Mar 30, 2011

SHEIKH SHARIF AHMED: Akabiliana na Spika wa Bunge nchini Somalia aliyetangaza azma ya kuwa Rais

 Rais wa Somalia, Sheikh Sharif Sheikh Ahmed

MOGADISHU
Somalia

MWEZI Januari mwaka huu Spika wa Bunge la Somalia, Sharif Sheikh Hassan alionesha azma ya kuwa rais wa Somalia baada ya kufanya mkutano na koo za Digil na Mirifle jijini Nairobi, Kenya.

Hata hivyo, mkutano huo ulitibuka baada ya wabunge waliowakilisha pande zote mbili kuchukuwa mirengo tofauti juu ya azimio hilo la spika dhidi ya rais Sheikh Sharif Ahmed. Kwa siku za hivi karibuni, Sharif Sheikh Hassan amekuwa akijitahidi kuungwa mkono na Wasomali walio nchi za nje na kuwepo utata kati yake na Rais wa serikali hiyo ya mpito, Sheikh Sharif.

Na katika kuendeleza kampeni zake mapema mwezi wa tatu, Spika huyo wa Bunge alitangaza kuwa, bunge la serikali ya mpito ya Somalia limeongeza muda wake kwa miaka mitatu. Muda wa bunge hilo pamoja na wa serikali ya mpito ya Somalia ulitarajiwa kumalizika mwezi Agosti mwaka huu lakini wabunge wa Somalia wamepiga kura na kuongeza muda huo.

Alisema kuwa, bunge litafanya mabadiliko makubwa katika kuwahudumia wananchi wa Somalia na kusisitiza kwamba hatua hiyo waliyochukua, itazuia Somalia kubaki bila serikali. Spika wa Bunge la Somalia aidha ameongeza kuwa, bunge la nchi hiyo litamchagua rais na spika mpya wakati kipindi cha kwanza cha bunge hilo kitakapofikia ukingoni hapo mwezi Julai mwaka huu.

Mwaka jana Rais Sheikh Sharif Ahmed, alimteua Mmarekani mwenye asili ya Kisomali kuwa Waziri Mkuu wa Somalia. Uteuzi wa Mohammed Abdullahi, mwanadiplomasia wa zamani aliyesomea nchini Marekani, ilikuwa ni juhudi mpya ya kuimarisha mchakato wa kukabiliana na wanamgambo wanaolidhibiti eneo kubwa la Somalia.

Abdulahi anakabiliwa na kibarua kipevu cha kuiongoza serikali ya mpito inayoyumba, inayokabiliwa na mizozo ya ndani ya kisiasa, rushwa na iliyobanwa na wanamgambo katika sehemu ndogo ya mji mkuu Mogadishu.

Lakini kubwa linaloisumbua nchi hiyo ni ugomvi wa madaraka unaojitokeza baina ya Spika na Rais, ugomvi ambao pia uliikumba serikali ya zamani ya mpito nchini humo.

Sheikh Sharif ni na hasa:

Sheikh Sharif Sheikh Ahmed alizaliwa Julai 25, 1964. Ahmed Alizaliwa katika eneo la Shabeellaha Dhexe, Jimbo la Kusini mwa Somalia, na alisoma katika vyuo vikuu vya nchi za Libya na Sudan.

Sharif Ahmed alianza elimu yake katika Taasisi ya Sheikh Sufi, ambayo ilikuwa ikihusishwa na Chuo Kikuu cha Al-Azhar kilichopo nchini Misri. Baada ya hapo alikwenda Sudan katika Chuo Kikuu cha Kordufan mwishoni mwa mwaka 1992, alikopata shahada ya kwanza katika lugha ya Kiarabu na Jiografia katika mji wa Aldalanj.

Mwaka 1994, Chuo Kikuu kilibadilishwa jina na kuitwa Chuo Kikuu cha Dalanj, na Sheikh Sharif alielekea Tripoli, mji mkuu wa Libya, baada ya kumaliza miaka miwili tu kati ya minne iliyohitajika. Nchini Libya, alijiunga na Chuo Kikuu Huria ambako alipata shahada ya kwanza ya Sheria na Sharia za Kiislam, na kuhitimu mwaka 1998.

Ameshawaahi kufanya kazi kama mwalimu wa shule ya sekondari wa masomi ya Jiografia, Lugha ya Kiarabu na masomo ya dini. Ukiachia lugha yake ya asili inayotumika Somalia, Ahmed huzungumza kwa ufasaha lugha ya Kiarabu, Kitaliano na Kiingereza.

Muungano wa Mahakama za Kiislamu (ICU):

Baada ya kurudi kutoka nje ya nchi, Ahmed akaingia ICU na kuchaguliwa kwa kiongozi wa mahakama ndogo ndogo za ukoo katika eneo la Jowhar. Miaka michache baadaye, genge moja la kihalifu lenye makao yake mjini Mogadishu, mji mkuu wa Somalia, lilimteka nyara mwanafunzi na kudai fidia kutoka kwa familia yake kama malipo ya kurudishwa kwa kijana huyo.

Tukio hili ni moja ya matukio mengi ya utekaji nyara na mauaji yanayofanywa na makundi yenye silaha katika mji mkuu wa Somalia ambao umesababisha serikali kuu ya Somalia kushindwa kuudhibiti. Tukio hili liliripotiwa kuwa lilikuwa ni jaribio la kiuongozi katika maisha ya Sheikh Ahmed na kupelekea ushiriki wake zaidi ndani ya ICU.

Mwaka 2004, Sheikh Ahmed alikuwa mmoja wa viongozi katika Mahakama za Kiislamu mjini Mogadishu. Marafiki wake wa karibu na washirika wake ni pamoja na Sheikh Hassan Dahir Aweys, mmoja wa waanzilishi wa ICU, na Aden Hashi Farah “Eyrow”, mtu ambaye Washington inadai ana uhusiano na mtandao wa kigaidi wa Al-Qaida na aliwahi kupigana vita vya Afganistan mwaka 2001.

