Apr 20, 2011

GOODLUCK JONATHAN ACHAGULIWA RAIS: Alipewa jina la Goodluck na baba yake akimtabiria kuwa na bahati

 Rais Goodluck Jonathan

ABUJA
Nigeria

UCHAGUZI wa rais nchini Nigeria umemalizika huku Rais aliyefanikiwa kutetea kiti chake, Jonathan Goodluck akitoa wito wa kusitisha kile alichokisema “mambo yasiyo ya lazima yanayoweza kuepukwa” yanayosababisha ghasia za baada ya uchaguzi katika eneo la Kaskazini ya nchi. Rais Jonathan ametangazwa mshindi katika uchaguzi wa rais, ambapo tume ya uchaguzi imesema kuwa amepata asilimia 57 ya kura.

Maandamano yameenea katika eneo linalokaliwa na Waislamu la Kaskazini – ngome ya upinzani – baada ya matokeo kubainika. Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Nigeria ya hivi karibuni kwa matokeo ya uchaguzi kuleta mgawanyiko mkubwa kati ya Waislamu walio Kaskazini na Wakristo walio Kusini mwa nchi.

Goodluck Jonathan ameshinda katika karibu eneo lote la Kusini, ambalo ni eneo linalokaliwa na Wakristo isipokuwa kwenye Jimbo moja, wakati mpinzani wake mkuu, Muhammadu Buhari ameshinda katika eneo la Kaskazini-Mashariki na Kaskazini-Magharibi linalokaliwa na Waislamu. Wagombea wote wawili wamepata kura katika eneo la Kaskazini ya Kati ambalo linakaliwa kwa pamoja na Waislamu na Wakristo.

Kiongozi wa kundi la waangalizi kutoka Muungano wa Afrika, rais wa zamani wa Ghana, John Kufuor, aliliambia Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), kuwa alikuwa ameridhishwa na jinsi uchaguzi huo ulivyoendeshwa.

Uchaguzi muhimu wa Rais nchini humo umefanyika mwishoni wa wiki iliyopita katika hali ambayo wagombea watatu wa upinzani ndiyo walionekana wangetoa ushindani mkubwa kwa Rais wa sasa wa nchi hiyo, Goodluck Jonathan, kati ya wagombea ishirini walijitokeza kuwania kiti cha Urais katika uchaguzi huo. Hata hivyo, ni wagombea wanne tu akiwemo Rais Goodluck Jonathan ndio waliotajwa kuwa na nafasi ya kuibuka na ushindi katika uchaguzi huo.

Kwa mujibu wa Katiba ya Nigeria mgombea yeyote anayejinyakulia theluthi mbili ya kura katika majimbo 36 ya nchi hiyo atatangazwa mshindi na hakutakuwa na haja ya uchaguzi huo kuingia katika duru ya pili. Wachambuzi wa mambo walikuwa wanaamini kuwa, Goodluck Jonathan ambaye ni Mkiristo hatopata kura za wakazi wa majimbo ya Kaskazini mwa nchi hiyo ambayo ni ya wakazi wengi wa Kiislamu. Pamoja na hayo, weledi wa siasa za Nigeria walitabiri kwamba, Jonathan ataibuka na ushindi hasa kutokana na kutokuweko nguvu moja na mgombea mmoja katika kambi ya upinzani.

Viongozi wa vyama vya upinzani hawakuweza kufikia mwafaka wa kusimamisha mgombea mmoja katika uchaguzi huo; hali ambayo bila shaka imeonekana kumpa ahueni mgombea huyo wa chama tawala nchini Nigeria cha PDP, yaani Rais Goodluck Jonathan. Hata hivyo hatua ya wapiga kura wa Kiislamu wa maeneo ya Kaskazini mwa Nigeria ya kuwaunga mkono wagombea watatu ilikuwa inatathminiwa na wajuzi wa mambo kuwa ni sawa na kuunda kambi moja ya wapiga kura dhidi ya Rais Jonathan.

