Mar 23, 2011

KALONZO MUSYOKA: Urais wa Kenya wamfanya ahahe kutaka Kenya ijitoe ICC

 Makamu wa Rais wa Kenya, Kalonzo Musyoka

 Kalonzo Musyoka (kulia) akifurahia jambo na swahiba wake, William Ruto

NAIROBI
Kenya

BAADA ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kukataa hoja ya serikali ya Kenya ya kutaka Mahakama ya Kimataifa ya ICC ihairishe kesi zinazowakabili watu wanaoshukiwa kuchochea ghasia za baada ya uchaguzi uliopita, Kenya imekuwa ikitafuta njia nyingine.

Njia pekee iliyobaki kwa Kenya ilikuwa kukata rufaa mbele ya mahakama hiyo. Lakini Kiongozi wa Mashataka, Louis Moreno Ocampo akiwa ziarani London alisema haoni uwezekano wa Kenya kufaulu katika hoja hiyo.

Kampeni za majuma kadhaa za serikali ya Kenya za kutaka kuungwa mkono na jamii ya kimataifa ili kesi hizo ziahirishwe zilifikia kikomo Ijumaa iliyopita, baada ya kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kisichokuwa rasmi, kukataa hoja hiyo ya Kenya.

Hatua hiyo ikapelekea kwa Kenya kuamua kutumia ibara ya 19 ya sheria iliyobuni mahakama ya ICC, inayoruhusu nchi kupinga uamuzi wa mahakama ya ICC. Hata hivyo Kiongozi wa mashtaka katika ICC, Luis Moreno Ocampo amesema ingawa serikali ya Kenya ina haki ya kukata rufaa, haoni uwezekano wa kesi kuahirishwa.

Ocampo aidha aliondolea mbali hofu ya kukamatwa kwa washukiwa hao sita watakapofika mbele ya mahakama ya ICC Mjini The Hague, tarehe 7 na 8 Aprili. Lakini alikumbusha kwamba yeyote anaweza kukamatwa akiwatishia mashahidi.

Ocampo alikuwa ameiandikia barua serikali ya Kenya akielezea wasiwasi wake kwamba washukiwa wawili: Naibu Waziri Mkuu, Uhuru Kenyatta na Mkuu wa Utumishi wa Umma, Francis Muthaura wanashikilia nafasi serikalini zinazowapa uwezo kuingilia ushahidi.

Washukiwa wanaotarajiwa kufika mahakamani The Hague tarehe saba mwezi ujao ni aliyekuwa Waziri wa Elimu ya Juu, William Ruto, Mbunge Henry Kosgey, Mtangazaji wa Radio, Joshua Arap Sang, Uhuru Kenyatta, Francis Mutahura na aliyekuwa Mkuu wa Polisi, Hussein Ali. Baada ya hatua hiyo, kwa mujibu wa Bwana Ocampo, watasubiri kipindi cha miezi sita kuipa mahakama muda wa kuthibitisha mashtaka.

Hata hivyo Chama cha Orange Democratic Movement (ODM), kimeonekana kupinga hatua ya serikali ya Kenya kutaaka kuwanusuru watuhumiwa kwa kuliandikia barua Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UN), kikilitaka kukataa ombi la kuahirisha kesi zinazowakabili watuhumiwa hao katika Mahakama ya Uhalifu ya Kimataifa (ICC).

Katika barua kali, ODM walilitaka Baraza la Usalama kutambua kuwa ombi la Kenya ni ushahidi kwamba Rais Mwai Kibaki pamoja na chama chake cha PNU ‘hawawezi na hawako tayari kuwaadhibu waliotenda uhalifu baada ya uchaguzi.
Chama hicho kilieleza sababu 16 kwa nini ombi hilo lipuuzwe, miongoni mwao zikisema kampeni za kutaka kuahirishwa kwa kesi hizo zinaendeshwa na vinara hao sita, ambao wametakiwa kufika ICC huko Hague, Aprili 7.

Hata hivyo, William Ruto aliyesimamishwa Uwaziri wa Elimu ya Juu ameiponda barua hiyo ya ODM kwenda Baraza la Usalama, akisema wanachama wa chama hicho hawakushirikishwa.

Kwa kadiri nijuavyo, huu ni uamuzi wa Profesa Nyong’o na Raila (Waziri Mkuu Raila Odinga) na washirika wao. Hawakutushirikisha kutaka maoni yetu au kutujulisha kuwapo kwa suala hilo,” alisema.

Mbunge huyo wa Eldoret Kaskazini alisema yeye na wafuasi wake ndani ya ODM wanatarajia kuandika barua nyingine kwa Baraza la Usalama la UN kuunga mkono kuahirishwa kwa kesi za ICC.

Hawaimiliki ODM. ODM ni mali yetu sote na tunatarajia kupinga uamuzi wao,” alisema.

Katika barua yake, ODM ilisema kwamba Kenya haina mahakama au wachunguzi wenye uwezo wa kushughulikia uhalifu uliotendeka wakati wa machafuko yaliyotokana na uchaguzi wenye utata.

Kampeni za kutaka kuahirishwa kwa mashtaka dhidi ya watuhumiwa hao sita katika Mahakama ya Uhalifu ya Kimataifa (ICC) zinaongozwa na Makamu wa Rais wa Kenya, Kalonzo Musokya.

Musyoka ambaye anahofia nguvu za Raila Odinga katika kuusaka urais wa Kenya aliamua kuunda ushirika na watu wawili katika ya watuhumiwa hao sita: Uhuru Kenyatta na Wiiliam Ruto katika umoja wao unaojulikana kama “K 3”.

