Aug 3, 2011

ISAIAS AFEWERKI: Serikali yake yajiunga tena Igad ili kuepuka kutengwa kimataifa

Isaias Afewerki

ASMARA
Eritrea

ERITREA ni nchi ya Afrika Kaskazini-Mashariki. Upande wa Magharibi imepakana na Sudan, upande wa Kusini imepakana na Ethiopia, na Kusini-Mashariki kuna nchi ya Djibout. Mashariki na Kusini-Mashariki Eritrea ina pwani ndefu ya Bahari ya Shamu. Eneo hili hujulikana pia kama Pembe ya Afrika. Nchi hii inaongozwa na Isaias Afewerki tangu ilipojikomboa kutoka Ethiopia mwaka 1991.

Jina la nchi hii lilitungwa mnamo mwaka 1890 na wakoloni wa Italia kutokana na neno la Kigiriki "erythraia" linalomaanisha “bahari nyekundu”. Hii ni kwa sababu Bahari ya Shamu iliitwa "Sinus Erythraeus" na mabaharia Wagiriki au “Mare Erythraeum” kwa Kilatini na Waroma wa kale – maana yake ni "bahari nyekundu" – tazama Kiingereza “Red Sea”.

Eritrea imeruhusiwa kujiunga tena na shirika la maendeleo la Afrika Mashariki, Igad, baada ya kujitoa kama mwanachama mwaka 2006.

Katibu mtendaji wa Igad, Mahboub Maalim, ameiandikia serikali ya Eritrea kuiarifu kuwa ombi lake la kutaka kujiunga tena limekubalika na watapokewa na wanachama kwa moyo mkunjufu.

Utawala wa mjini Asmara uliamua kufuta uanachama wake wa Igad baada ya mahasimu wao Ethiopia kutuma majeshi yake nchini Somalia kupambana na vikosi vya umoja wa mahakama ya Kiislamu waliokuwa wanatawala sehemu kubwa ya Kusini mwa nchi hiyo.

Mwezi uliopita Igad ilipendekeza kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa liiwekee vikwazo serikali ya Eritrea kufuatia vitendo vyake vya kushirikiana na kundi la wapiganaji wa Al Shabaab wanaoipinga serikali ya mpito ya Somalia.

Wadadisi wanasema huenda utawala mjini Asmara umeamua kujiunga tena na Igad ili kuepuka mikakati ya jumuiya ya kimtaifa kuitenga au kuiwekea vikwazo.

Wiki iliopita tume maalum inayochunguza utekelezaji wa vikwazo vya kuingiza silaha nchini Somalia, ilidai kwenye ripoti yake kuwa Eritrea ilihusika na mpango wa kushambulia mkutano wa viongozi wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika uliofanyika mwezi Januari mwaka huu.

Ingawa mpango huo ulitibuliwa na vyombo vya usalama nchini Ethiopia, tume hiyo ilisema harakati za Eritrea za kuhujumu usalama katika eneo la Afrika Mashariki ikishirikiana na wanachama wa Al Shabaab zipo wazi.

Hata hivyo serikali ya Eritrea imekanusha madai hayo na badala yake kunyooshea mahasimu wao Ethiopia ambao wanasema ndio chanzo cha uvumi huo.

Uhusiano kati ya Eritrea na Ethiopia upo katika hali mbaya kufuatia mzozo wao kuhusu umiliki wa mji wa Badme ulioko kwenye mpaka wa nchi hizo mbili. Licha ya mahakama ya kimataifa kuamua kuwa mji huo upo nchini Eritrea, utawala wa Addis Ababa umekataa kutii amri ya mahakama hiyo.

Historia ya Afewerki

Isaias Afewerki amezaliwa mjini Asmara, tarehe 2 Februari 1946. Ni Rais wa kwanza na wa sasa wa Eritrea, aliyeongoza kundi la Eritrean People's Liberation Front hadi kupata ushindi kwa watu wa Eritrea katika kujikomboa mnamo Mei mwaka 1991, hivyo kumaliza miaka 30 ya mapambano ya ukombozi wa silaha waliyoyaita kwa jina la "Gedli".

Maisha ya awali na kuingia madarakani

Afewerki alijiunga na Eritrean Liberation Front (ELF) mwaka 1966, na mwaka uliofuata alipelekwa China kupata mafunzo zaidi ya juu ya kijeshi. Miaka minne baadaye aliteuliwa kuwa kamanda wa jeshi la ELF. Hata hivyo, akitoa sababu ya tofauti ya kiitikadi, yeye na kikundi kidogo cha wapiganaji walijitenga na ELF na kuanzia kikundi kingine cha Eritrean People's Liberation Front (EPLF).