Jenerali wa zamani, Muhammadu Buhari wa Chama cha CPC ndiye aliyekuwa anahesabiwa kuwa mpinzani mkuu wa Jonathan. Buhari anapendwa mno na wakazi wa maeneo ambayo kawaida ni majimbo ya Waislamu na inatabiriwa kuwa hiyo ndio nguvu ya mgombea huyo. Muhammadu Buhari amewahi pia kuwa mgombea wa kiti cha Urais wa nchi hiyo katika miaka ya 2003 na 2007.

Historia ya Goodluck Jonathan:

Goodluck Ebele Jonathan Azikiwe, amezaliwa 20 Novemba 1957, ni Rais wa 14 na wa sasa wa Nigeria. Alikuwa Gavana wa Jimbo la Bayelsa tangu Desemba 9, 2005 hadi Mei 28, 2007, na aliapishwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Shirikisho la Nigeria tarehe 29 Mei 2007.

Jonathan ni mwanachama wa chama tawala cha People's Democratic Party (PDP). Tarehe 13 Januari 2010, mahakama ya shirikisho ilimkabidhi Jonathan mamlaka ya kuendesha mambo ya serikali wakati Rais Umaru Yar'Adua alipokuwa akipata matibabu katika hospitali nchini Saudi Arabia. Aliyekuwa Waziri wa Habari wa Nigeria, Prof. Dora Akunyili alikuwa wa kwanza kulaani uongozi kwa kutokuwa na hakika.

Hoja ya Baraza la Seneti la Nigeria ya tarehe 9 Februari 2010, ilithibitisha mamlaka hayo ya Jonathan kama Kaimu Rais, huku wakiyatambua maoni ya Prof. Akunyili. Tarehe 24 Februari 2010, Yar'Adua alirejea Nigeria, lakini Jonathan aliendelea kukaimu Urais. Baada ya kifo cha Yar'Adua tarehe 5 Mei 2010, Jonathan alichukuwa madaraka ya Urais, na kula kiapo tarehe 6 Mei 2010.

Maisha ya awali, elimu na maisha ya binafsi:

Jonathan alizaliwa katika eneo la Otueke, katika halmashauri ya Ogbia iliyopo eneo la Jimbo la Mashariki, ambalo baadaye lilijulikana kama Jimbo la River, na sasa linajulikana kama Jimbo la Bayelsa, kutoka kwenye familia ya watengeneza mitumbwi. Makundi mengi ya kikabila ndani ya Nigeria yana utamaduni wa kutoa majina kwa watoto ambapo jina la mtoto linaelezea matarajio fulani ya wazazi kuhusu mtoto au mazingira yake ya kuzaliwa. Baba mzazi wa Jonathan, Ebele Jonathan (Mkristo wa kabila la Ijaw kutoka sehemu ya Kusini mwa Nigeria) alisema kuwa jina la mwanaye, Goodluck lilimjia baada ya mtoto wake kuzaliwa, alimpa jina hilo alipogundua kwamba mtoto huyo alionekana kuwa na chembe chembe za bahati.

Jonathan amefuzu shahada ya kwanza (B.Sc.) ya Zoology. Pia ana shahada ya uzamili (M.Sc.) katika biolojia ya Uvuvi na Hydrobiology, na shahada ya uzamivu (Ph.D.) ya Wanyama kutoka Chuo Kikuu cha Port Harcourt. Baada ya kupata shahada yake, alifanya kazi mbalimbali kama mkaguzi wa elimu, mhadhiri, na afisa mazingira, mpaka alipoamua kuingia katika siasa 1998.

