Jul 14, 2011

FILAMU NYINGINE: Bunge la rusha jiwe gizani ukisikia mmh jua limempata!

 Jengo la Bunge

Wabunge wakiwa kwenye kikao

Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki (EAC), 
Samuel Sitta

 Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

HAKIKA haya yanayoendelea ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano ni kama maigizo ingawa ndiyo hali halisi inayoendelea kwenye vikao vya bunge letu (tukufu?) mjini Dodoma, ambapo kumekuwepo hali ya kutofautiana kihoja na kimawazo kiasi cha kufikia hatua ya kuporomosheana vijembe na kejeli hizi na zile, tena zikiwa zinatoka kwa watu ambao wanaheshimika mno ndani ya jamii.

Hakika kile kinachoendelea huko bungeni hakina tofauti na ule upinzani uliokuwepo kwenye bendi zetu za muziki wakati ule; Extra Bongo walipokuwa wakiimba kibwagizo chao kwamba 'zama za kurusha jiwe kwenye giza na ukisika mmmh… ujue limempata', ambapo mwanamuziki mwingine, Muumini Mwinjuma alipingana nao na kuimba kuwa 'unaporusha mawe kuwa mwangalifu usije ukampiga mkweo...'

Hali hii pia inanikumbusha simulizi ninazosikia kila mara kuhusu wenyeji wa mikoa ambayo uwindaji ni moja ya shughuli zao kuu za kila siku. Simulizi ambazo zimekuwa zikisema kuwa wawindaji hawa wamekuwa na msemo usemao, "Ukirusha mshale usiku mawindoni, ukasikia chwiiii! Chwiii! Jua umempata mnyama.”

Hali hii ni dhahiri kabisa kuwa ipo katika vikao vya bunge linaloendelea mjini Dodoma. Ambapo wabunge wa Kambi ya Upinzani Bungeni wamekuwa wakirusha mishale (wakitoa hoja kali) ambazo zimekuwa zikiwatikisa sana mawaziri na wabunge wa chama tawala kiasi cha kuomba muongozo wa spika kila mara.

Mfano ni ile hoja ya ufisadi na mafisadi katika akaunti ya EPA ilipotolewa kwa mara ya kwanza katika bunge lililopita, wabunge wa chama tawala wakiongozwa na spika wa wakati huo wakazomea. Spika akasema kuwa hayo ni majungu. Lakini baada ya muda ukweli ukajulikana.

Hali kadhalika hoja ya posho iliyoibuka katika bunge hili linaloendelea imekwisha wainua takribani mawaziri wote na wabunge wengi wa chama tawala, ambapo wamesimama kupinga hoja hiyo kwa nguvu zao zote.

Katika kikao cha Jumanne wiki hii, Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), alipokuwa akichangia katika hotuba ya Wizara ya Afya alisema kwa kunukuu kauli ya Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere kuwa 'serikali corrupt haiwezi kukusanya kodi', yeye akisema kwamba serikali ya Rais Kikwete ni legelege kwa vile imeshindwa kukusanya kodi, kauli iliyosababisha mawaziri zaidi ya watatu kuomba mwongozo wa mwenyekiti.

Hata alipotakiwa na kiti cha mwenyekiti, Jenista Mhagama, kufuta kauli hiyo, Kafulila alikataa na kusisitiza kwamba yuko tayari kufia msimamo huo ambao ni mchungu kwa watu fulani (serikali na wabunge wa CCM), ndipo Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki (EAC), Samuel Sitta, alipoamua kusimama kutuliza mzozo huo. Alisimama na kuwasihi wabunge wa CCM kuwa watulivu, kwani wapinzani kazi yao ni kubeza kila kitu kinachofanywa na serikali.

“Wabunge wa upinzani kazi yao ni kubeza kila kitu kinachofanywa na serikali, lakini sisi tutahukumiwa na wananchi. Siku zote wapinzani mambo yao ni ya unafikinafiki,” alisema Sitta na kuibua zogo zaidi.

Nitatoa mfano, baadhi yao wanadai posho za vikao ni kuwaibia wananchi, lakini wapo baadhi yao walichukua posho hizo miaka mitano iliyopita. Warejeshe posho hizo ndiyo wananchi watawaelewa… na wataendelea kuwa wapinzani,” alisema.

Hata hivyo, maelezo ya Sitta hayakuweza kuzima mzozo uliokuwapo kwani wabunge wengi wa upinzani walisimama wakitaka mwongozo wa mwenyekiti, lakini mwenyekiti aliahirisha Bunge kutokana na muda wa kikao kwisha.

Majibu ya Sitta ambaye amekuwa kiongozi wa shughuli za Bunge akikaimu nafasi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, yalikuja wakati akitoa ufafanuzi wa kauli iliyoibua zogo hayakuwafurahisha wabunge wa kambi ya upinzani.
Wapinzani waliona kana kwamba kuwaita wafaniki ni lugha yenye kuudhi pia, kinyume cha kanuni za Bunge.

Kurusha mawe pia kumefanywa na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa alipoirushia jiwe serikali ambayo yeye pia aliwahi kuwa Waziri Mkuu wake kabla hajajiuzulu kwa kashfa ya Richmond. Haukupita muda tukasikia mmhhh! Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kujaribu kukwepa jiwe la Lowassa na kisha Samuel Sitta naye wiki iliyopita akatumia nafasi hiyo kumjibu Lowassa.

Hata hivyo, imesemwa kuwa hata Makamu wa Kwanza wa Rais wa serikali ya umoja ya Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, pia amevipongeza vyama vya Chadema na NCCR-Mageuzi kwa hoja ya posho waliyoisimamia kidete, hadi kieleweke.

Katika hili imeonesha wazi kuwa wabunge wa kambi ya upinzani safari hii wana shabaha kwa kulenga ipasavyo mishale na mikuki yao, maana kila wanapolenga ama kutupa mawe tunasikia mmmh ama chwiii. Maana kila jiwe walilotupa, mkuki na mshale waliourusha umeonekana kuleta majibu hata kama bado wanayarusha gizani.

Hoja zao zinatuingia sisi tunaosikia kwamba zina mantiki lakini mshangao ni wenzao wa CCM ambao kinachoonekana ni kwamba wameacha jukumu lao la kuisimamia serikali na kuwa watu wa kuibeba, nadhanai wakijiona ni mawaziri watarajiwa!

Mimi ninawahamasisha wapinzani waendelee kurusha mawe gizani kwani yanawapata na sisi tunaona, hata kama ikipigwa kura wao wanashinda lakini wanaondoka na majeraha. Majeraha haya yatakapowazidi, watakufa na hapo bila shaka umma wa Watanzania utanufaika na uwepo wa hili Bunge.

Alamsiki...

No comments:

Post a Comment