Jul 20, 2011

NELSON MANDELA: Nembo ya demokrasia duniani atimiza miaka 93 ya kuzaliwa

 Mzee Nelson Mandela

 Mzee Nelson Mandela katika sherehe yake ya kutimiza miaka 93 ya kuzaliwa, hapa akiwa na famila

AFRIKA KUSINI

MWANZO wa wiki hii, Jumatatu ya Julai 18, Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, alitimiza miaka 93 tangu azaliwe. Mandela, hata hivyo, kwa sasa ni mnyonge kiafya na yuko chini ya uangalizi wa karibu kutoka kwa madakatari kwa muda wa saa 24. Hii ni tangu atoke hospitali mwezi Januari pale alipolazwa baada ya kuugua.

Lakini hali hii haijawazuia raia wa Afrika Kusini na watu wengi duniani kumtakia kheri njema wakati alipokuwa akisheherekea miaka 93 tangu azaliwe. Kuadhimisha siku hii, wimbo maalum umetungwa kwa heshima yake.

Raia wa Afrika Kusini waliweka historia ambapo yamkini watu milioni 12 waliimba wimbo huo kwa wakati mmoja. Shirika la utangazaji nchini humo (SABC) pamoja na idara ya elimu walifanya mapango kuwa ifikiapo saa mbili asubuhi, wanafaunzi katika shule zote nchini humo wawe wanauimba wimbo huo maalum uliotungwa kwa heshima ya Madiba.

Siku ya kuzaliwa kwa Nelson Mandela, rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini ni mojawapo ya siku ya kimataifa iliyoorodheshwa na Umoja wa Mataifa. Nchini Afrika Kusini kila mtu alipaswa kujitolea dakika 67 za muda wake kufanya huduma za kijamii.

Viongozi mbalimbali duniani wamemtumia salamu za kheri njema mzee Mandela wakiongozwa na Rais Barack Obama wa Marekani, ambaye alisema kuwa Mandela ni nembo ya demokrasia na haki duniani na amemshukuru kwa kujitolea maisha yake kwa huduma ya jamii. Kiongozi huyo wa Marekani amesema Mandela ataacha urithi wa busara, nguvu na fadhila nyingi.

Historia yake

Nelson Rolihlahla Mandela au Madiba kama anavyojulikana kwa jina la utani, alizaliwa katika Jimbo la Transkei, Afrika Kusini Julai 18, 1918. Baba yake alikuwa ni Chifu Henry Mandela, wa kabila la Tembu. Ni rais wa kwanza aliyechaguliwa kidemokrasia nchini Afrika Kusini. Alikuwa mwanasheria na mwanachama wa ANC aliyepinga siasa za Ubaguzi wa rangi katika Afrika Kusini.

Nelson Mandela ni wa nasaba inayotoka tawi la cadet la Thembu, ambalo linatawala katika mkoa wa Transkei, Jimbo la Cape ya Mashariki nchini Afrika Kusini. Alizaliwa katika kijiji kidogo cha Mvezo, ambacho kipo katika wilaya ya Umtata.

Wakati Mandela alipokuwa na miaka tisa, baba yake alifariki kwa kifua kikuu, na Jongintaba, aliyekaimu utawala kwa muda akawa mlezi wake.

Mandela alipata elimu yake katika Chuo Kikuu cha Fort Hare na Chuo Kikuu cha Witwatersrand na kuhitimu katika sheria mwaka 1942. Alijiunga na African National Congress (ANC) mwaka 1944 na kushiriki katika upinzani dhidi ya sera za chama tawala cha National Party ya ubaguzi wa rangi baada ya 1948.
Baada ya ushindi wa chama cha Makaburu cha National Party katika uchaguzi wa 1948, chama ambacho kiliunga mkono sera ya ubaguzi wa rangi, Mandela alianza kushiriki kikamilifu katika siasa. Awali, Mandela na watu wengine 150 walikamatwa tarehe 5 Desemba 1956 na kushtakiwa kwa uhaini, aliachiwa huru mwaka 1961.

Kutoka 1952 hadi 1959, daraja jipya la wanaharakati weusi lililojulikana kama Africanists lilivuruga shughuli za ANC katika makazi duni, na kutaka hatua kali zaidi dhidi ya utawala wa National Party.

Uongozi wa ANC chini ya Albert Luthuli, Oliver Tambo na Walter Sisulu waliona si tu kwamba Africanists walikuwa wanasonga kwa kasi lakini pia walitoa changamoto kwa uongozi wao. Uongozi wa ANC uliimarisha nafasi yao kwa njia ya muungano na vyama vya siasa vya Weupe wachache, Machotara, na Waasia katika jaribio la kutaka uwakilishi mpana zaidi ya ule wa Africanists.