Ilipoonekana wazi kuwa EPL ilielekea kusambaratika, EPLF kiliungana na makundi mengine mawili ambayo yalikuwa yamejitenga kutoka ELF kabla: kundi la PLF1, lililoongwa na Osman Saleh Sabbe, na kundi lingine lililojulikana kama OBEL.

Mwaka 1976, EPLF ilijimega kutoka kundi la Sabbe baada ya kutia saini makubaliano ya umoja na ELF (Mkataba wa Khartoum). Isaias Afewerki ndiye aliyekuwa kiongozi wa EPLF wakati wa harakati za muda mrefu kwa ajili ya uhuru wa Eritrea ambao hatimaye ulipatikana baada ya miaka 30 ya mapambano ya silaha.

Mwezi Aprili 1993, Umoja wa Mataifa ulisimamia kura ya maoni kuhusu uhuru, na mwezi uliofuata Eritrea ilitangazwa huru. EPLF ilijibadili jina na kuwa People's Front for Democracy and Justice (PFDJ) mnamo Februari 1994 kama sehemu ya maandalizi yake ya kujikaribisha yenyewe kuwa chama cha siasa katika Eritrea ya kidemokrasia.

Hata hivyo, kutokana na ukweli kwamba Eritrea ilijikuta kwenye vita kutokana na mgogoro wa mpaka na Ethiopia tangu mwaka 1998, wakaandaa Katiba ya Eritrea na utekelezaji wake umewekewa muda usiojulikana. Lakini bado PFDJ inatawala Eritrea.

Mwaka 2001, kundi lililoundwa na maafisa 15 wa juu wa serikali, lililojulikana kama G-15, lilitoa barua ya wazi kuikosoa serikali ya Isaias Afewerki kuwa ipo "kinyume cha sheria na katiba" na kutoa wito kwa ajili ya utekelezaji wa katiba iliyotayarishwa. Hata hivyo, maombi yao hayakufaulu na wawanachama wa kundi la G-15, kumi na mmoja kati yao wakawekwa kizuizini nchini Eritrea na bado hawajashtakiwa.

Baada ya Uhuru

Baada ya uhuru wa Eritrea mwaka 1991 na mwaka 1993 baada ya kura ya maoni, Afewerki akawa mkuu wa nchi wa kwanza. Katika miaka ya kwanza ya utawala wake katika serikali hii mpya, taasisi ya utawala iliwekwa katika muundo. Hii ni pamoja na marekebisho ya miundo ya utawala kutoka juu hadi chini na mfumo wa mahakama ya muda iliyochaguliwa kupanua mfumo wa elimu katika mikoa mingi iwezekanavyo.

Mnamo Novemba 1993, Rais aliamuru kufungwa kwa askari wastaafu waliopigana vita vya ukombozi kwa kuandamana kuhusu hali ya maisha magumu katika kambi ya kijeshi. Shirika huru pekee la haki za binadamu lilifungwa. Mwaka 1997, Rais aliamuru kufungwa kwa mashirika yote ya maendeleo ya kimataifa kufanya kazi katika nchi hiyo.

Uchaguzi wa rais, ulipangwa kuwa mwaka 1997, lakini haikutokea na Eritrea bado ni ya chama kimoja, ikitawaliwa na People's Front for Democracy and Justice (PFDJ), chama pekee kilichoruhusiwa kufanya kazi. Mwezi Mei 2008, Afewerki alitangaza kuwa uchaguzi utaahirishwa kwa “miongo mitatu au minne” au zaidi.

Pia mwaka 1998 mgogoro wa mpaka na nchi jirani ya Ethiopia ulioashiria barugumu la vita kamili. Mnamo Septemba 2001, Afwerki alitoa amri ya kukamatwa kwa wanachama kumi na mmoja wa ngazi za juu zaidi katika utawala wake, wengi wao wakiwa ni rafiki zake wa karibu na wenzake aliopigana nao pamoja bega kwa bega vita vya ukombozi kwa karibu miongo minne. Walikamatwa kwa 'kutuhumiwa uhaini', wakapewa adhabu ya kifo kwa kutoa wito wa mageuzi ya kidemokrasia.

Aina zote za vyombo vya habari mpaka sasa vinadhibitiwa na serikali. Eritrea ni nchi pekee ya Afrika kutokuwa na vyombo vya habari vya binafsi. Mwaka 2009, Waandishi Wasiokuwa na Mipaka waliiweka Eritrea katika nafasi ya chini kabisa katika orodha ya nchi katika Ripoti ya Uhuru wa Habari, nyuma ya Korea Kaskazini.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa.

No comments:

Post a Comment