Mar 23, 2011

Inahitajika elimu ya mahitaji maalum kwa Walemavu


 Watu wenye ulemavu wanapaswa kupewa fursa zilizo sawia kama watu wengine wasio na ulemavu.

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

HIVI karibuni nilisikitishwa sana na habari niliyoelezwa kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu na mwananchi mmoja mwenye ulemavu aliyedai kunyanyaswa kutokana na ulemavu wake na wafanyakazi wa chombo kimoja cha usafiri.

Mwananchi huyo aliyewasiliana nami kwa namba ya simu 0754 440155 aliniandikia ujumbe huu: “Nilisafiri na Basi la (analitaja jina) toka Dar hadi Arusha, tulifika Arusha saa 2 usiku, watu wote walipoteremka nilibaki ndani ya gari huku kiti changu cha magurudumu (wheel chair) kinachoniwezeshwa kutembea kikiwa kwenye buti ya gari. Kila nilipowaomba wafanyakazi wa gari hiyo kunipatia kiti changu walikaa kimya hadi ilipotimu saa 5:00 usiku walipotaka kulaza gari ndipo walipoitoa wheel chair yangu. Nikapeleka shauri langu polisi, na sasa shauri lipo mahakamani. Kwa kweli nilifedheheka sana.”

Mwananchi huyo ambaye sintomtaja jina, naamini kuwa atakuwa ameumia sana moyoni kutokana na kitendo alichofanyiwa na wafanyakazi hao kutokana na ulemavu wake. Sipendi kuliongelea kwa kina suala lake kwa kuwa lipo mahakamani, lakini itoshe tu kusema jamii hii inahitaji kuelimishwa kuhusu walemavu.

Juzi asubuhi, wakati naangalia taarifa ya habari ya asubuhi kupitia televisheni nilimsikia mwananchi mmoja ambaye ni mlemavu wa macho, Amon Anastaz, kiongozi kutoka taasisi ya watu wenye ulemavu (Shivyata), akizungumza kuhusu uzinduzi wa mkakati wa watu wenye ulemavu 2010-2015 wenye lengo la kuhakikisha “kunakuwepo na taifa jumuishi” hasa ikizingatiwa kuwa asilimia 10 ya idadi ya watu nchini ni jamii ya watu wenye ulemavu.

Mkakati huo uliozinduliwa Jumatano ya Machi 23, 2011 katika hoteli ya Blue Pearl, Ubungo Plaza una nia ya kuielimisha jamii juu ya mtazamo wake na dhana kuwa watu wenye ulemavu ni watu wanaohitaji hisani badala ya kuwezeshwa.

Bahati mbaya wakati naandaa makala yangu sikuwa nimepata taarifa rasmi kuhusu kilichozungumzwa hapo Ubungo Plaza, lakini kwa kuwa tayari nilikuwa nimehuzunishwa na kitendo kilichofanywa huko Arusha, nilidhani ipo haja ya kuandika makala hii ili kuieleza serikali yetu pamoja na mambo mengine, umuhimu wa kuwepo elimu ya mahitaji maalum kwa walemavu.

Kama alivyodokeza kiongozi wa Shivyata kuwa watu wenye ulemavu hawahitaji hisani bali kuwezeshwa, hivyo pamoja na kusisitiza uwepo wa elimu ya mahitaji maalum pia watu wenye ulemavu katika jamii yetu wanatakiwa kutotengwa kwenye masuala mbalimbali ya kuliletea Taifa maendeleo, hususan kwenye suala la ajira ili kuwawezesha kuwaondoa katika hali ya utegemezi na hatimaye kujitegemea wenyewe.

Watu wenye ulemavu wanapaswa kupewa fursa zilizo sawia kama watu wengine wasio na ulemavu. Imekuwa ni kawaida kuona katika jamii zetu, taasisi ama katika mashirika walemavu wakinyimwa fursa hiyo hata kwa wale walemavu wenye elimu nzuri huku wakiwatolea visingizio vyenye lengo la kutowaajiri kutokana na ulemavu wao.

Kwa kweli hali hii inakatisha tamaa sana hasa kwa wale walemavu waliopata nafasi ya kujiendeleza kielimu kupitia tasnia tofauti hapa nchini lakini jamii ikawachukulia kama mzigo kwa taifa au kundi la watu wenye kungoja hisani.

Suala la mwananchi aliyenyanyaswa huko Arusha kwa sababu ya ulemavu wake linadhihirisha jinsi ambavyo jamii yetu bado haijastaarabika katika suala la walemavu, kitendo kinachopaswa kukemewa kwa nguvu zote za wanaharakati na wananchi wapenda usawa na maendeleo.

Na katika kutilia mkao suala hili, walezi na wazazi walio na watoto wenye ulemavu wanapaswa kuwatoa watoto hao bila kuwaficha au kuwaweka ndani pekee kwani kwa kufanya hivyo ni kuwanyima haki zinazostahili kwa watoto wote pasipo kubagua na hata misaada inayotolewa kwa watoto walio na ulemavu hususan katika elimu.

