachana) mabango na matangazo yote ya chama cha National (mpinzani wa ANC) kinyume cha sheria.

Elimu

Ilimchukua Malema miaka minne kumaliza darasa la 8 na 9 la shule ya sekondari. Alimaliza darasa la 12 katika Shule ya Juu ya Mohlakaneng katika eneo la Seshego, Limpopo, akiwa na umri wa miaka 21, baada ya kuwa mtoro wa shule kwa muda wa miezi mitano katika mwaka huo. Matokeo yake ya mtihani wa darasa la 12 yaliyoonesha kupata alama mbaya yalichapishwa katika gazeti la taifa mnamao Oktoba 2008, yakionesha kumkejeli.

Kazi ya siasa

Malema alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa tawi la vijana la Seshego na mwenyekiti wa kikanda mwaka 1995. Mwaka 1997 akawa mwenyekiti wa Shirikisho la Wanafunzi wa Afrika Kusini (Cosas) wa jimbo la Limpopo, na alichaguliwa kuwa rais wa kitaifa wa shirikisho hilo mwaka 2001. Mwaka 2002, Malema aliongoza maandamano ya Cosas ya wanafunzi, katika mitaa ya Johannesburg yaliyofunikwa na matukio ya ghasia na uporaji.

Kiongozi wa Vijana wa ANC

Malema alichaguliwa kuwa rais waVijana wa ANC mwezi Aprili 2008. Uchaguzi - na mkutano – ulioelezewa na kile ambacho Malema mwenyewe alikisema baadaye kuwa "mwenendo wa yanayotokea". Uadilifu wa uchaguzi wake umekosolewa na kuhojiwa. Alichaguliwa tena bila ya kupingwa kwa awamu ya pili mnamo 17 juni 2011.

Ziara ya Zimbabwe, Aprili 2010
3 Aprili 2010, Malema alitembelea Zimbabwe, kwa kile kilichoelezwa kama ziara ya uzawa. Alitarajiwa kukutana na Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe. Alipotua Harare, Malema alisalimiwa na wafuasi wa Zanu-PF pamoja na Waziri wa Vijana na Uzawa wa Zimbabwe, Mwokozi Kasukuwere, na Mwenyekiti wa Vijana wa Zanu-PF, Absolom Sikhosana, pamoja na wafanyabiashara maarufu wa Zimbabwe.

Morgan Tsvangirai, Waziri Mkuu wa Zimbabwe, aliishutumu ziara ya Malema, baada ya Malema kukikosoa chama cha Tsvangirai, cha MDC. Wakati wa ziara hiyo, Malema alimuelezea Tsvangirai kama mshirika wa "mabeberu". Mashirikisho ya Vijana wa Zimbabwe yaliikosoa ziara ya Malema, yakitoa maelezo yake ya ubaguzi wa rangi na madai ya rushwa. Wakati wa ziara yake kulizua hofu kwamba Afrika Kusini itafuata mageuzi ya ardhi kama ya Zimbabwe. Malema pia aliilaumu MDC kwa kuanzisha ghasia za kisiasa nchini Zimbabwe, na kutetea rekodi ya kisiasa na haki za kibinadamu ya Robert Mugabe.
Baada ya Malema kurudi kutoka Zimbabwe, Vijana wa ANC walitoa taarifa kumsifu Mugabe na sera zake za kutaifisha ardhi Zimbabwe. Pia walitoa wito kwa vijana wa Afrika Kusini wa kufuata mfano wa vijana wa Zimbabwe, na kushiriki katika kilimo ili kupunguza utegemezi wao juu ya wakulima wa kizungu. Msaada wa Malema ndani ya Vijana wa ANC bado ni imara.

Kushiriki katika mikataba ya nchi

Taarifa juu ya kuhusika kwa Malema katika zabuni za nchi (mikataba) ilianza kuonekana Novemba 2009. Maswali kuhusu maisha yake binafsi yalitolewa na vyombo vya habari Afrika Kusini. Machi 2010, alijibu madai hayo katika mkutano uliofanyika kampasi ya chuo kikuu, Malema, aliimba wimbo wa mapambano "piga risasi Makaburu", na aliwakemea wanasiasa wa upinzani. Pia alimshambulia Katibu Mkuu wa COSATU, Zwelinzima Vavi.

Agosti 2010, ilitolewa ripoti iliyomsafisha Malema kushiriki kwake katika zabuni za nchini katika mkoa wa Limpopo. Hii ilipokelewa kwa wasiwasi na baadhi ya watu.

Vitisho kwa waandishi wa habari
Wiki chache baada ya utata wa zabuni kuibuka kwa mara ya kwanza, Vijana wa ANC walitoa maelezo binafsi ya Mhariri wa Uchunguzi wa City Press, Dumisane Lubisi, mke wake na watoto wake, ikiwa ni pamoja na namba zao za vitambulisho, maelezo ya benki, anuani ya makazi na maelezo ya gari zao. Lubisi alikuwa ametoa taarifa kuhusu kiwango duni cha ujenzi wa miradi katika Limpopo uliofanywa na makampuni ya Malema.

Vijana wa ANC walitoa madai kuwa walikuwa na ushahidi kuwa waandishi walikuwa wanapokea rushwa katika mambo kadhaa. Katika majibu, kundi kubwa la waandishi wa habari wa kisiasa walilalamika kwa mamlaka mbalimbali ndani ya ANC na Jukwaa la Wahariri la Afrika Kusini (SANEF) wakisema kwamba taarifa hiyo ilikuwa kama jaribio la kuwatisha wasichapishe habari zaidi, na kama tishio kwa uhuru wa vyombo vya habari.

Ufafanuzi wa vyombo vikubwa vya habari

Malema anajulikana kwa taarifa zake tata na mara kwa mara amekuwa akishutumiwa. Awali, wachora katuni, Zapiro na Jeremy Nell mara nyingi walimchora akiwa amevaa nepi. Hivi karibuni, wasifu wa Malema kwa umma umeongezeka, amekuwa akielezwa na wakosoaji katika vyombo vya habari kama "kiongozi wa kisiasa anayeshawishi watu kwa kutumia hisia badala ya fikra zao". Pia alitajwa katika orodha ya watu wasio na ushawishi ya gazeti la Time kwa mwaka 2010.

Kupatwa hatia kwa kauli za chuki

Machi 15, 2010 Malema alipatikana na hatia ya kutumia lugha ya chuki katika Mahakama ya Usawa, akatozwa faini ya R50 000 na kuamriwa kuomba msamaha, kufuatia tukio la 2009 alipowaambia kundi la wanafunzi wa Cape Town, katika Mkutano wa Wanafunzi wa Afrika Kusini (SASCO) kwamba mwanamke aliyemshitaki Rais wa ANC, Jacob Zuma kwa ubakaji alipata “wakati mzuri” kwa sababu baada ya kuamka asubuhi alipata “kifungua kinywa na fedha za teksi”. Kufuatia hukumu hiyo SASCO walionesha "furaha", na kumshambulia Malema kwa “matumizi mabaya” ya jukwaa ambalo SASCO walimpa.

Malema alitoa taarifa mbalimbali kuhusu Wachina nchini Afrika Kusini katika chakula cha jioni cha Umoja wa Wanafunzi wa Afrika Kusini na Wayahudi Aprili 2011. Aliwakebehi wawekezaji wa China ambao "hawakuleta chochote nchini" na kukosoa Uwekezaji wa China nchini Afrika Kusini, kuhoji Afrika Kusini kujihusisha na biashara ya Brazil, Russia India na China.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment