Apr 13, 2011

RAIS RUPIAH BANDA: Akina mama wa Zambia waapa kumnyima usingizi uchaguzi ujao

 Rais wa Zambia, Rupiah Banda

LUSAKA
Zambia

ELIZABETH Phiri aliwahi kukasirishwa mno alipopuuzwa kama mgombea wa ubunge wa chama cha Patriotic Front katika uchaguzi mdogo mwaka 2008 kutokana na jinsia yake na hivyo kujiondoa katika chama hicho. Miaka mitatu baadaye, amejiunga tena na chama hicho lakini bado ana wasiwasi – lakini wanawake wengine wanasiasa wanaona kuna sababu ya matumaini katika uchaguzi wa mwaka huu 2011.

Edith Nakawi ni kiongozi katika chama cha Forum for Democracy and Development (FDD), anakubali kuwa kuna tabia ya kawaida kwa wanaume “kuwadharau wagombea wanawake”. Nakawi, ambaye ameongoza chama chake tangu mwaka 2005, ameweka historia kwa kuwa rais wa chama cha siasa mwanamke wa kwanza katika taifa la Zambia. Kabla ya hapo, alivunja rekodi nyingine ya kuwa waziri wa fedha wa kwanza mwanamke nchini Zambia na Kusini mwa Afrika mwaka 1998. Pia aliwahi kushika nafasi ya uwaziri katika wizara mbalimbali kati ya mwaka 1992 na 2001.

Siku za karibuni imekuwa ikisemwa kuwa siku za wanaume pekee kugombea urais zimeisha nchini Zambia. Wakati tarehe za uchaguzi wa mwaka huu zitakapotangazwa, Nakawi ataingiza jina lake, pamoja na wengine ambao wanataka kuongoza nchi ya Zambia kwa miaka mitano ijayo.

Baada ya uchaguzi wa mwaka 2006, kulikuwa na kilio hasa kutoka kwa mashirika ya kiraia juu ya uwakilishi mdogo wa wanawake. “Lakini siyo wakati huu,” anasema Nakawi. Ana imani kuwa mwaka huu wanawake wengi zaidi watashinda uchaguzi.

Kwa sasa kuna wabunge 24 tu kati ya wabunge 150. Katika Baraza la Mawaziri kuna wanawake watano mawaziri kati ya 21. Kuna manaibu waziri wanawake 6 kati ya 20.

Pia kumekuwepo habari ambazo ni nzuri kwa rais Banda kuhusu kuvunjika kwa Muungano kati ya vyama viwili vikubwa vya upinzani nchini Zambia baada ya kutokea sintofahamu miongoni mwa viongozi wa vyama hivyo. Muungano huo uliobuniwa mwaka 2009 uliviunganisha pamoja vyama vya Patriotic Front (PFP) na United Party for National Development (UPND).

Muungano huo ulikuwa ukimkosesha usingizi Rais Rupia Banda pamoja na chama tawala. Habari zilisema kuwa ndoa hiyo ya kisiasa kati ya PFP na UPND ilivunjika baada ya pande mbili hizo kushindwa kufikia makubaliano juu ya nani hasa anafaa kuwania urais kwa tiketi ya muungano huo.

Weledi wa siasa za Zambia wamelitaja tukio hilo kuwa pigo kwa demokrasia ya nchi hiyo kwani hakuna chama chochote cha upinzani kinachoweza kushinda uchaguzi kikiwa peke yake.

Historia ya Rupiah Banda

Rupiah Bwezani Banda alizaliwa Februari 13, 1937, ni rais wa nne wa Zambia tangu ijipatie uhuru wake kutoka kwa wakoloni. Ameshika wadhifa huo tangu 2008.

Wakati wa Urais wa Kenneth Kaunda, Banda alishika nyadhifa muhimu za kidiplomasia na alikuwepo katika ulingo wa siasa kama mwanachama wa United National Independent Party (UNIP). Miaka iliyofuata, aliteuliwa kuwa Makamu wa Rais na Rais Levy Mwanawasa Oktoba mwaka 2006, baada ya uchaguzi wa marudio. Alishika madaraka ya urais baada ya Mwanawasa kuugua kiharusi mwezi Juni 2008, na kufuatia kifo cha Mwanawasa mwezi Agosti 2008, alikuwa Kaimu Rais.

Kama mgombea wa chama kilicho madaralani cha Movement for Multiparty Democracy (MMD), alishinda uchaguzi wa urais Oktoba 2008 kwa kupata ushindi mwembamba, kwa mujibu wa matokeo rasmi.

Maisha ya awali na diplomasia

Banda alizaliwa katika mji wa Miko, Gwanda, Rhodesia ya Kusini (sasa Zimbabwe); wakati wazazi wake walipokwenda huko wakitokea Rhodesia ya Kaskazini (Zambia), walikwenda kutafuta ajira kabla ya kuzaliwa kwake, na alifadhiliwa na mhubiri Kiholanzi aliyemsaidia kuendelea elimu yake. Aliweza kushiriki siasa wakati alipojiunga na tawi la vijana wa UNIP mwaka 1960.

Banda kamuoa Hope Mwansa Makulu, mwaka 1966 na wana watoto watatu. Banda pia ana watoto wawili kutoka katika mahusiano yake ya awali.

Alikuwa mwakilishi wa UNIP katika nchi za Ulaya ya Kaskazini miaka ya 1960, na 1965 aliteuliwa kuwa Balozi wa Zambia nchini Misri. Wakati huo, akawa na urafiki na kiongozi wa UNITA, Jonas Savimbi, na uamuzi wa kuruhusu UNITA ifungue ofisi mjini Lusaka wakati huo ulitokana na ushawishi wa Banda.

Banda aliteuliwa kuwa Balozi nchini Marekani Aprili 7, 1967. alifanya kazi kwa miaka miwili, kisha akarudi Zambia na kuwa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Vijijini kwa miaka miwili na baadaye akawa Meneja Mkuu wa Bodi ya Masoko ya Kilimo ya Taifa kwa miaka miwili.

Kisha aliteuliwa kuwa Mwakilishi wa Kudumu wa Umoja wa Mataifa, na wakati akiwa katika nafasi hii aliongoza Baraza la Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Namibia. Baada ya mwaka mmoja katika Umoja wa Mataifa, aliteuliwa katika Baraza la Mawaziri kama Waziri wa Mambo ya Nje. Katika kipindi kifupi cha Uwaziri wa Mambo ya Nje (1975-1976), Banda alikuwa na kazi ya ngumu kujaribu kusitisha vita vilivyopamba moto Angola.

Siasa

Banda alichaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Munali mwaka 1978 na kuchaguliwa tena mwaka 1983. Ingawa alishindwa katika uchaguzi wa mwaka 1988, alifungua kesi mahakamani. Pia, wakati huo alifanya kazi kama Waziri wa Nchi anayeshugulikia Madini. Mwaka 1991, alishindwa katika uchaguzi wa ubunge wa jimbo la Munali na mgombea wa Movement for Multiparty Democracy (MMD), Ronald Penza. Ingawa awali alikuwa na nia ya kuwania tena katika uchaguzi wa mwaka 1996, aliunga mkono mgomo ulioitishwa na UNIP kugomea ya uchaguzi.

Baada ya Rais Mwanawasa kuchaguliwa tena Septemba 2006, alimteuwa Banda kuwa Makamu wa Rais Oktoba 9, 2006 pamoja na baraza jipya la mawaziri. Baadaye alijiunga na MMD baada ya uteuzi wake. Uteuzi wa Banda ulichukuliwa kama zawadi ya Wazambia wa Mashariki kwa kuikiunga mkono MMD katika uchaguzi, hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa watu wa Mashariki kufanya hivyo.

Kabla ya mkutano uliopangwa wa Jumuia ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) Agosti 2007, Banda alitumwa na Mwanawasa kuboresha mahusiano na nchi jirani ya Zimbabwe kufuatia Mwanawasa kuukosoa utawala wa Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe.

Kaimu Rais

Baada ya Mwanawasa kuugua kiharusi wakati akihudhuria mkutano wa Umoja wa Afrika nchini Misri 29 Juni, 2008, Banda alikaimu nafasi ya Rais.

Kama Makamu wa Rais, Banda pia alifanya kazi kama kiongozi wa shughuli za serikali katika Bunge la Taifa, hata hivyo, wakati Bunge lilipokutana Agosti 5, 2008, kufuatia ugonjwa wa kiharusi wa Mwanawasa, Banda alimteua Waziri wa Ulinzi, George Mpombo, kuongoza serikali katika biashara ndani ya ubunge.

Mwanawasa hakupona kiharusi, alikufa wakati akiwa bado yupo hospitali mjini Paris Agosti 19, 2008. Akielezea “huzuni kubwa na masikitiko makubwa”, Banda alitangaza kifo chake kwa taifa na kutangazwa kipindi cha siku saba za maombolezo ya kitaifa, kuwataka Wazambia “kubaki watulivu na kumuomboleza Rais wetu kwa heshima.” Banda alichukua rasmi nafasi ya kaimu rais kabla ya uchaguzi mpya wa rais, ambao kwa mujibu wa Katiba unafanyika ndani ya siku 90 baada ya kifo cha Mwanawasa.

Banda aliomba ateuliwe kuwa mgombea wa MMD Agosti 26, 2008. Siku hiyohiyo, chama cha MMD katika jimbo la Mashariki kilitoa taarifa kuunga mkono ugombea wa Banda. Halmashauri Kuu ya Taifa ya MMD ilimchagua Banda kuwa mgombea urais kwa kura ya siri Septemba 5. Alipata kura 47 dhidi ya 11 za Ngandu Magande, Waziri wa Fedha. Katika tukio hili, Banda aliahidi “kuunganisha chama na taifa zima” na “kuendelea kutekeleza mipango ya Mwanawasa”.

Uchaguzi wa rais ulifanyika Oktoba 30. Matokeo ya awali yalimuonesha mpinzani mkuu wa Banda, Michael Sata wa Patriotic Front (PF), kuongoza, lakini kura kutoka maeneo ya vijijini zilipohesabiwa, Banda alipunguza pengo na hatimaye kumshinda Sata. Matokeo ya mwisho ya Novemba 2 yalionesha Banda kupata asilimia 40 ya kura dhidi ya asilimia 38 za Sata.

Banda aliapishwa katika Ikulu siku hiyohiyo, alitumia hotuba yake kutoa wito wa umoja. Chama cha PF kilitoa madai ya kuwepo udanganyifu na kilikataa kuutambua ushindi wa Banda, wakati wafuasi wa Sata walipofanya vurugu katika miji ya Lusaka na Kitwe.

Urais

Kama Rais, Banda alilenga kwenye maendeleo ya kiuchumi, alisafiri nje ya nchi kutangaza biashara ya Zambia kwa viongozi wengine wa dunia. Mwezi Disemba 2010, alisafiri hadi Misri kukutana na Rais Hosni Mubarak.

Katikati ya 2009 ilitangazwa kwamba Halmashauri Kuu ya Taifa ya MMD imemteua Banda kuwa mgombea wa chama hicho kwa uchaguzi wa rais 2011. Baadhi ya watu wamekosoa, wakisema kuwa mchakato wa uteuzi unapaswa kuwa wazi kwa wagombea wengine; Mpombo, Waziri wa Ulinzi, alijiuzulu wadhifa wake mwezi Julai 2009 wakati akikosoa mchakato huo kuwa haukuwa wa kidemokrasia.

Makala hii imeandalaiwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari

No comments:

Post a Comment