Apr 13, 2011

CCM KUJIVUA GAMBA: Suala lisiwe kujisafisha tu bali kuleta maendeleo kwa wananchi

 Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM) na Mjumbe wa NEC, 
Andrew Chenge anahusishwa kwenye kashfa ya rada.

 Mbunge wa Igunga (CCM) na Mjumbe wa NEC, 
Rostam Aziz anahusishwa kwenye kashfa ya Dowans.

BISHOP J. HILUKA
Dar es Salaam

WIKI hii imetawaliwa na habari kuhusu Chama Cha Mapunduzi (CCM) kwenye vyombo mbalimbali vya habari na kila mtu ameonekana kuguswa kwa kile kilichokuwa kikiendelea huko Dodoma, hasa kufuatia chama hicho kuamua kufanya mabadiliko makubwa kwenye safu yake ya uongozi ndani ya Kamati Kuu kwa nia ya kujisafisha.

Mabadiliko hayo ya kiuongozi yamekuja katikati ya tuhuma mbalimbali na za muda mrefu za ufisadi wa viongozi wakuu ndani ya chama zilizokuwa zikiharibu sifa ya chama hicho kikongwe katika siasa za Tanzania, kulikopelekea mkakati wa kujisafisha kuanza na sekretarieti ya chama hicho iliyokuwa ikiongozwa na Yusuf Makamba ijiuzuru.

Sikuwepo kwenye kikao cha CCM lakini kutokana na taarifa zilizonifikia nikiwa mdau wa habari, inasemekana kuwa mwenyekiti alikuwa na mtihani mkubwa sana kuwatosa wanaotuhumiwa kwa ufisadi kwa kuwa bado wameonekana kukita mizizi yao ndani ya Halmashauri Kuu na chama kwa ujumla.

Mabadiliko hayo ya kiuongozi ndani ya Kamati Kuu yamepelekea chama kupata Katibu Mkuu mpya aliyechukua nafasi ya mzee Yusuf Makamba ambaye ni Wilson Mukama, akiwa na manaibu, John Chiligati, Naibu Katibu Mkuu upande wa Bara na Vuai Ali Vuai, Naibu Katibu Mkuu upande wa Zanzibar.

Nadhani kwa hatua hii Chama Cha Mapinduzi kinastahili pongezi japo kwa mtazamo wangu naona kuwa bado hakijakidhi matarajio ya wengi kwani mafisadi wanaolalamikiwa bado wanaonekana kuwa na nguvu na wamo kwenye NEC. Si hivyo tu, inaonekana imeshindikana kuwatosa kabisa, hali inayoashiria kuwa kama gamba walilojivua ni gamba la kichwani tu, bado gamba la mwilini.

Sitaki kusema kuwa kujivua gamba kwa maana ya kubadilisha uongozi ndani ya sekretarieti ya chama na kuwatosa mafisadi inatosha, nadhani bado haitoshi kuishia kwenye kuwastaafisha mafisadi tu bali iwe ni pamoja na kuwashitaki na kuwafilisi mali zote walizopata kwa njia ya kifisadi.

Hata hivyo, isionekane kufanya kazi na maamuzi yake kama wanavyotaka tuelewe kuwa ni kwa faida ya Tanzania na vizazi vijavyo, bali ionekane inafanya hivyo na wananchi waone, kwa kuanzia iwe ni kuwaongoza Watanzania kujipatia Katiba mpya bila ya kuangalia maslahi ya chama peke yake.

Na kama ni kweli kauli ya mwenyekiti wa CCM kuhusu kujivua gamba ilimaanisha CCM ni kama nyoka, ujumbe huo utakuwa na maana kubwa kwani tumeshang'atwa sana na mwenyekiti atakuwa ametambua kile kinacholalamikiwa muda mrefu na wananchi kuhusu IPTL, Deep Green, Meremeta, Richmond/Dowans, EPA na mengine kibao. Hivyo gamba jipya litusaidie kumwona nyoka huyo hata kama atajificha gizani.

Kama kweli Chama Cha Mapinduzi kina nia ya dhati kujivua gamba na kuwatumikia wananchi, kinapaswa kianze sasa kuwekeza katika kuhakikisha kunakuwepo uwiano sawa kwenye mgawanyo wa rasilimali ili kwenda sawa na kaulimbiu ya mwenyekiti wake ya “Maisha bora kwa kila Mtanzania”.

Watawala waelewe kuwa asilimia kubwa ya wananchi wa Tanzania wanaishi vijijini kwa kutegemea jembe la mkono, kipato wanachopata kutokana na kilimo cha aina hiyo sote tunatambua kwamba hakiwasaidii kukidhi mahitaji yao muhimu ya kila siku. Ile kauli ya mtaji wa masikini ni nguvu zake mwenyewe ingekuwa na ukweli, basi wananchi wengi wa Tanzania wangekuwa matajiri.

CCM sasa kiangalie namna ya kuinyima ajenda Chadema kwa kuboresha maisha ya Watanzania, wasikalie kulalamika tu pindi Chadema inapotumia nguvu ya umma na wananchi wanapoamua kuandamana kwa kuwa hawana ajira. Sijui watawala wanataka wananchi wakafanye kazi gani, wakati wakulima huko vijijini hawapati kile kinachostahili kwa kutumia jembe la mkono?

Wananchi wanalalamika kwa kuwa wakija mijini hali bado ni ngumu wakati watawala waliopewa dhamana ya kuweka mazingira hayo wakiwa wamelala usingizi na kufikiria jinsi ya kutengeneza mikataba feki ili wachote fungu wanaloliona lipo 'idle'.

Ni wakati sasa watawala wetu waelewe kuwa Watanzania siyo wavivu kama wanavyofikiria, uchumi siyo kutoa takwimu tu bali kuwawezesha Watanzania kuwa na matumaini ya kuuza mazao yao kwa wakati kutoka mashambani. Kwa hiyo kujivua gamba kwa chama hicho kikongwe kusiishie kwenye kubadilisha uongozi tu, wanapaswa wayaone haya na kuyatekeleza kivitendo.

Hili jambo la kila uchaguzi mmoja ukiisha wanaanza kufikiria kupata pesa ya uchaguzi mwingine linapaswa liachwe sasa kama kweli mabadiliko hayo yana lengo la kumnufaisha mwananchi wa kawaida. Ninavyoamini mimi, adui namba moja wa maendeleo ya nchi hii ni viongozi mafisadi hasa walio ndani ya CCM ambao wengi wanakosa maadili.

Chama kinatakiwa kuwaondoa viongozi wengi ambao wanafikiria kujilimbikizia mali ili Mungu siku akiwaita, watoto wao na jamaa zao waendelee kutumia walichoiba na si kutafuta vyao kwa kuwa wamewaachia mazingira mazuri ya wao kufanikiwa kwenye nchi yao bila kufanya kazi.

Kwa hiyo nadhani bado kazi ya kujivua gamba ni ngumu sana na chama hicho kikaze buti zaidi maana inaeleweka wazi kuwa kiongozi mtendaji mkuu aliyekuwepo alikuwa mwanamipasho, lakini si yeye aliyetumia pesa za Kagoda. Yupo anayewalinda wahalifu na kufanya kuwepo uzito hata kuwakemea watumishi wengine wa serikali wanaofanya ufisadi wa kufuru.

Chama hiki kwa kuwa ndicho chama tawala hakina budi kiangalie pia mfumo wa elimu uliopo ili kuwasaidia wananchi kuondokana na ujinga, maana hiyo imekuwa ikitumiwa kama njia (loop-hole) ya kuwakandamiza wananchi wasiozijua haki zao. Wanachama wake pia wapewe nafasi ya kukikosoa chama, kukaa pamoja na kuzungumza chochote juu ya mustakbali wa nchi.

Suala la elimu ni nyeti maana imeonekana kuwa hata pale elimu nzuri inapotolewa huwa ni kwa kundi la watu maalumu ambao wanaaminika kwamba watakuwa tayari kuendeleza mfumo uleule wa kudumaza fikra za wananchi kwa propaganda kinyume na hali halisi ilivyo.

Nakubaliana na wanaosema kuwa serikali ya CCM imeshatengeneza bomu la kwanza kupitia sekondari za kata, na sasa inatengeneza bomu jingine kubwa iwapo itatekeleza mpango wake wa kuwaita wawekezaji wakubwa kupora ardhi ya wananchi kupitia sera yake ya kilimo kwanza.

Siku hizi kila kukicha ni migogoro ya ardhi tu inayorindima na imepelekea kumwagika damu za watu wasio na hatia, hivi hali hii itaisha lini? Viongozi wetu wataendelea kulifumbia macho suala hili hadi lini?

Nilishangazwa siku moja kusikia kauli za wawaziri wakiwasihi wananchi wasiokuwa na ardhi wasiharibu mali (mashamba, matrekta) za wawekezaji wala wasiwatumie meseji za kuwatisha. Lakini cha ajabu hakuna waziri hata mmoja aliyekuwa tayari kukiri kwamba serikali itawatafutia ardhi sehemu nyingine au ardhi kubwa iliyogawiwa wawekezaji itapunguzwa ili wananchi wagaiwe.

Mungu ibariki Tanzania

No comments:

Post a Comment