Apr 27, 2011

JENERALI MUHAMMADU BUHARI: Asababisha vurugu kubwa Kaskazini mwa Nigeria baada ya kupinga matokeo

 Jenerali Muhammadu Buhari

ABUJA
Nigeria

BAADA ya Tume ya uchaguzi ya Nigeria (INEC) kumtangaza rasmi mgombea wa chama kinachotawala nchini humo, Goodluck Jonathan, kuwa rais baada ya uchaguzi mkuu kumalizikika nchini humo kwa kupata kura milioni 22.5, zilizuka ghasia kubwa Kaskazini mwa Nigeria zilizopelekea vifo vya mamia ya watu.

Awali ghasia ziliripotiwa kuzuka Kaskazini mwa Nigeria wakati matokeo ya awali ya urais yalipokuwa yakionesha kuwa Goodluck Jonathan anaelekea kushinda. Nyumba za wafuasi wa Jonathan, mgombea aliyekuwa anatetea kiti cha urais, zilishambuliwa katika miji ya Kano na Kaduna.

Wafuasi vijana wa mgombea urais mwenziye, Muhammadu Buhari, ambaye ana umaarufu upande wa Kaskazini mwa nchi, walikuwa wakipambana na polisi na wanajeshi. Wafuasi hao walifanya vurugu hizo wakiwa wanahisi kuwa uchaguzi ulikuwa umevurugwa katika baadhi ya maeneo upande wa Kusini.

Baada ya kutangazwa mshindi, Rais Jonathan alitoa wito wa kuwepo kwa hali ya utulivu, akisema "Hakuna mwanasiasa mwenye thamani ya kumwaga damu ya Wanigeria".

Kwa sasa hali ya ghasia nchini humo imeanza kuwa shwari huku mji wa Kaskazini mwa Nigeria wa Kaduna ukiwa umeanza kutulia baada ya kuzuka machafuko makubwa ya kupinga matokeo hayo ya Uchaguzi Mkuu.

Duru za habari zinasema watu 400 wamekamatwa kuhusiana na machafuko hayo yaliyoambatana na uchomaji wa makanisa, vituo vya polisi na nyumba za watu katika siku mbili za ghasia. Shirika la msalaba mwekundu lilikaririwa likisema kuwa watu wengi wameuawa na wengine 48,000 kuzikimbia nyumba zao.

Chanzo cha machafuko hayo ni baada ya mgombea urais kupitia upinzani, Jenerali Muhammadu Buhari kupinga matokeo akidai kuwa kulikuwa na udanganyifu. Kadhalika ilikuwa kufuatia hali ya baadhi ya wafuasi wake sehemu za kusini mwa nchi hiyo kushindwa kupiga kura.

Ingawa waangalizi wa kiamataifa wanasema kuwa uchaguzi huo ulikuwa huru na Goodluck Jonathan kutangazwa mshindi, lakini Jenerali Buhari anayetoka Kaskazini mwa nchi amesema chama chake kitapinga kisheria matokeo hayo na ametoa wito wa kuwepo utulivu baada ya ghasia.

Historia ya Buhari

Muhammadu Buhari alizaliwa Desemba 17, 1942, aliwahi kuwa kiongozi wa kijeshi wa Nigeria kuanzia Desemba 31, mwaka 1983 hadi 27 Agosti 1985, na mgombea urais katika chaguzi za mwaka 2003, 2007 na uchaguzi wa mwaka huu 2011. Buhari anatokea katika kabila la Fulani, na ni mwenye imani ya Uislamu, huku familia yake ikitoka Jimbo la Katsina.

Waziri wa Petroli

Buhari alifamahika kwa mara ya kwanza kwenye umma mwaka 1976 wakati alipokuwa Waziri (au "Kamishna wa Shirikisho") wa Petroli na Maliasili chini ya aliyekuwa Mkuu wa Nchi wakati huo, Olusegun Obasanjo. Kabla ya hapo aliwahi kuwa Gavana wa Jimbo jipya la Kaskazini-Mashariki wakati wa utawala wa Murtala Mohammed. Baadaye akawa mkuu wa Shirika jipya la Petroli la Nigeria mwaka 1977.

Serikali ya Buhari

Meja Jenerali Buhari alichaguliwa kuongoza nchi ya Nigeria baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyofanikiwa kuuondoa madarakani utawala wa kiraia wa Rais Shehu Shaghari tarehe 31 Desemba, 1983. Wakati huo, Buhari alikuwa mkuu wa Idara ya Tatu ya Jeshi iliyopo Jos. Buhari aliteuliwa kuwa Mkuu wa Nchi na Amiri Jeshi Mkuu wa vikosi vya jeshi, na Tunde Idiagbon aliteuliwa kuwa Kiongozi Mkuu wa Wafanyakazi.

Buhari aliyaelezea mapinduzi hayo ya kijeshi kama nguvu ya kuiondoa madarakani serikali ya kiraia iliyokuwa imekithiri kwa rushwa, na utawala wake hatimaye ulianzisha kampeni ya umma dhidi ya ukosefu wa maadili iliyojulikana kama "Vita dhidi ya ukosefu wa maadili". Masuala ya kampeni hii ilikuwa ni pamoja na udhalilishaji wa umma wa watumishi wa umma ambao waliwasili kazini wakiwa wamechelewa, walinzi waliokuwa na silaha na mijeledi waliwekwa kuhakikisha kunakuwepo utaratibu mzuri wa foleni katika vituo basi.