Historia ya Kalonzo Musyoka:
Stephen Kalonzo Musyoka amezaliwa tarehe 24 Desemba 1953, ndiye Makamu wa Rais wa Kenya. Musyoka aliwahi kufanya kazi katika serikali ya Rais Daniel arap Moi akiwa Waziri wa Mambo ya Nje kati ya 1993 hadi 1998, na hatimaye, chini ya Rais Mwai KIbaki, akiwa Waziri wa Mambo ya Nje tena kati ya 2003 hadi 2004, na baadaye Waziri wa Mazingira 2004 hadi 2005. 
 
Alikuwa mmoja wa wagombea urais katika uchaguzi wa rais 2007 lakini hakufua dafu, ambapo baada ya uchaguzi aliteuliwa kuwa Makamu wa Rais na Kibaki mwezi Januari 2008. Pia amewahi kushika wadhiofa wa Kamishna Mkuu wa Chama cha Skauti cha Kenya (The Kenya Scouts Association).

Maisha ya awali:
Alizaliwa katika eneo la Tseikuru, sehemu ya Wilaya ya Mwingi (ambayo siku hizi ni sehemu ya Wilaya ya Kitui), mkoa wa Mashariki wa Kenya. Kati ya 1960 na 1967 alisoma katika Shule ya Msingi Tseikuru. Kisha akaenda Kitui High School iliyopo Kitui na hatimaye Meru High School, Meru ambapo alihitimu mwaka 1973. 
 
Kalonzo Musyoka alihitimu Shahada ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi mwaka 1977. Aliendelea na masomo zaidi katika Shule ya Sheria ya Kenya na Taasisi ya Usimamizi ya Mediterranean ya Cyprus.

Siasa:
Musyoka alijitosa kugombea ubunge katika Jimbo la Kitui Kaskazini mwaka 1983, lakini alishindwa. Wakati huo, Kenya ilikuwa nchi ya chama kimoja na wagombea wote walikuwa wa chama cha Kanu. Hata hivyo, miaka miwili tu baadaye, mwaka 1985, kiti cha ubunge cha Kitui Kaskazini kilibaki wazi na Musyoka alishinda katika uchaguzi huo mdogo, hivyo kuwa mbunge katika umri wa miaka 32. 
 
Mwaka 1986, aliteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Ujenzi. Alichaguliwa tena katika uchaguzi wa bunge wa mwaka 1988. Kuanzia 1988 hadi 1998 alikuwa Katibu wa oganaizeshi wa Taifa wa Kanu.

Uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi Kenya ulifanyika mwaka 1992. Musyoka alibaki katika chama cha Kanu, alifanikiwa kutetea kiti chake cha ubunge na kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Pia alishika nafasi nyingine katika wizara kadhaa katika serikali ya Kanu. Mwaka 1997 alichaguliwa tena kuwa mbunge, lakini sasa akiwa mbunge wa Jimbo la Mwingi Kaskazini, baada ya jimbo lake la zamani, Kitui Kaskazini kugawanywa katika majimbo mapya.

Katika mwezi wa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2002, chini ya uongozi wa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Kanu, Raila Odinga, alijotoa Kanu na kujiunga na Liberal Democratic Party (LDP) chini ya mwamvuli wa muungano wa NARC (National Rainbow Coalition), ambao ulishinda uchaguzi mkuu.

Musyoka akawa Waziri wa Mambo ya Nje kwa mara ya pili chini ya Rais Mwai Kibaki, lakini baada ya kufanya mabadiliko ya baraza la mawaziri 30 Juni, 2004 alihamishiwa Wizara ya Mazingira. Mwishoni mwa Agosti 2004, aliondolewa kutoka nafasi yake kama mwenyekiti wa mazungumzo ya amani wa Sudan na Somalia na nafasi yake kuchukuliwa na John Koech.

Kalonzo Musyoka ilikuwa na matarajio ya kuwa urais katika uchaguzi wa Desemba 2007. Musyoka alifanya kampeni kupitia tiketi ya ODM-Kenya, huku akikabiliwa na wagombea wengine. Ufanisi wake kwa ajili ya uchaguzi wa Desemba 2007 ulishuka kwa kasi, na wachambuzi wa kisiasa walijiuliza kama angeweza kuwa na athari kubwa. Uhusiano wake na kiongozi mwenzake wa ODM-Kenya, Raila Odinga, ambaye pia aliutaka urais kupitia ODM-Kenya, ulisababisha kuwepo uvumi mwingi. 
 
Waangalizi wengi walihoji kama watarajiwa wa urais kupitia ODM-Kenya, hasa Raila na Musyoka, wangeweza kuunganisha nguvu na kumuunga mkono mgombea mmoja katika uchaguzi mkuu. 
 
Chama cha ODM-Kenya kiligawanyika katika makundi mawili, moja la Musyoka na jingine la Odinga, Agosti 2007. Musyoka alichaguliwa na chama chake kama mgombea urais, Agosti 31, 2007, akipata kura 2,835 dhidi ya Julia Ojiambo, aliyepata kura 791. Alizindua kampeni zake za urais katika Uwanja wa Uhuru Park mjini Nairobi, Oktoba 14, 2007.

Kwa mujibu wa matokeo ya uchaguzi, Musyoka alishika nafasi ya tatu nyuma ya Kibaki na Odinga kwa kupata asilimia 9 ya kura. Ulizuka mgogoro mkali kuhusu matokeo kati ya wafuasi wa Kibaki na Odinga, Kibaki alimteua Musyoka kuwa Makamu wa Rais na Waziri wa Mambo ya Ndani tarehe 8 Januari, 2008.

Maisha ya binafsi
Kalonzo Musyoka amemuoa Pauline. Wana watoto wanne.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyombo mbalimbali vya habari.

No comments:

Post a Comment