Kama nilivyoandika katika makala ya wiki iliyopita
“Ni lini walemavu watapewa fursa sawa kwenye jamii yetu?” nikashauri kuhusu kuangalia upya suala la miundombinu mbalimbali, jamii inatakiwa sasa kujenga mazingira rafiki yatakayoepusha malalamiko ya kuonekana kutengwa kwa walemavu, ikiwa ni pamoja na ofisi binafsi, mahoteli, nyumba za wageni, viwanda kwani yapo maeneo yanayowabana walemavu hasa wa miguu kushindwa kupita kwa urahisi kutokana na hali zao.

Naishukuru serikali japo imeanza kuona tatizo lililopo hasa katika muundo wetu wa elimu ya lazima ambao upo katika kipindi cha mabadiliko kwa kuanza kutoa fursa, ingawa bado hakuna juhudi za makusudi za kivitendo katika kumaliza tatizo hili linalopelekea watoto walemavu kuwa wengi kati ya wale wanaoacha shule.

Watoto walemavu wana fursa ndogo ya kupata elimu, hasa sehemu za mashambani. Shule chache za elimu maalum ziko kwa watoto wenye shida ya kusikia, watoto wasioona na wenye upungufu wa akili. Shule kama hizi zinapatikana katika maeneo machache kwa baadhi ya miji mikubwa tu.

Kwa kweli bado kuna shida nyingi zinazowakabili watoto walemavu. Watoto wengi wenye ulemavu ambao wanastahili kusoma mashuleni hawawezi kwenda kwa sababu ya uzito wa ulemavu kwenye maeneo ya vijijini. Ubaguzi wa jinsia katika elimu uko chini sana na kuna asilimia kubwa ya watoto walemavu katika shule za kawaida (badala ya shule maalum) kuliko nchi zingine.

Lakini, elimu waipatayo mara nyingi haileti faida, na ufikiaji mbaya kwa watoto walemavu. Mara nyingi utaratibu wa mafunzo hauwezi kubadilika sambamba kwa watoto walemavu, na walimu wengi hawana ufahamu mzuri wa mahitaji ya watoto walemavu, ama uwezo wao.

Walimu wengine bado wana hali ya ubaguzi kwa watoto wenye ulemavu, ambao mara nyingi hawatambulikani kwa sababu ya ukubwa wa madarasa. Watoto wengi wenye ulemavu mkubwa bado wako nyumbani.

Kufanikiwa katika kuendeleza miradi ya elimu ya mjumuisho kunahitaji uhusishaji na usaidizi wa wazazi wa watoto wenye ulemavu katika daraja zote. Tunahitaji kuwa na program ya usaidizi wa mradi wa kuokoa watoto, vikundi vya familia zenye watoto walemavu wanapaswa kuunda chama kitakachohusishwa kwa karibu sana programu hii katika kuanzisha shughuli za elimu ya mjumuisho kwao.

Tunaweza hata kujifunza kutoka Mongolia, moja ya nchi zenye matatizo ya sera kuhusu jamii ya watu wenye ulemavu ambao waliwahi kuwa na warsha ya kimataifa kuhusu sera za elimu mjumuisho kwa watoto walemavu, iliyofanyika Ulaanbaatar mnamo machi 2003, neno 'elimu mchanganyiko' lilibadilishwa kuwa 'elimu mjumuisho' kwa ajili ya mradi wa kuokoa watoto [SC UK].

Warsha hiyo ilisimamiwa na mradi wa watoto uliolenga: kuupa sura mpya uanzilishi wa elimu mjumuisho nchini Mongolia; kusaidia wahusika kusaidiana, na kujifundisha kutoka, nchi zingine kuhusu maendeleo na utekelezaji wa sera; kutambua mambo muhimu na mapendekezo ya kuendeleza na kutekeleza sera hizo nchini Mongolia. Mradi huo wa kuokoa watoto [SC UK] unaamini kwamba kuhimiza sera ndio njia ya kusuluhisha matatizo.

Mongolia pia wameanzisha ushirikiano thabiti na muungano wa wazazi wenye watoto walemavu [APDC], na, kupitia ushirikiano na programu maalum, utaratibu wa elimu mjumuisho kwa watoto walemavu ukabuniwa. Hii ilikubaliwa kwa pamoja na Waziri wa Elimu, Waziri wa Afya na Waziri wa Maswala ya Jamii na Uchumi mnamo Disemba 2003. Kwa sasa wizara hizi, mradi wa kuokoa watoto [SC UK], APDC na vyama vingine vyenye uhusiano vimeunda kamati tekelezi ya kuangalia utekelezaji wa mradi.

Kuwashirikisha wazazi ni njia bora ya kuwafanya kuamini kuwa kuhusika kwao na sauti yao ni kiungo muhimu katika kutekeleza elimu mjumuisho. Muungano wao una uwezo wa kusaidia katika uendelezaji wa huduma zaidi za elimu na kuinua hali ya kuishi ya watoto wao.

Kwa kweli kila mtoto hapa Tanzania ana haki ya kupata elimu. Kila mtoto angependa kwenda shule ya watoto wadogo na shule yenyewe, lakini kwa sasa sio kila mtoto ana fursa hii. Naamini elimu mjumuisho ndio njia mwafaka ya kufuata ili kutimiza haki ya kila mtoto ya kupata elimu. Hatua ya kwanza kwa elimu mjumuisho ianze kujengwa sasa hapa nchini, kwa usaidizi wa sehemu zote za jamii: watoto, wazazi, na hata mashirika ya serikali na yasiyokuwa ya kiserikali.

No comments:

Post a Comment