Pia alifanya kazi ya kuwanyamazisha wakosoaji wa utawala wake, akapitisha amri kupambana na uhuru wa vyombo vya habari na kuruhusu wapinzani wake watiwe kizuizini hadi miezi mitatu bila mashtaka rasmi. Pia alipiga marufuku migomo na wafanyakazi kuwafungia mabosi, na kuanzisha jeshi la kwanza la polisi wa siri nchini Nigeria, Shirika la Usalama wa Taifa. Serikali yake ilimhukumu mwanamuziki maarufu na mkosoaji wa siasa za nchi hiyo, Fela Kuti kwa miaka kumi gerezani. Kuti baadaye alipata msamaha na aliyekuwa mrithi wa Buhari.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Uingereza (BBC), “Buhari alijaribu kuweka uwiano wa fedha za umma kwa kupambana na bidhaa zilizopelekea wengi kupoteza kazi na hasara nyingi zilizopelekea kufungwa kwa biashara.” Hasara hizo ziliambatana na kupanda kwa bei na kushuka kwa hali ya maisha.

Mapinduzi ya 1985 na kuwekwa kizuizini

Kufuatia kuwepo hali mbaya ya kiuchumi, na kuendelea kuenea kwa rushwa, Buhari aliangushwa katika mapinduzi yaliyoongozwa na Jenerali Ibrahim Babangida na wanachama wengine wa Halmashauri Kuu ya Jeshi (SMC) Agosti 27, 1985.

Babangida aliwachukuwa watu wengi zaidi walioonekana kama wakosoaji wa serikali ya Buhari na kuwaingiza katika utawala wake, ikiwa ni pamoja na ndugu wa Fela Kuti, Benko Ransome-Kuti, daktari ambaye alikuwa ameongoza mgomo dhidi ya Buhari kupinga kupungua huduma za afya. Kisha Buhari aliwekwa kizuizini Katika jiji la Benin hadi mwaka 1988.
Miaka iliyofuata

Buhari alifanya kazi kama Mwenyekiti wa Mfuko wa Petroli, chombo kilichoanzishwa na serikali ya Jenerali Sani Abacha, na kufadhiliwa na mapato yanayotokana na kuongezeka kwa bei ya mafuta ya petroli, ili kutekeleza miradi ya maendeleo nchini kote.

Mwaka 2003, Buhari aligombea katika uchaguzi wa rais kama mgombea wa All Nigeria People's Party (ANPP). Alishindwa na mgombea wa People's Democratic Party, Rais Olusegun Obasanjo, kwa kiasi cha zaidi ya kura milioni kumi na moja. Hata hivyo, ilidaiwa na wafuasi wa Buhari na wanachama wengine wa chama cha upinzani kwamba katika baadhi ya majimbo, kama Ebonyi, kulikuwa na kura nyingi zaidi ya wapiga kura.

Pamoja na madai ya kuwepo udanganyifu yaliyothibitishwa katika mahakama na mwenendo wa uchaguzi ulikosolewa mno na Kundi la Waangalizi kutoka Jumuia ya Madola, makubaliano kati ya Wanigeria yalikuwa kwamba Buhari asipoteza muda wake katika mahakama kwa kuwa hakuwa na rasilimali za kumsaidia "kujinunulia" haki.

Hatimaye, mahakama hiyo pia iliamua kwamba madai ya udanganyifu yaliyothibitishwa hayakutosha kuathiri matokeo ya uchaguzi na uthibitisho wa kufuta uchaguzi mzima wa Rais.

Tarehe 18 Desemba 2006, Jen. Buhari aliteuliwa tena kuwa mgombea wa All Nigeria People's Party. Mpinzani wake mkuu safari hii katika uchaguzi wa Aprili 2007 alikuwa mgombea wa chama tawala cha PDP, Umaru Yar'Adua, waliyetoka sehemu moja ya Katsina.

Katika uchaguzi, Buhari alipata asilimia 18 ya kura dhidi ya asilimia 70 ya Yar'Adua, lakini Buhari aliyakataa tena matokeo haya. Baada ya Yar'Adua kuingia madarakani, chama cha ANPP kilikubali kujiunga na serikali yake, lakini Buhari alikataa.

Machi 2010, Buhari alijiondoa katika chama cha ANPP na kujiunga na Congress for Progressive Change (CPC). Buhari aligombea tena urais katika uchaguzi mkuu wa 16 Aprili 2011, dhidi ya rais wa sasa, Goodluck Jonathan wa People's Democratic Party (PDP), na wengineo. Alikuwa anagombea akiwa na sera kubwa ya kupambana na rushwa na kuahidi kuondoa ulinzi na kinga kutoka kwa maafisa wa serikali.

Pia aliunga mkono utekelezaji wa sheria za Kiislamu (Sharia), katika Majimbo ya Kaskazini mwa Nigeria, sera ambayo hapo awali ilimsababishia matatizo makubwa ya kisiasa miongoni mwa wapiga kura Wakristo katika maeneo ya Kusini.

Hata hivyo, matokeo ya mwaka huu yaamemwacha Buhari akishika nafasi ya pili kwa kupata kura 12,214,853, nyuma ya rais rais Goodluck Jonathan, aliyepata kura 22,495,187 na kutangazwa mshindi.

Makala hii imeandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa vyanzo mbalimbali vya habari

No comments:

Post a Comment