Septemba 9, 2006, chini ya mwamvuli wa Abdiqasim Saladi Hassan, Rais wa zamani wa Serikali ya Mpito ya Taifa nchini Somalia, Sheikh Ahmed na wenzake kadhaa walihudhuria sherehe za Umoja wa Afrika (AU) mjini Sirte, Libya, kuashiria kumbukumbu ya miaka saba ya mkutano wa kilele wa viongozi wa Afrika.

Katika mahojiano na mashirika ya habari ya Reuters na BBC, Sheikh Ahmed alipendekeza kuwa ujumbe wake utafute msaada kutoka Libya na mataifa mengine ya Afrika ili kupata suluhu kati ya Waislam na Serikali ya Mpito ya Taifa nchini Somalia.

Hata hivyo, aliripotiwa kuwasili Khartoum, Sudan saa 48 kabla ya kuanza kwa mkutano kati ya serikali ya Somalia na ICU. Sheikh Ahmed alisema Ethiopia ilikuwa adui wa Somalia kwa zaidi ya miaka 500, na alitoa mashtaka kutokana na vikosi vya Ethiopia kuingilia kati nchini Somalia. Ethiopia ilikana kwa askari wake kuhusika na mapigano nchini Somalia.

Disemba 28, 2006, baada ya miezi sita tu ya kuwa madarakani na kushindwa kwa jeshi la ICU, aliamua kupambana na vikosi vya Ethiopia nchini Somalia. Baada ya ICU kushindwa katika vita ya Jilib na kutelekezwa Kismayo, aliamua kukimbilia mpaka wa Kenya.

Kabla ya kukimbia, Sheikh Sharif aliishi na mke wake na watoto wawili, Ahmad, mwenye umri wa miaka 9 na Abdullah, ambaye alikuwa ameanza kutembea, katika nyumba ya kawaida mjini Mogadishu. Alikutana na Balozi wa Marekani nchini Kenya kwa ajili ya mazungumzo kuhusu ushirikiano na TFG. Wakati huo alikuwa akiishi chini ya ulinzi wa mamlaka ya Kenya akikaa katika hoteli jijini Nairobi.

Tarehe 1 Februari 2007 Ahmed Sharif aliondolewa kutoka mamlaka ya polisi wa Kenya. Februari 8, alielekea Yemen ambapo wanachama wengine wa ICU walikwenda pia.

Uchaguzi wa rais 2009:

Duru ya kwanza ya upigaji kura ilipoanza, wagombea kadhaa walijiondoa, na kuongeza uvumi kwamba ulikuwa ni uchaguzi kati ya Nur Hassan Hussein na Sharif Ahmed. Katika raundi ya kwanza, Sharif Ahmed alipata kura 215, Maslah Mohamed Siad alipata kura 60, na Hussein alipata kura 59.

Hata hivyo Hussein alijiondoa katika kugombea, hivyo kuongeza uwezekano wa Sharif Ahmed kuwa rais. Katika raundi ya mwisho ya uchaguzi wa rais, Sharif alishinda kwa kura 293. Baada ya kushinda uchaguzi mapema Januari 31, 2009, Ahmed aliapishwa baadaye mchana wa siku hiyo katika hoteli ya Kempinski iliyopo Djibout.

Mwezi Aprili na Mei 2010, kulijitokeza ufa mkubwa kati ya Waziri Mkuu wa Somalia, Omar Abdirashid Ali Sharmarke na aliyekuwa Spika wa Bunge, Adan Mohamed Nuur Madobe, ambao ulipelekea Spika ajiuzulu mbele ya bunge, baada ya bunge kupiga kura ya kumuondoa.

Licha ya Madobe kukubaliana na uamuzi wa kuondoka madarakani kama Spika, Rais Sharif alitangaza muda mfupi baadaye kufukuzwa kazi kwa Waziri Mkuu, Sharmarke na nia yake ya kuunda serikali mpya. Hatua hii haraka ilikaribishwa kwa mikono miwili na Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, Ahmedou Ould-Abdallah, mshirika wa karibu na msaidizi wa Sharif.

Katika kujibu, Waziri Mkuu Sharmarke aliwaambia waandishi wa habari kwamba Sharif hakuwa na mamlaka ya kumfukuza, na alisema kuwa angeweza kubaki madarakani hadi bunge lipige kura ya kutokuwa na imani naye.

Mei 20, Rais Sharif aliacha uamuzi wake wa kumtimua Waziri Mkuu Sharmarke. Mabadiliko yalikuja baada ya kushauriana na wanasheria, waliomshauri kuwa kufukuzwa kwa waziri mkuu huyo kulikuwa ni kinyume cha katiba.

Mei 26, kufuatia kutokubaliana tena na Waziri Mkuu Sharmarke, Rais Sharif alitangaza tena mpango wake wa nchi moja kuteua Waziri mpya. Washirika wa Sharif pia waliripotiwa kujaribu kumshawishi Sharmarke kujiuzulu, lakini alikataa tena hatua hiyo na aliapa kukaa madarakani mpaka muda wake wa kikatiba uishe.

Na ilipofika mwezi Oktoba 14, 2010, ndipo Rais Sharif alipofanikiwa adhma yake na kumteua katibu maalum wa kwanza wa zamani wa ubalozi wa Somalia mjini Washington, Mohamed Abdullahi Mohamed, kuwa Waziri Mkuu mpya wa Somalia.

Makala haya yameandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa mashirika mbalimbali ya habari ya kimataifa.

No comments:

Post a Comment