Jul 27, 2011

BINGU WA MUTHARIKA: Atwishwa zigo la lawama baada ya wafadhili kujitoa kuisaidia Malawi

 Bingu wa Mutharika

 Prof. Peter Mutharika

LILONGWE
Malawi

LICHA ya kukabiliwa na changamoto nyingi, Rais Bingu wa Mutharika wa Malawi amemteua mkuu mpya wa jeshi, siku mbili baada ya waandamanaji 18 kuuawa, pale polisi walipofyatua risasi na moshi wa kutoa machozi, ili kuzima maandamano sehemu mbalimbali za nchi.

Brigadier-Jenerali Henry Odillo amechukua nafasi ya Jenerali Marko Chiziko, ambaye mkataba wake wa ajira umemalizika. Nchi sasa ni shwari lakini viongozi wa maandamano, wameonya kuwa watafanya maandamano mengine iwapo rais hatozungumza nao.

Maafisa wa matitabu kutoka hospitali moja nchini Malawi wanasema kuwa kwa uchache watu 18 wameuawa katika ghasia za maandamano nchini humo. Jeshi lilipelekwa katika mji mkuu wa Lilongwe, wakati ambapo maandamano yalikuwa yamerejelewa katika miji jirani. Msemaji wa polisi alithibitisha kifo kimoja tu lakini maafisa kutoka hospitali wakasema watu wanane wameuawa.

Waandamanaji walighadhabika kwa kuongezwa kwa bei za bidhaa na vilevile na Rais Bingu wa Mutharika. Rais wa Mutharika alilihutubia taifa na kusema yuko tayari kwa mazungumzo na wapinzani na makundi ya kiraia.

Makundi ya kiraia yalioandaa maandamano hayo yamesema kuwa Malawi inakabiliwa na mzozo mbaya zaidi wa kiuchumi tangu kupatikana uhuru miaka 47 iliyopita. Serikali hivi karibuni iliidhinisha bajeti ya kubana matumizi na kuongeza kodi ili kupunguza kutegemea misaada baada ya wafadhili wengi kukatiza misaada yao kwa Malawi.

Kufuatia hatua ya nchi ya Uingereza kutangaza kutotoa msaada wa fedha kusaidia bajeti ya nchi ya Malawi, upinzani nchini humo umemtupia lawama rais Bingu wa Mutharika kuifikisha nchi hiyo hapo ilipo. Msemaji wa chama cha Malawi Congress Party, Nancy Tembo, amesema kuwa serikali ilifanya maamuzi yenye hasira kuvunja uhusiano wa kibalozi na nchi ya Uingereza wakati akijua fika nchi hiyo inategemea kwa kiasi kikubwa msaada wa nchi hiyo.

Miezi michache iliyopita rais Mutharika alitangaza kusitisha uhusiano wa kibalozi na nchi ya uingereza kufuatia matamshi ya balozi wake nchini humo ya kukosoa utendaji wa serikali yake. Wafadhili wameishutumu Malawi kwa kufuja uchumi na kukosa kuzingatia haki za binadamu. Maandamano hayo yamefanyika katika miji mingi lakini vifo vimetokea katika mji wa Mzuzu kilomita 300 Kaskazini mwa Lilongwe.

Siku ya Alhamisi wiki iliyopita msemaji wa mfuko wa kuchangia maendeleo wa serikali ya Uingereza alitangaza mfuko huo kusitisha msaada wa kifedha wa zaidi ya euro milioni 19 kwenye bajeti ya serikali ya malawi kwa kile kilichotokea.

Wabunge wa upinzani nchini humo wameishutumu serikali yao wakitaka iombe radhi kwa nchi ya Uingereza ili kuweza kupatiwa fedha hizo ambazo nchi ya Uingereza ndio mshirika mkubwa wa bajeti ya nchi hiyo.

Askofu Maurice Munthali, naibu katibu mkuu wa kanisa la Kipresbyteri aliyekwenda katika chumba cha kuhifadhia maiti kutambua waliouawa alisema wote waliokufa wanaonesha walipigwa risasi, jambo ambalo limethibitishwa na wauguzi. Askofu huyo alisema pia baadhi ya wale walio hospitali hawakushiriki katika maandamano bali walijikuta katikati ya vurugu hizo.

Mashambulio
Taarifa zaidi zasema kuwa mali ya Waziri mmoja wa serikali imeshambuliwa na waandamanaji katika mji huo. Baadhi ya waandamanaji hao wanaomtaka Rais Bingu wa Mutharika ajiuzulu. Polisi nao wametumia gesi za kutoa machozi mjini Lilongwe kuwatawanya waandamanaji na vilevile wameweka vizuizi kuwazuia watu kuingia katika mji huo.

Mmiliki wa radio moja ya kibinafsi nchini humo, Alaudin Osman, aliliambia Shirika la Habari la Uingereza (BBC) kuwa ameagizwa na vyombo vya utawala kutopeperusha matangazo ya moja kwa moja kwa kuwa inadaiwa yanachochoea kinachoendelea hivi sasa.

Malawi ni mojawapo ya nchi masikini zaidi ulimwenguni ambapo asilimia 75 ya idadi ya watu nchini humo hutumia chini ya dola moja katika matumizi yao ya kila siku.

Historia yake

Bingu wa Mutharika amezaliwa 24 Februari 1934. Ni mwanauchumi, mwanasiasa, na Rais wa aasa wa Malawi. Aliingia madarakani mnamo Mei 24, 2004, baada ya kushinda uchaguzi wa urais.