Miaka ya mwanzo katika kisiasa

Ugavana wa Jimbo la Bayelsa: Jonathan alianza siasa mwaka 1998, alipojiunga na People's Democratic Party (PDP) mwaka 1998. Jonathan, ambaye mwanzo alikuwa Naibu Gavana wa Jimbo la Bayelsa, alichukuwa nafasi ya Gavana Diepreye Alamieyeseigha, ambaye alituhumiwa na Bunge la Jimbo la Bayelsa baada ya kushtakiwa kwa kujihusisha na biashara ya fedha haramu nchini Uingereza.

Mbio za Urais:
Desemba 2006, Jonathan alichaguliwa kuwa mgombea mwenza wa aliyekuwa rais wa nchi hiyo, Umaru Yar'Adua kwa tiketi ya chama tawala cha PDP katika uchaguzi wa rais wa Aprili 2007. Tarehe 20 Aprili 2007, muda mfupi kabla ya uchaguzi wa rais, mashambulizi ya kijeshi ambayo ilikuja kuelezwa na polisi kuwa lilikuwa ni jaribio la mauaji dhidi ya Jonathan yalitokea katika Jimbo la Bayelsa.
Makamu wa Rais:
Kufuatia mgogoro baada ya ushindi wa PDP, wanamgambo waliishambulia nyumba ya Jonathan iliyoko eneo la shamba katika eneo la Otu-Eke, Jimbo la Bayelsa, tarehe 16 Mei; polisi wawili waliuawa katika shambulio hilo. Jonathan hakuwepo wakati wa tukio hilo. Baada ya kuchukua madaraka, Yar'Adua alitangaza mali zake, na tarehe 8 Agosti 2007, Jonathan pia alifanya hivyo.

Kaimu Rais:
Rais Umaru Yar'Adua aliondoka Nigeria tarehe 23 Novemba 2009 kwa ajili ya matibabu. Hakutoa idhini kwa mtu yeyote kuchukua nafasi yake kwa kipindi ambacho yeye hakuwepo. Tarehe 13 Januari 2010, mahakama ya shirikisho ilitoa idhini kwa Makamu wa Rais, Jonathan kufanya kazi za rais katika kipindi cha kutokuwepo rais.

Tarehe 22 Januari 2010, Mahakama Kuu ya Nigeria ilifanya maamuzi kuwa Baraza Kuu la Shirikisho (FEC) lilikuwa na siku 14 kuamua juu ya azimio kama Rais Yar'Adua “hawezi kutekeleza majukumu yake ya kiofisi.” Katika hotuba ya kitaifa mwezi Februari 2010, Jonathan alitoa wito kwa Wanigeria wote kuweka kando tofauti zao za kidini na kikabila na kufanya kazi pamoja kwa faida ya wote.

Tarehe 9 Februari 2010, Seneti iliamua kuwa madaraka ya rais lazima yahamishiwe kwa Makamu wa Rais. Aliteuliwa kutumikia nafasi ya Kaimu Rais, akipewa mamlaka yote ya maamuzi, mpaka pale Yar'Adua atakapopata afya kamili.

Kuhamisha madaraka kwa Makamu wa Rais iliitwa “mapinduzi bila ya neno” na wanasheria wa upinzani na wabunge. Katiba ya Nigeria inatamka uwepo wa barua iliyoandikwa na Rais mwenyewe kuthibitisha kashindwa kuongoza au Baraza la Mawaziri lipeleke timu ya madaktari kumchunguza, lakini takwa hili halikutimizwa kabla ya kukabidhiwa madaraka Jonathan na kuacha wasiwasi wa kikatiba.

Urais:
Umaru Yar'Adua alifariki tarehe 5 Mei 2010. Goodluck Jonathan aliapishwa kumrithi Yar'Adua tarehe 6 Mei 2010, na kuwa Rais wa 14 wa Nigeria na ameitumikia nafasi hiyo hadi uchaguzi wa mwaka huu ambapo amefanikiwa kushinda.

Makala hii imeandaliwa na Bishop J. Hiluka kwa msaada wa mashirika mbalimbali ya habari.

No comments:

Post a Comment