Africanists waliudharau Mkataba wa Uhuru wa 1955 katika Mkutano wa Kliptown wa mkataba wa wanachama wa ANC 100,000 wenye nguvu ya kupiga kura moja katika muungano.

Baada ya kupigwa marufuku kwa ANC mwaka 1960, Nelson Mandela alitaka kuanzishwa tawi la jeshi ndani ya ANC. Mwezi Juni 1961, mtendaji wa ANC alilikubali pendekezo lake juu ya matumizi ya mbinu za vurugu na walikubaliana kwamba wanachama waliotaka kujihusisha wenyewe katika kampeni ya Mandela hawatazuiwa kufanya hivyo na ANC. Hii ilisababisha kuundwa kwa Umkhonto we Sizwe. Mandela alikamatwa mwaka 1962 na kuhukumiwa kifungo cha miaka mitano pamoja na kazi ngumu.

Mwaka 1963, wakati viongozi wenzake wengi wa ANC na Umkhonto we Sizwe walipokamatwa, Mandela aliletwa kujibu mashtaka yao kwa kupanga njama za kuipindua serikali. Juni 12, 1964, washitakiwa wanane, ikiwa ni pamoja na Mandela, walihukumiwa kifungo cha maisha. Kutoka 1964 hadi 1982, aliwekwa kizuizini katika gereza la Robben Island, nje ya Cape Town; baada ya hapo, alikuwa katika Gereza la Pollsmoor.

Katika miaka yake gerezani, sifa ya Nelson Mandela ilikua kwa kasi. Alikubaliwa sana kama kiongozi muhimu zaidi mweusi nchini Afrika Kusini na akawa mtu muhimu mwenye nguvu ya upinzani kama harakati za kupambana na ubaguzi wa rangi. Mara kwa mara alikataa kukubaliana au kubadili msimamo wake wa kisiasa ili aachiwe.

Kwa kutumia mbinu za Mahatma Gandhi, Mandela hatimaye alifanikiwa kwa ajili ya vizazi vya wanaharakati wa Afrika Kusini dhidi ya ubaguzi wa rangi. Baadaye alishiriki katika mkutano tarehe 29-30 Januari, 2007, uliofanyika New Delhi kuadhimisha kumbukumbu ya miaka 100 ya Gandhi kuanzisha satyagraha (upinzani usio wa vurugu) nchini Afrika Kusini.

Tarehe 2 Februari 1990, Rais wa nchi hiyo, Fredreck W de Klerk aliachana na amri ya kupiga marufuku shughuli za ANC na vyama vingine vya kupambana na ubaguzi wa rangi, na kutangaza kuwa Mandela muda mfupi atafunguliwa kutoka gerezani. Mandela ilitolewa kutoka gereza la Victor Verster Februari 11, 1990. Tukio hilo lilitangazwa moja kwa moja duniani kote.

Kufuatia kuachiliwa kwake kutoka gerezani, Mandela akarudi kwenye uongozi wa ANC na, kati ya 1990 na 1994, alikiongoza chama katika mazungumzo ya vyama vingi ambayo yalisababisha uchaguzi wa kwanza nchini humo usio wa ubaguzi wa rangi.

Mwaka 1990 alianzisha sera ya maridhiano. Yeye mwenyewe kwa moyo wote alijiimarisha katika maisha yake ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya yeye na wengine yaliyowekwa gerezani karibu miongo minne kabla. Mwaka 1991, katika mkutano wa kwanza wa kitaifa wa ANC uliofanyika ndani ya Afrika Kusini baada ya uanzishwaji wake kupigwa marufuku mwaka 1960, Mandela alichaguliwa kuwa Rais wa ANC wakati rafiki yake wa muda mrefu, Oliver Tambo, kuwa Mwenyekiti wa Taifa wa chama. Mwaka wa 1993, pamoja na Frederick de Klerk, alikuwa mshindi wa Tuzo ya Nobel ya Amani.

Mandela anakumbukwa kwa ushujaa wake, uzalendo wake na kutanguliza mbele maslahi ya wengi kuliko ya kwake. Hata aliposhika madaraka ya kuongoza taifa hilo lenye uchumi borea zaidi kuliko mengine Afrika, hakutaka kung’ang’ania madarakani kama walivyo wenzake akina Robert Mugabe wa Zimbabwe. Alitoka madarakani huku wananchi bado wakimpenda na kuwapisha wengine. Je, viongozi wengi wa Afrika ni akina nani wanafuata nyayo zake?
Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari.

No comments:

Post a Comment