Kwa msaada wa Rais Bakili Muluzi, Mutharika alishinda uchaguzi wa 2004 kama mgombea wa United Democratic Front (UDF), akaimega UDF (ambayo imebakia chini ya utawala wa Muluzi) mwezi Februari mwaka 2005, hata hivyo, kutokana na kutokubaliana juu yake kuhusu kampeni ya kupambana na rushwa. Kisha alianzisha chama kipya, Democratic Progressive Party (DPP), lakini hakuwa na wingi wa wabunge kwa muhula wake wote wa kwanza. Alishinda awamu ya pili katika uchaguzi wa Mei 2009, na pia kupata wabunge wengi.

Maisha binafsi

Alizaliwa akiwa Brightson Webster Ryson Thom katika eneo la Thyolo, kilomita 30 kutoka mji mkuu wa kibiashara wa Malawi, Blantyre. Aliamua kulitumia jina la familia la Mutharika na kujipa jina la kwanza la Bingu katika miaka ya 1960 wakati Umoja wa Afrika ulipokuwa ukifanya kazi ya ukombozi katika bara hili.

Baadaye aliongeza kiambishi cha 'wa' kati ya majina yake ili kuficha utambulisho wake ili kuukwepa usalama wa taifa wa Hastings Kamuzu Banda, hata kama hakuwa mpinzani wa kisiasa wa Banda.

Muda mfupi baada ya Mgogoro wa Baraza la Mawaziri mwaka 1964, Mutharika alikuwa mmoja wa Wamalawi 32 waliochaguliwa na Banda kusafiri kwenda India kwa udhamini wa Indira Gandhi kwa masomo ya diploma ya muda mfupi (fast track). Alipokuwa India, Mutharika alipata shahada yake ya Uchumi.

Maisha ya kifamilia

ETHEL MUTHARIKA:
Amemuoa Ethel Mutharika Zvauya, mwanamke wa asili ya Zimbabwe, ambaye aliwahi kuwa sababu ya kuleta utulivu katika kipindi cha kwanza cha siasa za Bingu kati ya 2004 na wakati wa kufariki kwake. Mutharika na Ethel walikuwa na watoto wanne pamoja. Baada ya kusumbuliwa muda mrefu na kansa ambayo ilimpeleka Ufaransa na Afrika Kusini kutafuta tiba, mke wa Mutharika alifariki Mei 28, 2007. Siku ya maombolezo ilitangazwa kwa ajili yake mnamo Januari 22, 2010.

CALLISTA MUTHARIKA (CHAPOLA-CHIMOMBO):
Baadaye mwaka 2010, Mutharika alitangaza mipango ya kuoana na Callista Chapola-Chimombo, Waziri wa zamani wa Utalii ambaye aliyekuwa na miaka 50. Wawili hao walioana mwaka 2010 katika harusi iliyogharimu milioni 200 pesa za Malawi kwenye Uwanja wa Civo mjini Lilongwe. Harusi ilifadhiliwa kwa gharama ya umma.

PETER MUTHARIKA:
Ni ndugu wa Mutharika, profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha Washington mjini St Louis. Mei mwaka 2009, alichaguliwa kwenye Bunge la Malawi, na Aliteuliwa kwenye Baraza la Mawaziri la Malawi kama Waziri wa Sheria na Mambo ya Katiba. Kwa sasa ni Waziri wa Elimu. Mutharika anamuandaa mdogo wake kuchukua urais, na Peter anatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuwa mgombea kupitia DPP katika uchaguzi wa 2014.

Elimu

Mutharika alikuwa mtoto wa mwalimu mkuu wa shule ya msingi. Alipata elimu India katika Chuo cha Biashara cha Shri Ram, Chuo Kikuu cha Delhi, ambapo alipata shahada ya Uchumi. kisha alisoma na kufuzu shahada ya uzamili katika uchumi. Baadaye akapata shahada ya uzamivu katika Uchumi na Maendeleo kutoka Pacific Western University.


Kazi na siasa

Mutharika aliwahi kuhudumia katika asasi za kiraia na alitumia muda katika serikali ya Zambia. Mwaka 1978, alijiungana na Umoja wa Mataifa, ambapo hatimaye akawa Mkurugenzi wa Biashara na Fedha wa Maendeleo ya Afrika. Mwaka 1991 alichaguliwa kuwa Katibu Mkuu wa Soko la Pamoja la Mashariki na Kusini mwa Afrika (COMESA), kanda yenye nchi 20.

Baada ya Banda kulazimishwa kuanisha vyama vingi, Mutharika nadaiwa kuwa mmoja wa waanzilishi wa UDF, chama kilichoshinda uchaguzi wa kwanza wa Malawi wa vyama vingi mwaka 1994. Mutharika wakati huo alikuwa msaidizi wa kiongozi wa UDF, Rais Bakili Muluzi, lakini akawa mkosoaji wa sera za Muluzi za uchumi, na kuondoka UDF.

Alianzisha United Party (UP) mwaka 1997 na kushindana na Muluzi bila mafanikio katika uchaguzi wa 1999, akiambulia chini ya asilimia 1 ya kura. Mutharika aliifuta UP na kurudi UDF baada ya kuteuliwa naibu gavana wa Benki Kuu ya Malawi. Aliteuliwa kuwa Waziri wa Uchumi, Mipango na Maendeleo mwaka 2002, na baadaye kuteuliwa na Muluzi kama mrithi wake.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari vya kimataifa

No comments:

Post a Comment